Saturday, 7 February 2026

WAANDISHI WA HABARI WAHIMIZWA KUANDIKA HABARI ZA UCHUNGUZI KUCHOCHEA UWAJIBIKAJI NA MABORESHO YA SERA



Na Bora Mustafa,Arusha.

Waandishi wa habari za mazingira Kanda ya Kaskazini na Kati wametakiwa kuandika habari za uchunguzi zitakazochochea mabadiliko ya sera na sheria pamoja na kuhimiza uwajibikaji katika jamii.

Wito huo umetolewa wakati wa mafunzo ya waandishi wa habari za mazingira yaliyoandaliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) kwa kushirikiana na Taasisi ya Wanahabari Inayosaidia Jamii za Asili (MAIPAC), yaliyofanyika jijini Arusha.

Akitoa mada katika mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), Kenneth Simbaya, amesema kuwa katika uandishi wa kisasa, waandishi wanapaswa kujikita zaidi kwenye habari za uchunguzi badala ya kuandika habari za matukio ya kila siku.

Amesema kuwa lengo la uandishi wa habari linapaswa kuwa kuchochea mabadiliko ya sera na sheria, lakini pia kuibua uwajibikaji kwa wadau mbalimbali.

 “Mafunzo haya yameandaliwa ili waandishi muandike habari za uchunguzi za mazingira zitakazochochea mabadiliko ya kweli huku mkizingatia maadili ya taaluma,” amesema Simbaya.

Aidha, Mkurugenzi wa MAIPAC, Mussa Juma, amesema kuwa licha ya umuhimu wa kuandika habari za uchunguzi zinazobainisha changamoto katika jamii, waandishi wanapaswa kuzingatia maadili, mila na tamaduni za jamii wanazoziandikia.

Amesema waandishi wanapaswa kuandika habari zinazoonesha mapungufu katika sera, kanuni na sheria, lakini pia habari zinazoongeza ushiriki wa jamii katika kusoma, kuelewa na kushiriki katika kufanya maamuzi.

 “Habari zetu zinapaswa kuwa daraja kati ya jamii na watunga sera,” amesema Juma.

Akizungumzia uandishi wa habari kwa jamii za asili, Juma amewataka wanahabari kuheshimu mila na tamaduni zao, kuwaheshimu viongozi wa kimila na kutoandika habari bila kupata idhini ya mtu au jamii husika.

Hata hivyo, amesema kumekuwepo na tabia ya baadhi ya watu kwenda kwenye maeneo ya jamii za asili kama Wahadzabe, kupiga picha na kuandika habari bila ridhaa au uelewa wa jamii hizo, hali ambayo ni kinyume na misingi ya maadili ya uandishi wa habari.

 Pia ameongeza kuwa katika kuandika habari za jamii za asili ni muhimu kutumia lugha isiyodhalilisha, kuepuka maneno yanayokera, lakini pia kuwapa fursa jamii husika kujieleza na kusimulia changamoto zao kwa sauti yao wenyewe.

Kwa upande mwingine, Juma amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo waandishi kwenda kuchunguza athari za mabadiliko ya tabianchi kwa jamii za pembezoni, pamoja na migogoro ya ardhi ambayo imeanza kujitokeza katika maeneo mbalimbali.

Akitoa mada kuhusu ulinzi na usalama wa waandishi wa habari za mazingira, Wakili Paul Kisabo amewataka wanahabari kufanya tathmini za kiusalama kabla ya kwenda kufanya uchunguzi na kuchukua tahadhari stahiki ili kujilinda wao na vyanzo vyao vya habari.

Aidha, Wakili Kisabo ameanisha sheria mbalimbali za habari na mazingira ambazo waandishi wanapaswa kuzijua na kuzitumia ipasavyo katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Mafunzo hayo yamewakutanisha waandishi wa habari 35 kutoka mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Singida, Dodoma na Manyara, yakidhaminiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO).

 Mafunzo kama hayo yanatarajiwa pia kufanyika katika Kanda ya Ziwa, Kanda ya Mashariki, Pwani pamoja na Zanzibar.




















Share:

Thursday, 5 February 2026

Video Mpya : ELIZABETH MALIGANYA 'OMKAYA ELIZA' - BHALEMI

Msanii wa nyimbo za asili nchini Tanzania, Elizabeth Maliganya maarufu kama Omkaya Eliza, ameachia rasmi wimbo wake mpya unaoitwa “Bhalemi (Wakulima)”, wimbo unaobeba ujumbe mzito wa kuwatambua, kuwahimiza na kuwaenzi wakulima kama mhimili wa uchumi na maisha ya jamii.

Kupitia sauti yake ya kipekee na ala za asili, Omkaya Eliza amefanikisha kuwasilisha ujumbe unaogusa maisha ya wakulima.

“Bhalemi (Wakulima)” ni wimbo unaoendana na uhalisia wa maisha ya Watanzania wengi, hususan wale wanaojihusisha na kilimo, huku ukiwahimiza kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kuthamini mchango wao katika maendeleo ya Taifa.

Video ya wimbo huo imejaa taswira halisi za maisha ya wakulima na shughuli za kilimo, jambo linalozidi kuupa uzito na uhalisia ujumbe unaowasilishwa. 

🎥 Tazama video ya wimbo “Bhalemi (Wakulima)” hapa:
👉 https://youtu.be/QtrGgWa_MJw?list=RDQtrGgWa_MJw



Share:

RAIS SAMIA AMEWEKA MCHORO, SASA KAZI IMEBAKI KWA VIJANA WENYEWE



Bunge la 13 limefanya uchambuzi wa hotuba ya kihistoria ya Rais Samia Suluhu Hassan aliyoitoa Novemba 14, 2025. Safari hii, wabunge hawakujadili namba pekee, bali walijadili "uhalisia wa maono."

Kuna watu wanajilalamikia tu bila kufikiri kama nyumbu kwamba wabunge walikuwa wanafanya uchawa, sio suala la 'uchawa' au sifa zisizo na msingi, bali ni kutambua ukweli wa mwelekeo mpya ambao Rais ameuweka kwa ajili ya mustakabali wa asilimia 60 ya Watanzania—ambao ni vijana.

Katika kile kinachoonekana kuwa ni mageuzi makubwa ya kiuongozi, Rais Samia amevunja ukimya na kutekeleza ahadi yake ya kuunda Wizara kamili ya Vijana chini ya Ofisi ya Rais. Hatua hii imepokelewa kwa 'tano' na wabunge, wakibainisha kuwa kuiondoa idara ya vijana kutoka kwenye wizara zilizosongwa na majukumu mengi ni kumpa kijana sauti, mamlaka, na jukwaa rasmi la kushughulikia changamoto zake, hususan ukosefu wa ajira na mitaji.

Wabunge, akiwemo Dk. Emmanuel Nuwa wa Mbulu na Hawa Chakoma wa Viti Maalum, wamethibitisha bungeni kuwa maono haya yameshaanza kuzaa matunda kwa vitendo. Tayari mabilioni ya fedha yameshaanza kutiririka; Shilingi bilioni 10.5 zimepelekwa Benki ya NMB kwa ajili ya mikopo yenye riba nafuu ya asilimia saba, huku Rais akiahidi jumla ya Shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kuimarisha shughuli za kiuchumi za vijana na wanawake. Huu ni ujumbe mzito kwa vijana kuwa "muda wa kulalamika umekwisha, sasa ni wakati wa kuchangamkia fursa."

Mjadala huo bungeni umeweka wazi kuwa ufunguo wa maendeleo ya kijana hautategemea tena 'mikopo umiza' au majukwaa ya kisiasa yaliyopoteza mvuto, bali utategemea sera madhubuti na programu za kimkakati.

Wabunge wamehimiza kuwa wizara hii mpya iwe mhimili wa kuunganisha vijana na sekta za kilimo, madini, na teknolojia ya habari.

Mbunge Agnesta Lambert amesisitiza kuwa hotuba ya Rais imekidhi matakwa ya wananchi wote bila kujali itikadi, akiamini kuwa utawala bora na uwajibikaji ndio utakaofanya matamanio ya Rais yatekelezwe mitaani.

Bunge pia limefanya vyema kwa kutoa rai kwa watendaji na viongozi waliopewa dhamana kuhakikisha "fyekeo" la Rais linafanya kazi kwa wale watakaochelewesha au kukwamisha fedha hizi kuwafikia walengwa.

Kwa uundwaji wa Baraza la Vijana na uimarishaji wa mifuko ya maendeleo, Tanzania inajipanga kuhakikisha nguvu kazi yake kubwa haipotei kwanye vurugu, bali inageuzwa kuwa injini ya uchumi kuelekea Dira ya 2050.

Ni dhahiri kuwa Rais Samia ameweka mchoro, na sasa kazi imebaki kwa vijana wenyewe "kukaa mkao wa kula" na kutumia zana zao, ikiwemo teknolojia, kutafuta na kutumia fursa hizi adimu.
Share:

SPIKA ZUNGU ASEMA HAKUNA MBUNGE ALIYEPEWA KIBALI KUHOJIWA NA TAKUKURU



Na mwandishi wetu, Dodoma

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mussa Azzan Zungu, amesema hadi sasa Ofisi ya Spika haijatoa kibali chochote kwa mbunge yeyote kuhojiwa na TAKUKURU. 

Hii ni kufuatia taarifa za vyombo vya habari zikidai baadhi ya wabunge wameitwa kuhojiwa kuhusiana na madai waliyoyatoa bungeni jambo ambalo Spika amekanusha.

Spika amesisitiza kuwa Bunge linaongozwa na Katiba na Kanuni zake, zinazolinda uhuru wa wabunge kutoa maoni bila shinikizo, hofu au kikwazo chochote. Uhuru huu umeainishwa na Ibara ya 100 ya Katiba, ikiwapa wabunge kinga ya kisheria.

Ameongeza kuwa endapo mbunge amekiuka Kanuni, mamlaka ya kuchukua hatua ipo ndani ya Bunge lenyewe kupitia Kiti cha Spika. Bunge litaendelea kulinda uhuru wa wabunge kuchangia masuala ya kitaifa kwa uwazi na ujasiri.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI FEBRUARI 5,2026

Magazeti

 


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger