Wednesday 1 December 2021

Vijana Watakiwa Kujitokeza Kupima UKIMWI

...


NA.MWANDISHI WETU
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama amewaasa vijana kujitokeza kupima Virusi vya UKIMWI ili kujua hali zao na kuishi kwa malengo.

Ametoa kauli hiyo  Novemba 30, 2021 wakati akihutubia vijana katika kuadhimisha siku ya vijana katika kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani tarehe 01 Disemba, 2021 yatakayofanyika katika Uwanja ya Ruanda Nzovwe Jijini Mbeya. Kaulimbiu ya Maadhimisho kwa mwaka huu inasema “Zingatia Usawa. Tokemeza UKIMWI, Tokomeza Magonjwa ya Mlipuko”.

Alieleza kuwa, Kauli mbiu ya mwaka huu inalenga kutoa msukumo kwa Watanzania wote kujitokeza kwa ajili ya upimaji wa hiari wa VVU baada ya ushauri nasaha, ikiwa ni pamoja na kuanza kutumia dawa za kufubaza VVU (ARV) mapema kwa watakaogundulika kuwa na mambukizo ya VVU. Kauli mbiu hii inakwenda sambamba na jitihada za nchi katika kufikia malengo ya Kidunia ya Sifuri TATU ambayo tumeyaridhia.

Akieleza umuhimu wa kundi la vijana nchini, alisema ni kundi linalotegemewa kwa asilimi kubwa hivyo ni vyema wakawa na desturi za kupima hali zao ili kuishi kwa malengo na kutimiza ndoto zao.

“Vijana ndio nguzo katika ujenzi wa Taifa imara. Katika Taifa letu vijana ni zaidi ya asilimia 68 ya nguvu kazi ya Taifa letu, hii ni kwa mujibu wa takwimu za makadirio ya ongezeko la idadi ya watu nchini ambayo imeonesha kuwepo na ongezeko kubwa la vijana na watoto, hivyo hakuna namna tunayoweza kufanya shughuli za maendeleo pasipo kutambua nafasi ya vijana ndani ya jamii yetu na kufahamu vipaumbele vyao ikiwa ni pamoja na afya bora,”alisema waziri Mhagama.

Waziri Mhagama alisema utafiti wa Viashiria vya UKIMWI wa mwaka 2016/17 hapa nchini, ulibaini kuwa moja ya makundi yaliyo nyuma katika kufikia malengo yaliyowekwa ni kundi la VIJANA ambapo inaonesha vijana wengi wenye umri wa miaka 15 hadi 24 hawajui hali zao za maambukizo ukilinganisha na watu wenye umri mkubwa. Hali hii inapelekea vijana hawa kutoanza dawa za ARV mapema kwani hawajui hali zao na hivyo kutoweza kufubaza VVU.

“Nitoe rai kwa vijana wote nchini, tujitokeze kwa wingi katika huduma za upimaji wa VVU kwa hiari zitolewazo sehemu mbalimbali nchini, ili wale wote watakaogundulika kuwa wana maambukizo ya VVU waweze kuanza dawa za ARV mapema na hivyo kutimiza kwa vitendo kauli mbiu ya mwaka huu,”alisisitiza

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jukwaa la Vijana wanaoishi na VVU Nchini Bi. Pudenciana Mbwiliza akitoa salamu wakati wa maadhimisho hayo alieleza ni vyema vijana wakajitokeza kupima na kujua hali zao ili kuendelea kuunga mkono jitihada za mapambano haya.

Aidha akibainisha changamoto zao alisema ni wakati sahihi kuwa na mikakati ya kuendelea kutokomea vitendo vya kikatili na kuendelea kuwafikiwa vijana kupitia miradi mbalimbli inayotekelea afua za masuala ya UKIMWI nchini.

Pia alizitaja changamoto wanazokabiliana nazi ikiwemo ya kasi ya maambukizi mapya hasa kwa wasichana walio katika umri balee, unyanyapaa katika jamii hususan ule wa mtu binafsi, ukatili wa kijinsia, ufuasi hafifu wa utumiaji wa dawa za ARV, elimu duni kwa vijana walio mashuleni hasa katika shule za bweni, matumizi yasiyosahihi ya kondom na mwamko mdogo wa watu kujitokeza kupima na kujua hali zao.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge inayoshughulikia masuala ya UKIMWI Mhe. Fatma Taufiq alipongeza jitihada zinazofanywa na Serikali katika mapambano dhiti ya UKIMWI na kuahidi kuendeleza ushirikiano kadiri inavyotakiwa.

“Kweli bajeti tunayoipitisha bungeni inafanya kazi kwa haya tuliyoona na mwitikio huu wa vijana na kuona kundi hili linashirikishwa kwa namna kubwa na hii ni ya kupongeza sana. Naamini Taanziania bila UKIMWI inawezekana na Tanzania bila unyanyapaa inawezekana,”alieleza Mhe. Fatma

Aliongezea kwamba, Kamati itaendela kuishauri Serikali kuwa na sera na sheria imara kuhakikisha kundi ka vijana linapata fursa nzuri na kuone namna bora ya kuweka mipango thabiti ili kuendela kulivusha kundi hili.


Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger