Thursday, 19 February 2026

SERIKALI YATOA FURSA KWA WASANII KAHAMA KUPITIA MIKOPO YA UTAMADUNI NA SANAA

 

Na Neema Nkumbi, Kahama

Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni tano kupitia Mfuko wa Utamaduni na Sanaa kwa ajili ya kuwakopesha wasanii nchini, hatua inayolenga kuinua vipaji, kukuza sekta ya ubunifu na kuwawezesha vijana kiuchumi.

Akizungumza katika mafunzo ya uelimishaji kuhusu namna ya kupata mikopo hiyo yaliyofanyika leo februari 18, 2026 katika ukumbi wa halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Afisa wa Mfuko wa Utamaduni na Sanaa, Jovita Godwin, amesema mfuko huo unatoa fursa kwa wasanii wa nyanja mbalimbali ikiwemo muziki, filamu, sanaa za maonyesho, fasihi na ufundi wa kazi za sanaa ili waweze kukuza kazi zao na kufikia malengo yao ya kisanaa na kibiashara.

Amesema serikali imekusudia kuona sekta ya sanaa inakuwa chanzo cha ajira na mapato kwa vijana wengi, hivyo amewahimiza wasanii wa Kahama kujitokeza kwa wingi na kuzingatia vigezo vilivyowekwa ili wanufaike na mikopo hiyo.

Kwa upande wake, Afisa Utamaduni wa Manispaa ya Kahama, Martha Kapela, amesema halmashauri imejipanga kuibua na kukuza vipaji kupitia matamasha, makongamano na ziara katika kata mbalimbali kwa lengo la kuwatambua wasanii na kuwaunganisha na fursa zinazotolewa na serikali.

Naye Meya wa Manispaa ya Kahama, Kaniki Mataluma, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira rafiki ya kiuchumi kwa vijana, akiwataka wasanii kutumia mikopo hiyo kama chachu ya maendeleo yao binafsi na ya taifa.

Baadhi ya wasanii waliohudhuria mafunzo hayo wameishukuru serikali kwa kuanzisha mfuko huo wakisema utawasaidia kupanua shughuli zao za kisanaa, huku wakiiomba serikali kuendelea kuboresha masharti ya mikopo ili kuwafikia wasanii wengi zaidi.


Share:

SHUWASA YATWAA TUZO YA MDAU SHUPAVU KANDA YA ZIWA


Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA) imeibuka mshindi wa Tuzo ya Mamlaka Bora inayosimamia upatikanaji wa huduma za maji safi na usafi wa mazingira katika Tuzo za Wadau Shupavu Kanda ya Ziwa, zilizofanyika Jumatatu tarehe 16 Februari 2026.

Tuzo hiyo ilipokelewa na Mkurugenzi Mtendaji wa SHUWASA, Mhandisi Yusuph Katopola, katika hafla iliyofanyika Hoteli ya  Golden Crest, jijini Mwanza.

Akizungumza wakati wa utambulisho, Mhandisi Katopola alisema SHUWASA imetekeleza kwa vitendo jitihada za kumtua mwanamke ndoo kichwani kwa kusogeza huduma karibu na wananchi na kuhakikisha upatikanaji wa majisafi kwa wastani wa saa 23 kila siku.

Aliongeza kuwa juhudi hizo, sambamba na usimamizi madhubuti wa usafi wa mazingira, zimeifanya Manispaa ya Shinyanga kuwa kinara wa usafi kitaifa kwa miaka mitatu mfululizo.

SHUWASA inatoa huduma katika eneo lote la Manispaa ya Shinyanga pamoja na miji midogo ya Didia, Tinde na Iselamagazi, iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. 

Mhandisi Katopola alibainisha kuwa mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mzuri kati ya Mamlaka na wadau wake, hususan wateja na wananchi, kwa kulipia ankara za maji kwa wakati na kutoa taarifa za uvujaji au uharibifu wa miundombinu.

Aidha Mhandisi Katopola alimshukuru Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Hamidu Aweso kwa maelekezo yake ya mara kwa mara katika kuhakikisha Mamlaka za Maji nchini zinatoa huduma bora za maji safi na usafi wa mazingira kwa wananchi katika maeneo yao ya huduma.

Tuzo hii ni chachu ya kuendelea kuboresha huduma na kudumisha viwango bora vya maji safi na usafi wa mazingira kwa maendeleo ya wananchi wa Tinde, Didia, Iselamagazi na Manispaa ya Shinyanga.  












Share:

DOTTO EMANUEL MANUMBU ASHINDA TUZO YA TOP 100 AFRICANS GLOBAL 2026 KAMA GLOBAL YOUNG MALE POLITICAL LEADER


Kiongozi kijana katika masuala ya Elimu, Habari na Siasa, Dotto Emanuel Manumbu, ametangazwa rasmi kuwa mmoja wa washindi wa tuzo za Top 100 Africans Global 2026, akitambuliwa katika kipengele cha Global Young Male Political Leader.

Tuzo hiyo imetolewa kwa kutambua mchango wake mkubwa katika uongozi na juhudi zake za kuleta maendeleo chanya kwa jamii pamoja na Taifa kwa ujumla. 

Kupitia nafasi mbalimbali za kiuongozi, Manumbu ameonyesha uwezo, ubunifu na dhamira ya dhati katika kutumikia nafasi yake na jamii kwa ujumla. 

Akizungumzia ushindi huo, Manumbu ameeleza kuwa ni heshima kubwa kwake na kwa Tanzania kwa ujumla, akisisitiza kuwa tuzo hiyo ni motisha ya kuendelea kufanya kazi kwa bidii, unyenyekevu, na uadilifu kwa manufaa ya jamii.

“Tuzo hii ya heshima namrejeshea Mungu, ambaye ndiye mgawaji wa riziki na neema zote. Nawashukuru kwa dhati wazazi wangu kwa malezi yao mema, viongozi wangu walionilea na kuniongoza katika utumishi wangu, Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Ukerewe kwa kuniamini na kunipa fursa ya kuwatumikia wananchi. Aidha, namshukuru DC Ngubiagai, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri (DED), pamoja na Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT) Tawi la Mwanza — kisima cha kuzalisha viongozi makini barani Afrika. Shukrani za pekee pia ziende kwa watumishi wenzangu wote wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe kwa ushirikiano na malezi yaliyonifikisha katika hatua hii,” amesema Manumbu.

Hafla rasmi ya ugawaji wa tuzo hizo inatarajiwa kufanyika tarehe 28 Februari 2026 katika ukumbi wa Morena Hotel jijini Dodoma, ambapo washindi kutoka mataifa mbalimbali barani Afrika watatunukiwa tuzo hizo rasmi.

Ushindi huo umeendelea kuiweka Tanzania katika ramani ya kimataifa kwa kuonyesha mchango wa vijana katika uongozi na maendeleo ya Bara la Afrika.




Share:

Wednesday, 18 February 2026

TUJIFUNZE KWA VIJANA WA MAKUNDUCHI WALIOGEUZA TAARABU ASILIA KUWA ‘MIGODI’ YA FEDHA MTANDAONI




Wakati baadhi ya vijana wakiendelea kulalamika kuhusu ukosefu wa ajira rasmi, kundi la vijana wanane kutoka Kijiji cha Makunduchi, Kusini Unguja, limeibuka na jibu la vitendo: Ubunifu ndio ajira ya kisasa.

Vijana hao, wakiongozwa na kijana mtanashati Ibrahim Suleiman, wameamua kutumia muziki wa Taarabu asilia—urithi ambao wengi waliuona kama kitu cha kizamani—na kuugeuza kuwa bidhaa adimu inayouzika kupitia mitandao ya kijamii. Wao badala ya kusubiri majukwaa makubwa, wameamua kutumia simu zao za mkononi kutengeneza maudhui yanayochanganya vichekesho na midundo ya jadi, jambo lililowafanya kuwa gumzo kote nchini na nje ya mipaka.

“Tumeamua kutumia kile tulichonacho mkononi. Hatukusubiri kuajiriwa, tuliamua kujiajiri kupitia kipaji chetu na utamaduni wetu,” anasema Ibrahim Suleiman, akisisitiza kuwa soko la sasa linataka kitu cha kipekee (Originality).

Ubunifu wa vijana hawa si tu unawaingizia kipato kupitia watazamaji wa mtandaoni (views) na matangazo, bali pia unalinda heshima ya muziki wa jadi wa Zanzibar usipotee.

Hii ni dhihirisho tosha kwa vijana wengine wa Kitanzania kuwa; uwe una ujuzi wa VETA, unalima parachichi, au unajua kuimba, nguvu ya kugeuza ujuzi kuwa utajiri iko kwenye ubunifu wako na matumizi sahihi ya teknolojia.

Huu ni ujumbe mzito kwa wale wanaopoteza muda kubeza juhudi za maendeleo: Wakati ninyi mkiandika vibaya mitandaoni, wenzenu wa Makunduchi wanatumia mitandao hiyo hiyo kuvuna fedha na kutangaza utamaduni wa nchi yao. Tanzania ya sasa inahitaji vijana wenye "misuli ya akili" kama hawa, wanaoona fursa pale wengine wanapoona matatizo.
Share:

Monday, 16 February 2026

MAVUNDE AZINDUA KISIMA CHA MAJI MSALATO, ASEMA NI UTEKELEZAJI WA AHADI YA 2025

Mbunge wa Jimbo la Mtumba Mkoani Dodoma, Mhe. Anthony Mavunde, ambaye pia ni Waziri wa Madini amezindua kisima cha maji katika Mtaa wa Msalato, Ubalozi wa Catherine Mwajoka, kwa ajili ya matumizi ya wananchi.

Uzinduzi huo ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 kuhusu kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama kwa wakazi wa eneo hilo.

Akizungumza na wananchi mara baada ya uzinduzi huo, Mheshimiwa Mavunde amewataka wakazi wa Msalato kulinda na kutunza miundombinu ya kisima hicho ili kiweze kudumu na kuwanufaisha kwa muda mrefu.

Amesisitiza umuhimu wa wananchi kushiriki kikamilifu katika kulinda miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao.

Aidha, ameahidi kuendelea kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii ya Msalato na Jimbo la Mtumba kwa ujumla, kwa kushirikiana na viongozi wengine wa Serikali.

Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Mavunde amewashukuru wananchi wa Msalato kwa imani kubwa waliyoionesha kwa kumpigia kura Samia Suluhu Hassan, yeye kama Mbunge pamoja na Diwani wao wakati wa Uchaguzi Mkuu wa 2025, akieleza kuwa ushindi huo unampa nguvu ya kuendelea kuwatumikia wananchi kwa bidii na uadilifu.

Share:

WALIOMHAMASISHA MTOTO KUVUTA SIGARA MIKONONI MWA POLISI

 


Kupitia mitandao ya kijamii kunasambazwa picha mjongeo akionekana mtoto mdogo wa kiume na zikisikika sauti zikimhamasisha kuvuta sigara Kitendo hicho ni kinyume cha sheria, kanuni na taratibu za kijamii na nchi. Jeshi la Polisi, limeanza uchunguzi na kuwafuatilia watu hao kwa hatua nyingine za kisheria.

 

Aidha, linatoa wito kwa yeyote anayewafahamu watu hao au mtoto huyo atusaidie kuwafikia na kuokoa afya ya mtoto huyo.


Pia, linatoa onyo kwa watu wenye tabia za kufanya vitendo vya kikatili na vya unyanyasaji kama hivyo na vinavyofanana na hivyo kwa watoto kwa lengo lolote lile ikiwepo msukumo wa kutafuta wafuasi (followers) kwa ajili ya mitandao yao ya kijamii kuziacha kwani halitasita kuwakamata kwa sababu ni kinyume cha sheria, kanuni na taratibu za nchi.

Share:

Sunday, 15 February 2026

Video Mpya : MASUMBUKO Ft. NELEMI MBASANDO - NARIDHIKA

 

Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI FEBRUARI 15,2026



Magazeti
 

   
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger