Thursday 30 August 2018

UTATA WATAWALA KIFO CHA MTAWA BUGANDO...MAPYA YAIBUKA

Suala kifo cha Mkurugenzi wa Fedha na Mipango wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Ziwa Bugando (BMC), Mtawa Suzan Bartholomew, limechukua sura mpya baada ya taarifa kusambazwa zikieleza huenda aliuawa.

Juzi, baada ya taarifa kwamba Mtawa huyo alijiua kwa kujirusha kutoka ghorofa ya pili kusambaa, kwenye mitandao ya jamii ulianza kusambaa ujumbe uliokuwa ukieleza kuna uwezekano mtawa huyo aliuawa na kwamba huenda alisukumwa na mtu au watu ambao hawajajulikana.

Akizungumzia suala hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Jonathan Shanna, alisema jana kuwa ameusoma ujumbe huo na kuufanyia kazi.

Alisema ujumbe huo hauna ukweli wowote kwa kuwa vipo vielelezo vingi ukiwamo ushahidi wa maandalizi ya mtawa huyo kujiua.

Kamanda Shanna alisema kabla ya kujirusha, Mtawa huyo alifungasha vitu vyake katika nyumba aliyokuwa akikaa ikiwa ni pamoja na kumkabidhi mmoja wa ndugu zake gari lake na picha zake na baba yake mzazi akimueleza kuwa anakwenda eneo asilolijua.

“Kwenye uchunguzi kuna mambo mengi, picha ya kamera ya CCTV po wazi, inamuonesha mtawa huyo akiwa anapanda ngazi kwenda eneo husika na alipojirusha kuna baadhi ya wafanyakazi wengine na wagonjwa ambao walimuona hivyo hakuna taarifa za kusukumwa wala kurushwa.

“Kabla ya tukio hilo Mtawa huyo alijiandaa na kufunga vitu vyake, aligawa baadhi ya vitu kwa watu ikiwa ni pamoja na kumpatia gari mmoja wa ndugu zake na picha zake na wazazi wake.

“… aliziondoa line za simu zake kutoka ndani ya simu na kuweka simu juu ya kiyoyozi eneo ambalo alijirusha,” alifafanua.

Kamanda Shanna alisema yeye binafsi alitembelea eneo alikojirusha Mtawa huyo na kupata maelezo kwa watu mbalimbali.

Alisema aliyesambaza ujumbe kuwa Mtawa huyo kuuawa alikuwa na lengo ambalo litashindana na ushahidi na polisi wanaendelea kuchapa kazi kwa kuwa ukweli wote umebainika.

Mtawa huyo anadaiwa kujirusha usiku wa kuamkia Agosti 27, mwaka huu na kuokotwa.

Alilazwa katika wodi ya wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU) na kuendelea kupatiwa matibabu lakini alifariki dunia usiku wa Agosti 28, mwaka huu wakati akiendelea kupatiwa matibabu.

Wizi wa fedha ulivyotokea:

Habari za ndani zilizopatikana zimedai kuwa Mtawa huyo akiwa mkuu wa kitengo cha fedha katika Hopsitali ya Rufaa Bugando, alikuwa amesimishwa kazi ikiwa ni pamoja na kushushwa cheo na bodi ya hospitali hiyo kutokana na kubainika upotevu wa Sh milioni 380.

Kwa mujibu wa uchunguzi, fedha zilizotoweka ni zile ambazo zilikuwa hazilipiwi katika mfumo wa benki ikiwa ni pamoja na sehemu ya fedha zilizokuwa zikilipwa benki moja kwa moja ambazo zilikuwa zikiinigizwa katika akaunti tofauti na kiasi kingine kikidaiwa kutoroshwa kwa njia ya mtandao.

“Wizi huu wa zaidi ya Sh milioni 300 ni wa kipindi cha miezi miwili tu hivyo ulipogundulika uongozi ulilazimika kufanya ukaguzi maalum.

“Lakini ukaguzi huo ulionyesha kulikuwa na wizi hivyo jukumu la kufuatilia likikabidhiwa kwa maofisa wa Benki ya CRDB, watalaamu wa mtandao, polisi kitengo cha fraud (udanganyifu) na Takukuru.

“Wiki mbili zilizopita baada ya kubainika hali hiyo uongozi wa hospitali ulitutangazia kusimamishwa kazi kwa Mtawa huyo ikiwa ni pamoja na kushushwa cheo.

“Hivyo alitakiwa kukabidhi ofisi lakini alikabidhi na baadhi ya vitu na siku ya kukabidhi ofisi hakutokea na hakuwapo nyumbani na ofisini hakufika mpaka siku iliyofuata ambako alikabidhi na siku moja baadaye kutokoea tukio hilo,” alieleza mtoa taarifa.

Akizungumzia kifo hicho, Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Kanda ya Rufaa ya Bugando (BMC), Dk. Abel Makubi alisema hajabahatika kuona ujumbe ambao umesambazwa katika mitandao ya jamii.

Hata hivyo baada ya kutumiwa na kuusoma alisema anachoamini ni kwamba ujumbe huo umeandaliwa na mmoja wa watu ambao walikuwa na nia ya kutaka kuvuruga upelelezi unaondelea.

“Sikua nimeusoma ujumbe huo, lakini kwa jinsi ulivyonisomea, nauona kama ujumbe huu una lengo fulani.

“Kwanza muandikaji amejificha kwa kutaka kuaminisha yupo ndani ya polisi na anaongea kama polisi, lakini unaona anataka kuhamisha tatizo lionekane kuwa kauawa na ananijua mkurugenzi… hebu tuwaachie polisi wafanye uchunguzi wa haya, hata juu ya ujumbe huu,” alisema.

Alikizungumzia suala la kamera za usalama hospitalini hapo, alieleza kuwa zipo lakini kutokana na ukubwa wa jengo hilo hazijawekwa jengo lote kwa asilimia 100 isipokuwa katika maeneo muhimu na yale ya njia za wanaoingia na kutoka.

“Kweli kuna kamera (CCTV camera), lakini hazitoshelezi jengo zima la hospitali, hivyo siyo rahisi kwa jengo lote kuwa nazo,” alisema.
Chanzo - Mtanzania
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger