Thursday, 30 July 2026

TADB YAFIKIA HATUA MPYA YA UKUAJI: MTAJI WAFIKIA SHILINGI BILIONI 452.16



Na Dotto Kwilasa, Dodoma

Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania, TADB, imeingia katika awamu mpya ya ukuaji baada ya mtaji wake kuongezeka kwa kiasi kikubwa kutoka Shilingi bilioni 60 hadi kufikia Shilingi bilioni 452.16.

Ongezeko hilo linaledwa na kuongezeka kwa uwekezaji wa Serikali ya Awamu ya Sita katika sekta ya fedha za kilimo. Kwa mujibu wa uongozi wa benki hiyo, mtaji mpya umeipa TADB nguvu zaidi ya kutoa mikopo na kufadhili miradi inayolenga kubadilisha kilimo cha asili na kuwa kilimo cha kibiashara.

Mkurugenzi Mwendeshaji wa TADB, Frank Nyabundege, amesema ongezeko la mtaji limekuja wakati sahihi ambapo nchi inahitaji kuongeza uzalishaji wa chakula na ajira kupitia kilimo.

Amesema asilimia 73.6 ya jumla ya mikopo yote iliyotolewa na benki hiyo tangu kuanzishwa kwake, imetolewa katika kipindi cha miaka mitatu kati ya 2022 na 2025. Hii inaonyesha kasi ya utoaji wa huduma za kifedha imeongezeka mara tatu.

“Kwa sasa tuna uwezo mkubwa zaidi wa kufikia wakulima wadogo, wafugaji na wavuvi katika mikoa yote. Pia tunaweza kuingia katika minyororo ya thamani kama usindikaji, uhifadhi na masoko,” amesema Nyabundege.

TADB imetangaza kuwa katika kipindi kijacho itaweka mkazo katika maeneo matano. Maeneo hayo ni pamoja na kuongeza upatikanaji wa mitaji yenye masharti nafuu, kuimarisha kilimo cha kibiashara, kukuza matumizi ya teknolojia shambani, kuwawezesha vijana na wanawake kiuchumi, na kusaidia miradi ya kuongeza thamani ya mazao.

Wataalamu wa uchumi wanasema hatua hii ni muhimu kwa kuwa sekta ya kilimo inachangia zaidi ya asilimia 26 ya Pato la Taifa na kuajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania. Kwa hiyo kuweka fedha zaidi katika benki maalumu ya kilimo ni njia ya moja kwa moja ya kukuza uchumi.

Benki hiyo pia imesema itashirikiana na taasisi za kifedha nyingine, makampuni ya bima na wadau wa teknolojia ya kilimo ili kuhakikisha mkulima anapata ufadhili kamili kuanzia pembejeo hadi soko.

Ongezeko hili la mtaji linakuja wakati Tanzania ikiijiandaa kwa Maonyesho ya Wakulima Nane Nane 2026, ambapo sekta ya kilimo inatarajiwa kuonyesha mafanikio mapya katika uzalishaji na uongezaji thamani.

Kwa wakulima wengi, taarifa hii inatoa matumaini mapya. Maana yake ni kwamba kupata mkopo wa kununua pembejeo, kununua matrekta au kujenga ghala kutakuwa rahisi zaidi kuliko miaka iliyopita.

TADB ilianzishwa na Serikali kwa lengo la kutoa ufadhili maalumu kwa sekta ya kilimo. Tangu kuanzishwa kwake imekuwa ikipitia mageuzi mbalimbali ili iweze kuwafikia wale wanaohitaji zaidi.

Kwa sasa, benki hiyo inasema mlango umefunguka zaidi. Na lengo ni moja: kuhakikisha kila shilingi inayowekezwa inarudi shambani na kubadilisha maisha ya mkulima.




Share:

ULINZI WAIMARISHWA MIPAKANI, SERIKALI YAZINDUA OFISI NA NYUMBA YA JESHI LA UHAMIAJI MPAKA NA MSUMBIJI

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, ametoa wito kwa wananchi wanaoishi maeneo ya mipakani kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutoa taarifa zinazohusu vitendo vya uvunjifu wa sheria za mipaka, viashiria vya uhalifu, na matukio mengine yanayoweza kuhatarisha usalama, kwa lengo la kulinda usalama wa taifa na maslahi mapana ya nchi.

Ametoa wito huo wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa Ofisi ya Uhamiaji Kituo cha Mkenda–Nakawale, kilichopo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji, iliyojengwa kwa gharama ya shilingi milioni 240.8 fedha  kutoka Serikali Kuu  na nyumba ya mtumishi iliyogharimu kiasi cha shilingi 133.7 zilizofadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM).

Akizungumza katika hafla hiyo, Brigedia Jenerali Ahmed amesema maendeleo ya taifa yanategemea uwepo wa usalama imara, amesema  kuwa ni wajibu wa kila mwananchi kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa salama 

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Dkt. Franklin Rwezemula, akimwakilisha waziri wa mambo ya ndani  amesema Serikali inaendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika vyombo vya ulinzi na usalama, ikiwemo Idara ya Uhamiaji, kwa lengo la kuboresha mazingira ya kazi, kuongeza ufanisi wa utendaji na kuimarisha usalama wa mipaka ya nchi

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Dkt. Lazaro Komba, ameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa jitihada zake za kuwaletea wananchi maendeleo kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali, akibainisha kuwa katika mwaka wa fedha 2026/2027 Serikali imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa awamu ya kwanza wa barabara ya Likuyufusi–Mkenda yenye urefu wa kilomita 60 kwa kiwango cha lami.




Share:

RC SHINYANGA AFANYA ZIARA YA UKAGUZI MIRADI YA MAENDELEO KISHAPU

Na Sumai Salum – Kishapu
  • ARIDHISHWA NA HATUA YA MIRADI YA MAENDELEO KISHAPU

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, Julai 29, 2026 amefanya ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani Kishapu mkoani humo, ikiwa ni pamoja na mradi wa sekta za elimu, afya, maji, miundombinu ya barabara, miradi inayotekelezwa kwa ushirikiano na wadau wa maendeleo pamoja na unufaishaji wa mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri. 

Akiwa katika ziara hiyo, Mhita amesema maendeleo yanayoonekana ni matokeo ya amani, utulivu na demokrasia ya kiuchumi inayowavutia wadau wa maendeleo na wawekezaji kushirikiana na Serikali kuboresha maisha ya wananchi.


Mhita amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza katika sekta ya elimu kwa kujenga vyumba vya madarasa na kuboresha miundombinu ya shule ili kuhakikisha kila mtoto anapata haki ya elimu katika mazingira bora, ikiwa ni pamoja na kuongeza uwiano wa madarasa na matundu ya vyoo kulingana na idadi ya wanafunzi. Aidha, amepongeza vikundi vilivyonufaika na mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri, ikiwemo kikundi cha Wachapakazi kilichotumia mkopo huo kununua trekta kwa ajili ya kuongeza tija katika shughuli za uzalishaji.

Hata hivyo mmoja wa wananchi kutokea Kata ya Mwataga Patricia Nkana ameipongeza Serikali kwa kuendelea kuboresha huduma za afya na upatikanaji wa maji safi na salama, akisema ujenzi na uboreshaji wa zahanati na upanuzi wa upatikanaji wa maji safi na salama umeongeza usalama wa akina mama wajawazito wakati wa kujifungua na kuinua ustawi wa wananchi kwa ujumla na kuchochea kuimarisha afya ya ndoa zao.
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani Kishapu ikiwa ni pamoja na mradi wa sekta za elimu, afya, maji, miundombinu ya barabara, miradi inayotekelezwa kwa ushirikiano na wadau wa maendeleo pamoja na unufaishaji wa mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri Julai 29, 2026
Katibu Tawala mkoani Shinyanga Cp. Salum Hamduni akiwa kwenye ziara ya Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Mboni Mhita Wilayani Kishapu Julai 29, 2026
Mkuu wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Mhe Peter Masindi akizungumza wakati wa ziara ya Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Mboni Mhita Wilayani humo ya kukagua miradi mbalimbali ikiwa ni pamoja na miradi ya sekta za elimu, afya, maji, miundombinu ya barabara, miradi inayotekelezwa kwa ushirikiano na wadau wa maendeleo pamoja na unufaishaji wa mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri Julai 29, 2026 Katibu Tawala wilayani Kishapu mkoani Shinyanga Fatma Mohamed akiwa kwenye ziara ya Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Mboni Mhita Wilayani Kishapu Julai 29, 2026
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Emmanuel Johnson
Mwananchi wa Kata ya Mwataga wilayani Kishapu mkoani Shinyanga Patricia Nkana akielezea namna wanavyonufaika na uboreshaji wa miundombinu hasa ya Elimu, Afya, Maji na Nishati ya Umeme hadi Vijijini Julai 29,2026 wakati wa ziara ya Mkuu wa Mkoa huo Mhe Mboni Mhita wilayani humo

Tazama picha za matukio mbalimbali👇👇👇























































































































































































Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger