Thursday, 5 March 2026

NAIBU WAZIRI WA HABARI - WAANDISHI WA HABARI WASIO NA USAJILI JAB WACHUKULIWE HATUA



Na Mwandishi Wetu.

Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, ameagiza kuimarishwa kwa udhibiti wa taaluma ya uandishi wa habari nchini ili kulinda hadhi ya tasnia hiyo na kuongeza imani ya umma kwa vyombo vya habari.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana wakati wa ziara yake katika Ofisi za Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Naibu Waziri huyo alisisitiza kuwa ni wakati wa bodi hiyo kusimamia kikamilifu utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari kwa kuhakikisha wanaojihusisha na kazi za habari wanakuwa na ithibati halali.
Alieleza kuwa kukithiri kwa watu kufanya kazi za habari bila usajili rasmi kunachangia kushuka kwa viwango vya taaluma na kuathiri taswira ya sekta hiyo, hivyo akaitaka JAB kuongeza kasi ya usajili, utoaji wa vitambulisho vya uandishi (Press Cards) na ufuatiliaji wa mienendo ya vyombo vya habari hususan vya mtandaoni.

“Ni lazima kulinda heshima ya taaluma hii. Uandishi wa habari ni mhimili muhimu katika ujenzi wa taifa, hivyo usimamizi wake haupaswi kulegalega,” alisisitiza.
Katika taarifa yake kwa Naibu Waziri, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, alisema katika kipindi cha mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwa bodi hiyo, hatua kubwa zimepigwa ikiwemo uanzishaji wa mifumo ya kidijitali ya usajili wa waandishi, utoaji wa ithibati na vitambulisho rasmi, pamoja na utoaji wa elimu kwa umma kuhusu maadili ya taaluma.


Hata hivyo, alibainisha kuwa bodi hiyo inakabiliwa na changamoto kadhaa, zikiwemo uhitaji wa rasilimali zaidi na changamoto za udhibiti wa maudhui katika vyombo vya habari vya mtandaoni ambavyo vinaongezeka kwa kasi

Ziara hiyo imekuja katika kipindi ambacho sekta ya habari nchini inaendelea kukua sambamba na mabadiliko ya teknolojia ya mawasiliano, hali inayodai uwajibikaji mkubwa zaidi kwa wadau wote ili kuhakikisha taaluma ya uandishi wa habari inabaki kuwa chombo cha kuhabarisha kwa weledi, maadili na uwajibikaji
Share:

Wednesday, 4 March 2026

ARUSHA DC YATENGA JUMATANO KUSIKILIZA KERO, WANAWAKE WAHIMIZWA KUMILIKI ARDHI KIHALALI

 

Na Bora Mustafa, Arusha.

Uongozi wa Wilaya ya Arusha umetangaza kuanzisha rasmi siku maalum ya kushughulikia kero za wananchi katika ngazi ya kata na mitaa, hatua inayolenga kupunguza mlundikano wa malalamiko katika ofisi za wilaya. 

Akizungumza katika mkutano wa hadhara Machi 03,2026 , Mkuu wa Wilaya ya Arusha,mhe. Joseph Mkude, amesema kuwa kuanzia sasa kila siku ya Jumatano wananchi watapata fursa ya kuwasilisha na kusikilizwa kero zao katika maeneo yao.

Amesema utaratibu huo utasaidia kupunguza idadi ya wananchi wanaolazimika kufika ofisi za wilaya kufuatilia malalamiko yao, pamoja na kutoa nafasi kwa uongozi kushughulikia masuala mengine ya maendeleo.

 Pia amesema kuwa lengo ni kusogeza huduma karibu na wananchi ili wapate majibu kwa wakati.

Pamoja na hilo, Mkude amesema kuwa kila Ijumaa katika ngazi ya kata kutakuwa na ufuatiliaji wa kero zilizowasilishwa ili kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi. 

Pia amesema kuwa Jumatano ya mwisho wa mwezi itatengwa kwa ajili ya kusikiliza kero katika viwanja vya wilaya, hatua itakayowapa nafasi wananchi wengi zaidi kuwasilisha changamoto zao.

Katika hatua nyingine, amesema kuwa kliniki maalum ya ardhi inaendelea kufanyika wilayani humo kwa lengo la kutoa elimu na kurahisisha taratibu za umiliki wa ardhi, hususan kwa wanawake. Amesema mwanamke ana haki ya kisheria ya kumiliki ardhi kama ilivyo kwa mtu mwingine yeyote, pamoja na kwamba jamii bado inahitaji kupewa elimu zaidi kuhusu haki hiyo.

Hata hivyo, amesema changamoto kubwa inayochangia migogoro ya ardhi ni ukosefu wa uelewa wa taratibu sahihi za ununuzi na umiliki wa ardhi. Amesema wanasheria wa wilaya pamoja na maafisa ardhi wameelekezwa kuhakikisha wananchi wanapatiwa elimu ya kutosha kuhusu sheria na taratibu hizo.

Aidha, amesema wananchi wote wenye uhitaji wa kupimiwa maeneo yao wanatakiwa kufika katika ofisi za ardhi ili kupatiwa huduma za upimaji pamoja na kuandaliwa nyaraka muhimu za umiliki.

 Pia amewahimiza kujitokeza kwa wingi kutumia fursa hiyo ili kuepuka migogoro ya baadaye na kumiliki ardhi kihalali.

Share:

ALIYEKATA TAMAA, ASHANGAA KUPANDISHWA CHEO GHAFLA




Je, kuna kitu kinaumiza kama kufanya kazi kwa bidii halafu ukaonekana kama hauonekani? Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Martin, kijana wa miaka thelathini kutoka Westlands, ambaye alifanya kazi katika kampuni ya bima kwa zaidi ya miaka mitano bila kupandishwa cheo wala kuongezewa mshahara.

Share:

NAIBU WAZIRI WANU AAGIZA CHUO MZENGA KUTOA MAFUNZO YANAYOENDANA NA UCHUMI WA ENEO


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, ameutaka uongozi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Mzenga, kilichopo Kata ya Mzenga, Wilaya ya Kisarawe, kuhakikisha kinatoa mafunzo katika fani zinazoendana na shughuli za kiuchumi za eneo hilo.

Mhe. Wanu ametoa agizo hilo Machi 03, 2026, wilayani Kisarawe wakati wa ziara ya ufuatiliaji na ukaguzi wa miradi inayotekelezwa na Wizara katika wilaya hiyo.

Amewataka viongozi wa wilaya na wananchi wa eneo hilo kuona umuhimu wa mafunzo ya ujuzi na hivyo kuhamasisha vijana kujiunga na chuo hicho ili kupata ujuzi utakaowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.

Amesema chuo hicho, pamoja na vyuo vingine vya maendeleo ya wananchi, vinapaswa kuzingatia mahitaji halisi ya kiujuzi ili vijana waweze kujiunga kwa wingi.

“Mmesema hapa mnazalisha zao la korosho, ufuta na mihogo; kwa nini sasa msianzishe kozi ya kusindika mazao hayo? Hii itawamasisha vijana kujiunga na chuo kwa kuwa wanasoma kile wanachofanyia kazi,” amesema Mhe. Wanu.

Aidha, ameutaka uongozi wa chuo hicho kusimamia ipasavyo mifumo ya usimamizi wa watumishi ili kuimarisha uwajibikaji.

Akiwa wilayani humo, Mhe. Wanu pia amekagua ujenzi wa VETA Kisarawe na kusema kuwa Serikali inaendelea kujipanga kupata rasilimali fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa chuo hicho ili malengo ya kutoa ujuzi kwa wananchi yafikiwe.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Mhe. Petro Magoti, amemuhakikishia Naibu Waziri Wanu ushirikiano katika kusimamia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa, ikiwemo kuhakikisha huduma za umeme na maji zinafika katika eneo la chuo ili kurahisisha hatua inayofuata ya ujenzi.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO MACHI 4,2026




Magazeti
Share:

Tuesday, 3 March 2026

FCC KUADHIMISHA SIKU YA HAKI YA MLAJI KWA KUTOA ELIMU KWA UMMA



Na Emmanuel Mbatilo, Dar es Salaam

Tume ya Ushindani (FCC) imetangaza kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Haki ya Mlaji Duniani kwa kuendesha kampeni maalum ya utoaji elimu kwa walaji na wafanyabiashara ili kuongeza uelewa wa haki na wajibu wao katika soko.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Khadija Ngasongwa amesema maadhimisho hayo yanalenga kuwawezesha walaji kufanya maamuzi sahihi wanaponunua bidhaa au huduma, pamoja na kuwahamasisha kuchukua hatua pale wanapobaini ukiukwaji wa sheria.

Amesema elimu hiyo pia itawalenga wafanyabiashara kwa kuwajengea uelewa kuhusu wajibu wao wa kumlinda mlaji na kuzingatia matakwa ya sheria katika utoaji wa bidhaa na huduma.

Kwa mujibu wa FCC, kilele cha maadhimisho hayo kitafanyika Machi 31, 2026 katika Hoteli ya Johari Rotana, jijini Dar es Salaam, ambapo Mgeni Rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga.

Amesema katika maadhimisho ya mwaka huu, Tume hiyo imejikita kutoa elimu kupitia vipindi vya redio na televisheni, pamoja na majukwaa ya mitandao ya kijamii ili kuwafikia wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.

Aidha, FCC itaendesha kliniki za walaji katika mikoa ya Pwani, Dodoma, Musoma, Njombe na Tanga kwa lengo la kupokea na kushughulikia hoja, malalamiko na changamoto zinazowakabili walaji.

Sambamba na hilo, Machi 10, 2026 Tume hiyo itaendesha semina kwa wafanyabiashara na taasisi zinazotumia mikataba ya walaji (Standard Form Consumer Contracts) katika ofisi zake za Dar es Salaam, ili kuwajengea uelewa kuhusu umuhimu wa mikataba inayozingatia haki za mlaji.

Vilevile, Machi 11, 2026 kutafanyika semina kwa wadau wa sekta ya ujenzi wakiwemo wazalishaji wa nondo, bati, nyaya za umeme na rangi za majumbani, pamoja na vyama vya kibiashara na wadhibiti wa kisekta.

Mbali na semina hizo, FCC itatumia magari ya matangazo (road shows) kufikisha elimu kwa wananchi moja kwa moja katika maeneo yao.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu huyo amewahimiza wananchi wenye changamoto zozote zinazohusiana na bidhaa au huduma kufuatilia vipindi vya elimu vitakavyorushwa na vyombo vya habari, kuhudhuria kliniki za walaji na kutumia fursa hiyo kuwasilisha malalamiko yao kwa ajili ya kupatiwa ufafanuzi au hatua stahiki.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger