
Na Lydia Lugakila - Kagera
Evance Kamenge, Mkulima na mchumi kutoka Wilaya ya Missenyi, Mkoani Kagera, ametangaza rasmi nia yake ya kugombea nafasi ya ubunge katika Jimbo la Nkenge katika uchaguzi wa mwaka 2025.
Akizungumza na waandishi wa habari katika Manispaa ya Bukoba, Kamenge amethibitisha kwamba yuko tayari kuwasilisha ombi lake la ridhaa kwa wananchi wa Nkenge.
"Niliwahi kugombea na sasa nataraji kugombea tena mwaka huu 2025," alisema Kamenge.
Kamenge ameeleza kuwa yeye ni sehemu ya mabadiliko na kwamba kuna umuhimu wa kuweka mikakati thabiti ya kuboresha hali ya maisha ya wananchi.
"Mimi ni mkulima na ninaajiri watu, haya ninayoyasema yanatokana na hali halisi ya maisha ya familia yangu," amesema Kamenge.
Mwanasiasa huyo pia amesisitiza kwamba anapokusudia kugombea, anataka kuwa sehemu ya mapinduzi siyo mageuzi.
Amesema kuwa ameona mambo mengi yanapaswa kubadilishwa ili kufikia maendeleo halisi huku akidai kutoridhishwa na hali ya maendeleo katika eneo hilo.
Aidha, Kamenge ameonesha kuwa ana imani kwamba viongozi wa sasa wanapaswa kutekeleza ahadi zao huku akiongeza kuwa anatazamia kuwaambia wananchi ukweli huo wakati atakapokuwa na afya njema.
Kamenge pia amegusia umuhimu wa viongizi kuwa waaminifu katika siasa, akitaja msemo ulioko kwenye kadi yake ya chama chake isemayo "Nitasema kweli daima, fitina kwangu ni mwiko." kauli ambayo imeonesh ya kukazia dhamira yake na kueleza haja ya kuwa na viongozi waaminifu na wanaojali maslahi ya wananchi.
0 comments:
Post a Comment