Sunday, 31 May 2026

JK AONGOZA WAOMBOLEZAJI KUMUAGA JACKSON ISDORY UDSM


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Viongozi wa Serikali, wanataaluma na jamii ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wameungana kumuaga Jackson Isdory Mushi, aliyefariki kwa ajali ya gari mkoani Mbeya, huku wakimkumbuka kwa mchango wake mkubwa katika kujenga taswira na mahusiano ya taasisi hiyo.

Jakaya Mrisho Kikwete ambaye Rais Mstaafu ambaye pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ameongoza mamia ya waombolezaji katika shughuli hiyo.

Katika shughuli hiyo ya maombolezo walihudhuria viongozi mbalimbali wengine ni Spika wa Bunge Mstaafu, Dkt. Tulia Ackson, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda, Waziri wa Uwekezaji Prof. Kitila Mkumbo pamoja na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Prof. William Anangisye, walioambatana na viongozi wengine wa chuo hicho.

Waombolezaji na watu mbalimbali wamemkumbuka marehemu kwa nidhamu, utu na weledi wake kazini, wakisema aliacha alama ya kipekee katika utumishi na mahusiano ya kijamii ndani ya chuo na nje yake.

Jackson Isdory Mushi anatarajiwa kuzikwa Jumanne, Juni 2, 2026 katika kijiji cha Usseri, wilayani Rombo, mkoani Kilimanjaro.
Share:

KAPINGA AITAKA TBPL KUONGEZA UZALISHAJI NA KUIMARISHA MIKAKATI YA MASOKO


Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, ameagiza Menejimenti ya Kiwanda cha Kuzalisha Bidhaa za Kibaolojia Tanzania (TBPL) kinachomilikiwa na Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) kuongeza uzalishaji na kuimarisha mikakati ya masoko ili kunufaika na mahitaji makubwa yaliyopo sokoni, kuhakikisha kiwanda kinaendelea kujiendesha kwa ufanisi wa kibiashara

Vilvile amezitaka Taasisi zote hususani TFC, TARI, TFRA na TPHPA zilizoingia makubaliano na TBPL kuhakikisha yanatekelezwa kwa vitendo na kuleta matokeo yenye manufaa kwa wakulima, sekta ya viwanda na uchumi wa taifa kwa ujumla.

Ametoa maagizo hayo Mei 30, 2026 katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano ya ushirikiano iliyofanyika katika Kiwanda cha TBPL kilichopo Kibaha mkoani Pwani, kwa lengo la kuimarisha uzalishaji, usambazaji na matumizi ya mbolea hai nchini.

Aidha, amesisitiza kuwa ushirikiano uliowekwa kati ya TBPL, na Taasisi hizo ni hatua muhimu katika kuimarisha minyororo ya thamani ya Mazao ya kilimo na viwanda pamoja na kukuza matumizi ya teknolojia na ubunifu.

Aidha, Waziri Kapinga amesema uzalishaji wa mbolea hai nchini utapunguza matumizi ya fedha za kigeni zinazotumika kuagiza pembejeo hizo kutoka nje ya nchi huku ukiwawezesha wakulima kupata bidhaa bora kwa wakati na kwa gharama nafuu.

Waziri Kapinga pia ameeleza kuwa matumizi ya mbolea hai kupitia TBPL ni hatua muhimu katika kuongeza tija ya kilimo, kuchochea ukuaji wa viwanda vinavyotegemea malighafi za ndani na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uzalishaji wa mbolea hai katika ukanda wa Afrika Mashariki..

Kapinga pia amempongeza Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), Dkt. Nicolaus Herman Shombe, kwa usimamizi wake wa miradi ya maendeleo ya kimkakati na mchango wake katika kuendeleza shughuli za uzalishaji viwandani.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger