Thursday 31 October 2019

Waziri Hasunga Awaasa Watumishi Wizara Ya Kilimo Kuwa Waadilifu

...
Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Dodoma
Watumishi wa Wizara ya Kilimo wameaswa kuwa waadilifu na kuzingatia ubora wa kazi wakati wanatoa huduma kwa wananchi.

Mwito huo umetolewa na Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) jana tarehe 30 Octoba 2019 wakati akizungumza na watumishi Jijini Dodoma alipotembelea ofisi za wizara hiyo eneo la Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).

Mhe Hasunga amesema kuwa udilifu, nidhamu na weledi kwa watumishi wa umma ni kinga dhidi ya matumizi mabaya ya ofisi za umma na ni moja kati ya njia zinazowawezesha watumishi wa umma kuwa wachapakazi hodari.

“Kiwango cha juu cha Ubora wa kazi zetu na utendaji wa kazi unaozingatia weledi vitaweza tu kufikiwa kwa kuajiri watumishi wenye sifa stahiki, maadili, na bidii ya kuchapa kazi na wanaoweza kwenda sambamba na kasi kubwa ya mageuzi katika wizara ya kilimo,” Alisisitiza Mhe Hasunga

Alisema kuwa utekelezaji mzuri wa majukumu yao ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi yam  mwaka 2015-2020.

Amewataka watumishi hao kusimama imara katika kufanya kazi na kutumia weledi wao kwa ajili ya kuwatumikia wananchi na kwamba uadilifu ndiyo silaha muhimu katika kufanya kazi ya Umma.

Amesema mtumishi atakayetumia vibaya rasilimali za serikali atahesabika adui namba moja wa Serikali na eneo analofanyia kazi huku akibainisha kuwa mtumishi wa aina hiyo kamwe hatohamishwa badala yake ataachishwa kazi.

Ziara ya waziri wa Kilimo kukutana na watumishi hao ilikuwa na lengo la kusalimiana na kusikiliza changamoto zinazowakabili katika utendaji kazi.


Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger