Friday, 10 July 2026

CHANJO ZA TVLA NI BORA NA ZINA MATOKEO CHANYA – RAS TANGA


Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Bw. Rashid Kassim Mchatta, amesema chanjo zinazozalishwa na Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) zimeendelea kuthibitisha ubora wake kwa kusaidia kudhibiti magonjwa mbalimbali ya mifugo na kuongeza tija kwa wafugaji nchini.

Bw. Mchatta alitoa kauli hiyo tarehe 9 Julai 2026 alipotembelea banda la TVLA katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Julius Nyerere, Dar es Salaam, ambapo alipata maelezo kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na TVLA pamoja na kuona aina za chanjo zinazozalishwa kwa ajili ya kuboresha afya ya mifugo.

"TVLA inaendelea kufanya kazi kubwa ya kulinda afya ya mifugo. Chanjo zake ni bora na zimeonyesha matokeo mazuri kwa wafugaji wengi, hivyo ni muhimu wananchi waendelee kuzitumia ili kuongeza uzalishaji na kuchangia maendeleo ya sekta ya mifugo."

“Serikali itaendelea kuhamasisha wafugaji kutumia chanjo zetu za mifugo kwa kuwa zimefanyiwa tafiti za kisayansi, zina ubora unaokidhi viwango na zimekuwa na mchango mkubwa katika kupunguza milipuko ya magonjwa ya mifugo nchini” amesema Bw. Mchatta.

Akimkaribisha Katibu Tawala katika banda la TVLA, Mtaalamu wa Maabara wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania, Bw. Henry Mlundachuma, alisema TVLA ina jukumu la kufanya uchunguzi wa magonjwa ya mifugo, kuzalisha na kusambaza chanjo, kufanya tafiti za mifugo, kusajili na kuhakiki ubora wa viuatilifu vya mifugo pamoja na kutoa huduma za ushauri na mafunzo kwa wadau wa sekta hiyo.

Alieleza kuwa katika maonesho hayo, TVLA imekuwa ikitoa elimu kwa wafugaji na wananchi kuhusu matumizi sahihi ya chanjo, umuhimu wa uchunguzi wa magonjwa kabla ya tiba, pamoja na huduma za maabara zinazosaidia kubaini magonjwa mbalimbali ya mifugo kwa wakati.

Bw. Mlundachuma aliongeza kuwa matumizi ya chanjo bora na huduma za kitaalamu za TVLA ni nguzo muhimu katika kuimarisha afya ya mifugo, kuongeza uzalishaji wa nyama, maziwa na mayai, pamoja na kuimarisha usalama wa chakula na uchumi wa wafugaji.

Banda la TVLA limeendelea kuvutia idadi kubwa ya wageni wanaotembelea Maonesho ya Sabasaba, ambapo wamekuwa wakipata elimu kuhusu huduma mbalimbali za Wakala na namna zinavyochangia maendeleo ya sekta ya mifugo nchini.

Matukio mbalimbali katika picha: Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Bw. Rashid Kassim Mchatta, akitembelea banda la Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Julius Nyerere, Dar es Salaam, tarehe 9 Julai, 2026. Katika ziara hiyo alipokea maelezo kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na TVLA, ikiwemo uzalishaji wa chanjo za mifugo, uchunguzi wa magonjwa ya mifugo, huduma za maabara, uhakiki wa ubora na usajili wa viuatilifu vya mifugo, pamoja na tafiti zinazolenga kuboresha afya za mifugo nchini.
Share:

SERIKALI KUENDELEA KUWAUNGA MKONO WAZALISHAJI WA NDANI



Na.Mwandishi Wetu

Serikali imeahidi kuendelea kuwaunga mkono wazalishaji wa ndani ili kuongeza uwezo wa uzalishaji na kukuza mauzo ya bidhaa nje ya nchi hatua inayolenga

kuimarisha uchumi wa viwanda na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kimataifa.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga(Mb), Julai 09, 2026 wakati akizungumza na Waandishi wa Habari baada ya ziara yake katika Kiwanda cha Kamal Refinery kilichopo Bagamoyo mkoani Pwani kinachojihusisha na uchakataji wa mafuta machafu ya mitambo na magari (Waste/Used Lube Oil) ili kuyasafisha na kuzalisha mafuta mapya ya vilainishi (lubricants) na mafuta mazito ya viwandani (heavy fuel oil).

Aidha, amesema Sekta ya Viwanda na Biashara imeweka kipaumbele cha juu katika kuongeza minyororo ya thamani ya uzalishaji hapa nchini mkakati unaolenga kupunguza utegemezi na uingizaji wa bidhaa kutoka nje ambazo zina uwezo na sifa ya kuzalishwa kikamilifu na viwanda vya ndani.

Amesema uwekezaji huo umebainika kuwa na manufaa makubwa kimazingira, kwani unachangia kuweka mazingira katika hali ya usafi na usalama katika wakati ambao Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwa kinara na “Champion” wa utunzaji wa mazingira.

Aidha, amesema ili kufanikisha azma hiyo, Sekta ya Viwanda na Biashara itashirikiana kwa karibu na Wizara yenye dhamana ya Mazingira, ambayo tayari ina uhusiano wa kikazi na kiwanda hicho ili kuhakikisha kiwanda hicho kinaongeza uzalishaji na kukuza biashara huku kikizingatia kikamilifu utunzaji endelevu wa ikolojia.

Vilevile, Amewasihi wadau mbalimbali kuunga mkono kiwanda hicho, kinachosaidia kulinda mazingira ya taifa kwa vizazi vijavyo huku akiwataka Watanzania kuendelea kuchangamkia fursa za kiuchumi zinazojitokeza.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hicho Bw. Sameer Santosh ametoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi ya biashara na kuwaunga mkono wazalishaji wa ndani.

Amesema kiwanda hocho kitaendelea kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji ili kupunguza uingizaji wa bidhaa hizo kutoka nje ya nchi.
Share:

Thursday, 9 July 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO IJUMAA JULAI 10, 2026

Share:

WAZIRI SANGU AHIMIZA NIDHAMU NA UWAJIBIKAJI KWA WAFANYAKAZI WA KITANZANIA NCHINI QATAR

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu akizungumza na Wafanyakazi Madereva wa Kitanzania wanaofanya kazi katika kampuni ya MOWASALAT iliyopo nchini Qatar alipofanya ziara katika kampuni hiyo, tarehe 8 Julai, 2026.

******************

Na: OWM (KAM) – Doha, Qatar

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amewahimiza Watanzania wanaofanya kazi nchini Qatar kuzingatia nidhamu, uwajibikaji na uadilifu wanapotekeleza majukumu yao ili kuendelea kujenga taswira nzuri ya Taifa la Tanzania na kufungua fursa zaidi za ajira na maendeleo kwa Watanzania wengine.

Mhe. Sangu ametoa wito huo tarehe 8 Julai 2026, jijini Doha, Qatar, alipokutana na kuzungumza na Wafanyakazi Madereva wa Kitanzania wanaofanya kazi katika kampuni ya MOWASALAT iliyopo nchini humo, ambapo alisisitiza umuhimu wa kufuata sheria, kuheshimu mikataba ya ajira na kutekeleza majukumu kwa weledi.

Amesema kuwa mafanikio yanayoendelea kupatikana kwa Watanzania katika nchi mbalimbali yanatokana na juhudi, kujituma na kuonesha uwezo katika maeneo yao ya kazi.

“Uwepo wa Watanzania wanaofanya kazi katika mataifa ya nje kwa bidii ni sifa kubwa kwa taifa, kwani inasaidia kujenga imani na mahusiano mazuri kati ya Tanzania na mataifa mengine, hivyo kutoa fursa zaidi kwa vijana wengine kupata nafasi za ajira na kujifunza,” amesema Waziri Sangu

Ameongeza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuweka mazingira wezeshi ya kuongeza fursa za ajira na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika masuala ya ajira na kukuza maendeleo ya rasilimali watu.

Vile vile, Waziri Sangu amewataka Watanzania hao kuendelea kushirikiana na viongozi wa Serikali hususan Ofisi za Ubalozi, ili kupata mwongozo na msaada pale inapohitajika kuhusiana na masuala ya kisheria, kanuni na taratibu za nchi wanayoishi.

Kadhalika, Mhe. Sangu amewahamasisha madereva hao kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa kulitangaza taifa la Tanzania kupitia juhudu zao katika kazi. Pia, amewahamasisha kujiunga katika Mfuko wa Taifa wa Hifadhi Jamii (NSSF) kupitia Hifadhi Scheme ili kujijengea usalama wa kipato na ustawi wa maisha yao baada ya kustaafu au wanapokumbwa na changamoto mbalimbali za maisha, kwa kuwa hatua hiyo ni uwekezaji muhimu kwa manufaa yao binafsi na familia zao.

Naye, Balozi wa Tanzania nchini Qatar, Mhe. Habibu Awesi Mohamed amewahakikishia wafanyakazi hao kupatiwa ushirikiano wakati wowote watakapokuwa wanahitaji kupata huduma, ushauri na msaada mbalimbali wanapokuwa katika nchi hiyo.

Kwa upande wa Madereva hao wakizungumza kwa nyakati tofauti, wameshukuru Serikali kwa kuwaunganisha na fursa za ajira nje ya nchi. “Tunaishukuru sana Serikali kwa kutufungulia milango ya ajira nje ya nchi. Tunaomba juhudi hizi ziendelezwe ili vijana wengi zaidi waliopo Tanzania wapate fursa kama tulizopata sisi kwa kuwa zitaboresha maisha yao pamoja na kuwawezesha kuchangia maendeleo ya Taifa,” amesema Zulekifli Ali Massawe.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu akizungumza na Wafanyakazi Madereva wa Kitanzania wanaofanya kazi katika kampuni ya MOWASALAT iliyopo nchini Qatar alipofanya ziara katika kampuni hiyo, tarehe 8 Julai, 2026.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu akiwa katika picha ya pamoja na Wafanyakazi Madereva wa Kitanzania wanaofanya kazi katika kampuni ya MOWASALAT iliyopo nchini Qatar alipofanya ziara katika kampuni hiyo, tarehe 8 Julai, 2026.
Mkurugenzi wa Uendeshaji kutoka Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Bw. Omary Mziya pamoja na Meneja Mahusiano na Elimu kwa Umma NSSF, Bi. Lulu Mengele wakitoa elimu kwa Wafanyakazi Madereva wa Kitanzania wanaofanya kazi katika kampuni ya MOWASALAT iliyopo nchini Qatar wakati wa ziara ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu alipotembelea kampuni hiyo, tarehe 8 Julai, 2026.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu akisikiliza maoni ya Wafanyakazi Madereva wa Kitanzania wanaofanya kazi katika kampuni ya MOWASALAT iliyopo nchini Qatar alipofanya ziara katika kampuni hiyo, tarehe 8 Julai, 2026.
Balozi wa Tanzania nchini Qatar, Mhe. Habibu Awesi Mohamed akieleza jambo Wafanyakazi Madereva wa Kitanzania wanaofanya kazi katika kampuni ya MOWASALAT iliyopo nchini Qatar wakati wa ziara ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu katika kampuni hiyo, tarehe 8 Julai, 2026.
Sehemu ya Viongozi kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Kampuni ya MOWASALAT pamoja na Wafanyakazi Madereva wa Kitanzania wanaofanya kazi katika kampuni ya MOWASALAT iliyopo nchini Qatar wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu (hayupo pichani) alipofanya ziara katika kampuni hiyo, tarehe 8 Julai, 2026.
Share:

SIDO RUVUMA YAIMARISHA UJASIRIAMALI KWA MIKOPO MAFUNZO NA FURSA ZA BIASHARA

Meneja wa SIDO mkoa wa Ruvuma Baraka Kandoga akiwa ofisini kwake akizungumza na waandishi wa habari waliomtembelea ofisini kwake na kuzungumza nae kuhusu wajasiriamali wadogo namna wanavyoweza kutoka katika hatua moja na kwenda hatua nyingine ya mafanikio katika uzalishaji wa bidhaa zao na kutambulika na jamii Meneja wa SIDO mkoa wa Ruvuma Baraka Kandoga akiwa nje ya jengo la ofisi hiyo ya SIDO  Halmashauri ya Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma

Na Regina Ndumbaro Songea-Ruvuma

Shirika la maendeleo ya viwanda vidogo (SIDO) mkoa wa Ruvuma limeendelea kuimarisha jitihada za kuwawezesha vijana na wajasiriamali kwa kuwapatia mikopo, mafunzo ya ujasiriamali na kuwaunganisha na fursa mbalimbali za kukuza biashara zao.

Meneja wa SIDO mkoa wa Ruvuma, Baraka Kandoga, amesema katika mwaka wa fedha 2025/2026 shirika limetoa mikopo ya zaidi ya shilingi milioni 700 iliyowanufaisha wakulima, wamiliki wa viwanda vidogo na wafanyabiashara, lengo likiwa kuwaondolea vikwazo vya mitaji na kuongeza uzalishaji wa bidhaa nchini.

Akizungumza katika ofisi za SIDO zilizopo Manispaa ya Songea, Kandoga amesema Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira rafiki ya kuwawezesha vijana kujiajiri kupitia mfuko maalumu wa mikopo.

Amesema SIDO imepokea takribani shilingi bilioni nne zinazotolewa kwa kushirikiana na CRDB Foundation kwa ajili ya vijana wenye umri wa miaka 18 hadi 35, huku tayari vijana 24 kutoka mkoa wa Ruvuma wakiwasilishwa kupata mikopo hiyo.

Amewahimiza vijana kujitokeza katika ofisi za SIDO ili kutumia fursa hizo badala ya kusubiri ajira za kuajiriwa.

Mbali na mikopo, Kandoga amesema SIDO inaendelea kutoa mafunzo ya ujasiriamali, teknolojia za uzalishaji na programu za kuwajengea uwezo wakufunzi (Training of Trainers - ToT), sambamba na kuwawezesha wajasiriamali kushiriki maonesho ya biashara yanayowakutanisha na masoko mapya pamoja na wadau kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Amesema maonesho ya kitaifa ya SIDO yatakayofanyika Kahama mkoani Shinyanga mwezi oktoba 2026 yatakuwa fursa muhimu kwa wajasiriamali wa mkoa wa Ruvuma kutangaza bidhaa zao, kujifunza mbinu mpya za biashara na kujenga mitandao ya kibiashara.

Aidha, Kandoga amekanusha dhana kwamba mafunzo ya SIDO ni kwa watu walioshindwa maisha, akisema kwa sasa hata watumishi wa umma na wataalamu mbalimbali wanajiunga kupata ujuzi wa kuongeza thamani ya bidhaa na kuanzisha biashara.

Amesema mtu anaweza kuanzisha kiwanda kwa mtaji mdogo, hata wa shilingi laki tano, huku SIDO ikitoa mafunzo na kuwezesha matumizi ya mashine zake kwa wanaoanza uzalishaji.

Amewataka vijana kuacha hofu ya kuanza biashara ndogo, akisisitiza kuwa mafanikio makubwa huanza na hatua ndogo na kwamba ujasiriamali ni njia ya kujenga uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.
Share:

Wednesday, 8 July 2026

WAZIRI KIKWETE AWASILI MKOANI TABORA KWA ZIARA YA KIKAZI


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, amewasili mkoani Tabora kwa ziara ya kikazi inayolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuzindua miradi mbalimbali pamoja na kusikiliza changamoto zinazowakabili wananchi ili kutafuta ufumbuzi wake.

Mara baada ya kuwasili katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Kikwete amesaini kitabu cha wageni ikiwa ni ishara ya kuanza rasmi ziara hiyo ambayo inatarajiwa kugusa sekta mbalimbali za maendeleo katika mkoa huo.

Katika ziara yake, Waziri huyo atatembelea miradi inayotekelezwa chini ya Serikali, kukagua maendeleo yake, kujionea hatua zilizofikiwa pamoja na kutoa maelekezo ya kuboresha utekelezaji wake ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na zenye tija.

Aidha, ziara hiyo itatoa fursa kwa wananchi wa Mkoa wa Tabora kuwasilisha maoni, changamoto na mapendekezo yao moja kwa moja kwa Serikali, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuimarisha utawala bora, uwajibikaji na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Hatua hiyo ni kutokana na Serikali kusisitiza umuhimu wa viongozi kuwafikia wananchi kupitia ziara za kikazi, hatua inayochangia kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuhakikisha fedha za umma zinatumika ipasavyo kwa manufaa ya Watanzania.





Share:

WAZIRI SANGU AKUTANA NA KUZUNGUMZA NA WAZIRI WA KAZI QATAR




Na.Mwandishi Wetu.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Kazi wa Qatar, Mhe. Dkt. Ali bin Samikh Al Marri, leo Julai 8, 2026, jijini Doha, nchini Qatar.

Mazungumzo ya Viongozi hao yamelenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Qatar katika sekta ya kazi na ajira, hususan eneo la kukuza maendeleo ya rasilimali watu, ulinzi na haki za wafanyakazi pamoja na kuongeza fursa za ajira kwa Watanzania.

Vilevile, wamejadili kuhusu Mkutano wa Uhamaji wa Wafanyakazi (Labour Mobility Dialogue) utakaowakutanisha nchi wanachama wa Baraza la Ushirikiano la Nchi za Ghuba (GCC), Jordan, Lebanon na nchi za Afrika zinazotuma wafanyakazi nje ya nchi chini ya mwamvuli wa Umoja wa Afrika (African Union). Mkutano huo unatarajiwa kufanyika Oktoba 2026 Tanzania, jijini Dar es Salaam, ukiwa na lengo la kuimarisha ushirikiano, kubadilishana uzoefu na kupanua fursa za ajira salama na zenye staha kwa wananchi wa nchi shiriki.

Katika kikao hicho, Waziri Sangu aliambatana na Balozi wa Tanzania nchini Qatar, Mhe. Habibu Awesi Mohamed, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Zuhura Yunus, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Vijana, Ajira na Uwezeshaji Zanzibar, Khalid Masoud Waziri, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kazi na Uwekezaji, Rashid Ali Salim, pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Ajira kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Jane Songoro.



Share:

KAMANDA MULIRO AIPONGEZA NEMC KWA JUHUDI ZA USIMAMIZI NA UHIFADHI WA MAZINGIRA


-Aipongeza NEMC kwa juhudi za Usimamizi na Uhifadhi wa Mazingira

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro amelipongeza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa juhudi za Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini licha ya changamoto linazokabiliana nazo katika Utekelezaji wa majukumu.

Kamanda Muliro ametoa pongezi hizo alipozuru Kijiji cha Mazingira cha Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) tarehe 7/7/2026 katika sikukuu ya maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (sabasaba 2026)

"Nawapongeza sana kwa kazi nzuri mnayofanya, siku hizi malalamiko ya uchafuzi wa mazingira yamepungua sana sio sawa na hapo zamani hasa Maeneo ya Mbagala." Alipongeza Kamanda Muliro

Aidha ametoa wito kwa Baraza kuongeza nguvu katika eneo la Utoaji elimu ya Mazingira kwa umma na kuongeza matangazo ili Jamii ipate uelewa mpana kuhusu Ulinzi na Uhifadhi wa Mazingira.

Kamanda Muliro pia amewatembelea wadau wote wa Mazingira wanaoshiriki maonesho katika Kijiji cha Mazingira na kuwapongeza kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuibua Teknolojia zinazoibua Fursa za kiuchumi na kuhifadhi Mazingira hasa katika eneo la urejelezaji wa taka.
Share:

Monday, 6 July 2026

FCC YATUMIA MAONESHO SABASABA KUKUZA ELIMU YA BIASHARA


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

WAFANYABIASHARA na wananchi kwa ujumla wametakiwa kutumia Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kutembelea banda la Tume ya Ushindani (FCC) ili kupata huduma mbalimbali za papo kwa papo pamoja na elimu kuhusu ulinzi wa mlaji, ushindani wa biashara na udhibiti wa bidhaa bandia.

Wito huo umetolewa leo Julai 6, 2026 na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Mahusiano kwa Umma wa FCC, Roberta Feruzi, ambapo ameongeza kuwa maonesho hayo yameipa tume hiyo fursa ya kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwaelimisha kuhusu haki zao pamoja na huduma zinazotolewa na taasisi hiyo.

Amesema mbali na kutoa elimu, FCC pia inatoa huduma za moja kwa moja kwa wananchi wanaotembelea banda lake, ikiwemo kupokea na kushughulikia malalamiko, usajili wa mikataba na huduma nyingine zinazotolewa na tume hiyo.

"Tunawaalika wananchi wote kufika katika banda la Wizara ya Viwanda na Biashara, ambalo ni banda jumuishi lenye taasisi zote zilizo chini ya wizara hiyo, ikiwemo FCC, ili wapate huduma na elimu kuhusu masuala ya ushindani, ulinzi wa mlaji na udhibiti wa bidhaa bandia," amesema.

Amebainisha kuwa FCC haijajikita kutoa huduma ndani ya banda pekee, bali imeandaa programu ya kuwafuata wafanyabiashara na wajasiriamali katika maeneo mbalimbali ndani ya viwanja vya Sabasaba kwa lengo la kuhakikisha elimu inawafikia wadau wengi zaidi.

Amesemakuwa FCC imekuwa ikiendesha semina kwa makundi mbalimbali ya wafanyabiashara, ikiwapa mafunzo kuhusu sheria za ushindani, namna ya kufanya biashara kwa kuzingatia misingi ya ushindani wa haki pamoja na wajibu wao katika kulinda maslahi ya walaji.

Amesema tangu kuanza kwa maonesho hayo, FCC imefanikiwa kuwafikia zaidi ya wajasiriamali 700, wakiwemo wazalishaji wadogo na wa kati, ambao wamepatiwa elimu kuhusu namna ya kulinda alama na nembo za biashara zao, kuendeleza ubunifu na kuongeza ushindani katika soko.

Aidha, amesema taasisi hiyo inaendelea kuwalea vijana wabunifu wanaoshiriki maoneshoni kwa kuwapatia mwongozo wa namna ya kukuza biashara zao katika mazingira ya ushindani wa haki.

Amesisitiza kuwa kampeni ya utoaji elimu haitakoma baada ya kumalizika kwa maonesho ya Sabasaba, bali itaendelea kupitia ofisi za FCC zilizopo Dar es Salaam na ofisi za kanda za Mwanza, Arusha, Mbeya na Dodoma.

Ameongeza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi jumuishi kwa kuweka mazingira bora ya biashara, huku FCC ikiendelea kuwa mlezi, mwezeshaji na mdhibiti wa ushindani wa haki nchini.

Amewahimiza wafanyabiashara, wabunifu na wananchi ambao hawajapata nafasi ya kushiriki maonesho hayo kufika katika ofisi za FCC zilizo karibu nao ili kupata elimu, ushauri na huduma mbalimbali zinazotolewa na tume hiyo kwa maendeleo ya biashara zao.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger