Tuesday 30 August 2016

UVCCM Waahirisha Maandamano Yao, Watii Agizo la Jeshi la Polisi

...

Agosti 22, 2016 Umoja wa Vijana wa CCM tuliutangazia umma na dunia kwamba ifikapo Agosti 31 mwaka huu tutaitisha maandamano ya amani nchi nzima yenye lengo la kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dk John Pombe Magufuli kwa utendaji wenye tija, ufanisi na uliorudisha imani na matumaini kwa wananchi.


Msimamo na dhamira ya kufanya maandamano hayo ya amani yenye maudhui na kusudio hilo, bado uko pale pale ingawaje si kwa tarehe tuliopanga na kutangaza awali yaani Agosti 31 mwaka huu.


Jumuiya yetu kama mjuavyo ni ya Vijana wa CCM, (UVCCM) inapata malezi kwa karibu mno na Jumuiya ya Wazazi ya CCM. Wiki ya jana Mwenyekiti wa Wazazi Taifa Nd. Abdallah Bulembo alikutana na waandishi wa habari akitutaka UVCCM tuahirishe maandamano ya Agosti 31 mwaka huu hadi wakati mwingine.


Kwa mujibu wa Katiba ya Chama Cha Mapinduzi, Jumuiya ya Wazazi ndiyo Msimamizi wa Malezi, Maadili na Adabu kwa Vijana wote nchini, sisi UVCCM tunaamini kuwa sikio halishindani na kichwa, mtoto ni mtoto kwa Wazazi wake hakui, hana jeuri wala ubishi.


Mtoto au watoto wanaokaidi amri, ushauri au maelekezo ya Wazazi wao huitwa watukutu, wenye viburi, manunda na wasioambilika. UVCCM si watukutu, hatukufunzwa tuwe wabishi, wakaidi na wenye viburi. Tumezingatia kutii maelekezo, makatazo na maonyo , tumeambiwa tuahirishe maandamano yetu nasi tumekubali na kuheshimu mambo tuliyoaswa.


Sambamba na hilo tumepata majibu ya barua yetu tuliyomwandikia Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP Ernes Mangu) inayotutaka tuache kufanya maandamano yetu kwa sababu Polisi wamezuia mikutano ya hadhara ya Vyama vya Siasa na maandamano nchi nzima.


Jambo jingine ambalo limetufanya pia tuahirishe maandamano yetu ya Amani ni taarifa ya kintelejinsia iliowasilishwa na Kamati yetu ya Usalama na Maadili ya UVCCM mbele ya kikao cha Sekreteriet yetu, nayo ilipendekeza suala hilo liahirishwe kwa wakati huu hadi muda mwingine.


Pia jambo jingine ambalo limefanya maandamano hayo tuyabatilishe ni kulipisha Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ ) ambalo litakuwa katika shughuli za maadhimisho miaka 52 tokea kuanzishwa kwake.


Wanajeshi wetu watakuwa katika kazi mbalimbali za kijeshi kwenye kambi zao na mitaani kufanya usafi wa mazingira, hivyo isingependeza na wala si heshima wakati sisi tukiandamana, wao wakifanya kazi muhimu kila mmoja wetu zinazomgusa badala yake ni vyema kuwaunga mkono jambo wanalolifanya la usafi wa mazingira.


UVCCM tumekubali, hatutaki kuingia katika uvunjaji wa sheria hasa baaada ya kutakiwa kuahirisha na mamlaka za Kisheria hadi wakati mwingine muafaka na si wakati huu.


Tunaelewa kwamba uamuzi wetu wa awali wa kutaka kuandamana kwa amani hata kama tungenyimwa kibali ungetugharimu, ungetusababishia madhara na pengine hasara, kwa wakati huu na kuona jambo lenyewe ni la kuipa Ari serikali katika kuhimiza Uwajibikaji, Utendaji na Usimamizi bora wa Uendeshaji wa masuala ya kiutawala.


Tulishusha maagizo kwa Makatibu wetu wote wa Mikoa yote 32 na Wilaya 171 ya Kichama tukiwataka waandike barua katika Ofisi za Ma RPC na OCD, washirikiane ili kuratibu maandamano na kuyafanikisha kama tulivyokusudia.


Watendaji wetu wa ngazi husika wamefuata maelekezo, wametii taratibu zetu za kiutendaji na leo tumewajulisha tena wasitishe maandamano hadi tutakapowapa tena maelekezo mengine. Tunawahimiza na kuwataka ni vyema kutii mamlaka za Kikanuni na Kisheria.

UVCCM kwa wakati huu tumeamua kuachana na maandamano badala yake tunajikita katika matayarisho ya kuwapeleka Vijana wetu wakashiriki katika Mafunzo ya Siasa, Utawala, Uongozi, Ufundi na Ujasiriamali yatakayoanza kufanyika katika Chuo chetu kilichopo huko Ihemi Mkoani Iringa ambapo kitakuwa kielelezo na alama nzuri ya kumuunga mkono Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli kwa vitendo.

Tumewataka Makatibu wetu wa Mikoa na Wilaya kuendelea na zoezi la Uratibu na Uhakiki kwa Vijana ambao watateuliwa kushiriki Mafunzo hayo huko Ihemi.

UVCCM tunarejea kusema tena kwamba dhamira ya maandamano yetu ya kusifu Utendaji wa Serikali ya awamu ya tano iko pale pale ila tutapanga tarehe nyingine katika wakati ujao badala ya kufanyika Agosti 31 mwaka huu kama tulivyotangaza hapo awali.

UVCCM tunawataka Vijana wote kuendelea kuheshimu Tunu ya Amani Umoja na Mshikamo wetu kwa Taifa.

KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI
Shaka Hamdu Shaka (MNEC)

KAIMU KATIBU MKUU.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger