Sunday 3 March 2024

BARRICK BULYANHULU YAFANIKISHA KUWAJENGEA UWEZO WALIMU WA SEKONDARI HALMASHAURI YA MSALALA

...

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Msalala, Khamis Katimba akifunga mafunzo hayo.
Afisa Elimu Halmashauri ya Msalala, Seleko Ntobi
Mmoja wa wakufunzi waliondesha mafunzo hayo akongea wakati wa hafla hiyo.
Mwakilishi wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu, William Chungu, akiongea katika hafla ya kufunga mafunzo hayo.
Walimu walioshiriki mafunzo hayo wakifuatilia mada mbalimbali
Walimu walioshiriki mafunzo hayo wakifuatilia mada mbalimbali
Walimu walioshiriki mafunzo hayo wakifuatilia mada mbalimbali
**

Katika jitihada za kuinua kiwango cha elimu ya sekondari kwa kuinua ufaulu wa wanafunzi katika mitihani ya taifa kidato cha pili na nne, Halmashauri ya wilaya ya Msalala iliyopo mkoani Shinyanga kwa ufadhili wa mgodi wa Barrick Bulyanhulu, imeendesha mafunzo kwa walimu 336 wa masomo ya sanaa na Lugha, kuhusu namna ya kufundisha kwa kuwajengea umahiri wanafunzi.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo ya siku mbili , Afisa Elimu Halmashauri ya Msalala, Seleko Ntobi, amesema mafunzo waliyopatiwa walimu yatakuwa na manufaa makubwa katika sekta ya elimu na kuleta tija na matokeo mazuri .


"Kwa muda wa siku mbili tumepata mafunzo kutoka kwa timu ya wakufunzi wabobezi kutoka chuo cha ualimu SHYCOM, ambao wamekuwa msaada mkubwa sana kwa walimu wetu, kwani kabla ya mafunzo haya walikuwa hawana uelewa unaofanana katika kufundisha na kupima kwa kuzingatia umahili wa wanafunzi", alisema Ntobi.


Kwa Upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo ambaye alikuwa Mgeni rasmi katika hafla ya kufunga mafunzo hayo, Khamis Katimba, alisema baada ya Mafunzo hayo Halmashauri inatarajia kuona utofauti mkubwa wa ongezeko la ufaulu katika shule zote za Halmashauri hiyo.


"Nichukue nafasi hii kuwapongeza ndugu zetu wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu kwa kazi kubwa mnayoifanya hasa kwa kushirikiana na serikali katika masuala mbalimbali ya kimaendeleo lakini niwaombe walimu wote mliopata mafunzo haya yakalete tija kwa wanafunzi wetu lakini mkawe wazazi pia huko shuleni Unyanyasaji wa kijinsia hautakiwi", Katimba alisema.


Naye Mwakilishi wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu katika hafla hiyo, William Chungu alisema, Barrick itaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali kuboresha maisha ya wananchi hususani katika sekta za elimu na afya.

"Tunafurahi kuona jinsi Serikali inavyofanya jitihada za kuboresha maisha ya wananchi, nasi kama wawekezaji tutaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali husuani katika suala la elimu ikiwemo kufanikisha miradi ya ujenzi wa miundo mbinu ya shule ili kuwawezesha wanafunzi kusomea katika mazingira rafiki", alisema.

Nao baadhi ya walimu waliohudhuria na kushiriki mafunzo wamesema wamenufaika na wameahidi kwenda kuleta mabadiliko chanya katika ufundishaji na upimaji wa wanafunzi wanaowafundisha.

Barrick Bulyanhulu pia imekuwa ikitekeleza Mpango wa kuinua ufaulu shuleni wa wanafunzi wa sekondari (Performance Improvement Program (PIP) kwa kushirikiana na Halmashauri za Nyang’hwale na Msalala kwa lengo la kufanikisha kupata matokeo mazuri kwa kuongeza idadi ya ufaulu wa wanafunzi wilayani kwenye wilaya hizo kupitia fedha za uwajibikaji kwa jamii (CSR) zinazotolewa na mgodi huo.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger