Saturday 29 August 2020

KISHINDO DODOMA DK.MAGUFULI ATAJA ATAYAKAYOANZA NAYO

...
*Ni iwapo watapata ridhaa CCM kuongoza tena kwa miaka mitano ijayo
 *Kununua ndege nyingine mpya tano kuimarisha usafiri wa anga nchini



Na Said Mwishehe, Michuzi TV-Dodoma

CHAMA Cha Mapinduzi(CCM) kimezindua rasmi kampeni zake katika uchaguzi mkuu mwaka huu huku mgombea wake wa urais Dk.John Magufuli akitumia nafasi hiyo kuelezea mambo kadhaa yenye tija kwa Taifa hili iwapo watapata ridhaa tena ya kipindi cha miaka mitano ijayo.

Dk.Magufuli ambaye ametumia nafasi huyo kuzungumzia Ilani ya Uchaguzi Mkuu yaCCM ya mwaka 2020-2025 amewaomba Watanzania wa vyama vyote, dini zote na makabilia yote kuhakikisha wanakipa ushindi Chama chake ili kuendeleza yale ambayo wameyaanza katika miaka mitano ya kwanza.

Katika ufunguzi huo wa kampeni uliofanyika Uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma na kuhudhuriwa na maelfu ya wananchi wa Jiji hilo na mikoa jirani ,Dk.Magufuli ametoa hotuba iliyojitosheleza kwa kuelezea hatua kwa hatua mambo ambayo Serikali yake imefanya na yale wanayotarajia kuyafanya iwapo watapewa ridhaa ya kushika dola.

Mgombea huyo wa CCM ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amesema katika miaka mitano ya kwanza wamefanya mambo makubwa yakiwemo ya kurudisha nidhamu katika utumishi wa umma.

Pia kukomesha rushwa, kudhibiti rasilimali za nchi ili ziwanufaishe Watanzania pamoja na kuboresha huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo sekta ya afya,elimu, maji, barabara, usafiri wa anga na sekta nyingine muhimu.

“Katika miaka mitano ya kwanza ya uongozi wetu tumejitahidi kwa kadri ya uwezo wetu na sasa tunakuja kwenu tena watanzania kuomba ridhaa yenu mtupe tena miaka mitano mingine.

“Ili tuendelee na kazi ya kuwatumikia maana hatuna hakika kama mkiwapa wengine wataweza kuifanya kazi hii nzuri ambayo tumeianza na tunataka kuimalizia,”amesema Dk.Magufuli

Hata hivyo ameeleza alivyofurahishwa na na wananchi wa Dodoma kwa kujitokeza kwa wingi katika uzinduzi huo wa kampeni, hivyo amewaahidi atakapochaguliwa kazi ya kwanza akiwa madarakani itakuwa ni kuendelea kulijenga Jiji la Dodoma.

“Wananchi wa Jiji la Dodoma ambako ndiko makao makuu ya Serikali niwahakikishie tutaendelea kuijenga Dodoma, tutajenga uwanja mkubwa wa michezo ambao utawezesha wananchi wengi kuingia na kutosha tofauti na uliopo sasa,”amesema.

Pia amesema katika Jiji la Dodoma utajengwa uwanja mkubwa wa ndege wa kilometa tatu na hivyo ndege zote kubwa zitatokea Dodoma kwenda  nchi za Ulaya kwani fedha zipo na Tanzania ni tajiri.

Hata hivyo amesema mwaka2015 Watanzania walitaka mabadiliko na hivyo baada ya kuingia madarakani walianza kufanya mabadiliko makubwa katika maeneo mbalimbali yakiwemo ya kusimamia uwajibikaji , kudhibiti mianya ya upotevu wa makusanyo ya fedha yatokanayo na kodi.

Ameongeza katika mabadiliko hayo Serikali anayoingoza ilisimama imara kuhakikisha sekta za ajira zinaimarishwa ili kuotoa ajira kwa Watanzania.” Tutahakikisha zinapatikana ajira milioni 8 ili kukuza uchumi kupitia ajira hizo.”

Pamoja na kuwepo kwa mambo mbalimbali ya kimaendeleo ambayo watafanya baada ya kuchaguliwa kwa mara nyingine tena, Dk.Magufuli amesema wataendelea kuimarisha usafiri wa anga kwa kununua ndege nyingine mpya tano.

Kati ya ndege hizo mbili zitakuwa za masafa marefu,mbili za masafa ya kati na ndege moja itakuwa ya mizigo.Kwa sasa tayari kuna ndege mpya nane na hivyo itafanya kuwa na jumla ya ndege 11.



Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger