Monday, 16 March 2026

WANANCHI WA MOHORO WAMSHUKURU RAIS SAMIA


-Mhe. Mchengerwa afuturisha, Mohoro, Chumbi,Mbwala na Shela

-Maelfu ya wananchi washiriki futari, wamsifu Mchengerwa

Na Yohana Kidaga- Mohoro

Wananchi wa kata nne za Muhoro, Chumbi, Mbwala na Shela katika wilayani Rufiji wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha katika miradi mbalimbali ya maendeleo katika Wilaya hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti kwenye tukio maalum la kuwafuturisha wananchi wa kata hizo Machi 15, 2026 lililofanywa Mbunge wa Rufiji na Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa ambapo takribani wananchi elfu kumi walishiriki kutoka katika kata hizo wamesema katika kipindi hiki chini ya Rais Samia miradi mingi ya maendeleo imetekelezwa, hali ambayo imeleta mabadiliko makubwa.

“Ukweli lazima usemwe, ni katika kipindi hiki ambapo tunaishukuru Serikali yetu, kwa uongozi thabiti wa Mheshimiwa Rais ambapo ameweza kutusimamia na kupitia mbunge wetu ambaye amekuwa na moyo wa kizalendo na upendo na sisi watu wake, miradi kwenye sekta zote imeendelea kutekelezwa”. Alisema Abdul Bakari Chobo ambaye ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji na Diwani wa Kata ya Mohoro.

Akizungumzia suala la ujenzi wa barabara katika jimbo hili Mhe. Chobo alifafanua kwamba tayari Serikali imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara yenye mtandao wa wa zaidi ya kilomita 20 kwa kiwango cha lami na amesisitiza kuwa kata zote zinakwenda kuunganishwa kwa barabara.

Aidha, amesema katika kipindi cha sasa tayari Serikali imeshaleta takribani shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kukarabati hospitali ya Wialaya ya Utete, Kituo cha Afya cha Mkongo,na zahanati kadhaa katika wilaya ya Rufiji.

Kabla ya kuanza kufuturisha, Mhe. Mchengerwa pia alimshukuru Mhe. Rais kwa niaba ya wanachi kwa kuwaletea wananchi maendeleo ambapo alisema Serikali imefanya maboresho makubwa siyo tu katika eneo la miundominu ya barabara bali ujenzi wa madaraja makubwa yanayoiunganisha Rufiji na mikoa mbalimbali, ujenzi wa Shule za Sekondari na Msingi, Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali na kuleta watumishi wa kutosha.

Alitumia fursa hiyo kuwashukuru wananchi kwa kujitokeza kwa wingi kwenye matukio ya kufuturu yanayoendelea katika jimbo lake huku akifafanua kuwa mwitikio huo ni ishara ya upendo mkubwa walionao kwake na Serikali yao, kwani kama wasingekuwa na imani na yeye hata kama angewaandalia futari wasingeweza kushiriki.

“Natambua watu wameacha kazi zao kwa ajili ya kuja kushiriki kwenye futari hii, huu ni upendo mkubwa sana kwangu binafsi na Serikali yao, pia wamenithibitishia maamuzi waliyoyafanya wakati wa kupiga kura za ubunge na urais ambapo walinichagua kwa kura za kishindo mimi na chama changu.” Jambo hili linanifanya niwe na deni kubwa kwao la kuendelea kuwatumikia, naahidi kufanya hivyo kwa moyo wangu wote” alifafanua Mhe. Mchengerwa.
Akizungumzia msingi wa uongozi bora Mhe. Mchengerwa alisitiza viongozi kushuka chini kwa wananchi na kuwatumikia wananchi kwa katika kipindi chote ili kuwaletea maendeleo ya kweli badala ya kusubiri vipindi vya kampeni pekee.

Ni vizuri kama kiongozi mwenye dhamana kushuka chini kushirikiana na wananchi katika ambapo amesema katika kipindi chake amekuwa nyakati zote na wananchi ili kuhakikisha ahadi ambazo amezitoa kwa kushirikiana na wananchi wanakwenda kuzitekeleza kwa manufaa na maendeleo ya wananchi.

Ikiwa ni mwendelezo wa mwaka wanne mfululizo wa kuwafuturisha wananchi wa jimbo la Rufiji leo Machi 16, 2026 Mhe. Mchengerwa anakusudia kuendelea kufuturisha katika kata ya Mwaseni baada ya jana kufuturisha kata nne za Muhoro, Chumbi,Mbwala na Shela katika eneo la Muhoro ,kabla ya juzi kufuturisha katika eneo la Utete.


Katika hatua nyingine, mbali na kuwafuturisha wananchi hao,Mhe. Mchengerwa alipata fursa ya kuwasikiliza wananchi mmoja mmoja na kutoa ufumbuzi wa changamoto zao ambapo wananchi waliopata fursa walipongeza hatua hiyo.

“Tunampongeza mbunge wetu kwa kutuandalia futari katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani na pia Kwaresma kwani inatuunganisha sisi sote, hii ni alama ya upendo na kwa kweli tunapata fursa ya kukutana na kiongozi wetu na kujadiliana naye mambo mbalimbali na anatutatulia hapo hapo huu ndiyo uongozi”. Alisema Ayubu Issa Mkazi wa Mohoro.

Share:

Sunday, 15 March 2026

KAMATI YA BUNGE YA SHERIA YATEMBELEA KONGANI YA BUZWAGI NA KUPONGEZA BARRICK KWA KUFUNGA MGODI KITAALAMU


Wabunge kutoka Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakitembelea maeneo mbalimbali walipofanya ziara ya kikazi ya kujionea maendeleo ya Kongani Maalum la Uwekezaji (BSEZ) ya Buzwagi ambayo ipo ndani ya mgodi wa Barrick Buzwagi ambao upo katika hatua za mwisho za ufungaji.
Wabunge kutoka Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakitembelea maeneo mbalimbali walipofanya ziara ya kikazi ya kujionea maendeleo ya Kongani Maalum la Uwekezaji (BSEZ) ya Buzwagi ambayo ipo ndani ya mgodi wa Barrick Buzwagi ambao upo katika hatua za mwisho za ufungaji.
Wabunge kutoka Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakitembelea maeneo mbalimbali walipofanya ziara ya kikazi ya kujionea maendeleo ya Kongani Maalum la Uwekezaji (BSEZ) ya Buzwagi ambayo ipo ndani ya mgodi wa Barrick Buzwagi ambao upo katika hatua za mwisho za ufungaji.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Utawala , Katiba na Sheria ya Bunge , Dkt Damas Ndumbaro akizugumza na wajumbe wa kamati hiyo , kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya kahama , viongozi wa halmashauri ya Kahama na wafanyakazi na menejimenti ya Barrick Buzwagi wakati wa ziara hiyo ya siku moja ya kutembelea kongani maalum la uwekezaji ya Barrick Buzwagi.
Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji , Dkt. Pius Chaya akiongea na Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria walipofanya ziara ya kikazi ya kujionea maendeleo ya Kongani Maalum la Uwekezaji (BSEZ) ya Buzwagi ambayo ipo ndani ya mgodi wa Barrick Buzwagi ambao upo katika hatua za mwisho za ufungaji.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi , Mhandisi Zonnastraal Mumbi akizungumza mbele ya Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria walipofanya ziara ya kikazi ya kujionea maendeleo ya Kongani Maalum la Uwekezaji (BSEZ) ambalo lipo ndani ya mgodi wa Barrick Buzwagi ambao upo katika hatua za mwisho za ufungaji.
Mkurugenzi Mkuu wa TISEZA,Gilead Teri akizungumza mbele ya Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria walipofanya ziara ya kikazi ya kujionea maendeleo ya Kongani Maalum la Uwekezaji (BSEZ) ambalo lipo ndani ya mgodi wa Barrick Buzwagi ambao upo katika hatua za mwisho za ufungaji.

***
# Kamati ya Bunge ya Sheria yaitaka Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum (TISEZA) kuisimamia Kongani hiyo badala ya Halmashauri ya Manispaa ya Kahama.

Kamati ya kudumu ya Bunge Utawala , Katiba na sheria imeelekeza serikali kupitia Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji kuikabidhi rasmi kwa ajili ya kusimamiwa Kongani Maalum ya Uwekezaji ya Buzwagi (BSEZ) kwa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum Tanzania (TESIZA) ili kuhakikisha inaendelea kuvutia wawekezaji na kutengeneza mazingira mazuri ya biashara ili kuleta matokeo Chanya pia imepongeza Barrick kwa kufunga mgodi kitaalamu .


Akizungumza kwenye majumuisho ya ziara ya kamati hiyo , Mwenyekiti wake , Dkt. Damas Ndumbaro (MB) amesema kamati imeonelea kwamba ni muhimu kwa mamlaka ya uwekezaji kusimamia kongani hiyo badala ya kuikabidhi kwa halmashauri ya Manispaa ya Kahama.

“Tunachukua fursa hii ya kipekee kwanza kwa kuwashuruku uongozi wa Barrick kwa kazi nzuri ya ufungaji wa mgodi huu wa Buzwagi kitaalamu na kuweka mazingira mazuri ya uanzishwaji wa kongani maalum ya biashara na uwekezaji ni jambo muhimu kwa maslahi ya nchini yetu,”

“Tumetembelea eneo hili mahususi kwa ajili ya uwekezaji tumeona wenyewe kwamba maji, miundombinu ya barabara , umeme vipo ambavyo ni kichochea cha kuvuta uwekezaji wa ndani na wa nje,” amesema Dkt. Ndumbaro.

Ameongeza kwamba kwenye mchakato wa kuvutia wawekezaji nchini moja ya changamoto ni sheria ya fedha ambayo kwa namna fulani si rafiki sana kwa kuvutia wawekezaji tutaendelea na kuishauri serikali na mapendekezo yetu ni baadhi ya vifungu vya sheria ya fedha viondolewe ili kufungua milango zaidi ya uwekezaji.

Dkt. Ndumbaro amesisitiza kuwa ni muhimu kwa Halmashauri ya Kahama kuendelea na shughuli zingine za wananchi na kuiachia Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) kwenye uendelezaji wa kongani hii na kuvutia wawekezaji nchini.

Dkt. Ndumbaro amesema Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) inaelekeza kila wilaya kuwa na kongani ya viwanda ili kuongeza ajira kwa wananchi na kukuza uchumi wa maeneo husika. 

Ameitaka pia (TISEZA) kuwa karibu na eneo hilo na kulitangaza zaidi ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi ndani ya nchini na nje.

“Kupitia Ilani ya uchaguzi ya chama cha mapinduzi ni lazima serikali iendelee kuutia wawekezaji wa ndani na wa nje ili kupunguza tatizo la ajira na kupanua wigo wa mapato ya serikali nchini,” ameongeza Dkt. Ndumbaro.

Amesema kongani hiyo ni ya kipekee ikilinganishwa na maeneo mengine ya uwekezaji kwa kuwa ina miundombinu muhimu ikiwemo umeme wa uhakika, maji ya kutosha, barabara pamoja na uwanja wa ndege unaorahisisha usafiri wa wawekezaji.

“Tunataka TISEZA wawe karibu na kongani hii ili wawekezaji watakapopatikana wasikumbane na changamoto za kiutaratibu katika hatua za kuanzisha uwekezaji wao,” amesema Dkt. Ndumbaro.

Kwa upande wake , Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji , Dktt. Pius Chaya amesema kuwa, serikali imeyachukua mapendekezo ya kamati ya kudumu ya Bunge kuhusu mamlaka ya uwekezaji kusimamia kongani hiyo badala ya halmashauri ya kahama kwa ajili ya kuongeza ufanisi.

Amefafanua kwamba serikali ya awamu ya sita kwa kushirikiana na sekta binafsi , kama vile Barrick itaendelea na mipango hiyo ambayo ipo kwenye dira ya taifa ya maendeleo 2020-2050 ili kuhakikisha tunaendelea kupunguza umasikini na kukuza uchumi wa nchini.

“Kupitia mpango wa ushirikiano kati ya sekta binafsi na serikali (PPP) tunataka mchango wa sekta binafsi kwenye pato la taifa lifike 70% ili kuendelea kufungua milango zaidi ya ushirikishwaji wa sekta hiyo muhimu kwenye nguzo za uchumi wa nchini yetu,” ameongeza Dkt. Chaya

Amesema serikali inaipongeza Barrick ambayo ina ubia nayo kupitia kampuni ya Twiga Minerals kwa kuendelea kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo na kuahidi kwamba ushirikiano huo utaendelea ili kufungua fursa zaidi na kupanua mazingira wezeshi ya uwekezaji hapa nchini.

Naye, Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Buzwagi Zonnastraal Mumbi amesema Barrick itaendelea kushirikiana na serikali katika kuvutia wawekezaji kwa kutengeneza mazingira mazuri ya uwekezaji na kuzingatia viwango vya kimataifa vya ufungaji wa mgodi na weledi.

“Mgodi wa Barrick Buzwagi ulianza mchakato wa ufungaji 2021 kwa kushirikiana na Tume ya Kitaifa ya Ufungaji na baadaye tukaanza rasmi safari ya kubadilisha eneo hili ilikuwa sehemu ya uwekezaji wenye tija baada ya kujiridhisha pamoja na serikali kwamba miundombinu ya hapa ni bora na ya kuvutia uwekezaji,” amesema.

Mhandisi  Magige Marwa kutoka Mamlaka ya Maji Safi wa Mazingira Kahama (KUWASA) akizungumza na kamati hiyo ilipotembelea mradi wa ujenzi wa chujio la maji la Mwendakulima ambayo unatazamiwa kuhudumia zaidi ya 66% ya wakazi waishio Manispaa ya Kahama na ina uwezo wa kutoa lita milioni 10 kwa siku.

“Mradi huu unatarajiwa kukamilika Mwezi Juni mwaka huu na mpaka sasa 78% ya mradi mzima umeshakamilika kutoka na kasi ya ujenzi wa mradi huu mkubwa kwenye mji huu wa kahama,” amesisitiza.

Mhandisi Marwa amefafanua kwamba mradi huo wa chujio la maji ya mvua 62% imefadhiliwa na mgodi wa Barrick- Buzwagi na 38% ni Kuwasa kupitia Wizara ya Maji na Serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania.

Kongani ya Barrick Buzwagi ina ukubwa wa hekta 1,333 na ipo katika eneo lililokuwa Mgodi wa Barrick Buzwagi. Hadi sasa jumla ya wawekezaji 35 wameonesha nia ya kuwekeza katika eneo hilo, ambapo mwekezaji mmoja tayari ameanza uzalishaji wa vipuri na vifaa vya migodini, watano wako katika hatua za kufuatilia leseni huku wawekezaji 29 wakiwa katika hatua za awali za uwekezaji.


Share:

Saturday, 14 March 2026

TAMESOT YAFANIKIWA KUUNDA TIMU YA VIONGOZI 10095 KWA MIKOA 13


 
Katibu Mkuu Lukas Mlipu wa TAMESOT (wanne kutoka kushoto) akiwa na viongozi  wa wa TAMESOT pamoja waganga mkoa Morogoro
Katibu mkuu  wa TAMESOT Lukas na waganga mkoa Katavi

Na Theophilida Felician -  Morogoro.

Kufuatia Chama cha Waganga wa Tiba Asili na Tiba Mbadala nchini (TAMESOT) kuendeleza juhudi za kuhakikisha tiba asili na tiba mbadala inainuka na kupiga hatua chama hicho kimeunda mfumo mpya wa kuwapata viongozi wenye uwezo wa kusimamia shughuli mbalimbali za tiba asili ndani ya chama hicho.

Ametoa kauli hiyo katibu mkuu wa TAMESOT taifa  Bw Lukas Joseph Mlipu baada kuhitimisha ziara mikoa kadhaa akilenga kuhamasisha waganga masuala muhimu yahusuyo taaluma hiyo pamoja na kuunda safu mpya ya viongozi ndani ya  chama.

Kiongozi huyo ambaye amehitimisha ziara yake kata Mziha wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro ameyataja mafanikio ikiwemo ya kuwapata viongozi kuanzia ngazi ya Vijiji, Kata, Wilaya na Mikoa kwa kila  mkoa ni viongozi 9 na wilaya 9 huku vijiji na kata wakiwa viongozi 7 na vijiji 7 hivyo vijiji 1105, kata 269, wilaya 40 na mikoa 13 tayari imekamilisha zoezi hilo na kupatika jumla ya viongozi 10095 katika maeneo hayo.

Katibu mkuu Lukas amesema licha ya kuwateua viongozi  pia zoezi hilo limekuwa sambamba na kuwapa  elimu elekezi viongozi hao ili kuwasaidia kufanya kazi kwa ueledi zaidi.

Amefafanua kuwa ziara hiyo  iliyowafikia jumla ya waganga 542 imekuwa na mafanikio  pamoja na changamoto ikiwemo ya baadhi ya waratibu wa baraza latiba asili na tiba mbadala katika halmashauri hususani kutotoa ushirikiano ipasavyo jambo ambalo amelitaja kama moja ya sababu yenye kukwamisha malengo na nia njema   ya serikali katika  kuuthamini na kuutambua mchango mkubwa  wa tiba hiyo kwa jamii, ambapo hakusita kuwapongeza waratibu wa halmshauri za Ilemela Mkoa wa Mwanza na Mvomero mkoa wa Morogoro kwa jinsi walivyokuwa naye bega kwa bega  katika kuwafikia waganga bila kulisahau Jeshi la polisi mikoa yote ambalo mara kadhaa limekuwa mstari wa mbele  kutoa  ushirikiano thabiti kwa kiongozi huyo.

Aidha  ameitaja mikoa iliyohusisha zoezi la kuwapata viongozi ni pamoja na Mbeya, Shinyanga, Geita, Mwanza, Mara,Pwani, Tanga, Morogoro, Arusha, Manyara, Kagera na Dare es salaam.

Hata hivyo ameongeza kuwa matarajio ya TAMESOT yenye ofisi zake Kibaigwa Dodoma imeendelea kujitanua zaidi ikiwemo  kupata Ardhi yenye ukubwa wa Hekari 100 itakayokuwa eneo mahususi  la kupanda mimea ya tiba pamoja na kuchapisha vitabu vya miongozo, kanuni na katiba kwa viongozi na waganga wote kwa ujumla.

 Mratibu wa bara za la tiba asili halmshauri ya Mvomero, David Rubadanja amekipongeza chama hicho kwa jinsi kinavyoendesha mambo yake kwakuzingatia mifumo iliyo wazi na yenye kufuata kanuni na taratibu za serikali tofauti na ilivyo kwa vyama vingine.

Ametoa wito kwa waratibu wengine kuuendelea kukiunga mkono chama hicho kutokana na dhamira kiliyonayo yakuyaleta mageuzi ya tiba asili ili iweze kupiga hatua mbele huku akiwasihi waganga  kutoa tiba sahihi kwa kufuata misingi ya taaluma hiyo  ili kuepukana na dhana potofu ya utapeli.
 
 

Share:

SHUWASA YAKUTANA NA WAANDISHI WA HABARI SHINYANGA, YAENDELEA KUBORESHA HUDUMA ZA MAJI



Mkurugenzi wa SHUWASA, Mhandisi Yusuph Katopola.

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA) imekutana na Waandishi wa Habari wa Mkoa wa Shinyanga kupitia Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Shinyanga (SPC) kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuboresha utoaji wa huduma za maji safi na usafi wa mazingira kwa wananchi.

Kikao hicho cha kazi kimefanyika leo Jumamosi Machi 14, 2026 mjini Shinyanga na kuongozwa na Mkurugenzi wa SHUWASA, Mhandisi Yusuph Katopola.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhandisi Katopola amesema SHUWASA inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha huduma za maji kwa wananchi wa Shinyanga, ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya maji, kupanua mtandao wa usambazaji na kuongeza upatikanaji wa maji katika maeneo mbalimbali ya mkoa huo.

Ameeleza kuwa ushirikiano kati ya SHUWASA na vyombo vya habari ni muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kuhusu huduma za maji, miradi inayoendelea pamoja na changamoto zinazojitokeza katika sekta hiyo.

Aidha amesisitiza kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa katika kuelimisha jamii kuhusu matumizi sahihi ya maji, kulinda miundombinu ya maji pamoja na kusaidia kufikisha maoni na changamoto za wananchi ili zipatiwe ufumbuzi kwa wakati.

Kwa upande wao, waandishi wa habari wameeleza utayari wa kuendelea kushirikiana na SHUWASA katika kuhabarisha umma kuhusu masuala ya maji, wakisema kuwa taarifa sahihi na kwa wakati zitasaidia kuongeza uelewa wa wananchi na kuchochea maboresho ya huduma kwa jamii.


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger