Wednesday 22 July 2015

Ulisema ukiolewa, ukipata kazi, ukiongezwa mshahara utafurahi; mbona sasa hufurahi?

...
INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
Karibu kila mtu anatafuta furaha kwa njia mbalimbali anazoona zinafaa. Wapo wanaoamini kuwa wakipata wake/waume, kazi, utajiri, wakijenga nyumba, wakipandishwa cheo na kufaulu mitihani watafurahi sana.
Lakini tafiti zinaonesha kuwa asilimia 87 ya wanaohangaika kutafuta hayo wanayodhani yatawafurahisha huwa hawafurahi sawa na matarajio yao ya awali.

Wataalamu wanakubaliana kuwepo kwa furaha katika siku za mwanzo za kutimia kwa malengo ya watu, lakini kiwango cha furaha kimebainika kupungua kadiri mtu anavyozidi kuishi ndani ya kile alichokitamani au alichodhani akikipata kitamfurahisha.
Ukubwa wa furaha ya siku ya kuchumbiwa, kununua gari, kuhamia katika nyumba mpya, kupandishwa cheo, kuongezwa mshahara, kuolewa au kuoa, hushuka kila siku na hivyo kumfanya mtu afikie hatua ya kuona alichokipata si kitu cha kufurahisha sana na hivyo kuingiwa na mawazo ya kutafuta vitu vingine ambavyo atavipa nafasi kubwa ya kumfurahisha.
Unaposoma haya jaribu kukumbuka moja kati ya vitu ulivyovihangaikia na hatimaye kuvipata, siku hiyo ulikuwa na furaha ya kiwango gani ukilinganisha na sasa?
Bila shaka unatambua kuwa ulivyofurahi siku ulipoolewa ni tofauti na unavyofurahi leo, ingawa ndoa uliyoitafuta ni ileile na mwanaume uliyenaye ni yuleyule, tena inawezekana mlipooana mlikuwa na maisha ya chini lakini leo mmefanikiwa isipokuwa furaha imepungua.
Hapo kuna jambo la kujiuliza kwa nini wengi wetu tunashindwa kupata furaha ya kweli na kubaki kila siku ni watu wa kuhangaika kutafuta hiki na kile cha kutufurahisha.
Mara nyingi kwa uzembe wa kuwaza anachokuwa nacho mtu si bora kuliko kile anachotafuta. Mwanamke mzuri daima hawi mkeo bali ni wa jirani (mtazamo tu), ndiyo maana wengi hufumaniwa na kwa mshangao wanawake ambao hufumwa nao huwa si wazuri ukilinganisha na walio nao.
Kama nilivyoeleza awali kwamba, tuna kila sababu ya kujifunza namna ya kutafuta na kupata furaha ya kweli, ambapo leo tutaangali baadhi ya mambo yanayoweza kutusaidia kupata furaha ya kweli katika maisha yetu ya kila siku. Mambo hayo tutayatafakari kwa kujiuliza aina hii ya maswali.
A-Je tunapokuwa tunatafuta furaha tunatumia uwezo wetu wote au kwa kiwango kidogo? Kama tunatumia kiwango kidogo basi tujue kuwa hata kama tutapata kitu tunachodhani kitatufurahisha tutajikuta hatufurahi, kwa sababu tulichopata kimeshindwa kukidhi matakwa yetu. Ili uwe na furaha ya kudumu tumia uwezo wako wote kutafuta kazi nzuri, biashara nzuri, mke mzuri ili uweze kufurahi kwa muda mrefu, la sivyo ulichopata kitakukinai mapema.
B- Je, tunafanya sawa katika maamuzi au tunabahatisha tu? Endapo tutakuwa tunafanya mambo ya kubahatisha ambayo hatujayahakiki, huzuni yetu itakuwa kwenye makosa na kamwe hatuwezi kufanikiwa kupata yale tunayotaraji yatufurahishe.
Kuna watu wanatafuta watoto lakini hawazingatii kalenda za mimba na wengine wanatafuta mali, elimu kubwa, mke mwema, lakini hawako makini katika kufanya maamuzi kwa usahihi. Ni vema tukathibitisha uchaguzi wa mambo ili tufanikiwe kupata yatakayotufurahisha.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger