Na mwandishi wetu, Mara
Askofu wa Jimbo Katoliki la Musoma Mkoani Mara Michael Msonganzila amesema Kanisa hilo haliruhusu kikundi chochote kuingia Kanisani kikiwa kimevalia sare za Chama cha siasa kwani Kanisa hilo halifungamani na upande wowote wa kisiasa isipokuwa lina waumini ambao ni wanasiasa na wanachama wa Vyama mbalimbali vya siasa nchini.
Askofu Msonganzila ametoa kauli hiyo mara baada ya Wanawake wanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema (BAWACHA) kuingia kwenye ibada ya Jumapili ya Machi 08, 2026 katika Kanisa Kuu la Jimbo la Musoma Mjini wakiwa wamevalia sare zao na baadae kutaka kufanya Mkutano na waandishi wa habari ndani ya eneo la Kanisa, suala ambalo lilisababisha mvutano kati yao na Jeshi la Polisi Mkoani Mara.
"Jumapili imefika hawa BAWACHA, bila sisi kufahamu kikanisa kama wamekuja pale Kanisani kwangu, wakaingia Kanisani na nadhani walibaini kuwa wanafuatiliwa na ninaambiwa hawakuingia getini na mavazi ya Kanisa, waliingia kawaida na wakaenda mafichoni ndani ya Kanisa wakavaa mavazi ya Chadema na baadae wakaingia kanisani na wameshiriki ibada."
"Kanisa tuna kanuni moja, haturuhusu mambo ya siasa yafanyike Kanisani lakini wakati mwingine tunaongozwa na busara na hekima ya hali ya juu na ndio maana aliyeongoza ibada hakusema ninyi mliovaa hivi ondokeni.
Alishangaa baada ya misa wametoka halafu ghafla wanataka kufanya mahojiano na waandishi wa habari, kitu ambacho baadhi ya walei waliona si kitu cha kawaida." Amekaririwa akisema Baba Askofu Msonganzila.
Wakati akizungumza na waandishi wa habari Jumanne Machi 10, 2026, Askofu Msonganzila amesema binafsi anaamini kuwa masuala au malalamiko ya kisiasa yalipaswa kutolewa ndani ya Ofisi ya Chadema tofauti na awali walivyokuwa wakitaka kufanyia Mkutano wao wa wanahabari ndani ya Viunga vya kanisa, akihoji kupatikana kwa Mwandishi huyo wa habari ikiwa aliandaliwa ama lah na ni kwanini aende kufanyia kazi zake ndani ya Kanisa Katoliki.
Akizungumzia kuhusu Kanisa kuruhusu Wanawake wa Chadema kufanya Kongamano lao katika Viwanja vya Matumaini kwa Vijana, uwanja unaomilikiwa na Kanisa hilo, Askofu Msonganzila amesema awali waliruhusu uwanja huo kutumika kwani hawakuwa wakifahamu kuhusu zuio la serikali kutokana na maamuzi ya Mahakama.












































