Na Sifa Lubasi
WAKULIMA mkoani Dodoma wametoa shime kwa Serikali na wadau wa kilimo kutoa mafunzo kwa wakulima hasa walio vijijini ili waweze kwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia ikiwemo umwagiliaji na kupatiwa elimu juu ya afya ya mimea ili kilimo kiwe na tija.
Wamesema hayo Jijini Dodoma wakati wa mafunzo ya wakulima juu ya afya ya mimea yaliyofanyika shamba darasa linalojulikana kama Agricultural Motivation and Technology Centre (AITEC).lililopo Don Bosco Dodoma
Mafunzo hayo yaliandaliwa na CultivAid ambalo ni shirika la kimataifa linalokuza usalama wa chakula, ustahimilivu wa hali ya hewa, na maendeleo ya kiuchumi yanayoongozwa na kilimo.
Mmoja wa wakulima kutoka Kijiji cha Mpunguzi Dk Fabian Matonya ambaye ni daktari mstaafu alisema kuwa mafunzo hayo yana manufaa makubwa kwa wakulima.
Alisema kulingana na kuwepo kwa tenolojia mbalimbali kwenye kilimo ikiwemo mfumo wa umwagiliaji, matumizi ya viuatilifu wakulima hasa wa vijijini wanahitaji elimu zaidi ya kilimo bora ili uzalishaji uwe na tija.
" Mimi ni mkulima wa zabibu elimu niliyoipata itanisaidia sana kwani zabibu inakuwa na matoleo mengi ambayo mengine hayahitajiki na yanatakiwa kutolewa ili mimea uwe na afya," alisema.
Mkulima mwingine wa kijiji cha Matumbulu, Caroline Manyungu alisema kuwa amejifunza juu ya matumizi salama ya viuatilufu bila kuathiri mimea.
Kwa upande wake,Mkurugenzi Mkazi wa CultivAid Tanzania, Eldad Barbar amesema ushirikiano wa Serikali na wadau umesaidia wakulima wakiwemo wa vijijini kuendesha kilimo cha umwagiliaji chenye sura ya uzalishaji wenye malengo.
Alisema kuwa kuna haja kwa Serikali kushirikiana na wadau ili kuunga mkono wakulima hasa wa vijijini ili kuendeleza kilimo cha umwagiliaji ambacho kimekuwa kikifanya vizuri kwenye maeneo mengi.
Alisema kuwa kilimo cha umwagiliaji kimekuwa na tija kubwa hasa kwenye kilimo cha mazao mbalimbali ikiwemo matunda , mbogamboga na parachichi ambazo zinalimwa kwenye shamba la AITEC.
"Kwenye shamba hili kuna uzalishaji mkubwa wa parachichi na limekuwa likifanya vizuri, ni zao linahitaji maji na ubaridi, tunatumia mfumo wa umwagiliaji wa matone," alisema.
Alisema kuwa, wakulima nchini wanatakiwa kuzingatia mbinu bora za kilimo, na matumizi ya teknolojia na kilimo cha umwagiliaji ili kuwa na matokeo makubwa.
Kwa upande wake mtaalam wa kilimo katika shamba hilo, Jackline Ihungo alisema kuwa wamekuwa wakitoa elimu ya kilimo bora, mbinu bora za kilimo ili kukuza sekta ya kilimo.
Alisema kuwa serikali imekuwa ikihakikisha wakulima wanapata mbinu bora za kilimo na matumizi ya viuatilufu ili kutunza usalama wa viumbe hai na mazingira.
Alitaja,mambo muhimu yanayosaidia afya ya mimea pamoja na udongo wenye rutuba , ambao unatakiwa uwe na virutubisho vya kutosha kama nitrojeni, fosforasi, na potasiamu.
Pia maji ya kutosha ikiwemo umwagiliaji sahihi husaidia ukuaji bila kuzidisha maji pamoja na mwanga wa jua kwani mimea mingi huhitaji mwanga wa kutosha kwa ajili ya kutengeneza chakula.
Aidha katika kudhibiti wadudu na magonjwa, wakulima wanapaswa kutumia mbegu bora, usafi wa shamba, na dawa salama
Hivi karibuni kulitolewa ripoti ya Maendeleo ya mwaka 2025 ya Programu ya AgriCluster ya CultivAid Tanzania ambayo ilisema iliwafikia zaidi ya wakulima 600, na kusambaza zaidi ya miche bora ya mbegu chotara 170,000, na ilikabidhi maeneo matatu kwa umiliki kamili wa jamii katika mikoa ya Dodoma na Singida.
Kulingana na ripoti hiyo, maendeleo ya programu ya pamoja na Innovation Africa na Water4Mercy katika mikoa ya Dodoma na Singida nchini Tanzania, Mwaka 2025, kazi ilifanyika katika maeneo 11 ya maonesho yanayofanya kazi,
"Programu iliwafikia zaidi ya wakulima 600, ilisambaza zaidi ya miche bora ya mbegu chotara 170,000, na ilikabidhi maeneo matatu kwa umiliki kamili wa jamii lkiwa ni ishara wazi kwamba mfumo huo unajenga uwezo wa kudumu na unaojiendesha wenyewe," ilisema sehemu ya ripoti hiyo.




