Sunday 27 April 2014

Wastaafu wamteka JK

...

wastaafu 13cf0
Na Hudugu Ng'amilo
RAIS Jakaya Kikwete amehujumiwa na viongozi wakuu wastaafu waliomlazimisha kuachana na msimamo wa muundo wa muungano wa serikali tatu na kukumbatia serikali mbili zilizopendekezwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Taarifa kutoka kwa baadhi ya vyanzo vya habari vilivyo karibu na rais, Ikulu na makao makuu ya CCM, zimelithibitishia  kwamba hadi Bunge Maalumu la Katiba linaanza, Rais Kikwete alikuwa na msimamo ule ule wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Baadhi ya viongozi wastaafu, wakiwamo marais na viongozi waandamizi wa CCM, walishinikiza rais aachane na serikali tatu, kwa vitisho kwamba zitaua muungano.
Baadhi ya wastaafu hao walimficha Rais Kikwete kwamba kwa kuwa yeye aliingia madarakani akiwa rais wa muungano wa serikali mbili, halikuwa jambo la busara kwake kujiingiza kwenye historia ya kuwa rais aliyevunja muungano.
Kwa mujibu wa vyanzo vyetu, shinikizo hilo liliambatana na jingine la kumtaka asizindue Bunge kabla ya rasimu ya pili ya katiba mpya kuwasilishwa bungeni, ili apate fursa ya kudhoofisha hoja ya serikali tatu.
Mara baada ya Rais Kikwete kukubaliana na "washauri wake", serikali ililazimika kuingilia kati ili Mwenyekiti wa Bunge, Samuel Sitta atengue kanuni, Mwenyekiti wa Tume, Jaji Joseph Warioba awasilishe rasimu kabla ya rais kuzindua Bunge, jambo ambalo limesababisha mvurugano unaotishia kuvuruga kabisa mchakato wa katiba mpya.
Hata hivyo, hali hiyo inasemekana kumnyima amani Rais Kikwete ambaye ndiye aliyepokea na kusaini rasimu hiyo, kwa maana kwamba aliridhia.
Uamuzi huo umefanya rais aonekane kiongozi asiye na msimamo thabiti katika masuala muhimu.
Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanadai hatua hii imemfanya ashindwe kuacha urithi makini na muhimu katika utawala wake wa miaka 10, kama ambavyo alikuwa amedhamiria.
Wadadisi wanasema wastaafu walimzuia rais kutekeleza azima yake kwa sababu ya hofu tu, wakidhani kwamba katiba mpya yenye mfumo mpya inaweza kufumua mambo yaliyofichika na kuwaingiza matatani.
Wanadai kwamba muungano wenye mfumo mpya una kila dalili za kuiondoa CCM madarakani, na kuhatarisha maslahi ya watawala waliopo na waliopita.
Hoja hii, kwa mujibu wa vyanzo vyetu, ndiyo ilimkuna Rais Kikwete hata akabadili msimamo.
Kwa hali halisi ilivyo, na mchakato unavyoendelea, ahadi ya Rais Kikwete kuwapa Watanzania katiba mpya mwezi huu imeshindikana.
Alipohutubia taifa na kutangaza kuanzisha mchakato wa katiba mpya miaka mitatu iliyopita, alisema kwamba lengo lake lilikuwa kuzindua katiba mpya katika maadhimisho ya sherehe za miaka 50 ya muungano iliyofanyika jana.
Hadi Bunge Maalumu la Katiba linaahirishwa juzi, zilikuwa zimepita siku 68 kati ya 70 zilizotengwa kwa ajili ya Bunge hilo, huku kukiwapo mgawanyiko mkubwa wa wajumbe na kutishia uhai wa muungano, hasa baada ya wajumbe wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kususia Bunge baada ya kukerwa na hujuma na matusi kutoka kwa wajumbe wenzao wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Hadi sasa Bunge la Katiba limefanikiwa kujadili sura mbili za rasimu bila ya kuzipigia kura. CCM imekataa maoni ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba yanayopendekeza mfumo wa muungano wa serikali tatu, wakatetea mfumo wa serikali mbili.
Mapendekezo hayo ni kinyume kabisa cha yaliyomo kwenye rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyowasilishwa ili ijadiliwe na wajumbe hao na kisha kutunga katiba mpya.
UKAWA wanadai kuchoshwa na vitisho na matusi kutoka kwa wajumbe wa CCM na viongozi wa serikali, wakisema kuwa kwa hali ilivyo katiba bora ya wananchi haiwezi kupatikana kwa shinikizo la muundo wa serikali mbili.
Katika hili, Rais Kikwete analalamikiwa kuwa ndiye mvurugaji wa kwanza wa mchakato ambao aliuasisi na kuahidi kuwapatia wananchi katiba bora kabla ya kuondoka madarakani.
Wakati akilihutubia Bunge la Katiba na kulizindua rasmi Machi mwaka huu, Rais Kikwete aliibeza rasimu ya Tume ya Jaji Warioba, akisema takwimu zao kuhusu watu waliotoa maoni ya muundo wa muungano zinatiliwa shaka.
Alisema kuwa muundo wa serikali tatu unaopendekezwa hautekelezeki kwani rais wa dola hiyo hatakuwa na mamlaka kwa vile hana ardhi, rasilimali na hivyo hataweza kukopa.
Kwa mujibu wa Rais Kikwete, katika hali kama hiyo, jeshi linaweza kupindua serikali na hivyo ukawa mwanzo wa kuvunjika kwa muungano, huku akisisitiza kwamba wao kama CCM muundo ambao unaweza kutatua kero zilizopo ni ule wa sasa wa serikali mbili.
Kauli hiyo ya rais iliibua mjadala mkubwa, na hivyo kufifisha ndoto za kupatikana kwa katiba bora kwani ilionyesha wazi kwamba mapendekezo ya wananchi ya serikali tatu yaliyomo kwenye rasimu hayatazingatiwa.
Hali hiyo imeendelea kujitokeza kwenye Bunge Maalumu la Katiba baada ya wajumbe wote wa CCM kuendeleza msimamo wa rais wa serikali mbili na kumshambulia Jaji Warioba binafsi kwa matusi mazito wakidai ana ajenda ya kuvunja muungano kwa kupendekeza serikali tatu.
Hatua ya Rais Kikwete kubadilika na kuvuruga mchakato aliyouasisi na kuusimamia kwa mafanikio makubwa, imeelezwa kusababishwa na mambo makubwa mawili, likiwemo hilo la kuburuzwa na viongozi wastaafu.
Duru nyingine za kisiasa katika suala hilo la kukwama kwa mchakato wa katiba, zinahusisha na rasilimali ya gesi na mafuta zilizopatikana nchini, ambapo inadaiwa mataifa makubwa yanayotaka kuwekeza ndiyo yanaishinikiza serikali isibadili muundo wa muungano uliopo.
Vyanzo vyetu vya habari vinaeleza kwamba mataifa hayo tayari yameweka msimamo wa kuisaidia CCM kifedha ili kuhakikisha inapigana kufa au kupona kutobadili muundo wa muungano katika katiba mpya.
Inaelezwa kuwa muundo wa shirikisho la serikali tatu unaopendekezwa kwenye rasimu ya katiba mpya, unatoa fursa ya wazi kwa wananchi wa serikali washirika kusimamia rasilimali zao tofauti na ilivyo katika muundo wa sasa ambapo mambo mengi yamefanywa siri na serikali.
Hadi sasa majaliwa ya kupatikana kwa katiba mpya yametoweka baada ya UKAWA kujiondoa, na hivyo kulifanya Bunge la Katiba kushindwa kufanya maamuzi ya kupitisha ibara na sura za rasimu kutokana na theluthi mbili ya wajumbe kutoka Zanzibar kushindikana.
Chanzo Tanzania Daima.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger