Wednesday 6 March 2024

MADIWANI WA HALMASHAURI YA MSALALA WAFANYA ZIARA YA KIKAZI BARRICK NORTH MARA NA KUPONGEZA UWEKEZAJI WENYE TIJA

...
Madiwani wa Halmashauri ya Msalala wakijionea mradi wa majisafi ya bomba uliojengwa kutokana na fedha za CSR Barrick North Mara katika kijiji cha Nyangoto kwa ajili ya matumizi ya wananchi wa vijiji wanaoishi katika maeneo yanayozungika mgodi.
Madiwani wa Halmashauri ya Msalala wakijionea mradi wa majisafi ya bomba uliojengwa kutokana na fedha za CSR Barrick North Mara katika kijiji cha Nyangoto kwa ajili ya matumizi ya wananchi wa vijiji wanaoishi katika maeneo yanayozungika mgodi.
Madiwani wa Halmashauri ya Msalala wakijionea shamba la kilimo biashara linaloendeshwa na vijana katika kijiji cha Matongo. Shamba hilo lilianzishwa kwa ufadhili wa mgodi wa North Mara kwa ushirikiano na Halmashauri ya Wilaya ya Tarime.
Madiwani wa Halmashauri ya Msalala wakitembezwa katika maeneo mbalimbali ya mgodi wa North Mara.
Meneja Mkuu wa Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara, Apolinary Lyambiko akieleza shughuli za mgodi katika kikao na madiwani wa Halmashauri ya Msalala waliotembelea mgodini hapo.
Madiwani wa Halmashauri ya Msalala wakipata taarifa ya shughuli za Mgodi wa North Mara mara baada ya kuwasili mgodini hapo
Madiwani wa Halmashauri ya Msalala wakipata taarifa ya shughuli za Mgodi wa North Mara mara baada ya kuwasili mgodini hapo


***
MADIWANI wa Halmashauri ya wilaya ya Msalala iliyopo Kahama mkoani Shinyanga, wamefanya ziara ya kikazi katika Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara na kutoa pongezi kwa uwekezaji wenye tija sambamba na kuleta maendeleo kwenye jamii zinazozunguka mgodi huo kupitia miradi iliyotekelezwa kwa fedha za uwajibikaji kwa jamii (CSR).

Pia, wamefurahishwa na ushirikiano uliopo kati ya mgodi huo na viongozi wa kijamii, wakiwemo madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime ulipo mgodi huo unaoendeshwa na Kampuni ya Barrick kwa ubia na Serikali ya Tanzania kupitia Kampuni ya Twiga Minerals.

Katika ziara hiyo, madiwani hao kutoka Halmashauri ya Msalala ulipo mgodi wa Dhahabu wa Bulyanhulu unaoendeshwa pia na Kampuni ya Barrick kwa ubia na Serikali ya Tanzania, wamepokelewa na uongozi wa Mgodi wa Barrick North Mara, madiwani na wakuu wa idara za Halmashauri ya Wilaya ya Tarime.

Katika ziara hiyo pia wameongozana na Mbunge wa Msalala, Iddi Kassim Iddi na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kahama, Thomas Muyonga.

Pamoja na mambo mengine, wamepewa taarifa ya shughuli mbalimbali zinazofanywa na mgodi wa North Mara, kabla ya kupelekwa kujionea miradi ya maendeleo ya kijamii inayotekelezwa na mgodi huo kupitia mpango wake wa Uwajibikaji wa Kampuni kwa Jamii (CSR), kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Tarime.

Miradi waliyotembelea ni bustani ya kilimo biashara - unaoendeshwa na vijana katika kijiji cha Matongo, Shule ya Sekondari Matongo na mradi mkubwa wa majisafi ya bomba uliojengwa kijijini Nyangoto,unaosambaza maji kwenye vijiji vilivyopo Nyamongo, kilomita chache kutoka mgodi wa North Mara.

“Tunawapongeza kwa utekelezaji wa miradi hii ya kijamii, viongozi wa mgodi na wananchi endeleeni kushirikiana na kuwa wamoja, na niseme viongozi wa mgodi huu na madiwani mnastahili pongezi kwa kuibadilisha hii wilaya na kupiga hatua kubwa ya maendeleo,” alisema Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kahama, Muyonga.

Awali, katika hotuba yake ya kuwakaribisha wageni hao kutoka Msalala, Meneja Mkuu (GM) wa Mgodi wa Barrick North Mara, Apolinary Lyambiko, alisema uhusiano kati ya mgodi huo na jamii inayouzunguka umeendelea kuimarika tangu Kampuni ya Barrick ianze kuuendesha.

“Nina furaha kuona tuna uhusiano mzuri na jamii inayotuzunguka. Zamani hii hali haikuwepo, tangu tuchukue huu mgodi tumekuwa mstari wa mbele kuleta maendeleo kwa jamii, na hii isingewezekana kama tusingekuwa na uhusiano mzuri.

“Nawashukuru viongozi na jamii kwa ushirikiano wanaotupatia na kufanya shughuli zetu kuwa na tija. Tunaendelea kuboresha uhusiano na kuona jamii inanufaika na mgodi,” amesema GM Lyambiko.

Kwa upande wake, Meneja Uhusiano wa Mgodi wa Barrick North Mara, Francis Uhadi amesema pamoja na juhudi kubwa wanazofanya katika kuboresha huduma za kijamii, bado mgodi huo unakabiliwa na tatizo la kuvamiwa na makundi ya watu kwa ajili ya kupora mawe yenye dhahabu.

Kutokana na hali hiyo, Meneja Uhadi ameendelea kuwaomba viongozi wa Serikali na wa kisiasa wakiwemo madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime kuusaidia mgodi huo kukomesha tatizo hilo.

Akijibu hoja hiyo, Mbunge wa Tarime Vijijini, Mwita Waitara ameahidi kufanya mkutano na madiwani kwa ajili ya kutafuta namna ya kuwasaidia vijana wanaohusika katika uvamizi huo ili waweze kuachana na uhalifu huo.

Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger