Tuesday, 16 June 2026

DHAHABU YA DABALO YAFUNGUA FURSA MPYA



Na Dotto Kwilasa, Dodoma

Ugunduzi wa mgodi mpya wa dhahabu katika Kata ya Dabalo, Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma, unatajwa kuwa fursa kubwa ya kiuchumi inayoweza kubadilisha maisha ya wananchi na kuongeza mapato ya Taifa, huku Serikali ikisisitiza uzingatiaji wa sheria za madini na tahadhari za kiusalama ili kuhakikisha rasilimali hiyo inanufaisha Watanzania.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, ametoa wito huo alipokuwa akizungumza na wananchi wa Dabalo katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo na kusikiliza kero za wananchi, akiwataka wachimbaji wadogo kuhakikisha wanaendesha shughuli zao kwa kufuata taratibu zote zilizowekwa na Serikali.

Senyamule amesema uwepo wa madini hayo ni neema kwa eneo hilo, lakini mafanikio yake yatategemea namna wachimbaji watakavyofuata sheria, kulipa kodi stahiki na kuchukua tahadhari dhidi ya watu wenye nia ovu wanaoweza kuhatarisha usalama wa mgodi na nchi kwa ujumla.

“Kunapokuwa na madini ya namna hii, tufuate taratibu za Serikali ili tuyatumie kwa tija, lakini tuwe na tahadhari nyingi za kiusalama. Tupokee wageni ambao wana tija na tusipokee wageni wenye hila kwa nchi yetu, huku tukizingatia pia huduma za afya kutokana na mikusanyiko inayoweza kujitokeza,” amesema Senyamule.

Ameongeza kuwa utii wa sheria za madini utasaidia kukuza uchumi wa wananchi mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla, huku ukiibua fursa mpya za maendeleo katika Kata ya Dabalo.

Mbali na masuala ya madini, Mkuu huyo wa Mkoa alikagua mradi wa maji uliotekelezwa na Shirika la World Vision Tanzania kwa gharama ya Shilingi 355,795,952.01 ambao umekamilika na kunufaisha wananchi wapatao 525 wa Kitongoji cha Muungano.

Pia ametembelea mradi wa umaliziaji wa maabara ya sayansi katika Shule ya Sekondari Dabalo uliogharimu Shilingi milioni 50 kutoka Serikali Kuu, ukiwa na lengo la kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia masomo ya sayansi pamoja na kuongeza idadi ya wanafunzi wanaochagua mkondo huo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Janeth Mayanja, amesema utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala unaendelea vizuri, huku elimu kwa vitendo ikiendelea kutolewa kwa wakulima ili kuwahamasisha kupeleka zao la ufuta maghalani na kuuzwa kupitia mfumo rasmi unaowawezesha kupata bei yenye ushindani.

Amesema mwitikio wa wakulima umeendelea kuongezeka kutokana na uelewa wa faida za mfumo huo katika kuongeza kipato na kuimarisha tija kwenye sekta ya kilimo.






Share:

TUNAYAKUMBUKA YA OKTOBA 29, HATUSHIRIKI MAANDAMANO- W/BIASHARA WA MWENGE


Na mwandishi wetu, Dar

Wafanyabiashara ndogondogo maarufu kama Machinga pamoja na waendesha pikipiki za kubeba abiria maarufu kama bodaboda wa eneo la Mwenge jijini Dar es Salaam wameweka msimamo mkali wa kutoshiriki maandamano yaliyopangwa na kuhamasishwa kufanyika Julai 07, 2026, wakisema hawatashawishiwa na mtu yeyote kujiingiza kwenye fujo hizo zinazoweza kuvuruga usalama na amani ya nchi.

Maamuzi hayo yamekuja baada ya kufanya vikao vya ndani na kukubaliana kulinda usalama wa maeneo yao ya kazi, msimamo unaotokana pia na hofu ya kurejea kwa athari kubwa zilizojitokeza wakati wa machafuko ya Oktoba 29, 2025. Katika kipindi hicho kibaya, wengi wakisema kuwa walipoteza ndugu na jamaa zao wa karibu huku biashara zikiharibiwa vibaya. Maduka mengi yalivamiwa, kuibiwa bidhaa zote na mengine kuchomwa moto na kusababisha hasara kubwa sana ya mitaji.

"Sisi wafanyabiashara wa Mwenge kwa kauli moja tunapinga maandamano yanayohamasishwa ya Tarehe saba Julai kwasababu hakuna faida ya maandamano haya hasa kwa tulivyojifunza katika maandamano yaliyopita ikiwemo kupoteza ndugu, marafiki na wengine biashara zao kuathirika kabisa. Sisi hiyo tarehe saba tutakuwa kwenye biashara zetu kama kawaida na tuiombe serikali kuimarisha ulinzi na usalama siku hiyo ya tarehe saba mwezi ujao." Amesema Bi. Tumaini Ulotu, mfanyabiashara soko la Mwenge.

Wafanyabiashara hao wameeleza pia namna ambavyo wao na familia zao walitaabika kupata mahitaji muhimu ya kibinadamu baada ya serikali kuweka amri ya kutotoka nje, waendesha bodaboda wengi wakikosa kipato kwa sababu hawakuweza kubeba abiria barabarani. Hali hiyo ilisababisha uhaba mkubwa wa chakula majumbani mwao na kuwaletea ugumu mkubwa wa maisha.

Kundi hili limesisitiza kuwa halitakubali kutumika kisiasa kwa ajili ya maslahi ya watu wachache wenye nia mbaya, wakitoa wito kwa vijana wote nchini kutokubali kurubuniwa na wanasiasa wanaotafuta umaarufu kwa kutumia nguvu kazi zao.


Share:

Monday, 15 June 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMANNE JUNI 16, 2026

Share:

Sunday, 14 June 2026

WANANCHI MSIKUBALI MANENO YA USHAWISHI; WAKOMALIENI WACHOCHEZI - KIHONGOSI



Wananchi na vijana kote nchini wanahimizwa kuwa macho na kutokubali kabisa kuyasikiliza maneno ya ushawishi yanayohubiri chuki na uharibifu.Badala yake, jamii inatakiwa kushikamana na "kuwakomalia" kikamilifu watu wote wanaojaribu kupandikiza mbegu za machafuko, iwe ni mitaani au kwenye mitandao ya kijamii.

Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Kenani Laban Kihongosi, alisisitiza kuwa kulinda amani ni wajibu wa kila mmoja:

"Ni wajibu wa kila mmoja wetu kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa salama, yenye amani na utulivu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho."

Aidha wananchi wametakiwa kuwa na Kumbukumbu za matukio ya nyuma, hususan Oktoba 29, ambayo yanasalia kuwa funzo kubwa na la kudumu kwa Watanzania wote.

Historia inatufundisha kuwa ghasia, vurugu, na uharibifu wa mali wakati wa harakati za kisiasa haujawahi kuleta tija, bali huacha makovu yasiyofutika, vifo, ulemavu, na kuporomoka kwa uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Wananchi wanatakiwa kukumbuka machungu ya nyuma na kukataa katakata kutumika kama kuni za kuwasha moto utakaoteketeza nchi yao wenyewe.

Kauli hioyo imetolewa huku upande wa upinzani kupitia kwa Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA Bara, John Heche, ukilalamikia misukosuko ya kisheria na kiutawala


Wadau wa amani wanasisitiza kuwa madai yoyote ya kisiasa lazima yafuate njia za kisheria na amani, bila kuingiza nchi kwenye dimbwi la damu na moto.


Siri nzito imevuja kuhusu uwepo wa mikakati ya kisiri inayoratibiwa na baadhi ya watu wenye nia ovu, inayolenga kutumia mwavuli wa maandamano na mikutano kufanya uharibifu mkubwa wa miundombinu ya umma, ikiwemo kuchoma moto shule na vyuo.


Taarifa za kiintelijensia na vyanzo vya kuaminika vinabainisha kuwa, baadhi ya vikundi na akaunti za mitandao ya kijamii zinazoendeshwa na watu wenye msimamo mkali—akiwemo mchochezi anayejulikana zimekuwa zikisuka mipango hiyo hatari kwa lengo la kuleta taharuki, kuvuruga usalama, na kuifanya nchi isitawalike.


Wachambuzi wa masuala ya usalama na maendeleo wameonya vikali dhidi ya fikra hizi za kiharifu. Swali kubwa linaloulizwa na kila Mtanzania mzalendo ni: "Ukishachoma nchi moto, ukaharibu shule na vyuo vinavyolelea watoto wetu, unatarajia kupata nini?"


Kuchoma shule na vyuo siyo kupigania demokrasia, bali ni kuharibu mustakabali wa elimu ya vizazi vya sasa na vijavyo. Kitendo cha kuharibu miundombinu ambayo imejengwa kwa kodi za Watanzania maskini ni kujirudisha nyuma kimaendeleo na kuongeza umaskini. Maisha ya wananchi yakishaharibika na amani ikitoweka, hakuna mshindi—sote tutakuwa waathirika.


"Maendeleo ya haraka yaliyopatikana Tanzania Bara na Zanzibar yametokana na kuwepo kwa amani na utulivu. Vijana wa Kitanzania msikubali kuiweka nchi yenu rehani," alikaririwa Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar (Itikadi na Uenezi), Khamisi Mbeto Khamis, akionya dhidi ya maandamano haramu.


Amewataka watanzania kulinda shule yako, linda chuo chako, na kemea kila sauti inayohamasisha uharibifu. Tanzania ni yetu sote, na kuichoma moto ni kujiteketeza wenyewe.
Share:

FILAMU YA KIFURUSHI YAZINDULIWA KUPAMBANA NA USAFIRISHAJI WA DAWA ZA KULEVYA


Dar es Salaam

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imezindua rasmi filamu ya Kifurushi, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kuelimisha wananchi kuhusu hatari za kubeba mizigo au vifurushi wasivyovifahamu na kushiriki kwa namna yoyote katika usafirishaji wa dawa za kulevya.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo uliofanyika katika Kituo Kikuu cha Mabasi cha Magufuli, Kamishna Jenerali wa DCEA, Aretas Lyimo, alisema tatizo la dawa za kulevya linaendelea kuwa tishio kwa maendeleo ya taifa kutokana na athari zake kwa afya, uchumi na ustawi wa jamii.

Alisema uchunguzi wa mamlaka hiyo umebaini kuwa baadhi ya wahalifu wamekuwa wakitumia mbinu mbalimbali za kuficha dawa za kulevya katika mizigo na vifurushi vinavyoonekana kuwa vya kawaida, hali inayowafanya baadhi ya wananchi kujikuta wakikabiliwa na mkono wa sheria bila kufahamu.

"Filamu hii imeandaliwa kuonesha uhalisia wa namna mtu anavyoweza kuingia kwenye mtego wa wahalifu kwa kubeba kifurushi au mzigo usiofahamika. Tunataka wananchi watambue kuwa mzigo unaoonekana wa kawaida unaweza kubeba dawa za kulevya na kubadilisha maisha yao kwa namna hasi," alisema Lyimo.

Aliongeza kuwa DCEA itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuimarisha mapambano dhidi ya dawa za kulevya kupitia operesheni, uchunguzi, tiba kwa waathirika na kampeni za elimu kwa umma.

Kwa upande wake, Mchungaji Richard Hananja alisisitiza umuhimu wa jamii kushiriki katika kuwasaidia waraibu wa dawa za kulevya kurejea katika maisha ya kawaida badala ya kuwanyanyapaa.

"Waraibu wanahitaji kusaidiwa na kupewa nafasi ya kubadilika. Viongozi wa dini, wazazi na jamii kwa ujumla wanapaswa kushiriki katika kuwaongoza na kuwatia matumaini," alisema.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Udhibiti Usafiri wa Barabara wa LATRA, Halima Lutabi, alisema sekta ya usafiri ni miongoni mwa maeneo ambayo wahalifu wamekuwa wakiyatumia kusafirisha dawa za kulevya, jambo linalohatarisha usalama wa abiria na taswira ya sekta hiyo.

Alisema LATRA itaendelea kushirikiana na vyombo vya dola na wadau wa usafirishaji kuhakikisha sheria, kanuni na taratibu zinazodhibiti matumizi ya vyombo vya usafiri katika shughuli haramu zinasimamiwa kikamilifu.

Kwa upande wa sekta binafsi, Naibu Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (TABOA), Abdallah Kiongozi, alisema chama hicho kiko tayari kushirikiana na Serikali katika kuzuia usafirishaji wa dawa za kulevya kupitia vyombo vya usafiri wa umma.

"Tunapokea filamu hii kwa mikono miwili na tuko tayari kuisambaza kwa wanachama wetu ili kuongeza uelewa kuhusu hatari za dawa za kulevya," alisema.

Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Tanzania, Dkt. Gervas Kasiga, alisema filamu ni nyenzo muhimu ya kuelimisha jamii na kuhamasisha mabadiliko ya kitabia, akieleza kuwa kazi hiyo itasaidia wananchi kutambua hatari za kubeba mizigo au vifurushi wasivyovifahamu.

Filamu ya Kifurushi inatarajiwa kuoneshwa katika mabasi yanayofanya safari za mikoani kote nchini kupitia ushirikiano kati ya DCEA, LATRA na Bodi ya Filamu Tanzania.

Ujumbe mkuu wa filamu hiyo ni kuwataka wananchi kutokubali kubeba mizigo, vifurushi au bidhaa za watu wengine bila kufahamu kilichomo, kwani kufanya hivyo kunaweza kuwahusisha na makosa ya jinai yenye madhara makubwa kwa maisha yao, familia na jamii kwa ujumla.

Kaulimbiu ya kampeni hiyo ni "Usafiri Salama Bila Dawa za Kulevya."
h="2560" src="https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEgutC7u41v6T0K_e1paCUYtjnWplohfAX2frzzitmYZm6RPOLVf3MwuB52RY2ewq0-CF0svFitzHj8nBGAb8iKETFLoKcJn9iT2fQv_1WQAX8UB-8bQ5dpPSQzN-yXowOZSpVJVLWT6lioFThKiPV9Ht7NPK9U-3KR7lqcraBROaAe0t7v8rMTPkzwl9sM/s600/4330696.jpg"/>
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger