Sunday 3 December 2023

WAZIRI PINDI CHANA ASISITIZA UADILIFU UTEKELEZAJI WA MIRADI YA MAENDELEO

...


Waziri Wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi H. Chana akizungumza Disemba 3,2023 jijini Dodoma ,wakati akizindua Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu Kitaifa, yanaongozwa na kauli mbiu ya ‘’Mapambano Dhidi ya Rushwa ‘’Zingatia Maadili, Utu, Uhuru na Haki kwa Watu Wote kwa Maendeleo Endelevu’
Mkurugenzi wa Elimu kwa Umma Bw. Joseph Mwaiswelo akizungumza Disemba 3,2023 jijini Dodoma ,wakati wa uzindua Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu Kitaifa, yanaongozwa na kauli mbiu ya ‘’Mapambano Dhidi ya Rushwa ‘’Zingatia Maadili, Utu, Uhuru na Haki kwa Watu Wote kwa Maendeleo Endelevu’

Na Okuly Julius-Dodoma

Waziri Wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi H. Chana amesema uwepo wa vitendo vya rushwa inaifanya Serikali kushindwa kutekeleza ipasavyo jukumu lake la kuwahudumia wananchi ipasavyo na kusababu miradi ya maendeleo kushindwa kufanyika au kufanyika kwa kiwango cha chini kutokana na fedha zinazotengwa kutekeleza miradi hiyo, kuingia katika mikono ya watu wachache.


Balozi Chana ametoa kauli hiyo Disemba 3,2023 jijini Dodoma ,wakati akizindua Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu ambapo amesema serikali kupitia TAKUKURU imekuwa ikifanya ufuatiliaji wa katika miradi mbalimbali ya maendeleo ili kukabiliana na ubadhirifu ikiwemo rushwa.


"Serikali yetu imekuwa ikifanya juhudi kubwa, kudhibiti rushwa nchini na ninyi nyote ni mashahidi kwa kuwa mlimsikia Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiielekeza TAKUKURU kufanya ufuatiliaji katika miradi mbalimbali ya maendeleo ili kukabiliana na ubadhirifu ikiwemo rushwa. Vita hii bado ni kubwa hivyo, nasi wanahabari tujitahidi kutumia vizuri kalamu zetu katika kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa kushiriki kwa vitendo katika kukataa na kufichua vitendo vya rushwa,"amesema Balozi Chana


Waziri huyo ameongeza kuwa Maadhimisho ya mwaka huu yanaadhimishwa sambamba na maadhimisho ya miaka 75 ya Tamko la Haki za Binadamu (‘’Universal Declaration of Huma Rights’’ ,tamko hilo tangu kutangazwa kwake tarehe 10 Desemba,1948 limeweka msingi wa mikataba mingine ya Haki za binadamu ambayo imefuata. Ni tamko ambalo limeainisha haki za kiraia, kisiasa, kiutamaduni na kiuchumi.


Amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zimeliweka Tamko hili katika Katiba zao ambapo Tanzania ni ibara ya 9 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaeleza kwamba Mamlaka ya Nchi na vyombo vyake vyote vinawajibika kuelekeza sera na shughuli zake zote katika lengo la kuhakikisha kwamba heshima ya binadamu inahifadhiwa na kudumishwa kwa kufuata Kanuni za Tangazo la Dunia kuhusu Haki za Binadamu.


"Tunapoadhimisha Siku hii muhimu ya Maadili na Haki za Binadamu ni jambo muhimu tukumbuke kuwa tunapaswa kutekeleza wajibu wetu kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa na hivyo, kuepuka kuathiri haki za binadamu kwa kushiriki rushwa. Wakati mwingine haki hizi za binadamu huathiriwa na tabia za baadhi ya watendaji wasio waadilifu ambapo rushwa huwa kigezo cha mtu kupata haki ya msingi,"ameeleza Balozi Chana


Akitoa taarifa kuhusu shughuli mbalimbali zitakazofanyika kuelekea kilele cha Maadhimisho hayo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU),Mkurugenzi wa Elimu kwa Umma Bw. Joseph Mwaiswelo amesema kuwa Desemba 4,2023 kutakuwa na Jukwaa la Kitaifa la Wadau wa Juhudi dhidi ya Rushwa ambapo mada maalum itawasilishwa na kujadiliwa katika jukwaa hilo ambalo ni matarajio kuwa litachangia kuimarisha misingi ya uwajibikaji na uadilifu katika sekta ya umma na sekta binafsi kwa ajili ya maendeleo endelevu ya Taifa .


Mwaiswelo amesema shughuli ya tatu iliyopangwa kufanyika wakati wa maadhimisho hayo ni kuwa na Wiki ya Huduma kwa Umma itakayoanza tarehe 5 hadi tarehe 10 Desemba, 2023 katika viwanja ya Nyerere, maarufu Nyerere Square ambapo wiki hiyo itatumika kutoa huduma mbalimbali ikiwamo elimu kuhusu majukumu ya Taasisi zitakazoshiriki, kujibu maswali au kutoa ufafanuzi kwa wananchi na huduma za afya.


Kilele cha Maadhimisho ya mwaka huu itakuwa Disemba 10, 2023 katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma na yanaongozwa na kauli mbiu ya ‘’Mapambano Dhidi ya Rushwa ‘’Zingatia Maadili, Utu, Uhuru na Haki kwa Watu Wote kwa Maendeleo Endelevu’. Kauli mbiu hii imekuja wakati muafaka kwani inatufanya tutafakari kwamba ili tupate maendeleo lazima tuzingatie maadili, utu, uhuru na haki za binadamu kwa watu wote ambayo ni masuala ya msingi sana kwa ustawi wa taifa letu na watu wake.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger