Wednesday, 22 July 2026

MUUNGANO WA TANZANIA NI TUNU, KILA MMOJA AULINDE - MASAUNI



Chalinze - Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema, kati ya jambo ambalo halipaswi kuchezewa ni Muungano ambao unatakiwa kulindwa na kila mmoja maana ndio alama kubwa ya
Tanzania.

Mhe. Masauni ameyasema hayo wilayani Bagamoyo mkoani Pwani katika ziara yake ya kikazi aliyoifanya Julai 22, 2026 akieleza kufurahishwa na shughuli za maendeleo katikaMkoa wa Pwani zinazofanyika ambazo zinaunganisha na Zanzibar ikiwemo bandari.

"Fursa ya Muungano inatakiwa kusaidia pande zote bara na Zanzibar na katika hili itakuwa inasaidia zaidi kwenye sekta ya utalii kwani mtalii anapokuja Zanzibar anaunganisha na Bagamoyo kwenye hifadhi ya Saadani",amesema.

Kadhalika amewataka vijana kuwa makini na matumizi ya mitandao ya kijamii katika kipindi hiki cha utandawazi kutokana na kuwepo kwa upotoshaji mkubwa unaofanywa na baadhi ya vijana.

Amewataka kutumia mitandao ya kijamii kwa mambo ambayo yatakuwa na faida kwao hususani kujifunza mbinu za kuboresha shughuli zao za kibiashara za kujikwamua kiuchumi.

Kwa upande wake Mbunge wa Chalinze ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema Chalinzi inabadilika kwa kasi kutokana na kazi kubwa inayofanywa na Serikali pamoja na wananchi wa eneo hilo.

Ameongeza kuwa ushirikiano baina ya viongozi na wananchi imesaidia kufanya kimbilio kwa wawekezaji wengi kutokana na kuwepo kwa miundombinu Rafiki jambo ambalo limeifanya Chalinze kukua kukua kila siku.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge alisema Wilaya ya Bagamoyo ni kati ya maeneo ya utalii ambayo kwasasa yanakuwa kwa kasi kwa kuwa na wawekezaji wengi wazawa na wageni wanaofika kuwekeza.

“Kuhusu suala la Muungano hapa Pwani watu wengi wanakutana na kufanya shighuli mbalimbali kutoka Zanzibar na Bagamoyo ni moja ya mji ambao wananchi wananufaika
na Muungano wa nchi yetu,”

Ameaema upo mpango wa ujenzi wa reli ya km 100 kutoka Bagamoyo kwenda bandari kavu ya Kwala ambayo itasaidia usafirishaji wa bidhaa mbalimbali kutoka katika mji huo.

Mhe. Kunenge amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ujenzi wa barabara ya Afrika Mashariki ambayo itafungua wigo wa usafirishaji wa na Barabara ya Mlandizi Manerumango.


Amewataka wawekezaji kujenga hoteli kubwa za kitalii kwani uwekezaji huo unahitajika kwenye Wilaya hiyo ya kitalii ambayo kwasasa imekuwa na fursa nyingi za kimaendeleo.


Mkuu huyo wa Mkoa amemuomba Waziri Masauni kufikisha ombi la Halmashauri ya Chalinze kuwa Manispaa kutokana na kuwa na vigezo vingi kikiwemo cha ongezeko la kukua kwa mapato.
Share:

TAASISI ZA UMMA ZATAKIWA KUACHANA NA UTENDAJI WA MAZOEA ILI KUFANIKISHA DIRA 2050



Na Mwandishi Wetu - Pwani.

Serikali imezitaka Taasisi, Mashirika ya Umma na Wakala za Serikali kuachana na utendaji wa mazoea na kujielekeza katika uongozi unaozingatia matokeo, ubunifu, uwajibikaji na ushirikiano wa karibu na sekta binafsi ili kuharakisha utekelezaji wa DIRA ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wito huo ulitolewa Jumanne jioni na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo, wakati akifungua Mafunzo Elekezi kwa Watendaji Wakuu wa Taasisi, Mashirika ya Umma na Wakala za Serikali yanayoratibiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina kwa kushirikiana na Taasisi ya UONGOZI katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.

Mafunzo hayo ya siku nne yanafanyika chini ya kaulimbiu "Kutoka Maono mpaka Matokeo: Kufungamanisha Utendaji wa Mashirika ya Umma na DIRA 2050."

Akizungumza katika hafla hiyo, Prof. Mkumbo alisema Tanzania imeweka lengo la kufikia uchumi wa kati wa juu na kukuza Pato la Taifa (GDP) kutoka dola za Marekani bilioni 85 hadi dola trilioni 1 ifikapo mwaka 2050 kupitia DIRA 2050.

Alisema mafanikio ya DIRA hiyo hayatategemea ubora wa sera na mipango iliyoandaliwa pekee, bali uwezo wa viongozi wa Taasisi za Umma kutafsiri maono hayo kuwa matokeo yanayoonekana katika maisha ya wananchi.

“Jukumu mlilonalo ni kubwa. Tunahitaji viongozi wenye maono, uwajibikaji, ubunifu na uadilifu watakaoweza kutafsiri DIRA 2050 kuwa matokeo yanayopimika,” alisema.

Prof. Mkumbo alisema dunia ya sasa inabadilika kwa kasi kutokana na maendeleo ya teknolojia, ushindani wa kimataifa wa kuvutia uwekezaji, mabadiliko ya tabianchi na mabadiliko ya masoko ya dunia, hivyo Taasisi za Umma hazina budi kubadilika ili ziwe sehemu ya suluhisho la changamoto za maendeleo.

Alisisitiza kuwa Serikali haitapima mafanikio ya taasisi kwa idadi ya vikao vinavyofanyika au taarifa zinazoandaliwa, bali kwa matokeo yanayopatikana kupitia utoaji wa huduma bora, ongezeko la tija, uwekezaji, ajira na mapato ya Serikali.

Aidha, aliwataka Watendaji Wakuu kuhakikisha mipango ya kimkakati ya taasisi zao, bajeti, mipango ya mwaka, mikataba ya utendaji na viashiria vya utendaji vinaendana na DIRA 2050 ili kila taasisi iwe na mchango unaopimika katika utekelezaji wa malengo ya Taifa.

Alisema DIRA hiyo imebainisha sekta za kimageuzi zitakazochochea ukuaji wa uchumi, zikiwemo kilimo, viwanda, utalii, ujenzi, madini, uchumi wa buluu, michezo na ubunifu, huduma za kifedha pamoja na sekta ya huduma, huku Taasisi za Umma zikipewa jukumu la kuwezesha ukuaji wa sekta hizo.

Prof. Mkumbo alisema utekelezaji wa DIRA 2050 unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, sekta binafsi, wananchi na wadau wa maendeleo.

Alieleza kuwa sekta binafsi ndiyo injini ya uwekezaji, ubunifu, uzalishaji na uundaji wa ajira, hivyo Taasisi za Umma zinapaswa kujiona si wadhibiti wa maendeleo pekee, bali pia wawezeshaji wa uwekezaji kwa kuweka mazingira rafiki ya biashara na kuvutia mitaji.

“Tunapaswa kujenga mazingira yatakayowezesha sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa DIRA 2050. Ushirikiano huo ndio utakaoharakisha ukuaji wa uchumi na kufikia malengo ya Taifa,” alisema huku akionya taasisi za umma kutokuwa kikwazo kwa wawekezaji.

Aliongeza: “Ninyi mmepewa dhamana ya kuongoza mageuzi ya Taasisi za Umma. Watanzania wanatarajia kuona matokeo kupitia uongozi wenu. Fanyeni kazi kwa bidii, uadilifu na ubunifu ili taasisi mnazoziongoza ziwe chachu ya kufanikisha DIRA ya Taifa ya Maendeleo 2050.”
Awali akizungumza katika hafla hiyo, Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alisema kaulimbiu ya mwaka huu inaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha DIRA ya Taifa ya Maendeleo 2050 haitabaki kuwa maono ya muda mrefu, bali inageuzwa kuwa matokeo yanayopimika kupitia utendaji wa Taasisi za Umma.

“Hatutaifikia Tanzania tunayoitamani kwa kutegemea sera pekee. Tunahitaji taasisi zenye viongozi wanaoweza kutafsiri maono ya Taifa kuwa matokeo yanayopimika katika kila sekta,” alisema.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Uwekezaji, Dk. Fred Msemwa, alisema Watendaji Wakuu wana wajibu wa kuhakikisha taasisi wanazoongoza zinakuwa chachu ya kuvutia uwekezaji, kuongeza ushindani wa uchumi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Alisisitiza kuwa uongozi wenye maono, unaozingatia uwajibikaji na matumizi bora ya rasilimali za umma ni nguzo muhimu katika kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kuharakisha maendeleo endelevu ya nchi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – UTUMISHI, Bw. Juma Mkomi, alisema mafunzo hayo ya siku nne ni sehemu ya utekelezaji wa sera za maendeleo ya rasilimali watu na uongozi katika Utumishi wa Umma, yakilenga kuwawezesha Watendaji Wakuu kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Alisema matarajio ya Serikali ni kwamba maarifa na ujuzi watakaoupata washiriki kupitia mafunzo hayo yataakisiwa katika utendaji wao wa kila siku, hivyo kuimarisha ufanisi wa taasisi wanazoongoza na kuchangia kwa kiwango kikubwa kufanikisha utekelezaji wa Dira 2050.

“Matarajio yetu ni kuwa maarifa na ujuzi mtakaoupata kupitia mafunzo haya vitaonekana katika utendaji wenu wa kila siku na hatimaye kuchangia kwa kiwango kikubwa kufanikisha utekelezaji wa Dira 2050,” alisisitiza Bw. Mkomi.

Akihitimisha, aliwataka washiriki kuwasilisha mapendekezo kuhusu mahitaji ya rasilimali watu yatakayowezesha taasisi wanazoongoza kuwa chachu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kwa mujibu wa Msajili wa Hazina, ndiyo sababu Ofisi ya Msajili wa Hazina, kwa kushirikiana na Taasisi ya UONGOZI, imeendelea kuwekeza katika maendeleo ya uongozi kupitia mafunzo elekezi kwa Watendaji Wakuu wa Taasisi, Mashirika ya Umma na Wakala za Serikali.

Alisema tangu programu hiyo ilipoanzishwa mwaka 2024, zaidi ya Watendaji Wakuu 187 wamepatiwa mafunzo hayo, huku viongozi wapatao 57 wakishiriki katika awamu ya mwaka huu.

Bw. Mchechu alisema mafunzo hayo yanawajengea viongozi uelewa wa matarajio ya Serikali, utawala bora, uwajibikaji, usimamizi wa uwekezaji wa umma, matumizi bora ya rasilimali na uongozi unaozingatia matokeo.

Alisema uwekezaji huo katika maendeleo ya viongozi tayari umeanza kuleta matokeo chanya, ambapo makusanyo ya gawio na michango yameongezeka kutoka Sh637 bilioni mwaka wa fedha 2020/21 hadi Sh1.327 trilioni mwaka 2025/26, sawa na ongezeko la asilimia 108.

“Matokeo haya yanaonesha kuwa uwekezaji katika uongozi ni uwekezaji katika uchumi wa Taifa. Kadiri tunavyojenga viongozi wenye uwezo, ndivyo tunavyojenga taasisi zenye tija na kuongeza mchango wake katika mapato ya Serikali,” alisema.

Alisema katika kipindi cha utekelezaji wa DIRA 2050, Ofisi ya Msajili wa Hazina imeainisha maeneo matano ya kimkakati yatakayoongoza mageuzi ya Taasisi za Umma.

Maeneo hayo ni kuimarisha utawala bora, kuendeleza uongozi na rasilimali watu, kuimarisha usimamizi wa utendaji unaotegemea viashiria na ushahidi, kuwezesha upatikanaji wa rasilimali kupitia ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP), masoko ya mitaji na mifuko ya uwekezaji, pamoja na kuongeza tija, faida na thamani ya uwekezaji wa Serikali.

Aliongeza kuwa mafanikio ya maeneo hayo yanategemea pia ushirikiano wa karibu kati ya Taasisi za Umma na sekta binafsi, ili kuongeza uwekezaji, matumizi ya teknolojia, ubunifu, ushindani wa uchumi na ajira.

Naye Bw. Kadari Singo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, alisema kuwa mafanikio ya utekelezaji wa Dira 2050 yatategemea kwa kiasi kikubwa uwepo wa mfumo imara wa uongozi.

Alisema ni muhimu kujenga mifumo ya kutambua na kuendeleza vipaji vya uongozi, kuhakikisha viongozi wanawekwa katika nafasi zinazolingana na uwezo wao, kuweka mipaka ya wazi ya mamlaka na majukumu yao, pamoja na kuimarisha uwajibikaji katika ngazi zote za uongozi.

"Masuala haya yanapaswa kupewa kipaumbele na kuzingatiwa kikamilifu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," alisema.

Katika mafunzo hayo ya siku nne, washiriki watapata mada kuhusu afya na ustawi wa viongozi, kufungamanisha mipango ya taasisi na DIRA 2050, uongozi wa kimkakati, usimamizi wa migogoro, usimamizi wa uwekezaji wa Serikali, utawala bora, usimamizi wa vihatarishi, ESG, fedha, ukaguzi pamoja na zoezi la kuandaa ahadi binafsi za utekelezaji wa DIRA 2050.

Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO ALHAMISI JULAI 22,2026



Magazeti

































Share:

Monday, 20 July 2026

RAIS SAMIA: AMANI NA USALAMA NI MSINGI MKUU WA MAENDELEO


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema amani na usalama ni msingi mkuu wa maendeleo ya Taifa, akiwataka wananchi kuendelea kulinda tunu hizo ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa na mazingira bora ya ukuaji wa uchumi na ustawi wa jamii.

Rais Samia amesema hayo leo Jumatatu Julai 20, 2026 mkoani Kigoma wakati akizungumza mara baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Tabora hadi Kigoma na uzinduzi wa meli nne za mizigo katika Bandari ya Kigoma.

Amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo miundombinu ya usafiri na usafirishaji, lakini mafanikio ya miradi hiyo yanategemea uwepo wa amani na usalama nchini huku akisisitiza kuwa suala hilo ni kipaumbele cha kwanza na halipaswi kupuuzwa kwani maendeleo hayatashamiri endapo amani itavurugwa.

Amewataka wananchi wa Kigoma na Watanzania kwa ujumla kuwa na utamaduni wa kuweka usalama mbele, akisisitiza kuwa maendeleo yanahitaji mazingira yenye utulivu na mshikamano.

Rais Samia pia amewataka wananchi kutokubali kushawishiwa au kutumiwa na watu wenye nia ya kuvuruga amani ya nchi, akieleza kuwa kulinda usalama ni jukumu la kila Mtanzania na kuwataka wote kuwa macho huku wakiepuka kuwa wasaliti na maadui wa nchi yao.

Ameongeza kuwa ulinzi wa amani na usalama utaendelea kuiwezesha Tanzania kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo, kuvutia uwekezaji na kukuza uchumi kwa manufaa ya wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.
Share:

WAZIRI SANGU: UANAGENZI UTAWATOA VIJANA KIMAISHA




Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuimarisha programu ya mafunzo ya uanagenzi kama mkakati madhubuti wa kuwajengea vijana stadi za kazi zitakazowawezesha kujiajiri na kuajiri wengine, hatua inayolenga kuongeza fursa za ajira na kukuza uchumi wa Taifa.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mheshimiwa Deus Sangu, amesema hayo Julai 18, 2026, wakati alipokagua utekelezaji wa mafunzo hayo katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST), Kampasi ya Rukwa.
Waziri Sangu alibainisha kuwa katika mwaka wa fedha 2025/26, Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imewezesha vijana 5,746 kupata mafunzo ya uanagenzi katika vyuo 46 nchini kwa kugharamia ada, bima ya afya, na nauli za mafunzo kwa vitendo.


Uwekezaji huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuwawezesha vijana kupata ujuzi unaokidhi soko la ajira, huku Waziri Sangu akiahidi kuwa kuanzia mwaka 2026, wahitimu wataanza kupatiwa vifaa vya kuanzia kazi ili kuwawezesha kujiajiri mara moja.


Akizungumzia utekelezaji wa programu hiyo mkoani Rukwa, Mkurugenzi wa Ajira na Ukuzaji Ujuzi, Alana Nchimbi, alieleza kuwa mkoa una vyuo viwili vinavyoshiriki, ambavyo ni MUST Kampasi ya Rukwa yenye wanagenzi 154 na Chuo cha Kilimo na Mifugo Laela chenye wanagenzi 120.


Mkuu wa Kampasi ya MUST Rukwa, Prof. Asheri Mwidege, aliongeza kuwa mafunzo hayo yamewawezesha wanagenzi kupata umahiri wa vitendo, ikiwemo ujenzi wa mageti na ukarabati wa hosteli ndani ya chuo, huku akishukuru Serikali kwa kugharamia bima ya afya na nauli kwa asilimia 100, hatua iliyoongeza ari ya vijana.


Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga, Mheshimiwa Nyakia Ally Chirukie, alipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa uratibu huo ambao umekuwa chachu ya uwezeshaji kwa vijana wa wilaya hiyo.


Wanagenzi wenyewe wameeleza kufurahishwa na mafunzo hayo ambayo yamekuwa suluhisho la changamoto ya ukosefu wa ajira. Digna Sebastian John, mhitimu wa chuo kikuu aliyebadili mwelekeo na kuanza kujifunza ufundi bomba, alibainisha kuwa ujuzi huo unampa uhakika wa kujiajiri.


Kwa upande wake, Ismail William Mbogo, ambaye awali alikuwa akijishughulikia na kilimo cha mpunga katika Bonde la Ziwa Rukwa, alitoa ushuhuda kuwa ndani ya miezi sita pekee amejenga uwezo mkubwa wa ufundi unaomfanya sasa kupata ajira za muda katika vijiji vinavyozunguka chuo hicho.


Ujumbe huu unadhihirisha kuwa programu ya uanagenzi si tu inatoa ujuzi, bali inabadilisha maisha ya vijana kutoka kwenye shughuli za kawaida na kuwaweka kwenye mkondo wa wataalamu wanaochangia moja kwa moja katika maendeleo ya jamii na uchumi wa nchi.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU JULAI 20, 2026

Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger