Monday 1 February 2016

Baba P… Baba Pili… Baba Pilima!-16

...
INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
ILIPOISHIA GAZETI LA IJUMAA:
“Mimi sijui,” alijibu baba Pilima. Alishaanza kuwa na wasiwasi sasa. Akashika simu na kuandika namba ya rafiki yake Juma wa Mbezi-Beach ili amuulize kisa cha kutoa namba yake kwamba anawajua wateja wa mbao wakati anajua yeye si mfanyabiashara.
JIACHIE MWENYEWE SASA…
Baba Pilima mwenyewe alitaka kumzuia, lakini moyoni akasema aache tu, atapambana mpaka mwisho na vile mkewe yuko njiani, mshindi atakuwa yeye tu…
“Haloo Juma…” alianza kwa kuita baba Pilima feki…
“Haloo, niambie…”
“Eti unamfahamu jamaa anaitwa…”
Kabla hajamaliza kusema, simu yake ilikatika kwa sababu ya mtandao, akapiga tena.
Simu iliita sana, lakini haikupokelewa upande wa pili.
Simu ya baba Pilima mwenyewe ikaita, mkewe alishafika…
“Nipo hapa nje ya Baa ya Sewa…”
“Ingia ndani sasa.”
“Poa.”
Mama Pilima alizama ndani na kushtuka kumwona baba Pilima mumewe akiwa amekaa na baba Pilima feki…
“Ha!” alihamaki mama Pilima, akaanguka tena.
Baba Pilima feki alishtuka sana. Alishtuka kwa mambo mawili. Kwanza kwa kumwona mama Pilima, pili kwa kuanguka…
“He! Huyu mwanamke namfahamu, ni mwanamke wangu, sasa sijui imekuwaje tena na sijui amekuja kufuata nini hapa?” alihoji baba Pilima feki huku akimtumbulia macho mama Pilima pale chini…
“Wewe ni mwanamke wako, mimi ni mke wangu,” alisema baba Pilima mwenyewe. Baba Pilima feki naye akaanza kuweweseka huku jasho jembamba likimtoka…
“Ina…ina…ina maana…ina maana,” alisema baba Pilima feki ambaye kwenye simu ya mama Pilima aliseviwa kwa jina la Baba P…
“Usisumbuke sana ndugu, kaja hapa kwa sababu yangu na mimi nimekutafuta wewe kwa sababu ya yeye. Wewe ndiye Baba P, unatembea na mke wangu huku ukijua ana mume…muda si mrefu nimetoka kwa Baba Pili…nadhani ni mapacha maana hata sura zenu zinafanana,” alisema baba Pilima huku akiwa amekasirika sana.
Watu walimzunguka mama Pilima, baba Pilima mwenyewe akiwa anamsaidia mkewe akae kwenye kiti maana safari hii hakupoteza fahamu kama kule DDC-Kariakoo…
“Pole sana jamani…pole,” watu walimpa pole mama Pilima akiwa amekaa kwenye kiti…
“Baba Pilima mume wangu,” aliita mama Pilima kwa sauti ya chini sana ikiashiria kuchoka na mambo yalivyokwenda…
“Nini?” baba Pilima alimjibu hivyo mke wake…
“Nimekukubali mume wangu. Hata kama leo utanipa talaka lakini nitakuheshimu kuliko mwanaume yeyote hapa duniani. Najua kukutana wewe na yule mwanaume Kariakoo ilikuwa mbinu yako, lakini pia kukutana na huyu hapa pia ni mbinu yako japokuwa mimi nimejikuta nikiingia kichwakichwa…
“Sikutaka kukusaliti. Imetokea tu! Lakini si kwamba sikupendi na huenda labda ni kwa sababu ya mambo yetu ya siri nyumbani…nisamehe kwa utangulizi lakini uamuzi ni wako ingawa mimi kama mimi ningependa unisamehe,” alisema mama Pilima huku akiona aibu kwa watu waliokuwa wakimsikiliza.
Baba Pilima alimwangalia mkewe kwa macho ya kumshangaa sana kisha akasema…
“Umemaliza kusema?”
“Nimemaliza baba Pilima mume wangu.”
“Kwa hiyo kama kuna matatizo nyumbani ndiyo ukaamua kutembea na mapacha?”
“Hiyo nayo ni stori ndefu mume wangu, inataka nafasi ya kusimulia kwa mapana,” alisema mama Pilima huku akizidi kuona aibu.
Baba Pilima alisimama, akamuaga baba P kwamba anaondoka huku akisema…
“Mkubwa mimi sifanyi biashara yoyote. Sina mbao wala miti. Ila nilitaka kukuona. Nimejikaza sana katika hii ishu.
Ningekuwa mwanaume mwingine nadhani ningeua mtu au ningeua watu. Lakini mjue kwamba mimi ni binadamu kama binadamu wengine, sijapenda mlichonifanyia. Nasema sijapenda kwa sababu wote mlijua huyu ni mke wa mtu japokuwa hata yeye alitakiwa kujijua kwamba ni mke wa mtu. Naye ana nafasi yake ya lawama.”
Wakati baba Pilima akimalizikia kutoka nje ya baa hiyo, mama Pilima kule ndani aliangua kilio huku naye akisimama…
“Nilishasema mimi sijawahi kusaliti jamani. Sijui shetani gani amenikuta katika kipindi hiki cha kuelekea uzeeni. Kwani kama ningemvumilia mume wangu na udhaifu wake nini kingenipata mama Pilima!”
Watu waliojua kisa hicho walimzomea mama Pilima huku baba P akibaki kushangaa. Simu yake ikaita, alipiga baba Pili…
“Haloo,” alipokea baba P…
“Ndugu yangu yamenikuta mazito,” alisema baba Pili…
“Nadhani hayo yako ni madogo, mimi zaidi…mwenzako si nimefumaniwa na mume wa mama Pilima…” alisema baba P.
yaani we acha tu…haya wewe mwenzangu yamekupata makubwa yapi?” alisema baba P…
“He! Mume wa mama Pilima?”
“Ndiyo…”
“Mbona hata mimi pia imekuwa hivyo…”
“Wewe lini?”
“Muda si mrefu ndugu yangu.”
Simu ya mama Pilima iliita akiwa nje ya baa hiyo, alipoangalia mpigaji ni mume wake…
Je, unajua nini kilitokea hapo? Usikose kusoma kwenye Gazeti la Ijumaa, siku ya Ijumaa.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger