Monday 21 July 2014

BREAKING NEWS:BASI LA AM COACH LAPINDUKA WILAYANI MASWA NA KUJERUHI WATU WATATU

...
INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
BASI LA AM COACH LAPINDUKA WILAYANI MASWA NA KUJERUHI WATU WATATU

Basi la AM Coach likiwa eneo la tukio katika kijiji cha Sayusayu wilayani Maswa mkoani Simiyu

Watu watatu wamejeruhiwa vibaya katika ajali ya Basi la AM Coach lililokuwa linatokea katika kijiji cha Sayusayu wilaya ya Maswa mkoa wa Simiyu kuelekea jijini Mwanza

 Majeruhi hao wamekimbizwa katika Hospitali ya rufaa ya Bugando jijini Mwanza kwa matibabu zaidi.

Abiria hao ni miongoni mwa abiria 54 waliokuwa katika Basi hilo lenye namba za Usajiri T607 AQN lililokuwa likitoka wilayani Meatu mkoani Simiyu kuelekea Jijini Mwanza.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Simiyu Charles Mkumbo amesema kuwa ajali hiyo imetokea leo majira ya saa 3:00 asubuhi wakati Basi hilo likitokea mjini Mwanhunzi wilayani Meatu kuelekea Jijini Mwanza mara baada ya kuacha njia na kuparamia mti na kupinduka.

Amesema dereva wa gari hilo Ismail Hassan (46) mkazi wa Mwanza alishindwa kulimudu basi hilo wakati akipishana na roli moja ya mizigo linalodaiwa kukatalia katikati ya barabara na kusababisha dereva wa basi kushindwa kumudu gari lake.

Akielezea hali ya abiria waliojeruhiwa Mkumbo amesema kuwa watu watatu hali zao ni mbaya wamekimbizwa katika hosptali ya rufaa ya Bugando jijini Mwanza.

Kamanda huyo amewataja abiria waliojeruhiwa vibaya kuwa ni Pili Abrahim (54)mkazi wa eneo la Mbugani jijini Mwanza ambaye amevunjika mkono wake wa kushoto na kichwani na mtoto wake wa kike Kwangu Daniel (5) aliyekuwa akisafiri na mama yake kwenda Bugando kwa uchunguzi zaidi wa daktari wake baada ya kuvunjika mguu wa kulia na katika ajali hiyo amevunjika mkono wa kushoto.

Pia mama wa mtoto huyo Mwalu Jilala (32)wote wakazi wa kijiji cha Somanda wilayani Maswa amevunjika mkono wa kushoto,michumbuko na maumivu makali sehemu ya kifua na kiuno.

Wengine katika ajali hiyo ambao wamelazwa katika hopitali ya wilaya ya Maswa ni Aziza Shaaban(42) mfanyabiashara na mkazi wa Ibaga wilaya ya Mkalama mkoani Singida ambaye amejeruhiwa sehemu za kichwani na kukatwa na kitu chenye ncha kali katika mikono wa kushoto,Madaraka Daudi (34)mkazi wa kijiji cha Bushingwamala wilayani Busega na Abel Yohana (27)mkazi wa Maswa na walimu wa nyimbo za injili aliyekuwa anakwenda kurekodi nyimbo jijini Mwanza.

Naye mmoja wa abiria aliyenusurika katika ajali hiyo Happines Mgugu(41)mkazi wa Mbugani jijini Mwanza Ambaye pia ni wifi waPili Abrahim amesema basi hilo lilikuwa katika mwendo kasi na ghafla katika moja ya kona lilikutana na roli moja la mizigo likielekea mjini Maswa ambalo halikupisha njia na kung’ang’ania katikatika ya barabara na kusababisha dereva wa basi kulikwepa na kwenda kuparamia mti na gari hilo kupinduka.


  CREDIT:Samwel Mwanga-Simiyu
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger