Wednesday 22 July 2015

Manyanyaso ya wadada wa kazi

...
INNOCENT-THE BLOGGER-BOY


UTAKUWA umesikia au kuona simulizi nyingi zinazowahusu wadada wa kazi wanazokutana nazo katika familia mbalimbali. Licha ya umuhimu wao mkubwa, lakini baadhi yao wamekuwa wakichukuliwa kama watu wenye shida, wasio na maana ambao licha ya kazi yao ngumu na muhimu kwa familia, wamekuwa wakibezwa, kutukanwa na hata kupigwa.
Filamu ya Kajala inawakilisha aina hii ya kazi zinazofanywa na wasichana, ambao uzoefu unaonesha wanatokana na maisha magumu katika familia wanazotoka, yatima  au hata manyanyaso kutoka kwa ndugu wa karibu.

Riyama amecheza kama ndiye msichana wa kazi akiigiza kwa jina la Kajala, ambaye alijikuta akiifanya kazi hiyo baada ya kuondoka kijijini kwao na kuja Dar es Salaam akiwa na lengo la kumtafuta baba yake mzazi, ambaye hakuwahi kumuona kabla.
Ni kazi inayoakisi ukweli, kwani wasichana wa kazi ni kama watu wenye gundu hivi, kwa mfano katika nyumba ya kwanza alikokuwa akiwafanyia Kajala Masanja na Haji Adam waliokuwa wanandoa, msichana huyo wa kazi anajikuta akichukiwa na mwanamke mwenzake kwa sababu tu mumewe alikuwa akimsifia kwa upishi wake mzuri.
Baada ya kufukuzwa kwa kosa la ‘kupika vizuri’, Kajala hajui pa kwenda lakini bahati nzuri anakutana na kaka mmoja ambaye baada ya kujieleza, anagundua kuwa ni watu wa kutoka sehemu moja, hivyo badala ya kumruhusu kurudi kijijini kwao, anamtaka kuishi chumbani kwake ili aendelee kutafuta kazi jijini Dar.
Anapata kazi ya usaidizi wa ndani katika nyumba ya wanandoa wawili ambao kwa bahati mbaya hawakujaaliwa kupata mtoto. Huko, kama inavyowatokea wasichana wengi, anakutana na mtihani mkubwa wa kutakwa kimapenzi na baba mwenye nyumba, ambaye anamuahidi vitu vingi endapo atamkubalia.
Kajala anakataa katakata kiasi hata cha kutishia kuondoka. Baba mwenye nyumba anamuomba msamaha na kuondoka, lakini anaendelea kumsumbua msichana huyo kupitia simu yake ya mkononi, akimpigia na kumtumia ujumbe, ambao siku moja unanaswa na mkewe.
Mkewe anakuja juu bila kujali utetezi wake, anamfukuza wakati mumewe akiwa kwenye mitikasi. Anarudi nyumbani akiwa na mawazo mengi, lakini ghafla mtu mmoja anamtupia begi naye kupotelea kusikojulikana. Alipolifungua, anakuta burungutu la fedha na kitambulisho kinachoonesha ni cha Mamboleo, yule tajiri aliyesababisha akafukuzwa.
Anajaribu kwenda kwa Mamboleo ili kumpelekea hela zake, lakini anafukuzwa na mkewe kama mbwa, akiamini bado wana uhusiano wa kimapenzi. Mumewe anaporudi nyumbani na kuulizia alipo Kajala, mkewe anamfahamisha kuwa alimfukuza kwa sababu ya mambo yao. Anasikitika sana.
Kutopata mtoto kunamfanya Mamboleo amkumbuke mwanamke aliyempa ujauzito kule kijijini, anakwenda na kuambiwa kuwa mkewe huyo alishafariki siku nyingi na binti aliyezaliwa kaenda mjini. Anaoneshwa picha ya bintiye na kukuta ni Kajala!
Ni filamu nzuri ingawa kama zinavyokuwa nyingi za Kibongo, zina kasoro kadhaa za kiufundi ambazo kama zingerekebishwa, zingekuwa nzuri zaidi. Kwa mfano, Mamboleo anapomuona Kajala akiwa kwenye Bajaj anaposhuka na kumfuata, anaonekana akimwelezea kuwa yeye ni binti yake na anaomba amsamehe kwa yote.
Lakini inashangaza kidogo kwamba wakati picha inawaonesha kuwa wako mbali, sauti inasikika kama wapo karibu. Na kitu kingine ni kwenye begi la fedha lililoporwa. Begi hilo lilikutwa siti ya mbele ya gari, dhahiri kwamba zilikuwa ni fedha za dili, katika hali ya kawaida mtu unawezaje kuweka kitambulisho chako kwenye begi la kubebea hela, hata kama alizitoa benki?
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger