Tuesday 30 July 2019

MKUU WA MKOA AWASHANGAA MADIWANI MANISPAA YA SHINYANGA KUVUNJA KIKAO CHA BARAZA,AKIRI MADUDU.. AAGIZA WATENGUE KAULI ...WAUFYATA!

...

Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack akizungumza kwenye kikao cha baraza la madiwani wa Manispaa ya Shinyanga leo

Na Marco Maduhu - Malunde1 blog Shinyanga.

Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack, ameagiza madiwani wa manispaa ya Shinyanga kutengua maamuzi yao ya kumkataa mkurugenzi wa halmashauri hiyo Geofrey Mwangulumbi, kwamba hawakufuata kanuni na taratibu.


Amesema jambo walilolifanya madiwani hao ni ukiukaji wa kanuni na taratibu, ambapo walipaswa kuitisha kikao maalumu pamoja na kumpeleka malalamiko hayo kwake ili ayafanyie kazi, lakini alishaghaa kusikia tu kikao cha baraza la madiwani kimevunjika madiwani wakimkataa mkurugenzi kutokuwa na imani naye.



Telack amebainisha hayo leo Julai 30, 2019 kwenye kikao cha kawaida cha baraza la madiwani la manispaa ya Shinyanga, ambapo madiwani hao waliamua kuendelea na baraza hilo mara baada ya kutengua maamuzi yao ya jana ya kuvunja kikao cha baraza kwa madai ya kumkataa mkurungezi kutokuwa na imani naye.


Mkuu huyo wa mkoa amesema baraza hilo haliwezi kuendelea kuwepo, endapo kama madiwani hawatatengua maamuzi yao ya kumkataa mkurugenzi, ikiwa kanuni na taratibu zilikosewa kufuatwa.

Kutokana na hali hiyo, madiwani hao walitengua maamuzi yao na kisha kikao cha baraza kuendelea na kujadili ajenda mbalimbali kwa ajili ya maendeleo ya manispaa hiyo.


“Taarifa hizi za kumkataa mkurungenzi nilizipata toka juzi nikaona ngoja niwapime upeo wenu madiwani kama mtafuata kanuni na taratibu... lakini nikashangaa tu mmechukua maamuzi, mkavunja kikao cha baraza bila ya kufuata taratibu, hivyo naagiza maamuzi yenu myatengue kwanza ndipo muendelee na kikao, tofauti na hapo baraza lenu ni batiri,”amesema Telack.


“Ninachotaka kusema madiwani achaneni na malumbano yasiyo na maana kwa kuvunja tu vikao bila ya kufuata taratibu, pale penye mapungufu tuwasiliane ili tuweze kwenda pamoja, nafahamu mapungufu ya manispaa hii, ni kweli yale ambayo mnalalamikia juu ya maazimio yenu kutotekelezwa mko sahihi kabisa,”ameongeza Mkuu wa mkoa.


Aidha amesema tatizo ambalo linasababisha migogoro hiyo kuwepo ni kutoelewana kati ya watumishi wa halmashauri na mkurugenzi wao, sababu kila mtu ni mbabe, na hivyo kusababisha miradi mingi kuwa na usimamizi mbovu na kutotekelezeka, na ndio maana maazimio yenu hayafanyiwi kazi.


Naye Katibu Tawala la mkoa wa Shinyanga Albert Msovela, amewataka watumishi wa manispaa hiyo, madiwani, pamoja na mkurugenzi, kuzungumza lugha moja ili kuondoa makandokando yaliyopo na kutekeleza miradi ya maendeleo kwa wananchi.


Kwa upande wake Naibu Meya wa manispaa hiyo ya Shinyanga John Kisandu, alisema wametengua maamuzi yao ya kumkataa mkurugenzi huyo, na kukiri kwamba hawakufuata kanuni na taratibu, hivyo wataendelea kufanya naye kazi, na kumtaka maazimio yao awe ana yafanyia kazi.


Aidha jana kikao cha baraza hilo la madiwani la halmashauri ya manispaa ya Shinyanga kilivunjika baada ya madiwani wa halmashauri hiyo kudai kutokuwa na imani na mkurugenzi wa halmashauri Geofley Mwangulumbi, kwamba amekuwa hatekelezi maazimio ambayo huazimia yakiwamo ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.



Baraza hilo limevunjika kwenye kikao cha kawaida cha robo ya nne, ambapo wakati wakusoma na kudhitisha muhtasari, mmoja wa madiwani hao David Nkulila (CCM )kutoka Kata ya Ndembezi, aliibua hoja kuwa kwanini maadhimio yao yamekuwa hayatekelezwi, na kudai kutokuwa na imani na mkurugenzi hoja ambayo iliungwa mkono na madiwani na hatimaye kikao cha baraza kuvunjika.




TAZAMA PICHA HAPA CHINI

Mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Mhe. Zainab Telack, akizungumza kwenye kikao cha baraza la madiwani la manispaa ya Shinyanga leo Julai 30,2019 na kuwataka watengue maamuzi yao ya kumkataa mkurugenzi wa halmshauri hiyo Geofrey Mwangulumbi, ndipo waendelee na kikao chao tofauti na hapo baraza lao ni batiri, ambapo madiwani hao walitengua maamuzi yao na kukiri hawakufuata taratibu za kumkataa mkurugenzi.Picha zote na Marco Maduhu- Malunde 1 Blog.

Mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Mhe. Zainab Telack, akikiri pia madai ambayo wanalalamikia madiwani hao ya kutekelezewa mazimio yao ni ya kweli, na kutoa maagizo kwa mkurugenzi akae na watendaji wake na kutekeleza maazimio hayo kwa ajili ya maendeleo ya wananchi.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Mhe. Jasinta Mboneko, akizungumza kwenye kikao cha baraza hilo la madiwani la manispaa ya Shinyanga, na kuonyesha naye kusikitishwa na tukio lililotokea la kuvunjika kwa kikoa cha baraza hilo la madiwani bila ya kufuata utaratibu.

Katibu Tawala wa mkoa wa Shinyanga Albert Msovela, akiwataka Madiwani, watumishi wa manispaa ya Shinyanga pamoja na mkurugenzi kuzungumza lugha moja ili kuondoa makandokando yaliyopo na kuwa kitu kimoja na kutekeleza miradi ya maendeleo kwa wananchi

Naibu Meya wa manispaa ya Shinyanga John Kisandu, akizungumza kwenye baraza hilo na kutengua maamuzi ya baraza ya kumkataa mkurugenzi wa mansipaa hiyo Geofrey Mwangulumbi kuwa hawana imani naye kutokana na kushindwa kutekeleza mazimio yao.

Madiwani wa manispaa ya Shinyanga wakiendelea na kikao cha baraza, mara baada ya kutengua maamuzi hayo ya kumkataa mkurugenzi wa manispaa hiyo Geofrey Mwangulumbi, kuwa walikosea sababu hawakufuata utaratibu.

Madiwani wakiendelea na kikao cha baraza wakijadili ajenda mbalimbali kwa ajili ya mustakabali wa maendeleo ya manispaa ya Shinyanga.

Diwani wa Kata ya Kolandoto Agnes Machiya akichangia ajenda kwenye kikao cha baraza hilo la madiwani la manispaa ya Shinyanga.

Diwani wa Kata ya Kitangili Khamis Ngunila akichangia ajenda kwenye kikao cha baraza la madiwani la manispaa ya Shinyanga.

Diwani wa viti maalumu manispaa ya Shinyanga Shela Mashandete akichangia ajenda kwenye kikao cha baraza la madiwani la mansipaa ya Shinyanga.

Madiwani wakiendelea na kikao cha baraza.

Watendaji wa manispaa ya Shinyanga wakiwa kwenye kikao cha baraza la madiwani.

Watendaji wa manispaa ya Shinyanga wakiwa kwenye kikao cha baraza la madiwani.


Picha zote na Marco Maduhu- Malunde 1 Blog.

Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger