Monday, 18 May 2026

Wimbo Mpya : GUDE GUDE - DUNIA

 

Share:

SERIKALI KUENDELEA KUBORESHA MAZINGIRA YA BIASHARA KARIAKOO


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SERIKALI imesema itaendelea kuboresha mazingira ya biashara nchini ili kuhakikisha wafanyabiashara wa Kariakoo wanakuwa na ushindani wa kikanda na kimataifa huku ikiitaja Kariakoo kuwa moyo wa biashara wa Tanzania na injini muhimu ya uchumi wa taifa.

Hayo yameelezwa leo Mei 17, 2026 katika hafla ya Utoaji wa Tuzo za Biashara Kariakoo ambapo Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Bw. Aristides Mbwasi, aliyemwakilisha Waziri wa Wizara hiyo, amesema Kariakoo si eneo la kawaida katika historia ya biashara nchini bali ni alama ya uchapakazi, uthubutu na mafanikio ya Watanzania wengi.

Amesema Kariakoo imekuwa sehemu iliyojenga maisha ya maelfu ya wananchi, huku vijana wengi wakianza biashara kwa mitaji midogo na baadaye kuwa waajiri wakubwa.

“Kila siku maelfu ya watu wanaingia Kariakoo kufanya biashara, kununua bidhaa, kuwekeza na kusafirisha bidhaa kwenda ndani na nje ya nchi ikiwemo DRC, Burundi, Rwanda, Zambia, Malawi, Uganda na Comoro,” amesema.

Mbwasi amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira bora ya biashara, uwekezaji na viwanda ili wafanyabiashara waweze kushindana katika soko la kimataifa.

Akizungumzia ujenzi wa Soko Kuu la Kariakoo baada ya janga la moto, amesema Serikali ilihakikisha soko hilo linajengwa upya kwa kiwango kikubwa zaidi ambapo mradi huo uligharimu takribani shilingi bilioni 28 na kuwa na zaidi ya maduka 2,000.

Amesema Serikali inaamini sekta binafsi ni mshirika mkuu wa maendeleo ya uchumi, ndiyo sababu imeendelea kuboresha mazingira ya biashara, kurahisisha uwekezaji, kupanua miundombinu ya masoko na kuimarisha huduma za kidigitali.

Aidha, amewahakikishia wafanyabiashara kuwa Serikali itaendelea kusikiliza changamoto zao na kuhakikisha wanapata mazingira yenye utulivu, uwazi na usalama wa mitaji yao.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kariakoo Business Awards, Zakayo Shushu, amesema tuzo hizo zimeanzishwa kwa lengo la kutambua ubunifu, uwekezaji na juhudi za wafanyabiashara wanaofanya biashara kwa uaminifu na weledi mkubwa.

Amesema tuzo hizo zinalenga kukuza biashara zinazoaminika pamoja na kuchochea ushindani wa kitaalamu ili wafanyabiashara wa Kariakoo waweze kushindana katika soko la ndani na la kimataifa.

“Tunataka kujenga mazingira ya ushindani wa kimataifa na kuhakikisha wafanyabiashara wetu wanakuwa sehemu ya ushindani mkubwa wa biashara duniani,” amesema.

Shushu ameongeza kuwa ajenda nyingine muhimu ni kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi pamoja na kuhakikisha sauti ya mlaji inasikilizwa na kuthaminiwa.

Amesema kwa kushirikiana na Serikali, wadau wa maendeleo na sekta binafsi, wamepanga kuanzisha majukwaa mbalimbali yatakayoinua Kariakoo pamoja na uchumi wa Tanzania kwa ujumla.

Aidha, amebainisha kuwa kuna mikakati ya kuanzisha mafunzo kwa wafanyabiashara pamoja na kampeni maalumu za kuitangaza Kariakoo duniani kama kitovu muhimu cha biashara.

Amesema maboresho ya miundombinu ya biashara, mazingira ya uwekezaji pamoja na utatuzi wa changamoto za wafanyabiashara yameendelea kuongeza imani ya wafanyabiashara kwa Serikali yao.

Share:

Sunday, 17 May 2026

CCM YAONYA SIASA ZA MAJITAKA KUVURUGA MAENDELEO YA JAMII



CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimeonya tabia ya baadhi ya wananchi kuruhusu itikadi na mipasuko ya kisiasa kuingilia au kuharibu kasi ya maendeleo ya nchi, huku ikionya uwapo wa uchochezi unaopelekea uharibifu wa miundombinu na miradi mikubwa inayotekelezwa na serikali kwa ajili ya manufaa ya jamii.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Kenani Kihongosi, alipokuwa akikagua mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Nyasariso iliyopo Kata ya Bunagi, Wilaya ya Tarime mkoani Mara, ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa ziara yake ya kikazi ya kukagua uhai wa chama na miradi ya maendeleo mkoani humo.

Akizungumza na wananchi pamoja na wanachama mara baada ya kukagua mradi huo, Kihongosi alisema kumekuwa na wimbi la baadhi ya watu kuendekeza chuki za kisiasa zinazowapelekea kushiriki au kushabikia uharibifu wa mali za umma, jambo ambalo ni kurudisha nyuma uchumi vya taifa.

Alisisitiza kuwa wananchi wa Tarime na Watanzania kwa ujumla wanapaswa kuwa walinzi wa kwanza wa shule, vituo vya afya na miundombinu ya nishati ya umeme, badala ya kuwa wepesi wa kubomoa kwa kufuata mihemko ya wanasiasa.

Kihongosi alibainisha kuwa siasa zinapaswa kufanyika kama uwanja wa kushindanisha hoja na sio jukwaa la kubomoa nchi, akionya kuwa athari za uharibifu huo haziichagui vyama vya siasa bali zinamgusa kila mwananchi.

Alitolea mfano kuwa kitendo cha kuchoma moto shule kinawaumiza watoto wa masikini wanaolazimika kurudi nyumbani, huku uharibifu wa vituo vya afya au kukatwa kwa nguzo za umeme ukisimamisha mnyororo mzima wa uzalishaji kiuchumi na kuhatarisha maisha ya wagonjwa.


Katika ziara hiyo, viongozi wa chama walipokea taarifa ya mradi kutoka kwa Mkuu wa Shule hiyo ya Sekondari ya Nyasariso, Paschal Sobu, ambaye alieleza kuwa shule hiyo ya mchanganyiko inayochukua wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha sita imejengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 1.6.


Sobu alifafanua kuwa katika kiasi hicho cha fedha, serikali kuu ilichangia shilingi bilioni moja wakati kiasi kilichobaki cha zaidi ya shilingi milioni 600 kikitokana na mapato ya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Tarime.


Mkuu huyo wa shule aliongeza kuwa miundombinu iliyopo inajumuisha madarasa 13, ofisi tano za walimu, jengo la utawala, maabara za kisasa za masomo ya kemia na baiolojia, bwalo la chakula pamoja na jiko la kisasa linalotumia nishati safi ya kupikia.


Alibainisha kuwa kwa sasa shule hiyo ina jumla ya walimu 13, wakiwemo wanaume 10 na wanawake watatu, kukiwa na mwalimu mmoja wa kujitolea anayelipwa kupitia ushirikiano wa karibu kati ya wazazi na halmashauri hiyo.
Share:

SERIKALI KUENDELEA KUIMARISHA UWEZO WA KUZUIA,KUJIANDAA,KUKABILIANA NA MAAFA






Na Mwandishi wetu- MBEYA

Serikali imeendelea kuimarisha uwezo wa Kitaifa wa Kuzuia, Kujiandaa, Kukabiliana na Kurejesha hali baada ya maafa ili kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama ya kuepuka madhara makubwa yatokanayo na maafa.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu Ofisi ya Mkoa wa Mbeya, Dkt. Noah Sikwese wakati akifunga mafunzo kwa Wajumbe Wateule wa Timu ya Kukabiliana na Dharura (RERT), Waatalamu wa Unendeshaji wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura (REOCC) katika Mkoa huo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa.


Dkt. Sikwese, amesema timu za kukabiliana na dharura zimejengewa msingi muhimu wa utendaji utakaowezesha Mkoa kuwa na uwezo wa kujiandaa na kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka na ufanisi mkubwa .


“Timu hizi zitahusika katika kufanya tathmini za awali na za kina wakati wa maafa kubaini mahitaji halisi ya waathirika, pamoja na kuratibu upatikanaji wa rasilimali muhimu kwa ajili ya kukabiliana na athari za maafa,” alisema Dkt. Sikwese.




Pia, aliongeza kwamba mafunzo yamekuwa nyenzo muhimu katika kujenga na kuimarisha uwezo wa kitaalamu na kiutendaji kwa watumishi wanaohusika katika Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya dharura.


“Kuanzishwa kwa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Mkoa wa Mbeya ni hatua muhimu katika kuimarisha uratibu wa shughuli za usimamizi wa maafa. Kituo hiki kitawezesha ufuatiliaji wa matukio kwa ukaribu, ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa kwa wakati, pamoja na kuimarisha mawasiliano miongoni mwa wadau,” alieleza.


Sambamba na hilo Dkt. Sikwese alifafanua kuwa, utekelezaji wa mafunzo hayo ulianza katika Mikoa a Mwanza, Arusha, Dodoma, ambapo hatua za kuanzisha Vituo vya Operesheni na Mawasiliano ya Dharura pamoja na kuimarisha Timu za kukabiliana na maafa zilianza kutekelezwa.







“Ni matarajio yangu mafunzo haya yataongeza ufanisi, uwajibikaji, ustahimilivu dhidi ya majanga katika Mkoa wetu wa Mbeya,”aliongeza.


Aidha, alitoa wito kwa wataalamu wote waliopatiwa mafunzo kuendelea kuyafanyia kazi maarifa na stadi, kudumisha nidhamu ya kazi na kujenga utamaduani wa ushirikiano wa kitaalamu huku akiwasisitiza kuendelea kufanya mazoezi ya mara kwa mara ya uokoaji na utoaji wa huduma ya kwanza kwa majeruhi au waliofikwa na maafa.


“Usimamizi wa maafa ni jukumu letu sote, kila mmoja ashiriki sasa na kuchukua hatua katika eneo lake ili kuokoa na kulinda maisha, mali na mazingira,” alisisitiza Dkt. Sikwese.




Ikumbukwe kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) kwa mujibu wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa yam waka 2004 (Toleo la 2025) pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya mwaka 202 imeipa jukumu la kuratibu masuala yote ya usimamizi wa maafa nchini.






Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI MEI 17,2026

Magazeti ya leo
 

Related Stories
Share:

Saturday, 16 May 2026

DIWANI MABAO AWASHUKURU WANANCHI NGOGWA KWA KUMPA IMANI YA UONGOZI, CCM YASISITIZA AMANI NA USHIRIKIANO


Diwani wa Kata ya Ngogwa katika Manispaa ya Kahama, Abel Mabao, akiwashukuru wananchi wa kata hiyo kwa imani waliomuonesha katika uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais uliofanyika Oktoba mwaka 2025

Na Neema Nkumbi, Kahama

Diwani wa Kata ya Ngogwa katika Manispaa ya Kahama, Abel Mabao, amewashukuru wananchi wa kata hiyo kwa imani waliomuonesha katika uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais uliofanyika Oktoba mwaka 2025, huku akiahidi kutowavunja moyo wananchi waliompa dhamana ya kuwa mwakilishi wao. 

Mabao amesema ataendelea kusimamia maslahi ya wananchi na kuhakikisha maendeleo yanapatikana katika maeneo mbalimbali ya kata hiyo.

Akizungumza mbele ya wananchi wa Ngogwa, Mabao amesema jukumu lake kubwa ni kufuatilia na kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ndani ya kata hiyo, akisisitiza kuwa ataendelea kupigania upatikanaji wa huduma muhimu ikiwemo maji, barabara na umeme ili kuboresha maisha ya wananchi.

Amesema tayari ameanza kushirikiana na madiwani pamoja na viongozi wa serikali kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa vitendo huku akibainisha kuwa baadhi ya maeneo tayari yameingizwa katika mipango ya bajeti kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali kuanzia mwezi Julai mwaka huu.

Katika hatua nyingine, Mabao ameipongeza Serikali ya Chama Cha Mapinduzi chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kupeleka huduma za maendeleo kwa wananchi akitaja miradi ya maji, umeme pamoja na miundombinu kuwa ni miongoni mwa mafanikio yanayoonekana katika maeneo mbalimbali ya Kata ya Ngogwa.

Diwani huyo pia amewataka wananchi kuendelea kudumisha amani, mshikamano na ushirikiano ili kuharakisha maendeleo ya kata hiyo, amesema amani ndiyo msingi wa maendeleo na kwamba wananchi wanapaswa kushirikiana kwa karibu na viongozi wao ili kujenga jamii yenye ustawi na maendeleo endelevu.

Kwa upande wake, Katibu wa itikadi na uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kahama, Joachim Simbila, amewataka wananchi kuendelea kulinda amani baada ya uchaguzi mkuu, akieleza kuwa amani ndiyo msingi wa maendeleo ya taifa na ustawi wa jamii, amesema wananchi wa Kahama wameonyesha ukomavu wa kisiasa kwa kushiriki uchaguzi kwa utulivu na kufanya maamuzi yao kwa amani.

Simbila amesema bila amani hakuna maendeleo, kwani hata biashara, uwekezaji na utekelezaji wa miradi ya maendeleo haviwezi kufanikiwa katika mazingira ya migogoro na vurugu.

Aidha, amegusia changamoto zinazoendelea kujitokeza duniani ikiwemo vita katika baadhi ya mataifa, akisema hali hiyo inaonesha umuhimu mkubwa wa kuendelea kuilinda amani iliyopo nchini Tanzania.

Naye Kaimu Katibu wa CCM Wilaya ya Kahama, Elia Wikunge, amewapongeza wananchi wa Kata ya Ngogwa kwa kuendelea kuonyesha ushirikiano na mshikamano katika shughuli mbalimbali za maendeleo ambapo amesema ushirikiano kati ya wananchi na viongozi wao ni msingi muhimu wa mafanikio ya maendeleo, huku akisisitiza kuwa CCM itaendelea kuwa karibu na wananchi katika kusikiliza changamoto zao na kushirikiana nao kutafuta suluhisho la maendeleo endelevu.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger