Saturday 6 June 2020

RC Gaguti Atoa Siku 7 Kurejeshwa Kwa Shilingi Milioni 224.

...
Na Allawi Kaboyo.
Mkuu wa Mkoa Kagera Brigedia Generali Marco Gaguti ametoa siku 7 kwa watumishi wa halmashauri ya wilaya Biharamulo waliokusanya fedha na kushindwa kuzipeleka Banki wawe wamezipeleka kabla hatua kali za kinidhamu hazijachukuliwa dhidi yao.

Gaguti ametoa agizo hilo wakati wakikao cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo lililolenga kujibu hoja za mthibiti mkuu wa hesabu za serikali CAG ambazo miongoni mwazo ni makusanyo ya fedha Zaidi ya shilingi milioni 224 ambazo hazikupelekwa bank.

Amesema kuwa licha ya halmashauri hiyo kufanya vizuri na kupata hati safi bado suala la ukusanyaji wa mapato ni changamoto ambapo ameongeza kuwa wapo watendaji ambao wanakusanya fedha lakini hawazipeleki Banki na kupelekea halmashauri kuendelea kuandamwa na mzimu wa kutofikia malengo ya ukusanyaji wa mapato ya ndani.

“CAG ametoa hoja mbalimbali kuhusu halmashauri hii na nyingi zinalalia masuala ya fedha, natoa siku saba kwa watendaji ambao wamehusika na kutopelekwa fedha hizi wawe wamezirejesha mara moja na kwenye hili sitanii kabisa tutakuja kuonana wabaya kwenye fedha za umma.” Amesema Gaguti.

Aidha amemuomba mwenyekiti wa halmashauri hiyo kuitisha kikao kingine maalumu ambacho kitakuwa na agenda za kuangalia mwenendo mzima wa watumishi ndani ya halmashauri hiyo ili hatua husika ziweze kuchukuliwa pale itakapostahili.

“Mwenyekiti nataka kabla ya baraza hili kumaliza muda wake niitiwe kikao kingine mahususi kwaajili ya madiwani pamoja na watumishi wote ili kuweza kuchukua hatua nyingine za kinidhamu kwa watumishi ambao wameonyesha vitendo vya ubadhilifu wa fedha za umma lakini na mienendo mibaya.” Alisisitiza Mkuu wa mkoa.

Kwaupande wao madiwani wakichangia kwa nyakati tofauti kwenye hoja za hizo za CAG wameitaka halmashauri kumalizia miradi mbalimbali ambayo wananchi tayari wameshaweka nguvu zao hasa vumba vya madarasa ili kusaidia watoto kusomea katika mazingira ambayo ni mazuri na salama kwaajili ya maisha yao ya baadae.

Madiwani hao wamesama kuwa halmashauri hiyo inatatizo la uhaba wa watendaji Zaidi ya 30 wa vijiji suala linalopelekea ukusanyaji wa mapato kuwa hafifu kwakuwa wanaopewa jukumu la kukusanya wengi wao hawana elimu juu ya mashine za pos zinazotumika kukusanyia mapato na kufanya kuwa changamoto ya kudumu.

Halmashauri ya wilaya Biharamulo ni miongoni mwa halmashauri 8 zinazouunda mkoa wa Kagera ambayo kwa kipindi cha miaka minne mfurulizo imepata hati safi licha ya kuwa na changamoto ya kufikia lengo la ukusanyaji wa mapato ya ndani hali ambayo mkuu wa mkoa ameagiza ishugulikiwae mara moja.


Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger