Tuesday 30 June 2020

PROF. MAKUBI AIPONGEZA TMDA KUZINDUA TOLEO JIPYA LA MKATABA WA HUDUMA KWA WATEJA

...
Mganga Mkuu wa Serikali Profesa Abel Makubi akikata Utepe kuashiria uzinduzi wa mkataba wa huduma kwa Wateja toleo la Nne wa TMDA, Kulia ni Kaimu Mkurgenzi Mkuu wa TMDA, Adam Fimbo na kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri wa Wizara (MAB) kwa TMDA, Eric Shitindi. Hafla iliyofanyika 29 Juni jijini Dar es Salaam.



Na Andrew Chale, Dar es salaam

MGANGA Mkuu wa Serikali, Profesa Abel Makubi amepongeza  Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), kwa kuzindua mpango mpya wa Huduma kwa Wateja ambao unaongeza ufanisi katika shughuli zake za kila siku baina ya taasisi na wateja wake.

Prof. Makubi amesema hayo jana 29 Juni, Jijini Dar es Salaam wakati akizindua toleo jipya la Nne la Mkataba wa Huduma kwa wateja lililoshuhudiwa pia na wadau mbalimbali wakiwemo wawakilishi kutoka Serikali, Wadau na washirika wa mradi wa FASTER (CRS, CHAI  na CSSC).

Akizungumza katika tukio hilo la uzinduzi, Prof. Makubi alitoa wito kwa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Afya kuwa na mkataba wa huduma kwa wateja kama wafanyavyo TMDA.

"Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jami, Jinsia, Wazee na Watoto inaendelea kutoa rai kwa Vituo vya Afya na Hospitali zote za Wilaya, Mkoa na Rufaa kuwa na dawati la Mkataba wa huduma kwa wateja.

"Taasisi zote zilizo chini ya Wizara ya Afya zinapaswa kuwa na dawati la mkataba wa huduma kwa  Wateja  ili kurahisisha utoaji wa huduma bora  kwa wananchi." Alisema Prof. Makubi.

Aliongeza kuwa TMDA imekuwa na mipango mizuri katika utoaji wa  huduma kwa kuzingatia muda katika utoaji wa leseni kwa wadau mbalimbali kama ilvyoelezwa katika taarifa.

"TMDA imekuwa na mifumo mizuri ya viwango ambapo Shirika la Afya Duniani inatambua pamoja na jumuiya  mbalimbali hii inatokana na mikakati ya watendaji wa taasisi waliojiwekea ya kuhakikisha wanakwenda kutatua matatizo ya  huduma katika utoaji wa huduma zake" Alisema Prof. Makubi.

Kwa upande wake Kaimu Mkurgenzi Mkuu wa TMDA, Adam Fimbo alisema waliweza kufanya mapitio ya Mkataba wa Huduna kwa wateja 'Clients Service Charter'  la kuandaa toleo la Nne (4) baada ya kutekeleza ule ulioandaliwa mwaka 2016.

"Mapitio ya Mkataba uliopita umechagizwa na mabadiliko mbalimbali  yamejitokeza katika kipindi cha miaka minne. Mabadiliko hayo ni pamoja na kubadilika majukumu ya iliyokuwa TFDA kwa masuala ya udhibiti  wa vyakula na vipodozi yalihamishiwa Shirika la TBS na kupelekea kubadilika kwa jina na kuwa TMDA." Alisema Fimbo

 Adam Fimbo alieleza kuwa wamefanikiwa kuweka mifumo ya TEHAMA ambapo umefanywa na TMDA na kurahisisha utoaji wa huduma.

"Toleo hili jipya la nne la mkataba wa huduma kwa wateja limepitiwa kwa kina na kupunguza maradufu muda wa utoaji ukilinganisha na Mkataba uliopita wa mwaka 2016.

Awali ilikuwa muda wa kusajili dawa zinazotoka nje ya nchi ulikuwa siku 240 kwa sasa umepungua hadi siku 180 za kazi. 

"Muda wa kusajili dawa zinazotengenezwa ndani ya nchi ulikuwa siku 120 Sasa umepungua hadi siku 60 na hio ni nusu ya siku zilizotengwa hapo awali. Muda wa usajili wa maeneo ya biashara za bidhaa zinazodhibitiwa na TMDA umepunguzwa kutoka siku 10 hadi 8.

"Pamoja na kupunguza siku za kuthamini na kusajili dawa, tumeweka pia utaratibu  rahisi wa kusajili dawa ambazo zimekwishasajiliwa kupitia Jumuiya zetu za Kikanda kama EAC na SADC pamoja na Shirika la Afya Duniani (WHO)." Alisema Fimbo. 

Aidha alipongeza wadau na washirika wa Maendeleo kupitia mradi wa FASTER, ambao ni Catholic Relief Services, CHAI na Christian Social Services Commission (CSSC) ambao walifanikisha kutolewa kwa mktaba huo wa huduma kwa wateja.

Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger