


Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano, Teknolojia ya Habari na Ubunifu, Fatma Mabrouk Khamis, wakati akifungua mafunzo ya siku tatu kwa wanafunzi wa vyuo vikuu kutoka Afrika Mashariki na India.
Fatma ameweka wazi kuwa Serikali ya Zanzibar Awamu ya Nane imeweka kipaumbele cha kufa mtu kwenye sayansi na teknolojia, ikilenga kuwabadilisha wasomi kutoka kuwa wasaka ajira na kuwa wabunifu wa miradi inayozalisha mali.
“Wasomi wetu, wakati wa kushinda mitandaoni bila tija umepitwa na wakati. Huu ni wakati wa kuongeza ubunifu, kubuni miradi ya uzalishaji na kuingia kwenye ujasiriamali,” alisema Fatma huku akisisitiza kuwa idadi ya wahitimu ni kubwa kuliko nafasi za serikalini, hivyo njia pekee ya ushindi ni kujiajiri kupitia sekta binafsi.
Katika kile kinachoonekana kama "mchongo" wa uhakika, Joseph Evarest kutoka Shirika la UNDP kupitia programu ya FUNGUO, amebainisha kuwa wapo tayari kuviunganisha vyuo vikuu vya Tanzania na mataifa kama India na Uingereza. Mpango huu si wa nadharia tu, bali unalenga kubadilisha mawazo ya ubunifu ya wanafunzi kuwa biashara halisi zinazopata ufadhili wa fedha, ili kijana aweze kusimama mwenyewe kiuchumi badala ya kukata tamaa.
Baadhi ya wanafunzi waliochangamkia fursa hiyo, akiwemo Kelvin Hemu (UDSM) na Happy Weston, wamethibitisha kuwa tayari wapo kwenye mchakato wa kuibua mawazo yatakayowapa fedha za kuendeleza kazi zao.
Huu ni ujumbe tosha kwa vijana: Badala ya kutumia bando lako kusononeka na hali ya maisha, tumia ubunifu wako kufungua milango ya maendeleo, kwani amani iliyopo nchini ndiyo uwanja mpana wa wewe kujiwekea akiba na kupata tija.


Na Bora Mustafa, Arusha.
Uongozi wa Wilaya ya Arusha umetangaza kuanzisha rasmi siku maalum ya kushughulikia kero za wananchi katika ngazi ya kata na mitaa, hatua inayolenga kupunguza mlundikano wa malalamiko katika ofisi za wilaya.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara Machi 03,2026 , Mkuu wa Wilaya ya Arusha,mhe. Joseph Mkude, amesema kuwa kuanzia sasa kila siku ya Jumatano wananchi watapata fursa ya kuwasilisha na kusikilizwa kero zao katika maeneo yao.
Amesema utaratibu huo utasaidia kupunguza idadi ya wananchi wanaolazimika kufika ofisi za wilaya kufuatilia malalamiko yao, pamoja na kutoa nafasi kwa uongozi kushughulikia masuala mengine ya maendeleo.
Pia amesema kuwa lengo ni kusogeza huduma karibu na wananchi ili wapate majibu kwa wakati.
Pamoja na hilo, Mkude amesema kuwa kila Ijumaa katika ngazi ya kata kutakuwa na ufuatiliaji wa kero zilizowasilishwa ili kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi.
Pia amesema kuwa Jumatano ya mwisho wa mwezi itatengwa kwa ajili ya kusikiliza kero katika viwanja vya wilaya, hatua itakayowapa nafasi wananchi wengi zaidi kuwasilisha changamoto zao.
Katika hatua nyingine, amesema kuwa kliniki maalum ya ardhi inaendelea kufanyika wilayani humo kwa lengo la kutoa elimu na kurahisisha taratibu za umiliki wa ardhi, hususan kwa wanawake. Amesema mwanamke ana haki ya kisheria ya kumiliki ardhi kama ilivyo kwa mtu mwingine yeyote, pamoja na kwamba jamii bado inahitaji kupewa elimu zaidi kuhusu haki hiyo.
Hata hivyo, amesema changamoto kubwa inayochangia migogoro ya ardhi ni ukosefu wa uelewa wa taratibu sahihi za ununuzi na umiliki wa ardhi. Amesema wanasheria wa wilaya pamoja na maafisa ardhi wameelekezwa kuhakikisha wananchi wanapatiwa elimu ya kutosha kuhusu sheria na taratibu hizo.
Aidha, amesema wananchi wote wenye uhitaji wa kupimiwa maeneo yao wanatakiwa kufika katika ofisi za ardhi ili kupatiwa huduma za upimaji pamoja na kuandaliwa nyaraka muhimu za umiliki.
Pia amewahimiza kujitokeza kwa wingi kutumia fursa hiyo ili kuepuka migogoro ya baadaye na kumiliki ardhi kihalali.