Sunday 27 April 2014

(CCM) kimepanga mkakati wa kuengua wataka urais wanaume

...

(CCM) kimepanga mkakati wa kuengua wataka urais wanaume.

migiro ec14d
Na Hudugu Ng'amilo
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimepanga mkakati mpya wa kuengua wataka urais wanaume kwa kuingiza hisia za kijinsia kama walivyofanya kumdhibiti aliyekuwa Spika wa Bunge la Tisa, Samuel Sitta, alipotaka kugombea tena nafasi hiyo mwaka 2010.
Wachunguzi wa masuala ya kisiasa wameliambia Tanzania Daima Jumapili kuwa mkakati huo unalenga zaidi kumng'oa Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, ambaye anaonekana tishio kwa wenzake wanaotajwa kutaka urais.
Kwa mkakati huo, kundi la wana CCM walio karibu na Rais Jakaya Kikwete, wameanza kuzungumzia jinsi ya kumpitisha Dk. Asha-Rose Migiro agombee urais katika uchaguzi mkuu ujao 2015.
Kisingizio wanachotumia katika kampeni yao ya siri, ni kusaka kura za wanawake.
Katika mkakati huo, wanamwandaa Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe, kuwa Waziri Mkuu. Tayari Membe ameshatangaza kuwa hatagombea ubunge mwaka 2015.
Kwa mujibu wa vyanzo vyetu, Membe ndiye alikuwa akipigiwa chapuo zaidi miongoni mwa makada wa CCM ili kurithi mikoba ya Rais Kikwete, lakini kutokana na uhusiano wa kifamilia uliopo baina ya wawili hao, sasa ameshawishiwa kuwa atakuwa waziri mkuu endapo Dk. Migiro atashinda.
Wiki hii, gazeti dada la Tanzania Daima Jumatano liliripoti mkakati wa kumzima Lowassa asigombee urais, ambao unaendeshwa na mtoto wa kigogo akishirikiana na Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM).
Dk. Migiro ambaye kwa sasa ni Waziri wa Katiba na Sheria, na pia Mkurugenzi wa Idara ya Mahusiano ya Nje wa CCM, tayari ameanza kuzungushwa mikoani ili kumjengea uwezo na uzoefu wa kisiasa.
Miongoni mwa wana CCM wanaotajwa kuutaka urais 2015 mbali na Lowassa na Membe, ni Waziri Mkuu mstaafu, Fredrick Sumaye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano), Stephen Wasira, William Ngeleja na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba.
"Ukiwalinganisha Membe na Lowassa kwa nguvu na umaarufu ndani ya CCM, hata vigogo wengine wanaotajwa kuutaka urais, utaona hakuna wa kumshinda Lowassa, sasa ndani ya chama wameamua kumchezea rafu.
"Kwa vile ana mtandao mrefu ndani ya CCM, wanafahamu wakikata jina lake itakuwa balaa, hivyo wameona waibuke na hoja ya zamu ya wanawake kama walivyomzima Samuel Sitta asigombee uspika wakampa Anne Makinda," alisema mtoa habari wetu.
Chanzo hicho kinaongeza kuwa mlengwa ni mtoto wa kigogo ambaye anaendesha mkakati wa kumchafua Lowassa ili 2025 ndiye awe mgombea urais baada ya Dk. Migiro kumaliza uongozi wake endapo atachaguliwa kwa vipindi viwili.
Pamoja na mkakati huo, kundi la Membe limeshauriwa kuendelea na harakati za kujiimarisha ili kuhadaa makundi mengine ndani ya chama yaamini kwamba naye ni miongoni mwa watakaochukua fomu za kuomba kuteuliwa kuwania urais.
Hata hivyo, wakati CCM ikiendesha mkakati huo dhidi ya Dk. Migiro ambaye amewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, baadhi ya wasomi wamemchambua mwanamama huyo wakisema hana uwezo huo.
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, alisema kuwa Dk. Migiro haonekani kubadilika licha ya kuwa na elimu kubwa.
"Nilimtembelea ofisini kwake akiwa UN kama Naibu Katibu Mkuu, nilikuwa na kazi za kitaifa kabisa kwa masuala yaliyoshirikisha mabalozi wa Ulaya, lakini aliponiona aliniuliza kwanini sitaki kurejea CCM.
"Huyu hawezi hata kubaini hapa tunazungumzia masuala ya kitaifa au kimataifa, yeye akili yake inawaza CCM tu kila wakati, hajaonyesha kutofautisha u-CCM wake na taaluma ili aweze kusaidia katika nyanja za kitaifa na kimataifa," alisema.
Dk. Slaa aliongeza kuwa aliposikia kuwa Dk. Migiro ndiye aliyeandaa rasimu ya kwanza na ya pili ya katiba kwa upande CCM ambazo zinaleta shida kwa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba zikikinzana na rasimu ya Tume ya Jaji Warioba, amedhihirisha kabisa udhaifu wake.
"Ukiangalia rekodi zake akiwa UN, huwezi ukaona matokeo yoyote, ndiyo maana Ban Ki moon hakutaka tena asaini mkataba kwa awamu nyingine kwani hakuwa na msaada kwake," alisema Dk. Slaa.
Dk. Azavery Lwaitama ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Bukoba ambaye alisema kuwa Dk. Migiro sio mtu mwenye umaarufu wowote ambao unaweza kumfanya amweke katika orodha ya watu wanaoweza kuwa viongozi wa nchi hii.
"Aliteuliwa kuwa Waziri wa Jamii, Jinsia na Watoto, akafanya kazi kipindi kifupi na baadaye akafanywa kuwa Waziri wa Mambo ya Nje wakati wa awamu ya Rais Kikwete.
"Kutokana na kunong'onezana kati ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki moon na Rais Kikwete, Dk. Migiro aliteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na baadaye kwa utaratibu huo huo wa kunong'onezana akarejeshwa tena nchini," alisema.
Dk. Lwaitama aliongeza kuwa vyombo vya habari vya nje viliandika vizuri kuhusu uwezo wa Dk. Migiro wakati akiwa Umoja wa Mataifa, lakini Watanzania hawakujishughulisha kuangalia yaliyoandikwa.
"Nilitarajia kuwa yeye atakuwa na mawazo tofauti katika mjadala wa rasimu iliyopo bungeni, lakini amerudi kwa wana CCM wenzake, anafikiri kama wao, analeta ushabiki wa makundi ya kisiasa, kwa utaratibu huo hawezi kuwa kiongozi anayefaa," alisema.
Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA) ambaye ni mwanafunzi wa Dk. Migiro, alisema haoni dalili au uwezo wowote wa yeye kuwa kiongozi katika wadhifa huo mkubwa wa urais.
"Huyu hajawahi kushiriki uchaguzi wowote akashinda, ukiwemo hata ubunge, isipokuwa nafasi za kuteuliwa ambazo hupewa na marais.
"Angalia kwa mfano katika Bunge hili la katiba ametoa mchango gani wa kukumbukwa na wananchi licha ya kuchangia na kubaki katika Bunge linalotoa matusi na kuacha kujadili rasimu?" alisema Lissu.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger