Tuesday 2 February 2016

UTARATIBU WA KUSHUGHULIKIA MALALAMIKO YA WANAFUNZI -MAAFISA MIKOPO WAGUSWA

...
INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
1.0    UTANGULIZI
Imebainika kwamba bado malalamiko ya baadhi ya wanafunzi hayashughulikiwi ipasavyo katika muda mfupi na kupelekea wanafunzi kwenda kulalamika ofisi za juu hata kwa masuala ambayo yako wazi na ambayo maelezo yake wangepaswa kuyapata katika ngazi za vyuo au katika Ofisi za Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu.
Aidha, itakumbukwa kuwa, ili kuboresha ufanisi wa utoaji mikopo, mwezi Agosti mwaka 2011, Serikali kupitia iliyokuwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ilivielekeza vyuo vyote za elimu ya juu kuanzisha madawati yatakayoratibu na kusimamia masuala ya mikopo na ruzuku kwa wanafunzi wa vyuo husika. Agizo hili limetekelezwa vizuri kiasi na hivi sasa kila chuo cha elimu ya juu kina Afisa anayesimamia masuala ya mikopo na ruzuku kwa wanafunzi wao wanaokopesheka.
Hivyo, Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) inapenda kuwakumbusha wadau wake wote, wakiwemo wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu, kuhusu utaratibu wa kuwasilisha malalamiko au maswali yanayohusu mikopo na ruzuku kwa wanafunzi wa elimu ya juu kama ifuatavyo hapa chini.

2.0    UTARATIBU WA KUWASILISHA MALALAMIKO

i.    KWANZA, mwanafunzi yeyote anayefadhiliwa na Serikali kupitia Bodi ya Mikopo mwenye swali au malalamiko anatakiwa kuwasilisha suala lake kwa Afisa mhusika anayesimamia Dawati la Mikopo/Ruzuku (Loan Officer) aliyepo chuoni kwake. Hao ‘Loan Officers’ hivi sasa wana uzoefu wa masuala ya mikopo na ruzuku zitolewazo na Bodi;
ii.    PILI, baada ya swali au malalamiko kupokelewa, ‘Loan Officer’ huyo anapaswa kuyapokea na kuyatafutia suluhisho malalamiko hayo na kumjibu mwanafunzi ndani ya siku mbili (02), kama siyo siku hiyo hiyo, tangu apokee swali au malalamiko hayo;
iii.    TATU, ikiwa siku mbili (02) zitapita bila mwanafunzi kupata jibu, mwanafunzi awasilishe malalamiko yake kwa mamlaka ya juu ya huyo ‘Loan Officer’ ambaye naye anapaswa kutoa majibu au kuchukua  hatua ndani ya siku mbili (02), kama siyo siku hiyo hiyo;
iv.    NNE, ikiwa kiongozi wa chuo husika cha elimu ya juu atakuwa hana jibu la swali au malalamiko yaliyowasilishwa kwake, anapaswa kuwasilisha suala hilo Ofisi ya Bodi ya Mikopo ya Kanda iliyo karibu na chuo chake. Ofisi ya Kanda itawajibika kutoa jibu siku hiyo hiyo ya kupokea maswali au malalamiko hayo au kuwasilisha suala hilo Makao Makuu ya Bodi ya Mikopo kama hana maelezo yake;
v.    TANO, kwa vyuo vya elimu ya juu ambavyo havipo karibu na ofisi za Kanda za Bodi ya Mikopo, uongozi wa chuo husika unapaswa kuwasiliana na makao Makuu ya Bodi ya Mikopo moja kwa moja kwa njia ya barua pepe ifuatayo: malalamiko@heslb.go.tz ;
vi.    SITA, baada ya kupokea malalamiko hayo, Bodi ya Mikopo Makao Makuu  itatoa majibu kwa malalamiko/maswali yaliyowasilishwa siku hiyo hiyo au ndani ya siku mbili (02) tangu kupokelewa kwa malalamiko au maswali hayo; na
vii.    SABA, mara tu baada ya kupokea majibu ya swali au malalamiko yaliyowasilishwa kutoka Bodi ya Mikopo, uongozi wa chuo cha elimu ya juu utayafikisha majibu hayo kwa mwanafunzi husika siku hiyo hiyo kupitia kwa ‘Loan Officer’ wa chuo husika.

3.0    HITIMISHO

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu inasisitiza kuwa ni muhimu kwa wanafunzi na wadau wote kuzingatia utaratibu huu ili kuongeza ufanisi katika kushughulikia malalamiko ya wanafunzi.


IMETOLEWA NA:
MKURUGENZI MTENDAJI,
BODI YA MIKOPO YA WANAFUNZI WA ELIMU YA JUU

Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger