Saturday, 7 March 2026

WATAALAMU WALIOSOMA JAPAN WACHOCHEA MIRADI YA MAENDELEO NCHINI




Wataalamu wa Kitanzania waliopata mafunzo nchini Japan wameelezwa kuwa rasilimali muhimu katika kuharakisha maendeleo ya sekta mbalimbali kwa kutumia ujuzi na teknolojia walizojifunza nje ya nchi.

Akizungumza katika mkutano uliofanyika jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Msaidizi wa Ofisi ya Rais – Utumishi, Fadhili Mitimingi, amesema ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Japan International Cooperation Agency (JICA) umewezesha Watanzania wengi kupata mafunzo ya kitaalamu nje ya nchi.

Mtimingi ambaye alimwakilisha Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Utumishi katika Mkutano Mkuu wa Japan Alumni of Tanzania Association (JATA), amesema wahitimu wa mafunzo hayo wamekuwa wakirejea nchini na kuanzisha miradi mbalimbali ya maendeleo.

Amesema kupitia miradi hiyo, wataalamu hao wamekuwa wakisambaza maarifa waliyopata kwa wananchi wengine ili kusaidia matumizi ya mbinu bora na za kisasa katika uzalishaji.

“Hatua hiyo imechangia kuboresha maisha ya wananchi kwa kuwahamasisha kutumia teknolojia na mbinu mpya katika sekta muhimu za uchumi,” amesema Mitimingi.

Kwa upande wake, Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mikami Yoichi, amesema mkutano huo ulihusisha mawasilisho ya miradi kutoka kwa washiriki watatu waliowasilisha kazi walizozitekeleza baada ya kurejea nchini.



Naye Mwenyekiti wa JATA, Gregory Mlay, amesema umoja huo unawakutanisha wataalamu kutoka sekta mbalimbali zikiwemo kilimo, mifugo, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), biashara na afya ili kushirikiana katika miradi ya maendeleo.

Katika hatua Nyingine, Mwakilishi Mkazi wa JICA Tanzania, Ara Hitoshi, amesema lengo kuu la mafunzo hayo ni kuchangia maendeleo ya Tanzania ili kufanikisha hilo, washiriki wanaporudi kutoka kwenye mafunzo wanapaswa kuchukua hatua za kuwasaidia wengine kwa kutumia maarifa na uzoefu walioupata.



Mmoja wa wanufaika wa mafunzo hayo, Godfrey Christopher, amesema wamejifunza mbinu za kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi kupitia usindikaji na uhifadhi bora, hatua inayosaidia kupunguza upotevu wa mazao na kuongeza kipato cha wananchi.










Share:

Friday, 6 March 2026

RIDHIWANI KIKWETE: TUMIENI MFUNGO KULIOMBEA TAIFA AMANI




WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, amewataka wadau wa sekta ya bima na Watanzania kwa ujumla kutumia kipindi hiki cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kuliombea Taifa amani ili kuchochea kasi ya uwekezaji nchini.

Akizungumza jijini Dar es Salaam katika hafla ya kufuturisha wadau wa bima iliyoandaliwa na Shirika la Bima la Zanzibar (ZIC), Waziri Kikwete alisema kuwa amani ndiyo msingi mkuu unaoifanya Tanzania kuwa kitovu bora cha uwekezaji, na hivyo ni wajibu wa kila mwananchi kuitunza kupitia fursa za kiroho kama mfungo.

Alibainisha kuwa sekta ya bima ina mchango mkubwa katika kulinda uchumi wa kisasa, kwani inatoa uhakika wa usalama kwa wafanyabiashara na wawekezaji dhidi ya majanga mbalimbali.

Alisisitiza kuwa bila mfumo imara wa bima, ni vigumu kwa Taifa kupata ustawi endelevu wa kiuchumi unaohitajika na serikali.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Uendeshaji na Utumishi kutoka Wizara ya Fedha na Mipango (SMZ), Rajab Uweje, alieleza kuwa Shirika la ZIC limekuwa likitekeleza wajibu wake kama kiungo muhimu cha mfumo wa kifedha nchini. Aliongeza kuwa shirika hilo litaendelea kushirikiana na wadau kubuni huduma rafiki zitakazowafikia wananchi wengi zaidi na kusaidia kukuza uchumi wa pande zote mbili za Muungano.
Share:

ACHENI HEKAHEKA ZA MTANDAONI ZENYE NIA OVU, CHANGAMKIENI FURSA





WAKATI baadhi ya vijana wakipoteza muda mwingi mitandaoni kukuza chuki, kulalamika na kushusha hadhi ya nafsi zao, Serikali imewapigia kipyenga wasomi wa vyuo vikuu kutumia akili zao kubuni miradi itakayowaingizia "mkwanja" na kuwafanya mabilionea wa kesho.

Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano, Teknolojia ya Habari na Ubunifu, Fatma Mabrouk Khamis, wakati akifungua mafunzo ya siku tatu kwa wanafunzi wa vyuo vikuu kutoka Afrika Mashariki na India.

 Fatma ameweka wazi kuwa Serikali ya Zanzibar Awamu ya Nane imeweka kipaumbele cha kufa mtu kwenye sayansi na teknolojia, ikilenga kuwabadilisha wasomi kutoka kuwa wasaka ajira na kuwa wabunifu wa miradi inayozalisha mali.

“Wasomi wetu, wakati wa kushinda mitandaoni bila tija umepitwa na wakati. Huu ni wakati wa kuongeza ubunifu, kubuni miradi ya uzalishaji na kuingia kwenye ujasiriamali,” alisema Fatma huku akisisitiza kuwa idadi ya wahitimu ni kubwa kuliko nafasi za serikalini, hivyo njia pekee ya ushindi ni kujiajiri kupitia sekta binafsi.

Katika kile kinachoonekana kama "mchongo" wa uhakika, Joseph Evarest kutoka Shirika la UNDP kupitia programu ya FUNGUO, amebainisha kuwa wapo tayari kuviunganisha vyuo vikuu vya Tanzania na mataifa kama India na Uingereza. Mpango huu si wa nadharia tu, bali unalenga kubadilisha mawazo ya ubunifu ya wanafunzi kuwa biashara halisi zinazopata ufadhili wa fedha, ili kijana aweze kusimama mwenyewe kiuchumi badala ya kukata tamaa.

Baadhi ya wanafunzi waliochangamkia fursa hiyo, akiwemo Kelvin Hemu (UDSM) na Happy Weston, wamethibitisha kuwa tayari wapo kwenye mchakato wa kuibua mawazo yatakayowapa fedha za kuendeleza kazi zao. 

Huu ni ujumbe tosha kwa vijana: Badala ya kutumia bando lako kusononeka na hali ya maisha, tumia ubunifu wako kufungua milango ya maendeleo, kwani amani iliyopo nchini ndiyo uwanja mpana wa wewe kujiwekea akiba na kupata tija.



Share:

Thursday, 5 March 2026

NAIBU WAZIRI WA HABARI - WAANDISHI WA HABARI WASIO NA USAJILI JAB WACHUKULIWE HATUA



Na Mwandishi Wetu.

Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, ameagiza kuimarishwa kwa udhibiti wa taaluma ya uandishi wa habari nchini ili kulinda hadhi ya tasnia hiyo na kuongeza imani ya umma kwa vyombo vya habari.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana wakati wa ziara yake katika Ofisi za Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Naibu Waziri huyo alisisitiza kuwa ni wakati wa bodi hiyo kusimamia kikamilifu utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari kwa kuhakikisha wanaojihusisha na kazi za habari wanakuwa na ithibati halali.
Alieleza kuwa kukithiri kwa watu kufanya kazi za habari bila usajili rasmi kunachangia kushuka kwa viwango vya taaluma na kuathiri taswira ya sekta hiyo, hivyo akaitaka JAB kuongeza kasi ya usajili, utoaji wa vitambulisho vya uandishi (Press Cards) na ufuatiliaji wa mienendo ya vyombo vya habari hususan vya mtandaoni.

“Ni lazima kulinda heshima ya taaluma hii. Uandishi wa habari ni mhimili muhimu katika ujenzi wa taifa, hivyo usimamizi wake haupaswi kulegalega,” alisisitiza.
Katika taarifa yake kwa Naibu Waziri, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, alisema katika kipindi cha mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwa bodi hiyo, hatua kubwa zimepigwa ikiwemo uanzishaji wa mifumo ya kidijitali ya usajili wa waandishi, utoaji wa ithibati na vitambulisho rasmi, pamoja na utoaji wa elimu kwa umma kuhusu maadili ya taaluma.


Hata hivyo, alibainisha kuwa bodi hiyo inakabiliwa na changamoto kadhaa, zikiwemo uhitaji wa rasilimali zaidi na changamoto za udhibiti wa maudhui katika vyombo vya habari vya mtandaoni ambavyo vinaongezeka kwa kasi

Ziara hiyo imekuja katika kipindi ambacho sekta ya habari nchini inaendelea kukua sambamba na mabadiliko ya teknolojia ya mawasiliano, hali inayodai uwajibikaji mkubwa zaidi kwa wadau wote ili kuhakikisha taaluma ya uandishi wa habari inabaki kuwa chombo cha kuhabarisha kwa weledi, maadili na uwajibikaji
Share:

Wednesday, 4 March 2026

ARUSHA DC YATENGA JUMATANO KUSIKILIZA KERO, WANAWAKE WAHIMIZWA KUMILIKI ARDHI KIHALALI

 

Na Bora Mustafa, Arusha.

Uongozi wa Wilaya ya Arusha umetangaza kuanzisha rasmi siku maalum ya kushughulikia kero za wananchi katika ngazi ya kata na mitaa, hatua inayolenga kupunguza mlundikano wa malalamiko katika ofisi za wilaya. 

Akizungumza katika mkutano wa hadhara Machi 03,2026 , Mkuu wa Wilaya ya Arusha,mhe. Joseph Mkude, amesema kuwa kuanzia sasa kila siku ya Jumatano wananchi watapata fursa ya kuwasilisha na kusikilizwa kero zao katika maeneo yao.

Amesema utaratibu huo utasaidia kupunguza idadi ya wananchi wanaolazimika kufika ofisi za wilaya kufuatilia malalamiko yao, pamoja na kutoa nafasi kwa uongozi kushughulikia masuala mengine ya maendeleo.

 Pia amesema kuwa lengo ni kusogeza huduma karibu na wananchi ili wapate majibu kwa wakati.

Pamoja na hilo, Mkude amesema kuwa kila Ijumaa katika ngazi ya kata kutakuwa na ufuatiliaji wa kero zilizowasilishwa ili kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi. 

Pia amesema kuwa Jumatano ya mwisho wa mwezi itatengwa kwa ajili ya kusikiliza kero katika viwanja vya wilaya, hatua itakayowapa nafasi wananchi wengi zaidi kuwasilisha changamoto zao.

Katika hatua nyingine, amesema kuwa kliniki maalum ya ardhi inaendelea kufanyika wilayani humo kwa lengo la kutoa elimu na kurahisisha taratibu za umiliki wa ardhi, hususan kwa wanawake. Amesema mwanamke ana haki ya kisheria ya kumiliki ardhi kama ilivyo kwa mtu mwingine yeyote, pamoja na kwamba jamii bado inahitaji kupewa elimu zaidi kuhusu haki hiyo.

Hata hivyo, amesema changamoto kubwa inayochangia migogoro ya ardhi ni ukosefu wa uelewa wa taratibu sahihi za ununuzi na umiliki wa ardhi. Amesema wanasheria wa wilaya pamoja na maafisa ardhi wameelekezwa kuhakikisha wananchi wanapatiwa elimu ya kutosha kuhusu sheria na taratibu hizo.

Aidha, amesema wananchi wote wenye uhitaji wa kupimiwa maeneo yao wanatakiwa kufika katika ofisi za ardhi ili kupatiwa huduma za upimaji pamoja na kuandaliwa nyaraka muhimu za umiliki.

 Pia amewahimiza kujitokeza kwa wingi kutumia fursa hiyo ili kuepuka migogoro ya baadaye na kumiliki ardhi kihalali.

Share:

ALIYEKATA TAMAA, ASHANGAA KUPANDISHWA CHEO GHAFLA




Je, kuna kitu kinaumiza kama kufanya kazi kwa bidii halafu ukaonekana kama hauonekani? Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Martin, kijana wa miaka thelathini kutoka Westlands, ambaye alifanya kazi katika kampuni ya bima kwa zaidi ya miaka mitano bila kupandishwa cheo wala kuongezewa mshahara.

Share:

NAIBU WAZIRI WANU AAGIZA CHUO MZENGA KUTOA MAFUNZO YANAYOENDANA NA UCHUMI WA ENEO


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, ameutaka uongozi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Mzenga, kilichopo Kata ya Mzenga, Wilaya ya Kisarawe, kuhakikisha kinatoa mafunzo katika fani zinazoendana na shughuli za kiuchumi za eneo hilo.

Mhe. Wanu ametoa agizo hilo Machi 03, 2026, wilayani Kisarawe wakati wa ziara ya ufuatiliaji na ukaguzi wa miradi inayotekelezwa na Wizara katika wilaya hiyo.

Amewataka viongozi wa wilaya na wananchi wa eneo hilo kuona umuhimu wa mafunzo ya ujuzi na hivyo kuhamasisha vijana kujiunga na chuo hicho ili kupata ujuzi utakaowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.

Amesema chuo hicho, pamoja na vyuo vingine vya maendeleo ya wananchi, vinapaswa kuzingatia mahitaji halisi ya kiujuzi ili vijana waweze kujiunga kwa wingi.

“Mmesema hapa mnazalisha zao la korosho, ufuta na mihogo; kwa nini sasa msianzishe kozi ya kusindika mazao hayo? Hii itawamasisha vijana kujiunga na chuo kwa kuwa wanasoma kile wanachofanyia kazi,” amesema Mhe. Wanu.

Aidha, ameutaka uongozi wa chuo hicho kusimamia ipasavyo mifumo ya usimamizi wa watumishi ili kuimarisha uwajibikaji.

Akiwa wilayani humo, Mhe. Wanu pia amekagua ujenzi wa VETA Kisarawe na kusema kuwa Serikali inaendelea kujipanga kupata rasilimali fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa chuo hicho ili malengo ya kutoa ujuzi kwa wananchi yafikiwe.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Mhe. Petro Magoti, amemuhakikishia Naibu Waziri Wanu ushirikiano katika kusimamia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa, ikiwemo kuhakikisha huduma za umeme na maji zinafika katika eneo la chuo ili kurahisisha hatua inayofuata ya ujenzi.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO MACHI 4,2026




Magazeti
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger