Tuesday 1 April 2014

MADAWA YA KULEVYA YAKAMATWA GEREZA LA KEKO

...
PIPI 60 za madawa ya kulevya aina ya heroine yanayokadiriwa kuwa na thamani ya shilingi milioni 60 yanadaiwa kukamatwa ndani ya Gereza la Keko jijni Dar es Salaam baada ya mtu mmoja kuingia nayo akiwa ameyameza.
Madawa ya kulevya.
Kwa mujibu wa chanzo, mtu mmoja aliyetambuliwa kwa jina la Mashujaa Udugu Matata, aliingia gerezani humo Machi 21, mwaka huu akitokea kusomewa shitaka la kukutwa na madawa ya kulevya katika Mahakama ya Kisutu jijini Dar es Salaam.
Inadaiwa Matata alikamatwa na polisi katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Machi 17, mwaka huu, saa 8.25 usiku akitokea nchini Brazil.
Baada ya kukamatwa alitoa pipi 102 za madawa hayo. Alipofikishwa gerezani hapo, inasemekana mtuhumiwa huyo hakuwa na hali nzuri kiafya, jambo lililofanya awekwe chumba cha mahabusu wagonjwa ili aweze kufuatiliwa kwa karibu na madaktari.
Mashujaa Udugu Matata aliyekuwa na madawa ya kulevya.
“Kesho yake asubuhi kuna mfungwa alikwenda kufanya usafi katika chumba hicho, wakati anachukua takataka, akaitwa na Matata na kumuomba achukue mzigo uliofungwa kwenye karatasi ambao ulikuwa unanuka kinyesi, akamweleza ampelekee mahabusu mwenzake anayeitwa Abbas Gede,” kilisema chanzo chetu.
Inasemekana Gede ni rafiki wa Matata ambaye naye ana kesi ya ‘unga’ na kwamba awali waliwahi kuishi pamoja Brazil.
Kutokana na sheria kutoruhusu mfungwa kuonana na mahabusu, alilazimika kumpatia mahabusu mwingine ili aufikishe mzigo huo, lakini badala ya kuufikisha, mahabusu huyo aliambiwa na rafiki zake kuwa unga huo ni wa mamilioni ya shilingi, hivyo asubiri awape ndugu zake wakija kumpelekea chakula.
Kamishina Mkuu wa Jeshi la Magereza Tanzania, John Minja.
Hata hivyo, akiwa katika harakati za kutaka kuwapa ndugu zake, askari wa magereza walimkamata na alipoulizwa alikoyatoa, alimtaja Matata na hivyo kufanikisha kukamatwa kwa wote waliohusika na mzigo huo.
Mkuu wa gereza hilo, Sena Shida amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa watu wote waliohusika wataadhibiwa. “Kwa upande wake, Matata ataadhibiwa mara atakapopata nafuu kulingana na sheria ya mwaka 1967, huo unga tumeuchoma moto,” alisema Shida.
Naye Kamanda wa Kikosi cha Kupambana na Kudhibiti Madawa ya Kulevya Tanzania, SACP Godfrey Nzowa alipoulizwa alikiri kukamatwa kwa Matata na kwamba alitoa pipi 102.
Kamanda wa Kikosi cha Kupambana na Kudhibiti Madawa ya Kulevya Tanzania, SACP Godfrey Nzowa.
Awali walijua kuwa zimeisha hata hivyo, Nzowa alisema alimwagiza mkuu huyo kuyapeleka madawa hayo ofisini kwake, akashangaa kusikia yalichomwa. Aidha, alisema aliwasiliana na mkuu huyo wa gareza ambaye alikiri kutokea kwa tukio hilo ingawa hakuweza kutoa ripoti kituo cha polisi kama ilivyo taratibu.
Taarifa zilizopatikana ndani ya jeshi la polisi zinadai kuwa, Matata aliwahi kukamatwa mwala 2007 kwa tuhuma ya kusafirisha madawa ya kulevya na kufikishwa mahakamani na alikuwa chini ya uangalizi wa jeshi hilo na wakati huo alikuwa hajabadili jina, aliitwa Abdallah Mauri Kaikai.
Kamishina Mkuu wa Jeshi la Magereza Tanzania, John Minja aliwahi kuufumua uongozi wa Gereza la Keko kutokana na tuhuma za kuwepo biashara ya madawa ya kulevya ndani ya gereza hilo.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger