Sunday, 22 March 2026

NIMEZINDUA MADARASA YATAKAYO ONDOA MSONGAMANO WA WANAFUNZI - PROF. SHEMDOE



Na OWM - TAMISEMI, Bumbuli
  
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM -TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema kuwa amezindua madarasa matatu katika Shule ya Sekondari Kilivicha wilayani Bumbuli ambayo yataondoa changamoto ya msongamano wa wanafunzi madarasani, uliokuwa ukiikabili shule hiyo kwa muda mrefu.

Prof. Shemdoe ameongeza kuwa madarasa hayo pia ni sehemu ya maandalizi ya kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza kwa mwaka 2028 ambao watakuwa wamehitimu darasa ya sita na la saba kwa pamoja na kutakiwa kujiunga na kidato cha kwanza kutokana na mabadaliko ya mtaala mpya wa elimu unaotekelezwa na Serikali.

Prof. Shemdoe amesema hayo leo Machi 21, 2026 wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa madarasa hayo matatu yaliyojengwa kwa ufadhiri wa taasisi ya VUGA DELOPMENT INITIATIVE kwa gharama ya Shilingi Milioni 84,086,600/=.

“Ni ukweli usiopingika kwamba, ujenzi wa madarasa haya utaondoa msongamano wa wanafunzi madarasani na ni maandalizi ya kupokea wanafunzi watakaojiunga na kidato cha kwanza mwaka 2028,  mara baada ya kumaliza darasa la sita na la saba kwa pamoja kwa mujibu wa mtaala mpya wa elimu,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Prof. Shemdoe amemshukuru Bw. Rama Kaoneka ambaye ni Meneja wa Miradi wa Taasisi ya A BETTER WORLD CANADA ambaye pia ni kiongozi wa Taasisi ya VUGA DEVELOPMENT INNITIATIVE ambazo zimeshirikiana kufadhili ujenzi wa madarasa hayo matatu katika shule hiyo ya Sekondari Kilivicha.

Akizungumzia jitihada za Serikali za kuboresha miundombinu ya Elimu, Prof. Shemdoe amesema, Serikali inayongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mwaka huu wa fedha imeleta Bumbuli Shilingi Bilioni 3.2 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya Shule za Msingi na Shilingi Bilioni 2.1 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya Shule za Sekondari. 

Aidha, Prof. Shemdoe amemuelekeza Katibu Mkuu wa Ofisi yake kuhakikisha anatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa maabara ya fizikia na biolojia katika Shule ya Sekondari Kilivicha kwenye Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2026/27 ambayo maandalizi yake yanaendelea.

Kwa upande wake  Bw. Kaoneka amesema kuwa, wamefadhili ujenzi wa madarasa hayo ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na ufundishaji shuleni hapo.

Mwanafunzi wa shule hiyo Bw. Emmanuel Francis Michael amesema kwamba miundombinu hiyo ya madarasa iliyojengwa itamuwezesha kufikia ndoto yake ya kuwa rubani, na kuongeza kuwa jamii itegemee ufaulu mzuri kutoka kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Kilivicha.

Naye, Mkazi wa Kijiji cha Kivilicha Bw. Moses Thomas amemshukuru Prof. Shemdoe kwa kuzindua madarasa hayo matatu ambayo yatawawezesha wanafunzi kusoma katika mazingira bora, na kuongeza kuwa madarasa hayo yataleta tabasamu kwa wanafunzi.

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Kilivicha Bi. Sophia Dossa ameshukuru kwa kujengewa madarasa mapya na kuahidi kwamba madarasa hayo yatainua kiwango cha taaluma katika shule hiyo ya Sekondari ya Kilivicha.












Share:

Saturday, 21 March 2026

KIJANA SERIKALI HAIHITAJI KELELE INAHITAJI USHIRIKA WAKO

 

Katika ulimwengu wa sasa unaoendeshwa na matokeo, dhana ya kijana kukaa pembeni na kupiga kelele kuishtumu serikali inazidi kupitwa na wakati, badala yake nafasi iliyo wazi na yenye tija ni ile ya kuwa mshirika (partner) wa maendeleo. 

Serikali, kama msimamizi wa rasilimali, inahitaji watu wenye masuluhisho ya ndani yanayotatua changamoto za kijamii, na mshirika namba moja ambaye taifa linamtafuta ni wewe kijana uliyejaa nguvu, ubunifu na maarifa.

Mfano bora na hai wa namna ushirika huu unavyoweza kuleta mageuzi makubwa ni kupitia kazi zilizotukuka za Doris Mollel na taasisi yake ya Doris Mollel Foundation. 

Kiukweli Doris hajaishia tu kulalamika kuhusu changamoto za watoto wanaozaliwa kabla ya wakati (njiti) au afya ya uzazi nchini, bali amekuwa mshirika mkuu wa serikali katika kuboresha huduma za afya, kiasi cha kuandika historia inayotambulika kimataifa.

Hivi karibuni, katika Makao Makuu ya Shirika la Afya Duniani (WHO) mjini Geneva, Uswisi, Doris Mollel amepokea tuzo ya utambuzi kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus. 

Tuzo hiyo ni kielelezo cha uongozi wake thabiti na ahadi yake isiyoyumba katika kuendeleza afya ya mama na mtoto nchini Tanzania, jambo ambalo limethibitisha kuwa masuluhisho yanayoongozwa na wazalendo wa ndani yana nguvu kubwa ya kubadili mfumo wa afya.

Utambuzi huu wa kimataifa kwa Doris Mollel si tu sifa kwake, bali ni ujumbe kwa kila kijana wa Kitanzania kuwa inawezekana kufanya makubwa ukiwa hapa nchini kwako. 

Badala ya kupoteza muda mwingi kwenye mijadala isiyo na tija mitandaoni , Doris amewekeza nguvu zake katika "locally-led solutions"—masuluhisho yanayotokana na jamii yenyewe—ambayo ndiyo mwelekeo wa sasa wa maendeleo duniani.

Serikali inapopata washirika kama Doris, mzigo wa huduma za kijamii unapungua na ufanisi unaongezeka, jambo ambalo linajenga taifa imara na lenye heshima kimataifa. Huu ni wakati wa vijana kuacha kulalamika kuwa hakuna fursa, na badala yake kuanza kutengeneza fursa kwa kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto zinazotuzunguka, iwe katika elimu, afya, kilimo au teknolojia.

Mafanikio ya Doris Mollel kule Geneva ni kielelezo kuwa ulimwengu unatazama, na unathamini wale wanaojitofautisha kwa vitendo kuliko maneno. Ni mwito kwa kila kijana kujitathmini: Je, wewe ni mpiga kelele au ni mshirika wa maendeleo? 

Share:

Friday, 20 March 2026

WAKALA WA VIPIMO WAITIKIA WITO WA RAIS SAMIA KUHUSU UPANDAJI MITI



Na WMA – Dodoma

Watumishi wa Wakala wa Vipimo (WMA), wameitikia wito wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unaowataka watanzania kupitia makundi mbalimbali kupanda miti katika maeneo yao ili kuhifadhi mazingira.

Akiongoza zoezi la upandaji miti katika eneo ilipo Ofisi Kuu ya WMA Medeli jijini Dodoma, mapema leo Machi 20, 2026 Meneja Utawala na Rasilimali Watu, Charles Mavunde amewasisitiza watumishi wa Wakala hiyo nchi nzima kuzingatia maelekezo ya Serikali kwa kupanda miti na kuitunza ili kulinda mazingira.
Amesema kuwa, Mheshimiwa Rais Samia amekuwa akisisitiza mara kwa mara kuhusu upandaji miti katika maeneo mbalimbali na kwamba yeye mwenyewe ameonyesha mfano kwa kuwa kinara wa upandaji miti, hivyo WMA imeona ni vyema pia iitikie wito huo.

“Mtakumbuka kwamba, hata Mheshimiwa Dkt. Emmanuel Nchimbi, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akimwakilisha Mhe. Rais katika maadhimisho ya siku ya upandaji miti duniani na maadhimisho ya upandaji miti kitaifa, jana Machi 19, 2026 kule Lindi aliagiza kuwa makundi mbalimbali ya watanzania waendeleze utamaduni wa kupanda miti,” ameeleza Mavunde na kuhitimisha kuwa WMA imeyachukulia kwa uzito maelekezo ya viongozi hao na itayatekeleza kikamilifu.

Viongozi na watumishi mbalimbali wa WMA Makao Makuu wameshiriki zoezi hilo la upandaji miti akiwemo Mkurugenzi wa Huduma za Biashara Phanuel Mtuki, Meneja Sehemu ya Fedha, CPA Ibrahim Mbinga, Meneja Mkoa wa Dodoma Said Ibrahim, Meneja Mawasiliano Veronica Simba na Mkuu wa Kitengo cha Mipango, Nelson Ruturagara.

Wengine walioshiriki ni watumishi kutoka Idara mbalimbali wakiwemo maafisa, maafisa usafirishaji na wasaidizi wa ofisi.

WMA ni wakala ya serikali iliyo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara yenye jukumu kuu la kumlinda mlaji kupitia usimamizi wa matumizi sahihi ya vipimo katika sekta mbalimbali.
Share:

MFUKO WA PAMOJA WA RUZUKU KWA MASHIRIKA YASIYO YA KISERIKALI KUIMARISHA UFADHILI NA UENDELEVU



Na WMJJWM Dar Es Salaam

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. John Jingu, amesema kuanzishwa kwa Mfuko wa Pamoja wa Ruzuku kwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs Basket Fund - NBF) kutarahisisha upatikanaji wa rasilimali fedha na uendelevu kwa Mashirika hayo nchini.

Akizungumza Machi 18, 2026, wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kwanza cha Kamati ya Kitaifa ya Kuratibu Mchakato wa Uanzishwaji wa Mfuko huo, kilichofanyika katika ukumbi wa Four Points by Sheraton Jijini Dar es Salaam, Dkt. Jingu amesema Mfuko huo utakuwa chombo muhimu cha kuimarisha sekta ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.

Dkt. Jingu ameeleza kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza changamoto za utegemezi wa ufadhili kutoka nje ya nchi, ambao wakati mwingine huambatana na masharti magumu yasiyoendana na maadili na utamaduni wa Kitanzania.

“Jukumu la Mfuko huu litakuwa ni kutafuta rasilimali fedha, kuratibu utoaji wa ruzuku na kuhakikisha Mashirika Yasiyo ya Kiserikali yanakuwa na uwezo wa kutoa huduma bora na kuchangia ustawi wa jamii na Taifa kwa ujumla,” amesema Dkt Jingu.

Aidha, amebainisha kuwa kutokana na mabadiliko ya sera za ufadhili kimataifa, ni muhimu kwa Mashirika hayo kubadilika na kujiimarisha kwa kutumia mikakati mbadala itakayohakikisha uendelevu wa shughuli zao.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Dkt. Abdulmajid Nsekela, ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB amesema mafanikio ya utekelezaji wa majukumu ya Kamati yanategemea uwajibikaji wa kila mmoja kwa nafasi yake huku akisisitiza kuwa ni muhimu Wajumbe wa Kamati kufanya kazi kwa weledi, kwa kuzingatia misingi ya uwazi na uwajibikaji ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NacoNGO), Jasper Makala, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, amesema Mashirika mengi kwa sasa yanafanya kazi bila uhakika wa uendelevu wa miradi yao hivyo uwepo wa Kamati hiyo itasaidia kuongeza uhakika wa rasilimali fedha na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumuwa Mashirika hayo.

“Mfuko huu utakuwa suluhisho muhimu kwa changamoto ya uhaba wa rasilimali fedha na utasaidia Mashirika kupanga na kutekeleza shughuli zao kwa ufanisi zaidi,” amesisitiza Makala.

Naye Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kutoka Wizara hiyo, ambaye pia ni Katibu wa Kamati hiyo, Vikness Mayao, amesema Mfuko huo utakuwa chachu ya maendeleo kwa Mashirika hayo, kwa kuwa utaongeza tija katika utekelezaji wa miradi ya kijamii.

Ameongeza kuwa kupitia Mfuko huo, Mashirika yatapata fursa ya kufanya kazi kwa ufanisi zaidi na kuchangia kwa kiwango kikubwa katika maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla.





Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA MACHI 20,2026

 

Magazeti

                                                                             
                                                                               
                  
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger