Monday 4 May 2015

Chadema yamng’ang’ania JK kuhusu Uchaguzi Mkuu

...
INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
Viongozi wa Chadema wakiomba dua kabla ya kuanza kwa kikao
cha Kamati Kuu ya chama hicho kilichofanyika Dar es Salaam jana. Kuanzia kulia ni Makamu Mwenyekiti, Profesa Abdallah Safari, Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, Katibu Mkuu Dk Willibrod Slaa na Naibu Katibu Mkuu (Zanzibar), Salum Mwalimu. Picha na Venance Nestory 
 
 

Dar es Salaam. Licha ya Rais Jakaya Kikwete kusema hana mpango wa kuongeza muda na kuwa Uchaguzi Mkuu utafanyika Oktoba, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimezidi kuonyesha wasiwasi wake kikieleza kuwa hakuna dalili za uchaguzi huo mwaka huu.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alikieleza kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho kuwa uchaguzi huo unaweza kuahirishwa kama ilivyotokea kwenye Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa.
Kikatiba, uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani unatakiwa kufanyika Jumapili ya mwisho ya Oktoba ambayo itakuwa Oktoba 25, mwaka huu ikiwa ni mwaka wa tano tangu kuchaguliwa kwa Serikali iliyopo madarakani.
Katika kipindi hicho, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilitakiwa kurekebisha mara mbili Daftari la Kudumu la Wapigakura lakini haijafanya hivyo hata mara moja na hii ya sasa inayoendelea katika baadhi ya mikoa bado inasuasua.
Kutokana na kusuasua huko, NEC ililazimika kuahirisha Kura ya Maoni iliyokuwa imepangwa kufanyika Aprili 30, hadi tarehe itakayotangazwa baadaye, licha ya awali kuelezwa mara kwa mara na tume yenyewe au viongozi wa Serikali kuwa kura hiyo ilikuwa palepale.
Ni kutokana na hali hiyo, Chadema na vyama washirika vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), vilieleza wasiwasi wa kuwapo uwezekano wa kuahirisha uchaguzi mkuu kwa kisingizio cha kutokamilika uandikishaji wapigakura kama ilivyofanyika kwa kura ya maoni.
Lakini akihutubia siku ya wafanyakazi (Mei Mosi), mjini Mwanza, Rais Kikwete alieleza kuwashangaa wapinzani hao, akisema ni aibu kwao kuzua jambo ambalo halipo, kwa kuwa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba uko palepale na hana mpango wa kuongeza muda.
Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu, Damian Lubuva jana alisisitiza kauli ya Rais akisema uchaguzi huo utafanyika kama Katiba inavyoeleza (wiki ya mwisho ya Oktoba), huku Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Uratibu na Bunge, Jenista Mhagama akisema uandikishaji unavyoendelea ni kielelezo kwamba uchaguzi utafanyika kama ulivyopangwa.
Wasiwasi wa Mbowe
Akifungua kikao cha siku mbili cha Kamati Kuu jana, Mbowe alisema: “Wote hatujui kama uchaguzi mkuu upo mwaka huu, waziri mkuu anasema upo, NEC wanasema upo lakini mazingira hayaonyeshi kwamba utakuwapo mwaka huu.”
Alisema bado uandikishaji wapigakura unasuasua na mazingira hayaonyeshi kwamba utakamilika kabla ya siku ya uchaguzi inayoelekezwa na Katiba.
Alisema hata kwenye kura za maoni ya Katiba Inayopendekezwa, mazingira yalionyesha kwamba isingewezekana ifanyike Aprili 30, mwaka huu kama Serikali ilivyotangaza.
  
BONYEZA HAPO CHINI KUSOMA ZAIDI
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger