Thursday 13 February 2014

WASTARA ANYWA SUMU

...

IKIWA imetimia mwaka mmoja na miezi kadhaa tangu kifo cha mumewe, Juma Kilowoko ‘Sajuki’, staa wa filamu za Kibongo, Wastara Juma, Jumamosi iliyopita amedaiwa kufanya jaribio la kutaka kujiua kwa kunywa sumu, Risasi Mchanganyiko limefuatilia tukio hilo hatua kwa hatua.
Wastara akiwa kitandani baada ya kunywa sumu.
KABLA YA YOTE
Awali, staa huyo ambaye amepitia mitihani mingi, alitundika picha katika Mtandao wa Kijamii wa Instagram na kulalamika kuumwa tumbo.
Katika maelezo aliyoyaandika sambamba na picha hiyo, Wastara alimshukuru msanii mwenzake, Tamrina Poshi ‘Amanda’ kwa msaada aliompatia kwa kuwa alikuwa katika hali mbaya.
SUMU YATAJWA
Siku chache baada ya kuweka picha hiyo, Risasi Mchanganyiko lilipata kisa kizima kupitia kwa chanzo chake makini kuwa staa huyo alisumbuliwa na maumivu ya tumbo baada ya kuokolewa katika jaribio lake la kutaka kukatisha uhai wake kwa kunywa sumu.
SUMU ILIYOTUMIKA
Inadawa kuwa Wastara aliamua kunywa vidonge aina ya fragile kwa kuchanganya na pombe kwa lengo la kukatisha uhai wake ili kuondokana na manyanyaso anayoyapa kutoka kwa baadhi ya watu.
HAUSIGELI AOKOA JAHAZI
Inadaiwa kuwa wakati staa huyo akiwa chumbani kwa lengo la kujiua, msaidizi wa kazi ‘hausigeli’ aliingia chumbani humo kwa nia ya kufanya usafi ndipo alipomkuta Wastara akiwa analia huku amejiinamia.
“Hausigeli alijaribu kumuuliza sababu ya kilio chake lakini Wastara hakumjibu kitu, aliendelea kulia bila kikomo,” kilisema chanzo hicho.
Inadaiwa kuwa baada ya kutojibiwa kitu, hausigeli huyo alitoka na kumfuata Amanda ambaye alikuwa katika chumba kingine na kumweleza hali aliyomkuta nayo Wastara chumbani humo.
AMANDA APATWA NA MSHTUKO
Baada ya kuingia chumbani kwa Wastara, Amanda alipatwa na mshtuko mkubwa alipomkuta shoga’ke akiwa na baadhi ya vidonge mkononi na kumuuliza kisa cha kutaka kumeza vidonge hivyo.
“Wastara alimwongopea Amanda kwamba vidonge hivyo ni kwa ajili ya kujitibia mguu wake lakini Amanda hakukubaliana na maelezo hayo baada ya kuiona chupa ya bia iliyokuwa pembeni, kwa kuwa anafahamu Wastara siyo mnywaji wa pombe, ndipo  alipobaini lengo lake la kutaka kujiua,” chanzo kiliendelea kushusha data hizo.
Chanzo hicho kimesema kuwa Amanda alimpatia huduma ya kwanza shoga’ake huyo kwa kumnunulia maziwa na kumpeleka katika dispensari ya karibu ili kupata matibabu zaidi ya kuondoa sumu ya vidonge alivyovimeza.
SABABU ZA KUTAKA KUJIUA
Kwa mujibu wa chanzo kingine cha habari, Wastara alitaka kukatisha uhai wake kutokana na kuchoka kunyanyapaliwa, kudhalilishwa na kutongozwa mara kwa mara na wanaume, hali ambayo imekuwa ikimfedhehesha mbele ya jamii.
Chanzo hicho kimesema kwamba kabla ya tukio hilo, Wastara alikuwa akilalamika kudhalilishwa na watu anaowadai fedha zake ambao hawataki kumlipa haki yake.
“Kuna watu wengi ambao Wastara anawadai lakini wanamsumbua kwa kumuona ni mwanamke asiye na nguvu na wengine wanatumia mwanya huo kumtongoza, mwenyewe anaamini haya yote yanatokea kwa kuwa Sajuki hayupo,” kimetoboa chanzo hicho.
Habari zaidi zinadai kwamba hivi sasa Amanda anaendelea kumwekea ulinzi wa karibu Wastara ili asiweze kuchukua uamuzi mbaya wa kukatisha maisha yake.
Baada ya kuyapata madai hayo, mwandishi wetu alimpigia simu Wastara ili kupata undani wa tukio hilo lakini kwa muda mrefu simu yake ilikuwa ikiita bila ya kupokelewa.
Jumapili iliyopita Risasi Mchanganyiko lilimtafuta Amanda ili kuweza kupata ukweli  wa madai hayo na kumuuliza kama bado yupo kwa Wastara.
HUYU HAPA AMANDA
“Wastara amepatwa na matatizo, kwa kuwa ni rafiki yangu ambaye aliwahi kunisaidia siku za nyuma niko naye kumfariji…” alisema Amanda.
Risasi Mchanganyiko: Hivi amepatwa na matatizo gani?’
Amanda: Ya kawaida tu.
Risasi: Inadaiwa kuwa amekunywa sumu?
Amanda: Miye siyo msemaji wake, ila elewa kuwa amepatwa na matatizo, si umpigie kwenye simu yake uzungumze naye?
Risasi: Simu yake haipokelewi !  Kama uko naye  karibu nipe basi nizungumze naye?
Amanda: (kimya kidogo halafu)… Siko naye hapa.
Risasi Mchanganyiko: Wewe uko kwa Wastara tangu lini?
Amanda: Nina muda kiasi kwa kuwa kuna kazi tulikuwa tunataka kufanya.
Baada ya kuachana na Amanda, jioni ya Jumapili iliyopita Risasi Mchanganyiko lilimtafuta tena kupitia simu yake ya kiganjani Wastara na kumpata.
Wastara: Haloo
Risasi Mchanganyiko: Naongea na Wastara…?
Wastara: Eeeh ndiyo miye.
Risasi Mchanganyiko:  Pole na matatizo.
Wastara: Asante, lakini nazungumza na nani?”
Risasi Mchanganyiko: Mwandishi wa habari wa Global Publishers, nasikia umekunywa sumu kwa lengo la kutaka kujiua….
Hata hivyo, upande wa pili wa simu haukuwa tena hewani, mlio wa kukatika kwa simu hiyo ulisikika.
Jitihada za kumpigia simu Wastara ziliendelea lakini  hazikuweza kuzaa matunda kwani iliita bila ya kupokelewa na baada ya muda simu yake haikuwa ikipatikana tena.
TUJIKUMBUSHE
Mwaka 2008, Wastara kabla ya kufunga ndoa na Sajuki alipata ajali  ya pikipiki iliyosababisha kukatwa mguu na kuwekwa mguu wa bandia.
Mwaka 2009, Wastara na Sajuki walifunga ndoa ya kihistoria na kuwavutia watu wengi.
Lakini Januari 2, 2013, staa huyo alipata pigo la kufiwa na mumewe huyo baada ya kumuuguza kwa muda mrefu na kuzua simanzi kwa watu wengi.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger