Saturday 24 May 2014

KIMENUKA BONGO MOVIE!!..WEMA NA MTITU WAKWIDANA

...

KIMENUKA! Beautiful Onyinye, Wema Isaac Sepetu na Mkurugenzi wa Kampuni ya Five Effects, William Mtitu wamekwinda ‘live’ ndani ya gari, Risasi Jumamosi lina kisanga kamili.
Staa katika tasnia ya filamu za Kibongo, Beautiful Onyinye, Wema Isaac Sepetu

UWANJA WA VITA
Taarifa za uhakika zilieleza kuwa, tukio hilo lilijiri juzikati maeneo la Bunju, Dar nyumbani kwa mke wa aliyekuwa mwigizaji na prodyuza wa Bongo Movies, Adam Phillip Kuambiana wakati ndugu, mastaa na jamaa walipokuwa wameweka matanga ya msiba.
Kwa mujibu wa chanzo makini kilichoomba kustiriwa gazetini, kisa cha yote kilidaiwa kuwa ni Mwenyekiti wa Bongo Movie Unity, Steven Mengere ‘Steve Nyerere’ kueneza sumu kwa mastaa kuwa wawachunie Mtitu na mwigizaji Jacob Steven ‘JB’ ambao alitofautiana nao msibani hapo.
TUJIUNGE NA CHANZO
“Steve alipishana kauli na JB, Mtitu akaingilia, sasa Steve akamwaga ‘sumu’ kwa wasanii wengine ambao ghafla walianza kuwachunia JB na Mtitu msibani hapo,” kilisema chanzo.
MTITI WAIBUKA
Chanzo hicho kilizidi kudai kuwa, Mtitu, baada ya kuchuniwa huko na wasanii wengine, kuna wakati alikuwa kwenye gari na kutaka kupishana na gari la mwigizaji Aunt Ezekiel ambalo ndani yake alikuwemo Wema, mtiti ukaibuka.
“Aunt alishusha kioo na kumuuliza Mtitu umemfanya nini Steve? Wakati Mtitu akitaka kumjibu juu ya kile kilichotokea, dada mkubwa au mama la mama (Wema) akaununua ugomvi usiomhusu,” kilitiririka chanzo.
KIHEREHERE CHA WEMA CHAANZISHA MTITI
Chanzo hicho bila kupepesa macho, kiliweka bayana kuwa, Wema alindandia kauli ya Aunt na kumwambia Mtitu ni mtu asiyempenda.
Mkurugenzi wa Kampuni ya Five Effects, William Mtitu akiweka shada la maua tatika kabuli la kuambiana.
“Wema alisema katika watu ambao hawapendi duniani, Mtitu ndiyo namba moja ndipo hapo uvumilivu ulipomshinda Mtitu na kushuka kwenda kumvaa Wema.
“Alipofika aliingiza mkono kupitia upenyo mdogo ulioachwa katika dirisha, akafungua loki ya mlango na kumkalia Wema mapajani huku akimkwida shingoni.
“Wema naye akajibu mapigo kwa kumkwida Mtitu huku akiporomosha maneno machafu (hayaandikiki gazetini) ndipo Mtitu alipoonesha uanaume na kumpa maneno ya kuashiria atampa kipondo ambacho hajawahi kukiona maishani mwake,” kilisema chanzo.
AUNT AOKOA JAHAZI
Ilidaiwa kuwa, baada ya Wema kutaitiwa vilivyo na Mtitu, Aunt ilibidi aingilie kati na kumuomba Mtitu amsamehe bure na amuondoe shetani eneo hilo.
“Aunt alimuomba sana Mtitu kuwa amuachie Wema kwa kumsihi kuwa yeye wanaheshimiana sana, Mtitu akamuachia na kushuka ndani ya gari huku akimtahadharisha Wema kuwa asije akarudia kuingia kwenye kumi na nane zake,” kilizidi kumwaga data chanzo.
WAO WANASEMAJE?
Baada ya kujiridhisha na chanzo hicho, wanahabari wetu walianza kuwasaka wahusika ambapo wa kwanza alikuwa ni Wema ambaye simu yake iliita bila kupokelewa (anaweza kututafuta akiisoma habari hii).
Baada ya Wema kutopokea, mapaparazi wetu walimgeukia Mtitu ambaye alijibu kwa kifupi kisha akakata simu na alipopigiwa tena, hakupokea:
“Mimi sipendi mambo ya kijinga, mtu hawezi kuingilia visivyomhusu nikamuangalia tu.”
Jitihada za kumpata Aunt ziligonga mwamba baada ya simu yake ya kiganjani kuita bila kupokelewa.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger