Thursday 28 February 2019

HATMA YA DHAMANA YA MBOWE,MATIKO KESHO

...
Hatma ya dhamana ya Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe na mbunge wa Tarime Mjini, Ester Matiko inatarajiwa kujulikana kesho March 1, 2019 katika Mahakama ya Rufani ambapo mahakama hiyo inatarajia kutoa uamuzi wa rufaa iliyokatwa na Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP) dhidi ya Mbowe na Matiko.

Katika uamuzi huo, mahakama inatarajiwa ama kukubali Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kuendelea kusikiliza rufaa iliyokatwa na Mbowe na Matiko, kutokana na kufutiwa dhamana katika kesi ya uchochezi iliyopo Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu au kuitupilia mbali rufaa hiyo.

Mapema Leo Februari 28.2019 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kesi ya uchochezi inayowakabili vigogo hao na wenzao saba wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), iliitwa kwa ajili ya kutajwa na Wakili wa Serikali, Wankyo Simon akadai kuwa bado wanasubiri hatua za rufaa zilizopo Mahakama ya Rufaa na Mahakama Kuu.

Hata hivyo, Wakili wa Utetezi, Profesa Abdallah Safari alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi kuwa ni muhimu mahakama ikapewa taarifa ya maendeleo ya rufaa zote na kwamba wao wamepata taarifa kuwa kesho Mahakama ya Rufaa itatoa uamuzi dhidi ya rufaa hiyo.

Wakili Wankyo alipoulizwa alidai kuwa yeye bado hajapata taarifa kuhusu uamuzi huo na kwamba hata kama isingekuwa hivyo bado wanaomba tarehe ya kutajwa.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Machi 14, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.

Novemba 23, 2018 Jaji Wilbard Mashauri akiwa Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Kisutu, alifuta dhamana ya Mbowe na Matiko kutokana na kukiuka masharti ya dhamana.

Wawili hao walikata rufaa katika Mahakama Kuu ya Tanzania kupinga uamuzi wa Kisutu kufuta dhamana yao ambapo rufani yao ilipangwa kwa Jaji Sam Rumanyika.

Hata hivyo, baada ya Mahakama Kuu chini ya Jaji Sam Rumanyika kusikiliza mapingamizi ya pande zote iliamua kuanza usikilizaji wa rufaa hiyo.

Upande wa serikali ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Paul Kadushi ulidai kuwa wamekata rufaa katika Mahakama ya Rufani kupinga maamuzi yaliyotolewa na Mahakama Kuu.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger