Friday, 24 April 2026
TAMCU YAIMARISHA UCHUMI WA WAKULIMA TUNDURU KWA UNUNUZI WA MALORI MAPYA MATANO
Chama Kikuu cha Ushirika Wilaya ya Tunduru (TAMCU) kimechukua hatua kubwa ya kuongeza ufanisi katika sekta ya kilimo kwa kununua malori matano mapya ya kubebea mazao, hatua inayolenga kurahisisha usafirishaji na kuongeza mapato ya chama pamoja na wanachama wake.
Uamuzi huo umepokelewa kwa furaha na wakulima wa wilaya hiyo ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakikumbwa na changamoto ya ucheleweshaji wa mazao kufika sokoni kutokana na uhaba wa vyombo vya usafiri.
Akizungumza kwa niaba ya wakulima, Rashid Chibwana amesema kuwa malori hayo yatasaidia kuwafikia wakulima mashambani na kusafirisha mazao yao kwa wakati hadi maghala na hatimaye kwenye minada.
Amebainisha kuwa hapo awali walitegemea chanzo kimoja cha mapato, lakini uwekezaji huo mpya utaongeza mapato ya chama huku ukipunguza gharama na usumbufu wa usafirishaji.
Mwenyekiti wa TAMCU, Mussa Manjaule, amesema ununuzi wa malori hayo umetokana na maombi ya wanachama waliotaka kuboreshwa kwa huduma za usafirishaji pamoja na kuongeza vyanzo vya mapato.
Ameeleza kuwa awali walikuwa wanapata changamoto hata katika kusafirisha pembejeo kama viuatilifu kutoka mikoa jirani, lakini sasa hali hiyo itaboreshwa kwa kiasi kikubwa.
Kwa upande wake, Meneja wa Benki ya CRDB Tawi la Tunduru, Emanuel Mwasuka, amesema benki hiyo imechangia sehemu kubwa ya fedha zilizotumika kununua malori hayo yenye thamani ya shilingi bilioni 1.5.
Ameahidi kuendelea kushirikiana na vyama vya ushirika kwa kutoa mikopo, huku akisisitiza umuhimu wa kuyatunza malori hayo ili yadumu na kuleta tija inayokusudiwa.
Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Denis Masanja, ameipongeza TAMCU kwa hatua hiyo akieleza kuwa ni mfano bora wa maendeleo katika sekta ya ushirika.
Amesema uwekezaji huo utachochea biashara ya mazao kama korosho, ufuta na mbaazi, kupunguza gharama za usafirishaji na kuongeza kipato kwa wakulima, huku akitoa wito kwa wanachama kushirikiana na viongozi wao ili kufanikisha malengo ya chama.
Thursday, 23 April 2026
HAMU YA MARIDHIANO: VIONGOZI WA DINI NA WANASIASA WAHIMIZA AMANI BAADA YA RIPOTI
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT), Alhad Mussa Salum, amesisitiza kuwa huu ni wakati wa kujenga imani miongoni mwa wananchi na kuamini uwezo wa ndani katika kutatua changamoto za kitaifa bila kutegemea msaada wa nje.
Salum amebainisha kuwa tume hiyo iliyoongozwa na Jaji Mkuu mstaafu, Mohamed Chande Othman, ina wajumbe wenye weledi mkubwa, hivyo ni muhimu ripoti hiyo ipokewe, ichambuliwe, na iwapo kutakuwa na upungufu, mifumo iliyopo itumike kurekebisha badala ya kujenga chuki.
Kiongozi huyo wa JMAT ameongeza kuwa kutokuaminiana kati ya wananchi na viongozi wao kunaweza kukwamisha juhudi za kujitawala, akionya kuwa matukio ya Oktoba 29 ya mwaka jana yanapaswa kuwa chachu ya kujenga taifa imara zaidi badala ya kurudia makosa yaliyopita.
Kwa upande wake, Kiongozi wa Kanisa la Evangelical Fellowship Church Tanzania (EFCT), Askofu Charles Howard, ameeleza hamu yake ya kuiona Tanzania inayojenga misingi ya kusikilizana na kuridhiana hata pale kunapokuwa na tofauti za kifikra. Amesema misingi ya dini zote inahimiza amani na kuheshimiana, hivyo Watanzania hawana budi kutumia maadili hayo kuimarisha umoja wa kitaifa.
Naye Askofu Godfrey Songambele wa Kanisa la Tumaini la Mataifa Yote (HOFAN), amekumbusha kuwa amani ya kweli inapaswa kwenda sambamba na utekelezaji wa haki kwa wananchi, akisisitiza kuwa "amani ni wimbo, lakini haki ni matendo."
Mtazamo huu wa hitaji la haki na maridhiano umeungwa mkono na Katibu Mkuu wa Chama cha National League for Democracy (NLD), Hassan Doyo, ambaye amesema mustakabali wa Tanzania unategemea wanasiasa wanaoweza kukaa pamoja na kujadili maendeleo, uchumi, na usalama wa nchi. Doyo ametoa mwito kwa wananchi kutokubali kushawishiwa kufanya vurugu na viongozi wa kisiasa, badala yake walinde tunu ya amani iliyopo.
Katika kutoa mwelekeo wa kisiasa, Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Dorothy Semu, amebainisha matarajio yake kuwa ripoti hiyo itasema ukweli mtupu kuhusu nini hasa kilisababisha uvunjifu wa amani uliotokea wakati wa mchakato wa uchaguzi. Maoni haya ya viongozi mbalimbali yanadhihirisha kiu ya Watanzania kuona taifa linasonga mbele kwa masikilizano na kurejea katika hali ya utulivu wa kudumu baada ya taarifa hiyo ya tume ya uchunguzi kuwekwa wazi kwa umma.
Magazeti



