Monday 30 November 2020

Serikali yatoa ufafanuzi wa hoja, ajira mpya za waalimu


 Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhandisi Joseph Nyamhanga, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimeti ya utumishi wa umma na utawala bora Dkt. Laurean Ndumbaro na Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo wametoa ufafanuzi juu ya hoja mbalimbali zilizojitokeza kwenye ajira mpya za waalimu.

Ufafanuzi huo umetolewa leo katika Ofisi ya Rais – TAMISEMI Jijini Dodoma  mara baada  kutokea hoja mbalimbali katika mitandao ya kijamii na vyombo vya habari  kuhusu ajira  mpya za walimu zilizotangazwa hivi karibuni.

Amesema ajira  hizo zilitangazwa  baada ya kukamilika kwa mchakato  wa uchambuzi  wa maombi  ya ajira  uliofanywa  na Ofisi ya Rais  TAMISEMI  kwa kushirikiana  na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi  wa umma  na utawala bora na  tume  ya utumishi wa walimu.

Mhandisi Nyamhanga  amesema hoja kubwa ilyojitokeza ni kwa jina la  Mwalimu mmoja kujitokeza katika kila ukurasa na kuonekana mara 196, badala ya mstari wa  maelezo ya Jedwali (Sub- titles) lakini shule aliyopangiwa ni moja, pamoja na jina hilo kujirudia  halikuchukua nafasi   ya mwombaji  yoyote  ya walimu waliotakiwa kuajiriwa au kuathiri  idadi ya waalimu  waliotakiwa kuajiriwa na  tayari marekebisho yamefanyika.

Mhandisi Nyamhanga amefafanua kuwa Shule binafsi kupangiwa mwalimu, Serikali imekuwa ikiingia ubia na baadhi ya Shule binafsi ambazo hupokea  wanafunzi wenye uhitaji maalum, shule hizo hupamgiwa  walimu na  kupewa ruzuku ya uendeshaji hivyo Shule ya Mwalimu Tutuba ilikuwa katika mchakato wa kuingia  ubia na serikali lakini haukukamilika, hivyo Serikali baada ya  kujiridhisha mwalimu aliyepangiwa katika shule hiyo amepangiwa  katika shule ya sekondari Malagarasi.

Kwa upande wa  wahitimu waliomaliza kidato cha nne mwaka 2017, 2018 na 2019 kupangiwa vituo vya kazi Mhandisi Nyamhanga ameeleza  waombaji wa ajira walitumia  mwaka wa kuhitimu chuo badala  ya mwaka wa kuhitimu  kidato cha nne ambapo waombaji 27 waliandika mwaka 2019, waombaji 27 waliandika mwaka 2019 na waombaji 13 waliandika mwaka 2017, Serikali ilihakiki vyeti vyao  na kubaini  kuwa waombaji hao walihitimu  kidato cha nne kati ya mwaka 2010 hadi 2014.

Kwa kuongezea amesema kuwa Serikali imefuata  utaratibu wa kuhakikisha Waombaji wote waliopata nafasi ya ajira wanazingatia  vigezo vilivyotolewa  katika tangazo la ajira ambapo lilifafanua kuwa mwombaji asizidi umri wa miaka 45.

Aidha Mhandisi Nyamhanga amewalekeza  Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakiki vyeti halisi  vya waliopata ajira na kujiridhisha  kabla ya kutoa barua  za ajira, na kusisitiza kuwa endapo  itabainika  udanganyifu au kasoro za vyeti vya kitaaluma  wahusika watachukuliwa hatua za kisheria.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimeti ya utumishi wa umma na utawala bora Dkt. Laurean Ndumbaro amesema  Serikali imetoa ajira za waalimu kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza  wametoa ajira 8000 na awamu ya pili watatoa kwa waalimu  5000  ili kupunguza malimbikizo ya mshahara kwa waalimu wapya.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo ameweka wazi kuwa Serikali itahakikisha waalimu wote waliomba ajira kwa masomo waliyoomba yanaendana na masomo wanayoyafundisha
.

Share:

STANDARD CHARTERED YAENDELEA KUBORESHA HUDUMA KWA WATEJA NCHINI

 

Mkurugenzi Mkuu wa benki ya Standard Chartered Tanzania, Sanjay Rughani akizungumza katika uzinduzi huo kulia ni  Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya bima ya Sanlam Tanzania Khamis Suleiman wakati walipofafanua mambo mbalimbali kuhusu huduma hiyo kwenye hoteli ya Hyatt Regency mwishoni mwa wiki.

Mkuu wa Mahusiano na Masoko wa Benki ya Standard Chartered nchini, Bi. Juanita Mramba (kushoto)  akizungumza jambo mara baada ya uzinduzi wa huduma za bima zitakazokuwa zikitolewa na benki hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa benki ya Standard Chartered Tanzania, Sanjay Rughani akipongeza na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya bima ya Sanlam Tanzania Khamis Suleiman mara baada ya kuzindua huduma za bima za benki hiyo kwa ushirikiano na Kampuni ya Bima ya Sanlam ya jijini Dar es salaam kwenye hoteli ya Hyatt Regency mwishoni mwa wiki iliyopita.

Mkuu wa Mahusiano na Masoko wa Benki ya Standard Chartered nchini, Bi. Juanita Mramba akifuatilia jambo wakati wa uzinduzi huo kulia ni  na Mkuu wa Wateja wa Kawaida wa Benki ya Standard Chartered nchini Tanzania Be.Ajmair Riaz.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Sanlam Tanzania Khamis Suleiman akielezea namna ushirikiano wa kampuni hiyo na benki ya Starndard Chatered zitakavyotolewa kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa benki ya Standard Chartered Tanzania, Sanjay Rughani.
Mkurugenzi Mkuu wa benki ya Standard Chartered Tanzania, Sanjay Rughani akipongeza na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya bima ya Sanlam Tanzania Khamis Suleiman  mara baada ya kuzindua huduma za bima za benki hiyo kwa ushirikiano na Kampuni ya Bima ya Sanlam ya jijini Dar es salaam kwenye hoteli ya Hyatt Regency mwishoni mwa wiki iliyopita.
Mkuu wa Mahusiano na Masoko wa Benki ya Standard Chartered nchini, Bi. Juanita Mramba  akizungumza jambo mara bmkatika uzinduzi wa huduma za bima zitakazokuwa zikitolewa na benki hiyo kulia ni Mkuu wa Wateja wa Kawaida Benki ya Starndard Chartered Bw Ajmair Riaz

Na Leandra Gabriel, Michuzi TV

KATIKA kuendelea kuwajali wateja katika kutoa huduma zao benki ya Standard Chartered kwa kushirikiana na kampuni ya Sanlam wamezindua huduma ya bima za bidhaa kwa wateja ili kuongeza thamani kwa wateja wao.

Uzinduzi huo wa bidhaa za bima uliokwenda kwa kauli mbiu ya "Tunavilinda vyenye Tija," umehusisha bidhaa mbalimbali ikiwemo nyumba na magari kwa ulinzi na usalama wa mali za wateja wao.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa uzinduzi huo leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Mkuu wa benki ya Standard Chartered Tanzania, Sanjay Rughani amesema kuwa suala la bima limekuwa na manufaa kwa sasa kutokana na ulinzi na usalama kupitia bima za bidhaa mbalimbali ikiwemo magari, nyumba na afya.

Amesema Tanzania ni sehemu salama na  Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Joseph Magufuli imekuwa ikishirikiana kwa karibu na sekta binafsi katika kujenga uchumi wa Taifa.

"Bima ina umuhimu mkubwa hasa katika ulinzi na usalama, watanzania lazima waelewe umuhimu wa  kukata bima katika mabenki kwa manufaa yao binafsi na mali zao."

Amesema kuwa huo ni ushirikiano wa kibiashara kwa maendeleo ya jamii na taifa la Tanzania na kuahidi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya tano kwa kuendeleza bima zikiwemo za sekta ya madini na afya.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Sanlam Tanzania Khamis Suleiman mabenki kuanza kuuza bima ni muhimu kwa kuwa wanafahamu ni nini mteja anacho na anachoweza kununua.

Amesema kuwa Kampuni hiyo iliyotimiza miaka 102 tangu kuanzishwa kwake ina malengo ya kufikia asilimia 50 ya watanzania wanaomiliki bima hadi kufikia mwaka 2030, na bima hizo zikiwa ni pamoja na bima za nyumba na magari.

Vilevile amesema, Sanlam imekuwa nchini kwa miaka 20, wakiwa katika nchi 44 zikiwemo nchi zote za Afrika Mashariki na kuahidi kuendelea kutoa huduma bora kwa ustawi wa jamii na taifa la Tanzania.

Amesema kuwa watanzania wachukue bidhaa za bima kutoka Standard Chartered kwa kuwa wanavilinda vyenye tija.

Share:

Waziri Mkuu Amaliza Mgogoro Wa Ardhi Kilosa


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemaliza mgogoro wa ardhi katika shamba la Chanzuru lenye ukubwa wa ekari 1,598 lililopo wilayani Kilosa, Morogoro kati ya Laizer Maumbi na Ameir Nahad kwa kuagiza likabidhiwe kwa Laizer ili aweze kuliendeleza kwa kulima mkonge.

Hata hivyo, Waziri Mkuu ameagiza eneo wanaloishi wananchi ndani ya shamba hilo kikiwemo kitongoji cha viwanja 60 na Chekeleni lihakikiwe na kupimwa ukubwa wake na kisha mkulima huyo akafidiwe eneo jingine na wananchi hao wasibugudhiwe.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatatu, Novemba 30, 2020) katika kikao chake na Makatibu Wakuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Ardhi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Viongozi wa mkoa wa Morogoro, wilaya ya Kilosa pamoja na Laizer. Kikao hicho kimefanyika kwenye ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma.

“Viongozi wa Serikali simamieni na mratibu vizuri ili wananchi wanaoishi katika vitongoji vilivyomo ndani ya shamba hilo wasibugudhiwe waachwe waendelee kuishi na eneo lililobaki lisilokuwa na mgogoro apewe Laizer. Sehemu hiyo iliyopungua Laizer atafutiwe shamba jingine ili kufidia.”

Amesema awali shamba hilo lilikuwa linamilikiwa na Sadruddin Rajabali ambaye alimuuzia Laizer ambaye aliamua kuachana na shughuli za ufugaji na kuanza kulima mkonge, na alipokuwa katika harakati za kubadilisha umiliki shamba hilo liliuzwa kwa mtu mwingine.

Waziri Mkuu amewataka watumishi wa sekta ya ardhi wilayani Kilosa wahakikishe suala hilo wanalisimamia vizuri ili haki itendeke kwa mkulima huyo kukabidhiwa shamba lake na watumishi waliohusika katika mgogoro huo wachukuliwe hatua.

Pia, Waziri Mkuu ameuagiza uongozi wa mkoa wa Morogoro uhakikishe inabainisha maeneo makubwa yote ambayo hayajaendelezwa na kutoa mapendekezo Serikalini.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Bw. Loatha Sanare ametumia fursa hiyo kumshukuru Waziri Mkuu kwa kumaliza mgogoro huo na kuahidi kwamba atasimamia utekelezaji wa maagizo na maelekezo yaliyotolewa.

Naye, Laizer ameishukuru Serikali kwa hatua iliyofikiwa ya yeye kukabidhiwa shamba hilo ambalo ndilo tegemeo lake kwa sasa, kwani aliuza mifugo yake yote na kununua shamba hilo ambalo amepanda mkonge
.

Share:

KATAMBI AANIKA MIKAKATI KULETA MAPINDUZI SHINYANGA...."SITACHEKA NA ANAYEKWAMISHA MAENDELEO"

Share:

Watu watatu wafa maji ziwa victoria.


Samirah Yusuph
Busega. Watu watatu wakazi wa wilaya ya Busega Mkoani Simiyu ambao ni wavuvi katika ziwa victoria wamekufa maji kwa kuzama maji baada ya mtumbwi waliokuwa wanautumia katika shughuri zao kupasauka.

Tukio hilo limetokea jana tarehe 29 mwezi wa 11 katika kata ya Kabita tarafa ya Busega wakati wavuvi hao wakiwa wanaendelea na shughuli zao za uvuvi kama kawaida.

Ambapo kamanda wa polisi mkoa wa Simiyu Richard Abwao aliwaambia waandishi wa habari kuwa kwa mujibu wa taarifa ya daktari aliyechunguza miili hiyo kifo chao kilitokana na kunywa maji mengi na kukosa hewa na kuonngeza kuwa:

"Waliokufa maji ni Mnaga Manyama miaka 28, Kulwa Juma miaka 15 na Bitulo Manyama wote wakazi wa Kabita wilayani Busega.

Aidha tukio hilo lilitokea baada ya mtumbwi waliokuwa wanatumia kuzama kufuatia mtumbwi huo kupasuka na kuanza kuingiza maji." Alisema Abwao.

Huku akitoa wito kwa wananchi wanaofanya shughuli za uvuvi kufanya ukaguzi na matengenezo hitajika ya vifaa vyao mara kwa mara.

Mwisho.


Share:

Video Mpya: Diamond Platnumz Ft. Koffie Olomide – Waah


Video Mpya: Diamond Platnumz Ft. Koffie Olomide – Waah


Share:

Somalia yamuita nyumbani balozi wake na kumfukuza wa Kenya

 Serikali ya Somalia imesema kuwa imemuita nyumbani balozi wake nchini Kenya Mohamud Ahmed Nur Tarzan, na kuishutumu nchi hiyo kwa kuingilia siasa za nchi yake.

Somalia pia imemtaka balozi wa Kenya nchini Somalia kufunga virago "kwa ajili ya majadiliano".

Somalia imeishutumu Kenya kwa kushinikiza serikali ya Jubbaland kukataa makubaliano ya uchaguzi yaliofikiwa Septemba 17, katika uchaguzi mkuu ujao utakaofanyika mwezi ujao.

"Serikali ya Somalia ilichukua uamuzi huo kulinda eneo lake la utawala baada ya kujitokeza kuwa Kenya inaingilia kimaksudi masuala ya Somalia eneo la Jubbaland," Mohamed Ali Nur, Waziri wa mambo ya nje wa Somalia amesema katika taarifa iliyotolewa.

"Serikali] ya Somalia imeonesha kusikitishwa kwake na serikali ya Kenya kwa kuingilia moja kwa moja masuala ya ndani ya siasa za Somalia hatua ambayo inaweza kuchangia ukosefu wa uthabiti, usalama na maendeleo kwa eneo zima,” taarifa hiyo imesema.

Kenya inaunga mkono utawala wa Ahmed Mohamed Islam maarufu kama "Madobe" huko Jubbaland, kwasababu ya maslahi yake ya kiusalama na kieneo.

-BBC



Share:

Taarifa Kwa Umma Kuhusu Kuapishwa Kwa Wabunge Wapya Wateule Wa Rais


Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai leo jioni atawaapisha wabunge wawili walioteuliwa Jumapili iliyopita na Rais Dkt. John Magufuli.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na kitengo cha mawasiliano cha Bunge hafla hiyo itafanyika saa 10 jioni kwenye viwanja vya Bunge, Dodoma.

Wabunge watakao apishwa na Spika Ndugai ni pamoja na Katibu wa Halmashauri kuu ya CCM- NEC, Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole na Riziki Lulida ambaye alikuwa mbunge wa viti maalum kwenye Bunge la 11 kwa tiketi ya CUF.


 


Share:

TUME YA TAIFA YA UMWAGILIAJI YAENDELEA NA MABORESHO YA MIUNDOMBINU YA UMWAGILIAJI


Kaimu MKurugrnzi Mkuu Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Bw. Daudi Kaali akizungumza mapema leo kuhusu shughuli za Ofisi hiyo pamoja na ukarabati wa Miundombinu ya Umwagiliaji unaoendela Mkoani Iringa.
Picha inaonesha mafundi wakiwa katika ofisi za Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Dodoma, wakijadili na kutengeneza moja ya  Mtambo Aina ya Cartapillar  D40 unaotumika katika shughuli za ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya Umwagiliaji
Bi Mary Mwangisa Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu toka Tume ya Taifa ya Umwagailiaji akizungumza kuhusiana na ushirikishwaji wa watumishi wa  kada mbalimbali katika mpango  wa elimu kwa wakulima unaondelea katika baadhi ya mikoa

Bw. Reginald Diamett Meneja Mfuko wa Maendeleo ya kilimo cha umwagiliaji toka Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, akiongea kuhusu shughuli za mfuko huo.


NA MWANDISHI WETU – DODOMA

Tume ya Taifa ya umwagiliaji inaendelea na shughuli za maboresho ya miondombinu inayopeleka maji katika skimu za kilimo cha umwagiliaji za Ruaha Mbuyuni, Namagozi na Mlenge Pawaga MkoaniI ringa,iliyoharibiwa na mafuriko katika msimu wa mvua zilizopita.

Hayo yameelezwa mapema leo na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiaji Bw. Daudi Kaali ambapo amesema katika skimu ya Ruaha Mbuyuni kazi ya kuchimba nakupanga mawe katika njia mpya yenye urefu wa mita 600 inakaribia kukamilika halikadhalika katika skimu za pawaga njia mpya yenye urefu wa mita 800 inachimbwa.

“Asimia (60%) yaukarabati wa miundombinu imekamilika katika skimu hizo, hivyo tunategemea mpaka mwishoni mwa wiki hii kazi itakuwa imekwisha kabisa.” Alisema Kaali

Akizungumzia Mradi wa Regrow unaosimamiwa na Wizara ya Maliasili na kutekelezwa na sekta husika Bw. Kaali alisema kuwa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ina kazi ya kuimarisha miundombinu ya umwagiliaji ili kuweza kuleta ufanisi mkubwa wa matumizi sahihi ya maji iliyaweze pia kutumika katika hifadhi za taifa za ukanda wa kusini pamoja na shughuli nyingine za miradi ya maendeleo.

“Tume ina jukumu la kujenga Mfereji mkubwa wa maji wenye urefu wa kilometa tatu, kazi ambayo imefikia hatua yakutafuta mkandarasi kwa ajili ya ujenzi huo katika skimu ya kilimo cha umwagiliaji ya madibila na unategemea kuanza mwezi ujao.” Alifafanua.

Akizungumza kuhusu Mfuko wa Maendeleo ya Kilimo cha Umwagiaji pamoja na mambo mengine unasimamia pia shughuli za maboresho ya miundombinu ya kilimo hicho.

 Meneja wa Mfuko huo kutoka Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Bw. Reginald Diamett alisema lengo lingine la  mfuko pia ni kujenga uelewa kwa wakulima na kuhamasisha tozo na makusanyo ya ada za hudu ma za umwagiliaji, jambo ambalo litaleta matarajio makubwa ya makusanyo katika sekta ya Umwagiliaji.

“Matarajio ni kwamba katika hekta zaidi ya laki sita zinazo mwagiliwa kwa sasa, katika msimu wa mavuno unaokuja, zaidi ya shilingi Bilioni hamsini na mbili (Bilioni 52)  zinaweza kukusanywa ambapo Asilimia 75 (75%)  itabakia kwa wakulima na asilimia ishirini na tano (25%)  ndiyo itakayochangiwa katika mfuko wa umwagiliaji kama ada ya huduma ya umwagiliji.” Alibanisha.

Akizungumza kuhusu ushiriki  wa kada mbalimbali za watumishi wa Tume katika kipengele cha  kutoa elimu kwa wakulima Mkurugenzi wa Utawala na Rasimaliwatu Bi. Mary Mwangisa amesema kuwa hili linachangia kuwajengea uwezo wafanyakazi wa ndani kuhusu shughuli za Tume kuwa na uelewa pamoja na kuboresha kada mbali mbali katika sekta ya umwagiliaji Jambo ambalo pia limepelekea kupanua sekta hiyo kwa kuwapeleka watalam wa umwagiliaji katika ngazi za mikoa na wilaya.

Kwalengo la  kusogeza huduma ya umwagiliaji karibu zaidi na wakulima ambao wengi zaidi wapo katika maeneo ya vijijini.

Share:

WADAU WASHAURI MBINU ZA KUINUA SEKTA YA KILIMO NCHINI


 
********************

NA MWANDISHI WETU

WADAU nchini wameshauri kurahisishwa kwa upatikanajii wa taarifa za utabiri wa hali ya hewa kulingana na eneo husika na kuongezwa kwa fungu la mikopo yenye masharti nafuu kwa wakulima wadogo, kwamba kufanya hivyo kutaongeza thamani katika sekta ya kilimo nchini.

Wamesema pamoja na mambo mengine pia ni muhimu kuwawezesha wakulima wadogo vitendea kazi ili kurahisisha shughuli zao, kadhalika wahusishwe katika safari za mafunzo na kujengewa uwezo mara kwa mara ili kukabiliana na mabadiliko ya teknolojia na masoko.

Ushauri huo ulitolewa jana na afisa miradi wa mtandao wa kitaifa wa asasi za kiraia zinazojihusisha na masuala ya mabadiliko ya tabianchi (FORUMCC) Sarah Ngoy, alipozungumza na Uhuru kuhusu utekelezaji wa mradi wao kwa kushirikiana na PACJA (Pan African Climate Justice Alliance) .

Alisema kilimo ni miongoni mwa sekta zinazokumbwa na athari za moja kwa moja za mabadiliko ya tabianchi ikiwemo kuwepo kwa mvua nyingi ama chache, hali ya ukame au mafuriko, mvua zisizotabirika, kuzuka kwa magonjwa ya mazao na wadudu waharibifu.

Sarah, alisema ili kukabiliana na changamoto zote zinazoikumba sekta ya kilimo na kufikiwa kwa adhma ya Malengo ya Maendeleo Endelevu, ni muhimu jukumu hilo lisiachwe kwa serikali pekee.

Alisisitiza ni muhimu kuwepo kwa jitihada za pamoja katika ngazi zote na ushirikishwaji mpana wa wadau wengine ikiwemo sekta binafsi, mashirika ya umma na asasi za kiraia.

Kwa mujibu wa Sarah, uzalishaji duni usio na tija, vikwazo na mienendo ya masoko ni miongoni mwa mambo yanayokwamisha mipango ya kupunguza umasikini na kuboresha lishe nchini kwani yanaathiri maamuzi ya wakulima katika uchaguzi wa aina ya mazao, kiwango cha uzalishaji na lishe.

Alisema ili kukabiliana na changamoto hizo na kufikia Malengo Endelevu ni muhimu kuboresha tija na kipato cha wakulima wadogo kwa kukuza upatikanaji sawa wa ardhi, teknolojia na kuboresha huduma za ugani.

“Nashauri kuongezwa kwa bajeti itakayochochea tafiti na matumizi ya teknolojia sahihi ili kusaidia uwepo wa pembejeo za kutosha na bora, kadhalika kutengenezwa kwa mfumo wa upelekaji taarifa muhimu na fursa kwa wakulima wadogo”.

Aliongeza, “Ni jukumu la wakulima kuanzisha ama kuimarisha shughuli mbadala za kujiingizia kipato nje na kilimo ikiwa ni njia ya kuongeza uhimili wa athari za mabadiliko ya tabianchi,” alisema.

Afisa miradi huyo, alisisitiza kuboreshwa kwa tafiti kulingana na mabadiliko yanayojitokeza, pia wakulima wapatiwe mrejesho wa tafiti hizo, huku sekta binafsi ikipaswa kuongeza ushiriki katika kuzalisha mbegu bora ili kusaidia wakulima kuzipata kwa gharama nafuu zaidi na kwa wakati.

“Kurahisisha upatikanaji wa huduma za kifedha na kuimarisha mnyororo wa thamani ni moja ya vitu vikubwa vinavyoweza kuchangia maendeleo endelevu kwa wakulima wadogo,” alisema.

Moses Mfinanga, ni Mkulima Mdogo katika Kijiji cha Makanya Wilayani Same, alisema hitaji lao ni kutengenezewa mazingira rafiki ya upatikanaji na umiliki wa teknolojia za kuhifadhia mazao kwa muda mrefu na zana za kuandalia mashamba.

Alitaja mengine kuwa ni vifungashio vyenye ujazo rafiki na vinavyoweza kukidhi mahitaji ya mkulima mdogo, ujuzi wa kuongeza thamani ya bidhaa zitokanazo na mazao ya kilimo, kutengenezwa kwa mfumo mzuri wa masoko ili waweze kuuza mazao kwa wakati na kupata faida kulingana na gharama za uzalishaji.

Miongoni mwa malengo ya maendeleo endelevu ya agenda 2030 (SDGs) ni kutokomeza umasikini wa aina zote kila mahali, kutokomeza njaa, kuwa na uhakika wa chakula, lishe bora na kukuza kilimo endelevu, kuchukua hatua za haraka kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi pamoja na athari zake.

Malengo haya yana kanuni za uendelevu wa kiuchumi, kijamii na mazingira; zinazoleta tija katika kushughulikia sababu kuu za umaskini na njaa kutokuacha mtu yeyote nyuma, kuhamisha ulimwengu kuingia katika uendelevu na uhimilivu, wenye utulivu na mabadiliko katika viwango vya maisha.

Malengo haya yanalenga mpaka ifikapo 2030 kuisaidia jamii kumiliki na kutumia teknolojia bora, kuitengenezea jamii mazingira wezeshi ya kupata kwa urahisi huduma za kifedha, kuhakikisha zana na pembejeo za kilimo zinapatika kwa urahisi, kwa wakati na gharama nafuu zaidi, kuboresha uvunaji na uhifadhi wa mazao, upatikanaji wa masoko yenye uhakika, kuendelea kuijengea jamii uwezo ili kuwaimarisha na kuboresha hali yao ya uchumi, kuwaondoa katika mazingira yaliyo duni na hatarishi, kukuza mifumo endelevu ya uzalishaji wa chakula inayoongeza tija na uzalishaji, inayodumisha mifumo ya ikolojia, kuboresha ardhi na udongo, kuimarisha uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na athari zake zitokanazo na ukame, mafuriko.

Licha ya kuwepo kwa malengo haya, wakulima wadogo ambao hutegemea kilimo kwa ajili ya ustawi wa maisha yao ya kila siku, na ambao ndio wenye mchango mkubwa katika pato la taifa; bado ni miongoni mwa kundi linaloathiriwa zaidi na mabadiliko ya tabianchi ambazo kwa kiasi kikubwa husababisha uzalishaji duni na mara nyingine kukosekana kabisa kwa mavuno.

Kiwango cha ukuaji wa uchumi kwa kiasi kikubwa hakiko sambamba na kiwango cha kupunguza umaskini na changamoto za lishe na usalama wa chakula nchini Tanzania. Katika sekta ya kilimo wakulima wakubwa ndio wanaonufaika zaidi ukilinganisha na wakulima wadogo.


 

Share:

Dk. Bashiru Awakaribisha CCM Wanawake Imara wa Upinzani

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Bashiru Ali, amesema chama chake kinawakaribisha wanasiasa wanawake ‘shoka’ wa upinzani watakao hitaji kujiunga na chama hicho.
Dk. Bashiru aliyasema hayo jana jijini hapa, wakati alipokuwa akifungua semina ya siku mbili kwa sekretarieti ya CCM na kamati za utekelezaji za jumuiya tatu za chama hicho.

Alisema katika uchaguzi mkuu 2020, wanawake kutoka vyama vya upinzani pamoja na wa CCM, wameonyesha ushindani mkubwa wa kisiasa hali iliyoonyesha walivyo na uwezo mkubwa wa uongozi.

“Mwaka huu tumeona nguvu ya kinamama wa upinzani na hata ndani ya CCM, katika kupambana kwenye nafasi za ubunge haijalishi wapo katika chama kikubwa au kidogo cha siasa kutokana na hali hii napenda kuwaambia kinamama wa vyama vya upinzani majembe wenye uwezo karibuni CCM,” alisema Dk. Bashiru.

Kadhalika, alisema kutokana na wanasiasa wanawake kuwagaragaza wagombea wa ubunge wanaume katika uchaguzi mkuu 2020, inamaanisha kuwa wana uwezo mkubwa ambao chama kinatakiwa kuutumia.

“Kama yule mbunge mwanamama wa CHADEMA aliyemshinda Kessy (Ally) kule Jimbo la Nkasi Kaskazini, pale kumtoa Kessy siyo jambo jepesi inatakiwa mtu mwenye uwezo, lakini pale Mbeya Mjini kwa Naibu Spika, hali hii inamaanisha kuwa kinamama wanastahili kupelekwa kwenye majimbo magumu ili kuyarejesha,” alisema Dk. Bashiru.

Aliziagiza jumuiya za CCM kufanya uchunguzi na tathmini ya kina kubaini mamluki na maadui waliokihujumu chama wakati wa uchaguzi mkuu, Oktoba 28, mwaka huu.

Dk. Bashiru alisema uchaguzi huo umeweka historia ya aina yake katika demokrasia za vyama vingi nchini ambao umeonyesha dhahiri maadui wa nchi na marafiki wa kweli kupitia mijadala na hoja mbalimbali zilizoibuka.

Alisema ushindi uliopatikana ni matokeo ya uchapakazi wa jumuiya zote kupitia mabalozi wa CCM zaidi ya 250,000 ambao ndio wenyeviti wa mashina ya chama.



Share:

Habari Zilizopo Katika Magazeti ya Leo Jumatatu Novemba 30



Share:

Sunday 29 November 2020

SIMBA SC YAWAZIMA WA NIGERIA KWAO, YAWACHAPA PLATEAU UNITED 1-0


SIMBA SC imetanguliza mguu mmoja mbele Raundi ya Pili ya Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya wenyeji, Plateau United jioni ya leo Uwanja wa Kimataifa wa Jos International, Jijini Jos nchini Nigeria.

Pongezi kwa mfungaji wa bao hilo pekee, kiungo Mzambia Clatous Chota Chama dakika ya 53 akimalizia kazi nzuri ya winga kutoka Msumbiji, Luis Jose Miquissone.

Sasa mabingwa wa Tanzania watakuwa na kazi nyepesi kwenye mchezo wa marudiano Jumapili ijayo Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
Wakifanikiwa kuitoa Plateau United, SImba SC watakutana na mshindi kati ya Costa do Sol ya Msumbiji na Platinum FC ya Zimbabwe kuwania kuingia Hatua ya 16 Bora inayochezwa kwa mtindo wa makundi.

Mechi ya kwanza jana, Platinum FC walishinda 2-1 ugenini Uwanja wa Taifa wa Zimpeto Jijini Maputo, Msumbiji na timu hizo zitarudiana Desemba 5 Uwanja wa Taifa wa Michezo wa Harare, Zimbabwe. 
Kikosi cha Plateau United kilikuwa; Adamu Abubakar, Ibrahim Babawo, Dennis Nya, Andrew Ikefe, Gabriel Wassa, Isah Ndala, Oche Ochewechi/Sunday Anthony, Sunday Adetunji, Abba Umar, Uche Onuasonya na Saheed Jibrin.
Simba SC; Aishi Manula, Shomari Kapombe, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Joash Onyango, Pascal Wawa, Jonas Mkude, Hassan Dilunga, Erasto Nyoni, John Bocco, Clatous Chama nba Luis Miquissone.

CHANZO- BINZUBEIRY
Share:

BAVICHA SHINYANGA WAMVAA MDEE NA WENZAKE, WATAKA WAKIOMBE RADHI CHAMA

 

Mwenyekiti wa Baraza la vijana (BAVICHA) Jimbo la Shinyanga mjini Samson Ng'wagi, katikati, akizungumza na waandishi wa habari, kushoto ni Mwenyekiti wa BAWACHA Jimbo la Shinyanga mjini Zena Gulam, na kulia ni Katibu mwenezi wa BAVICHA, Ibrahimu Isack.

Na Marco Maduhu Shinyanga

BARAZA la Vijana la Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema (BAVICHA) jimbo la Shinyanga mjini, limemtaka mwenyeki wa Baraza la wanawake Taifa (BAWACHA), Halima Mdee, pamoja na wenzake 18 wakiombe radhi chama hicho.

Mwenyekiti wa baraza hilo Samson Ngwa'gi, amebainisha hayo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye ofisi za Chadema Kanda ya Serengeti.

Amesema kitendo alichokifanya Halima Mdee pamoja na wenzake 18 kukisaliti chama, na kwenda bungeni Jijini Dodoma kuapishwa kuwa wabunge viti maalum ni kosa kubwa, na wamestahiri kuadhibiwa na kamati kuu.

"Baraza la vijana jimbo la Shinyanga mjini, tunaunga mkono maamuzi yaliyotolewa na kamati kuu ya kuwavua nyadhifa zao na uanachama Halima Mdee pamoja na wenzake 18," amesema Ng'wagi.

"Pia tun waomba wafuate maagizo ambayo yametolewa na Kamati kuu dhidi yao, ya kuomba radhi ama kukata rufaa, tunataka chama chetu tuendelee kuwa imara na tusigawanyike kwa maslahi binafsi," ameongeza.

Pia amesema ndani ya chama hicho hakuna mfumo dume ambao umedaiwa kuwepo na Halima Mdee, na kueleza kuwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu uliopita, chama hicho ndicho kilipitisha wagombea wengi wa nafasi ya ubunge ambao ni wanawake.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la wanawake jimbo la Shinyanga mjini (BAWACHA) Zena Gulam, ameeleza kusikitishwa na kitendo ambacho amekifanya Halima Mdee, akidai kuwa ni kiongozi ambaye alikuwa akimfuata nyayo zake, lakini kwa tukio hilo limemvunja moyo.

Novemba 24 Halima Mdee pamoja na wenzake 18, walikwenda Bungeni jijini Dodoma na kuapishwa kuwa wabunge viti maalum kupitia Chadema, lakini Novemba 27 wakafukuzwa na kamati kuu ya Chama hicho, wakidaiwa kukisaliti chama, kwa madai hawakuteuliwa kuwa wabunge wa viti hivyo ndani ya chama.
Mwenyekiti wa Baraza la vijana (BAVICHA) Jimbo la Shinyanga mjini Samson Ng'wagi, katikati, akizungumza na waandishi wa habari, kushoto ni Mwenyekiti wa (BAWACHA) Jimbo la Shinyanga mjini Zena Gulam, na kulia ni Katibu mwenezi wa BAVICHA, Ibrahimu Isack. Mwenyekiti wa (BAWACHA) Jimbo la Shinyanga mjini Zena Gulam, akizungumza kwenye kikao hicho.

Na Marco Maduhu- Shinyanga.
Share:

Jenerali Mabeyo Atunukiwa Nishani Maalum Ya Mlima Kilimanjaro


Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi akipokea Nishani Maalum ya juu ya Mlima Kilimanjaro kutoka kwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Iringa, Baba Askofu Mstaafu Elinaza Sendoro wakati wa Mahafali ya 23 ya Chuo hicho Mjini Iringa.
Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi akionesha Nishani Maalum ya juu ya Mlima Kilimanjaro aliyopokea kutoka kwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Iringa, Baba Askofu Mstaafu Elinaza Sendoro wakati wa Mahafali ya 23 ya Chuo hicho Mjini Iringa.


Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Brigedia Jenerali John Julius Mbungo akionesha Nishani Maalum ya juu ya Mlima Kilimanjaro aliyopokea kutoka kwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Iringa, Baba Askofu Mstaafu Elinaza Sendoro wakati wa Mahafali ya 23 ya Chuo hicho Mjini Iringa.

…………………………

Na Kanali Juma Nkangaa SIPE, Iringa

Chuo Kikuu cha Iringa (zamani Tumaini University) kimemtunukia Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Salvatory Venance Mabeyo Nishani Maalum ya Mlima Kilimanjaro (University of Iringa Miunt Kilimanjaro Award) ambayo hutolewa kwa Viongozi wa juu Serikalini ambao wametoa mchango wa kutukuka kwa Chuo au Tasnia ya Elimu kwa ujumla. Tukio hilo limefanyika wakati wa Mahafali ya 23 ya Chuo hicho yaliyofanyika katika “campus” ya Chuo Mjini Iringa tarehe 28 Nov 20.

Mwingine aliyetunukiwa Nishani hiyo Maalum ya juu wakati wa Mahafali hiyo ni Mkurugenzi wa TAKUKURU, Brigedia jenerali John Julius Mbungo. Kwa mara ya kwanza Nishani hiyo ilitunukiwa kwa aliyekuwa Rais (Mstaafu) wa Awamu ya Tatu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Benjamin William Mkapa na Mkewe Mama Anna Mkapa wakati wa Mahafali ya 22 ya Chuo hicho mwaka 2019.




Share:

Boko Haram Waua Wakulima 43 Nigeria


Amnesty International tawi la Nigeria inaripoti kuwa wakulima 43 wa Kijiji cha Maiduguri kilichopo Jimbo la Borno wameuawa na kundi la Boko Haram.

Wakulima 43 wa Jimbo la Borno, Nigeria wamechinjwa katika mashamba ya mpunga, Zabarmari na kikundi cha Boko Haram.

Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari ameonesha kusikitishwa na kitendo hicho, pia katika ukurasa wake wa tiwtter ameandika kulaani mauaji hayo.

Serikali ya Nigeria imefanya yote yanayowezekana kulinda nchi hiyo na watu wake, Rais amesema. Aidha shirika la kimataifa linalohusika na haki za binaadamu, Amnesty International lime laani kitend hicho.


Share:

Iran yaishtumu Israel kwa kuhusika katika mauaji ya mwanasayansi wake mkuu


Iran imeinyooshea kidole cha lawama Israel kuhusika katika mauaji ya Mohsen Fakhrizadeh, mwanasayansi mkuu wa nyuklia na mwanajeshi Iran, na kuahidi kulipiza kisasi kwa wale waliohusika na mauaji hayo.

Mohsen Fakhrizadeh aliuawa katika operesheni ya kushangaza Kaskazini mwa Tehran. Kwanza gari ndogo lililipuka barabarani, mbele ya gari lake, kabla ya kushambuliwa kwa risasi.

Waziri wa mambo ya nje wa Iran, Mohammad Javad Zarif, ameishutumu moja kwa moja Israel kwa kuhusika katika mauaji hayo.

Jina la Mohsen Fakhrizadeh lilitajwa mnamo mwezi Aprili 2018 na Waziri Mkuu wa Israeli katika hotuba yake kwenye televisheni. Benyamin Netanayhu alimshtumu kuwa mmoja wa maafisa wakuu wa mpango wa nyuklia wa Tehran. "Kumbukeni vizuri jina hili: Fakrizadeh", Bw. Netanyahu alisema wakati huo.

Mwanasayansi huyo mwandamizi pia alikuwa kwenye orodha ya vikwazo vya Umoja wa Mataifa dhidi ya Iran.


Share:

KIKAO CHA SEKRETARIETI YA HALMASHAURI KUU YA TAIFA YA CCM NA KAMATI ZA UTEKELEZAJI ZA JUMUIYA ZA CCM CAFANYIKA JIJINI DODOMA

KATIBU Mkuu CCM Dkt Bashiru Ally akizungumza wakati wa Kikao cha Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM na Kamati za Utekelezaji za Jumuiya za Chama - UVCCM, UWT NA WAZAZI ukumbi wa White House jijini Dodoma leo


Share:

WAZALISHAJI WA MAFUTA YA KULA FUATENI KANUNI ZA UZALISHAJI -BW.SUDI


Wazalishaji na wasindikaji wa Mafuta ya Kula Mkoani Kigoma wametakiwa kufuata kanuni za uzalishaji bora ili kuweza kukuza biashara ya Mafuta ya kula nchini.

Ameyasema hayo hivi karibuni Meneja Mafunzo na Utafiti wa TBS, Bw. Hamis Sudi katika kata ya Mkongoro wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa wasindikaji wa mafuta ya mawese yanayoendelea mkoani Kigoma. Mafunzo hayo yaliyofanyika katika Halmashauri ya wilaya ya Kigoma yalihudhuriwa na washiriki wapatao 200 kutoka kata za Mkongoro na Bitale.

Akizungumza katika mafunzo hayo Bw.Sudi amesema mzalishaji ili aweze kukuza biashara yake ya mafuta inamlazimu kufuata kanuni za uzalishaji bora ili kuweza kupata masoko ya uhakika.

"Mnapaswa kufuata kanuni za uzalishaji bora kwa maana hiyo mtakuwa mmeiongezea thamani bidhaa zenu na kuwawezesha kuzalisha kwa wingi na kupata masoko mengi". Amesema Bw.Sudi.

Aidha Bw.Sudi amewaomba wazalishaji kutumia fursa ya mafunzo wanayoyapata Wazalishaji hao kwa kuwauliza maswali maafisa wa Serikali ili kuweza kutatuliwa matatizo yanayowakabili katika uzalishaji wa mafuta ya kula.

Pamoja na hayo Bw.Sudi amesema iwapo wazalishaji na wasindikaji wa mafuta wakiyatumia vizuri mafunzo hayo wanayoyapata wataweza kukuza biashara yao ya mafuta.

Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger