Sunday, 2 August 2026

WAZIRI KAPINGA: UWEKEZAJI WA AZANIA GROUP UTAONGEZA AJIRA NA KUKUZA UCHUMI WA TAIFA


Serikali imeipongeza Azania Group kwa kutimiza miaka 25 ya mafanikio katika sekta ya viwanda na biashara, huku ikieleza kuwa kampuni hiyo imeendelea kuwa mfano wa uwekezaji wa wazawa baada ya kutangaza mpango wa kuwekeza zaidi ya Shilingi trilioni moja katika miradi mbalimbali ya uzalishaji nchini.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe Judith Kapinga (Mb) wakati akizindua maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 25 ya Azania Group yaliyofanyika Agosti 01, 2026 katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam.

Kapinga amesema kuwa kampuni hiyo imekuwa mshirika muhimu wa Serikali katika utekelezaji wa agenda ya uchumi wa viwanda.

Aidha, kukuza kwa uwekezaji huo unaonesha imani kubwa ya sekta binafsi katika uchumi wa Tanzania na utaongeza ajira, kukuza uzalishaji wa viwandani, kuinua kipato cha wakulima na kuongeza mapato ya Serikali.

Kwa kipindi cha robo karne, Azania Group imejijengea rekodi ya mafanikio kupitia uwekezaji katika viwanda, uongezaji wa thamani ya malighafi za ndani, utoaji wa maelfu ya ajira na mchango mkubwa katika mapato ya Serikali kupitia kodi.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji kwa kuimarisha miundombinu ya reli ya kisasa ya SGR, bandari, barabara, nishati na TEHAMA, hatua zilizopunguza gharama za uzalishaji na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara na uzalishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini.

Kapinga amesema Serikali itaendelea kushirikiana na sekta binafsi ili kuharakisha maendeleo ya viwanda na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA).

Hivyo amewataka wawekezaji kuendelea kuwekeza katika teknolojia, tafiti na ubunifu ili kuongeza thamani ya bidhaa zinazozalishwa nchini na kuifanya Tanzania kufikia azma ya kuwa uchumi wa dola trilioni moja.

Hata hivyo Waziri Kapinga ameipongeza Azania Group kwa mafanikio ya miaka 25 na kueleza kuwa uwekezaji mpya wa zaidi ya Shilingi trilioni moja ni hatua muhimu itakayochochea ukuaji wa viwanda, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi wa Taifa.
Share:

KAPINGA: WAKULIMA WASIZALISHE BILA UHAKIKA WA SOKO


Serikali yaweka mkakati wa kuondoa tatizo la wakulima kuvuna mazao bila kuwa na uhakika wa soko, ikisisitiza kuwa kuanzia sasa uzalishaji wa mazao, mifugo na uvuvi unapaswa kuongozwa na mahitaji ya soko badala ya utaratibu wa kuzalisha kwanza na kuanza kutafuta wanunuzi baada ya mavuno.

Mkakati huo unalenga kubadili mfumo wa uzalishaji nchini ili kuongeza kipato cha wakulima, kupunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno, kuimarisha viwanda vinavyotumia malighafi za ndani na kufungua masoko ya ndani na nje ya nchi.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb) wakati akifungua Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere Agosti 01, 2026 mkoani Morogoro.

Kapinga amesema kuwa uzoefu umeonesha kuwa ongezeko la uzalishaji pekee haliwasaidii wakulima endapo halitaambatana na masoko ya uhakika.

Kwa muda mrefu wakulima, wafugaji na wavuvi wamekuwa wakiongeza uzalishaji bila kuanza kwa kutambua mahitaji ya soko, hali iliyowafanya baadhi yao kuuza mazao kwa bei ya chini, kukosa wanunuzi au kupoteza sehemu ya mazao yao.

Kapinga ameongeza kuwa Maonesho ya Nanenane yanapaswa kuwa zaidi ya sehemu ya kuonesha teknolojia, yakitumika kuwaunganisha wazalishaji na wanunuzi, wasindikaji, vyama vya ushirika, taasisi za fedha na wasafirishaji ili kujenga mikataba ya kudumu ya biashara.

Hata hivyo Serikali sasa inataka kuona ongezeko la bidhaa zinazoongezwa thamani, viwanda vinavyojengwa karibu na maeneo ya uzalishaji, ajira mpya na mapato yanayobaki kwa wananchi badala ya kuendelea kuuza malighafi pekee.

Aidha, aliwahamasisha wawekezaji kutumia fursa zilizopo kuwekeza katika usindikaji wa nafaka, matunda, mbogamboga, viungo, maziwa, nyama, ngozi, samaki na mazao mengine pamoja na huduma za uhifadhi, usafirishaji na utengenezaji wa vifungashio.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Adam Malima aliwataka wakulima, wafugaji na wananchi kutoka ndani na nje ya mkoa huo kutumia siku zote za Maonesho ya Nanenane kujifunza teknolojia mpya zitakazowawezesha kuongeza tija katika uzalishaji.

Alisema maonesho hayo yamekusanya taasisi za utafiti, wataalamu na wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi, hivyo wananchi wanapaswa kutumia fursa hiyo kujifunza mbinu bora za uzalishaji na kuzitumia katika maeneo yao ili kuongeza kipato na kuchochea maendeleo ya uchumi.

Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki yanayoshirikisha mikoa ya Morogoro, Pwani, Dar es Salaam na Tanga yanaongozwa na kaulimbiu isemayo "Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," inayolenga kuhamasisha uzalishaji unaoendana na mahitaji ya soko na kukuza uchumi wa viwanda.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI AGOSTI 2,2026



Magazeti







Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger