Thursday 25 February 2016

TCU Yabani Madudu Vyuo Vikuu Tanzania,maamuzi kutolewa kesho

...
INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu nchini (TCU), Profesa Yunus Mgaya.
Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu nchini (TCU), Profesa Yunus Mgaya, amesema katika ukaguzi wa vyuo vikuu unaoendelea nchi nzima, wamebaini kasoro mbalimbali ikiwa ni pamoja na vyuo vyote kutokuwa na walimu wa kutosha huku vingine vingi vikitumia mitala isiyoendana na soko la ajira.
 
Alisema kwa vyuo vingi visivyo vya serikali, kati ya asilimia 60 mpaka 80 ya walimu wake, hawana kiwango cha elimu kinachotakiwa kwa mwalimu wa chuo kikuu (shahada ya uzamivu).
 
Ukaguzi wa TCU kwa vyuo vyote nchini, unafuatia Waziri wa  Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, kuiagiza taasisi hiyo kufanya ukaguzi kwenye vyuo vikuu vyote na vile watakavyobaini vimekiuka kanuni za kutoa elimu ya juu, vipewe adhabu ikiwa ni pamoja na kuvifutia ithibati.
 
“Ukaguzi umebaini Tanzania kwa ujumla wake kuna upungufu wa walimu kwenye vyuo vikuu vyote, hakuna kinachojitosheleza kwa walimu, hata Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Muhimbili...lakini tulichokiona kweye vyuo kama cha Dar es Salaam, Muhimbili, St. Augustine na Tumaini, vimekuwa vinawasomesha walimu wake, vina mradi na bajeti za kusomesha ili wapate shahada ya tatu ndani na nje ya nchi,” alisema na kuongeza:
 
“Baadhi ya vyuo vikuu binafsi, wao hawasomeshi, kazi yao ni kuwavizia wenzao wakisomesha ndipo wawachukue, bahati nzuri hawana fedha za kuwalipa, maana hawa wakisomeshwa mishahara yao ni mikubwa hawawezi kuwalipa, wanaishia kuwachukua kwa muda wa ziada,” alisema.
 
Kuhusu viwango vya elimu vya walimu, Profesa Mgaya alisema: “Ukiona chuo kina walimu karibu asilimia 60 hadi 80 ni wa shahada ya pili (shahada ya uzamili) tu, hawana ya tatu (shahada ya uzamivu).
 
Pia tumebaini vyuo vikuu vinavyofundisha sayansi vina upungufu kwenye maabara, hakuna vifaa vya kisasa vya kutosha vinavyoendana na idadi ya wanafunzi. Hii ipo karibu vyuo vikuu vyote binafsi tulivyovikagua angalau vile vya umma vina mpango wa kutekeleza hilo,” alisema Profesa Mgaya.
 
Akielezea kuhusu mitaala alisema baadhi ya vyuo binafsi vimekuwa vikizalisha wahitimu wasioendana na soko.
 
Alisema wanapobaini upungufu kama huo, hurudi chuoni kuwataka waipitie mitaala yao ili iendane na soko.
 
Pia alisema changamoto nyingine waliyoibaini ni ufinyu wa maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya ujenzi wa maktaba.
 
“Lipo tatizo la maktaba siyo kubwa na tatizo la vitabu, mfano UDSM kinaprogramu ya kuongeza ukubwa wa maktaba yake mara tatu ya iliyopo, lakini baadhi ya vyuo vikuu binafsi hawana program yoyote,” alisema.
 
Profesa Mgaya akizungumzia kuhusu ujio wa wanafunzi zaidi ya 100 wa Chuo Kikuu cha Mt. Joseph Tanzania (SJUIT) kampasi ya Arusha waliokuja Dar es Salaam ili kueleza changamoto zinazowakabili, alisema bahati nzuri waliyoyaeleza jopo la wataalam waliotumwa kuchunguza wameshakabidhi ripoti Jumatatu ya wiki hii.
 
Alisema wanafunzi hao walibainisha changamoto zao kuwa ni walimu hawatoshi, wengine hawana viwango, baadhi wakifundisha hawaeleweki kwa sababu lafudhi zao ni za Kihindi.
 
Alisema wataalam wa TCU wameshafanya ukaguzi kwenye chuo hicho na ripoti yake itajadiliwa leo kwenye Kamati ya Ithibati ya Vyuo Vikuu kisha kutoa mapendekezo ya hatua zinazotakiwa kuchukuliwa.
 
Alisema uamuzi wa kitakachoafikiwa yatatolewa kwa umma kesho.
 
Alisema matawi mengine ya chuo hiyo yaliyo Bagamoyo, Luguruni na Boko vya Dar es Salaam, ukaguzi wake umekamilika.
 
Pia alisema wanafunzi hao wamesema wana tatizo la maabara, maktaba, ada ni kubwa na kuzilalamikia sheria za chuo kuwa ni kali.
 
Kuhusu ada alisema serikali haijawa na ada elekezi, lakini Aprili 9, mwaka jana walipeleka mapendekezo yao serikalini.
Alisema kutokana na bajeti wakati huo ilikuwa imeshapita, wanatarajia mwaka huu watafanikiwa. 
 
"Changamoto zao serikali tumeshaunda tume ya uchunguzi juzi Jumatatu jopo lilituletea matokeo, kesho tunaingiza kwenye kamati yetu ya ithibaki," alisema.
CHANZO: NIPASHE
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger