Monday 30 September 2019

Waziri Mkuu Kuanza Ziara Ya Kikazi Ya Siku Tatu Mkoani Singida

...
Na Dotto Mwaibale, Singida
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa anatarajiwa kuanza ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani Singida na kutembelea miradi mbalimbali ya maendeleo.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt.Rehema Nchimbi alisema ziara hiyo ataianza Oktoba 4, 2019 na Oktoba 7 atafungua rasmi maonesho ya pili ya viwanda vidogo vidogo (SIDO) yatakayofanyika kitaifa mkoani humo.

NCHI sita za Jumuiya ya Kusini mwa Afrika (SADC) zinatarajiwa kushiriki maonesho hayo ambazo ni Kenya, Burundi, Ruanda, Uganda, China, India na Afrika kusini.

Dkt.Nchimbi alisema maonesho hayo yataanza kufanyika Oktoba 4 hadi 9 mwaka huu,na yatafunguliwa rasmi oktoba 7 na waziri mkuu Kassimu Majaliwa.

” Maonesho haya yatafanyika sanjari na maadhimisho ya wiki ya chakula duniani ambayo yatafanyika kuanzia Oktoba 10 hadi 16 mwaka huu katika Viwanja vya Bombadier zamani Peoples” alisema Nchimbi.

Alisema kufanyika maonesho hayo mkoani Singida ni fursa kwa wananchi wa mkoa huo ambao unakuwa kiuchumi kutokana na shughuli za kilimo, ufugaji, biashara na viwanda.

Pia alisema mkoa wa Singida wanajivunia kuchaguliwa kufanyika kwa maonesho hayo kitaifa na hii itawapa hamasa kubwa wananchi katika kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya usindikaji kutokana na mazao yanayolimwa mkoani hapa.

Dkt. Nchimbi alitumia nafasi hiyo kuwakaribisha wananchi wote wa mkoa huo na mikoa ya jirani kujitokeza kwa wingi kupokea ugeni huo na kushiriki katika maonesho hayo.

Aidha mkuu wa mkoa alisema kabla ya kufungua maonesho hayo waziri mkuu Kassim Majaliwa atafanya ziara ya kikazi kila wilaya na halmashauri zote za mkoa huo na kuzungumza na wananchi pamoja na watumishi katika mkutano wa hadhara.

Katika ziara hiyo Majaliwa atatembelea miradi mbalimbali ya kimkoa na miradi mikubwa ya kitaifa, ambapo miradi ya kitaifa ni mradi wa kupokea na kupozea umeme uliopo katika halmashauri ya manispaa ya Singida pamoja na mradi wa daraja Sibiti linalounganisha mkoa wa Singida na Simiyu lililopo wilayani
Mkalama.


Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger