Thursday 28 November 2019

Zaidi Ya Wakulima 500,000 Wamejengewa Uwezo Chini Ya Mfumo Shirikishi Wa Udhibiti Ubora Kwa Ajili Ya Soko La Ndani Na La Jumuiya Ya Afrika Mashariki

...
Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Dodoma
Nchi mbalimbali Duniani zinajadili na kuweka mikakati ya kuendeleza kilimo-hai. Mwaka 2010, Umoja wa Afrika kupitia Marais wake, ulipitisha Azimio la mpango na mkakati wa kilimo-hai kuelekea ajenda yake ya miaka 50 ijayo (Agenda 2063), na kuzitaka nchi zote kuchukua hatua kutekeleza azimio hilo.

Katika kufikia azimio hili la Umoja wa Afrika, Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na wadau imefanikiwa kuwa na Sera ya Kilimo iliyohusisha kilimo-hai kwa upana wake na uwekezaji kwenye viwanda vinavyo chakata mazao ya kilimo-hai.

Hii inaenda sambamba na jitihada za Serikali ya awamu ya tano chini ya Mheshimiwa Rais John Pombe Joseph Magufuli ya kutaka Tanzania ifikie uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 kupitia sera ya viwanda. Ambapo kumeanzishwa dawati la kilimo-hai katika idaya ya Maendeleo ya Mazao ili  kufikia idadi ya wakulima  na wafugaji 149,000 waliothibitishwa na kuingia katika fursa ya masoko ya bidhaa za kilimo-hai kimataifa, wanaozalisha kwenye eneo la hekta takribani 278,000.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) ameyasema hayo jana tarehe 26 Novemba 2019 wakati akifungua kongamano la kitaifa la kilimo-hai la siku mbili linalofanyika Jijini Dodoma na kuongeza kuwa zaidi ya wakulima 500,000 wamejengewa uwezo chini ya mfumo shirikishi wa udhibiti ubora (participatory guarantee system - PGS) kwa ajili ya soko la ndani na la Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Ameongeza kuwa kilimo-hai Duniani katika mataifa mbalimbali kinakua kwa kasi kubwa. Inakadiriwa kuwa soko la bidhaa na mazao ya kilimo-hai duniani ni wastani wa Euro 89 bilioni ambapo hiyo ni fursa kubwa kwa kwa Tanzania kwani ni nchi ya tatu kati ya tano barani Afrika zinazoongoza kwa kuwa na eneo na idadi kubwa zaidi zilizo thibitishwa katika mfumo huo wa kilimo-hai, ikiongozwa na Uganda na Ethiopia na kufuatiwa na Kenya na Jamhuri ya Kidemokrsi ya Kongo (DRC).

Waziri Hasunga amesema kuwa kufuatia kupitishwa kwa mtaala mpya unaojumuisha stadi na programu za kilimo-hai katika vyuo vya mafunzo ya kilimo na vyuo vikuu kikiwemo SUA, inatarajiwa idadi hiyo ikiongezeka mara dufu. Vyama vikuu vya ushirika – KCU, KNCU na KDCU pamoja na makampuni kama Biore, Biosustain, Biolands na OLAM  wamewezesha nchi yetu kufikia mafanikio hayo.

Pia, ametoa mwito kwa wadau wa kilimo-hai nchini kufanya kazi kwa karibu na Wizara na Taasisi zake na Serikali yote kwa ujumla ili kwa pamoja kuwezesha upatikanaji wa uhakika wa chakula na lishe na masoko utakao boresha maisha ya watanzania walio wengi kwenye sekta ya kilimo.

Amesema kuwa baadhi ya changamoto katika kuendeleza kilimo-hai nchini ni pamoja na uhakiki (certification) wa mazao hayo kuwa ya kilimo hai, fedha kwa ajili ya uwekezaji katika kilimohai kibiashara, kutoyafikia masoko maalumu (niche market) hususani katika nchi za Ulaya kutokana na kutokidhi vigezo vya masoko hayo na tishio la mabadiliko ya tabianchi ambayo ni fursa katika kuendelea kilimohai nchini.

Waziri Hasunga amewahakikishia wadau wote waliohudhuria katika mkutano huo kuwa Wizara ya kilimo itaendelea kushirikiana nao kwa karibu hivyo wasisite kuwasilisha mapendekezo yao wakati wowote ili Serikali iyashughulikie kwa maslahi ya kuendeleza kilimo-hai nchini.

Kadhalika, amewasihi wadau wote kupitia kongamano hilo, kujadili na kuzitafutia ufumbuzi changamoto hizo ili kuweza kuongeza uzalishaji kupitia kilimo-hai.



Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger