Sunday 30 June 2024

THPS YASISITIZA UMUHIMU WA KUWEKEZA KWENYE KINGA NA TIBA DHIDI YA DAWA ZA KULEVYA

...

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa akisikiliza maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa THPS, Dkt. Redempta Mbatia
kuhusu huduma za Tiba kwa Waraibu (MAT) na huduma za Kinga, Tiba na Matunzo ambazo zinatolewa na THPS katika mikoa ya Tanga, Pwani, Shinyanga na Kigoma alipotembelea Banda la THPS kwenye maonesho ya kilele cha maadhimisho ya kitaifa ya siku ya kupiga vita dawa za kulevya duniani yaliyofanyika kuanzia Juni  30,2024 katika viwanja vya Nyamagana Jijini Mwanza - Picha na Kadama Malunde
Mkurugenzi Mtendaji wa THPS, Dkt. Redempta Mbatia akimwelezea Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa kuhusu huduma za Tiba kwa Waraibu (MAT) na huduma za Kinga, Tiba na Matunzo ambazo zinatolewa na THPS katika mikoa ya Tanga, Pwani, Shinyanga na Kigoma.


Siku ya Kimataifa ya Kupiga Vita Matumizi na Usafirishaji wa Dawa za Kulevya Duniani huadhimishwa tarehe 26 Juni kila mwaka ili kuimarisha hatua na ushirikiano katika kushinda vita dhidi ya dawa za kulevya.

Hata hivyo, maadhimisho ya kitaifa kwa mwaka huu 2024 yamefanyika katika viwanja vya Nyamagana Jijini Mwanza kuanzia tarehe 27 hadi 30 Juni 2024 chini ya kaulimbiu: 'Wekeza kwenye Kinga na Tiba dhidi ya Dawa za Kulevya'.


Tanzania Health Promotion Support (THPS) iliungana na Serikali na wadau wengine katika kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kuwekeza katika huduma ya tiba kwa waraibu (MAT) na huduma za kinga, matunzo na matibabu ya maambukizi ya VVU na Kifua kikuu.


Katika hafla hiyo ya siku nne, shughuli mbalimbali ziliandaliwa kwa ajili ya kuelimisha jamii kuhusu madhara ya matumizi ya dawa za kulevya na umuhimu wa kuwekeza katika mikakati ya kujikinga. 

Mradi wa THPS Afya Hatua unaofadhiliwa na Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kukabiliana na Ukimwi (PEPFAR) kupitia Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa cha Marekani (U.S. CDC) umekuwa ukishirikiana na wadau mbalimbali katika kutoa huduma za MAT na huduma za Kinga, Tiba na Matunzo katika mikoa ya Pwani na Tanga.

"Tumefanikiwa kuandikisha watumiaji 2,442 wa dawa za kulevya katika mpango wa MAT, na kati yao 1,426 bado wanaendelea na matibabu", amesema Dkt. Redempta Mbatia, Mkurugenzi Mtendaji wa THPS. 


Pamoja na huduma za MAT, waraibu wote waliojiandikisha waliweza kupata ushauri nasaha na upimaji wa VVU. Kati ya hao, watumiaji dawa za kulevya 122 waligundulika kuwa na VVU na mara moja walianza kupata huduma za tiba na matunzo katika kliniki za tiba na matunzo (CTC) zilizopo maeneo yao. Huduma hizi zinasaidia sio tu kuokoa maisha bali pia kuboresha ustawi wa jamii tunazohudumia”, amesema.


Mradi wa Afya Hatua umekuwa ukiziwezesha Asasi za Kiraia (AZAKI) katika mikoa ya Tanga na Pwani katika utambuzi wa waraibu wa dawa za kulevya, kuwapatia elimu na kuwaunganisha na huduma za MAT. 

Dkt. Mbatia amesema kuwa kila mwezi AZAKI hizo zimefanikiwa kuandikisha wastani wa watumiaji wa dawa za kulevya wapya 30 na kuwarudisha tena watumiaji dawa za kulevya 45 ambao awali walikuwa wameacha matibabu. Utaratibu huu umesaidia kupunguza changamoto ya uraibu wa dawa za kulevya na kudhibiti maambukizi ya VVU katika mikoa hiyo. 

Katika hafla hii ya maadhimisho ya kupiga vita dawa za kulevya duniani, wanufaika wa huduma za MAT wameshiriki na kutoa ushuhuda wa jinsi huduma hizi zilivyotumika kama njia ya kuokoa maisha, zikiwasaidia kurejesha udhibiti wa maisha yao kutoka kwenye uraibu. 

Kupitia elimu, uhamasishaji, na ushirikishwaji wa jamii, inawezekana kushishinda vita dhidi ya dawa za kulevya.

Akizungumza wakati wa kilele cha Maadhimisho ya Siku ya kupiga vita dawa za kulevya, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa amesema serikali inaendelea na jitihada za kupambana na dawa kulevya hivyo kuwataka wadau kuongeza nguvu za pamoja.


" Dawa za kulevya ni janga,zina madhara makubwa kiafya na kiuchumi ni lazima litokomezwe.

Nitoe wito kwa vijana tuachane na dawa za kulevya, tufanye shughuli zingine za kujenga uchumi..Mamlaka ya kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), mnafanya kazi nzuri, endeleeni kutekeleza majukumu yenu, tunataka dawa za kulevya zipotee kabisa Tanzania", ameongeza Mhe. Majaliwa.


"Katika mapambano haya sisi serikali hatufanyi kazi peke yetu, tunawashukuru sana PEPFAR, ICAP, CDC, THPS hawa ni wadau wetu wakubwa tunafanya kazi nao vizuri katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya. Serikali itaendelea kushirikiana nanyi ili kuhakikisha vijana wetu wanabaki salama", amesema Mhe. Waziri Mkuu.


Kuhusu THPS

Tanzania Health Promotion Support (THPS) ni asasi isiyo ya kiserikali iliyoanzishwa mwaka 2011, chini ya Sheria ya asasi zisizo za kiserikali nambari 24 ya 2002.

THPS inafanya kazi kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania kupitia Wizara za Afya za Tanzania Bara na Zanzibar; Wizara ya Jinsia, Vijana, Wazee na Makundi Maalum; Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Kwa ufadhili wa Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Misaada ya UKIMWI (PEPFAR) kupitia Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (U.S. CDC), THPS inatekeleza afua mbalimbali za VVU/UKIMWI; Kifua kikuu; kuzuia ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto; huduma za afya ya uzazi, uzazi, watoto wachanga, watoto na vijana; mifumo ya habari ya maabara na usimamizi wa afya, na UVIKO-19.

Kuhusu mradi wa CDC/PEPFAR Afya Hatua (Oktoba, 2021- Septemba, 2026)

Mradi huu unalenga kutoa huduma jumuishi katika vituo vya afya (Kigoma, Pwani, Shinyanga na Tanga) na katika jamii (Kigoma, Pwani na Tanga). 

Huduma hizi ni pamoja na matibabu na matunzo ya watu wanaoishi na VVU, huduma za kitabibu za tohara kwa wanaume katika mikoa ya Kigoma na Shinyanga na programu ya DREAMS kwa wanawake katika mkoa wa Shinyanga.

Utafiti wa Ustawi na Afya wa Vijana na Watoto nchini Tanzania (WHYS 2024)

Utafiti huo unalenga kuelewa aina mbalimbali za ukatili, maambukizi ya VVU, na uhusiano wake na ukatili miongoni mwa vijana wenye umri wa miaka 13-24 Tanzania Bara na Zanzibar.

  

Mkurugenzi Mtendaji wa THPS, Dkt. Redempta Mbatia akimwelezea Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa kuhusu huduma za Tiba kwa Waraibu (MAT) na huduma za Kinga, Tiba na Matunzo ambazo zinatolewa na THPS katika mikoa ya Tanga, Pwani, Shinyanga na Kigoma

 Picha na Kadama Malunde
Mkurugenzi Mtendaji wa THPS, Dkt. Redempta Mbatia akimwelezea Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa kuhusu kuhusu huduma za Tiba kwa Waraibu (MAT) na huduma za Kinga, Tiba na Matunzo ambazo zinatolewa na THPS katika mikoa ya Tanga, Pwani, Shinyanga na Kigoma
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa (kushoto) akisikiliza maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa THPS, Dkt. Redempta Mbatia 
kuhusu huduma za Tiba kwa Waraibu (MAT) na huduma za Kinga, Tiba na Matunzo ambazo zinatolewa na THPS katika mikoa ya Tanga, Pwani, Shinyanga na Kigoma
alipotembelea Banda la THPS kwenye maonesho ya kilele cha maadhimisho ya kitaifa ya siku ya kupiga vita dawa za kulevya duniani yaliyofanyika kuanzia Juni  30,2024 katika viwanja vya Nyamagana Jijini Mwanza



 

Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger