Monday 28 January 2019

WATOTO 10 WAUAWA KWA KUKATWA KOROMEO,SEHEMU ZA SIRI,ULIMI NA MASIKIO

...

 Watoto 10 wenye umri kati ya miaka miwili hadi sita wamechinjwa na kukatwa koromeo, sehemu za siri, masikio na ulimi wilayani Njombe mwezi huu.

Kutokana na matukio hayo yanayodaiwa kuhusishwa na imani za kishirikina, mkuu wa wilaya hiyo, Ruth Msafiri ametoa amri kwa wazazi na walezi kuwapeleka na kuwafuata shule watoto wao. Pia, ameagiza watoto wote wilayani humo kuhakikisha kuwa wanatembelea kwa makundi.

Aidha, mkuu wa Mkoa wa Njombe, Christopher Ole Sendeka amesema, “Imani za ushirikina na malipizo ya visasi ndivyo vinaleta haya mambo, nimeagiza vyombo vya ulinzi na usalama hasa Jeshi la Polisi kupitia upya leseni za waganga wote wa jadi na kuwakamata wale wote wanaohusishwa kutoa maelekezo yanayosababisha vifo vya watoto na watu wazima kwa imani za kishirikina.”

Hata hivyo, Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola alisema taarifa alizonazo ni za matukio mawili ambayo polisi wanayafanyia kazi.

Lakini wakati Lugola akisema hayo, Msafiri alisema mtoto wa 10 aliokotwa jana akiwa amechinjwa na kunyofolewa viungo. Alisema watoto sita wamefanyiwa ukatili huo katika Halmashauri ya Mji wa Njombe na wanne wanatoka Halmashauri ya Wilaya ya Njombe.

“(Kati ya) sita waliookotwa (wakiwa wamekufa) Halmashauri ya mji Njombe, wawili walipotea na kuokotwa wakiwa wameuawa misituni, wawili wameokotwa maeneo tofauti wakiwa wamekufa na hawakutambulika, wamezikwa na halmashauri,” alisema.

Na Herieth Makwetta na Bakari Kiango, Mwananchi 

Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger