Thursday 31 October 2019

TRENI YASHIKA MOTO NA KUUA WATU 65

...
Takriban abiria 65 wamefariki dunia wakati treni iliyokuwa ikisafiri kutoka mji wa Karachi Pakistan kuelekea Rawalpindi iliposhika moto.

Waziri wa reli, Sheikh Ahmed, alisema kwamba moto huo ulisababishwa na kulipuka kwa mtungi wa gesi uliokuwa ukitumiwa na abiria kupikia kiamsha kinywa mwendo wa asubuhi.

Moto huo unadaiwa kusambaa hadi katika mabehewa matatu, kulingana na maafisa walionukuliwa katika vyombo vya habari vya eneo hilo.

Waathiriwa wengi walifariki walipojaribu kuruka kutoka kwa treni hiyo iliokuwa ikichomeka.

Watu wengine 30 wameripotiwa kujeruhiwa na maafisa wanasema kwamba idadi ya waliofariki huenda ikaongezeka.

"Majiko mawili aina ya stove yalilipuka. Walikuwa wakipika , walikuwa na mafuta ya kupikia ambayo yalichochea moto huo kuongezeka'', Sheikh Rashid Ahmed alisema.

Abiria wanaoingia na stove katika treni ili kupika chakula wakati wa safari ndefu ni swala la kawaida waziri huyo aliongezea.

Aliongezea kwamba abiria wengi walikuwa wakielekea katika kongamano lililoandaliwa na vuguvu la dhehebu la Kisuni Tablighi Jamaat.

Ajali hiyo ilitokea karibu na Rahim Yar Khan kusini mwa mkoa wa Punjab. Treni hiyo iliokuwa ikisafiri kutoka Karachi kupitia maeneo mengi ya Pakistan hadi Rawalpindi inaitwa Tezgam mojawapo ya treni za zamani ambayo ni maarufu sana.

Inahudumu kila siku na inachukua saa 25 na nusu.

Pakistan ina historia ya ajali za gari moshi zinazosababisha maafa mengi. Waathiriwa huwa wengi kwa kuwa treni hizo hubeba watu wengi zaidi ya viwango vyao.

Tarehe 11 mwezi Julai , watu walifariki katika ajali , huku wengine wanne wakifariki katika ajali nyengine mwezi Septemba.

Mwaka 2007, takriban watu 56 waliuawa na wengine zaidi ya 120 kujeruhiwa katika ajali karibu na eneo la Mehrabpur.

Mwaka 2005, zaidi ya watu 130 waliuawa wakati treni tatu zilipogongana katika mkoa wa Sindh katika kile kilichotajwa kuwa ajali mbaya zaidi inayohusisha treni kuwahi kutokea.
CHANZO - BBC
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger