Wednesday 22 July 2015

Mzazi umeharibika, utamnyoosha vipi mtoto?

...
INNOCENT-THE BLOGGER-BOY

Jamani mbona tunajisahau na kuamini kabisa kinachotokea leo tunaonewa. Mzazi jamani anazungumza mpaka mdomo unataka kupasuka lakini mtoto ndiyo kwanza kama katiwa moto anaambiwa afanye.
Juzi nimemkuta mama mtu mzima akitokwa na machozi baada ya mabinti zake kushindwa kumsikiliza kila alilokuwa akiwaambia, lilikuwa likipitia kulia na kutokea kushoto.

Nilipofika aliniomba nimsaidie kuwaeleza wanaye ili wamwelewe.
Ni kweli hii ndiyo kazi yangu kuwakumbusha watu waishi vipi katika uhusiano wao au familia zao. Siku zote samaki akikunjwa mdogo, ukubwani hupati kazi, ila ukifanya makosa akiwa mdogo akikua una kazi ya ziada.
Shoga yangu ni mtu niliyemfahamu vizuri alikuwa tofauti na mimi, yeye aliolewa na mtu mwenye uwezo. Hakuwa na majivuno ila alijitahidi kwenda na wakati kwa vile ankra ilikuwa inamruhusu.
Mavazi yake hayakuwa tofauti na machangudoa, ukikutana naye ghafla utajua yupo kwenye mawindo. Watoto wake aliwalea kizungu, heshima ilikosa  nafasi, kwake kukaa nusu utupu hata mbele ya watoto wa kiume haikuwa tabu. Hali ile iliendelea mpaka mumewe alipofariki ghafla.
Ilibidi  arudie hali ya zamani ya ustaarabu, siku hizi swala tano lakini wanae wa kike hawashikiki kwa mavazi ya aibu hata heshima imepotea, midomo yao imekosa staha, hawamsikii mama yao kwa kila jambo.
Baada ya kupewa kazi hiyo naomba wiki hii nizungumze na wazazi wanaojisahau ili wiki ijayo nizungumze na watoto wenu. Wazazi wengi ambao Mungu amewaangalia kwa jicho la neema, wamekuwa wakijisahau na kuhadaika na kile walichokuwa nacho kwa muda ule.
Neema ile imewafanya kudharau mila na desturi yao, wengi tumekuwa tukiishi kizungu, kuvaa nguo zisizostahili kuvaliwa mbele ya watoto na jamii inayotuzunguka. Tumekuwa tukitokwa na maneno machafu bila kujua lile ni somo tosha kwa wanetu.
Mtoto anapokuwa na mzazi wake hujifunza mambo mengi ambayo huyaona anapenda kuyafanya. Kama mama ukiwa na heshima basi mwanao atakuwa na heshima, kama ukiwa msafi au kupenda kupika vilevile mwanao atajifunza kutoka kwako.
Lakini ukiwa hujiheshimu, huna staha na maneno yako, mvivu unapenda maisha ya starehe, mwanao lazima atachukua hivyo kwa vile ameviona kwako.
Tunajisahau kuwa kila kukicha ndivyo umri unavyokwenda.
Umefika wakati ni mtu mzima mambo ya kijinga hutaki tena  na umegundua uliyofanya ni ya kijinga, sasa unataka kuisaidia familia yako isifanye uliyoyafanya kwa vile hayana faida.
Lakini kila ukisema hawakusikii na hata ukitishia kuwatolea radhi hawakuelewi, unajua kwa nini? Kwa sababu tabia hizo wamejifunza kwako.
Jamani wazazi wenzangu hebu tuwe mfano bora kwa watoto wetu ili tusipate wakati mgumu katika kuwanyoosha. Ni kweli dunia sasa hivi imevaa msuli, watoto wa kike wamekuwa mtihani. Lakini tukiwalea vizuri tangu mwanzo kwa kukemea lolote unaloliona linakwenda vibaya kwa nguvu zote itasaidia sana kutengeneza kizazi chenye heshima na kujifahamu. Lakini mama hujiheshimu, mwanao heshima ataitoa wapi. Tubadilike ili tutengeneze familia bora.
Yangu kwa leo yanatosha. Ni mimi Anti Nasra Shangingi Mstaafu
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger