Monday 29 June 2020

Rais Magufuli Ampa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi Siku 7

...
Rais Magufuli  amempa siku saba Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi, amkabidhi  hati ya shamba lenye ukubwa wa hekta 5,000, linalomilikiwa raia wa kigeni wilayani Kilosa, Mkoa wa Morogoro. 
 
Rais Magufuli ametoa agizo hilo leo Jumatatu tarehe 29 Juni 2020, baada ya kupokea malalamiko ya mgogoro wa ardhi, kutoka kwa wananchi wa Kibamba, wilayani Kilosa.

Amemuagiza Waziri Lukuvi aliyekuwepo kwenye msafara wake kumkabidhi hati ya shamba hilo, ili aligawe upya, kisha  sehemu yake wapewe wananchi wa Kibamba, kwa ajili ya kumaliza changamoto ya mgogoro wa ardhi.

Rais Magufuli amesema katika uongozi wake, atahakikisha analinda maslahi ya wananchi wanyonge, pamoja na kuwadhibiti wenye nguvu ambao wamekuwa wanadhurumu haki za wanyonge.

“Mnakodishiwa mashamba sababu hati ni za wakubwa, nataka nilale nao hao wakubwa, nimesema siku saba waziri pamoja na mkuu wa mkoa ataleta hati, yale mashamba yakufuta, sababu kwa mujibu wa sheria ardhi iko chini ya rais, na mimi nitaenda na watu wanyonge,” amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli amewataka wananchi wa Kibamba, kutumia vyema mashamba watakayopewa.

“Naweza futa nusu au kutokana na mapendekezo nitakayopewa nitayagawa kwenu. Mjipange vizuri kugawiwa kwenu isije kuwa chanzo cha kupigana, mtumie uongozi mlio nao kila mmoja apate kipande, kutakuwa sehemu ya wafugaji na wakulima sababu wote tunategemeana,” amesema Rais Magufuli.


Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger