Tuesday 19 April 2016

Aliyemtukana Rais Magufuli Aachiwa kwa Dhamana

...
INNOCENT-THE BLOGGER-BOY
HAKIMU Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Augustine Rwezile jana amempa dhamana aliyemtukana Rais John Magufuli, Isack Emiliy (40) ambaye ni mkazi wa Olasiti jijini Arusha.

Hakimu Rwezile alitoa uamuzi wa dhamana dhidi ya Emiliy baada ya mahakama hiyo kusema haioni sababu za kisheria inayomzuia mshtakiwa huyo kupata dhamana kwani kosa analoshtakiwa nalo lina dhamana kisheria.

Alisema ili mahakama imnyime Emiliy dhamana ni lazima upande wa mashtaka ulete ushahidi mahakamani hapo unaoonesha kama mshtakiwa akipewa dhamana atadhurika huko uraiani au la. Alisema mahakama haichukulii taarifa za maneno bali ushahidi ndio utakaoonesha kama mshtakiwa huyo akipewa dhamana ataweza kudhurika huko uraiani au la.

Alisema kwa mujibu wa kifungu cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai namba 148 kifungu kidogo cha 5(i -e), mahamaka ndio itakayothibitisha kama mshtakiwa akipewa dhamana kutokana na kosa hilo anaweza kupata madhara uraiani au la, lakini kwa sababu upande wa mashtaka haukutoa uthibitisho huo kwa maandishi bali umetoa kwa maneno basi mahakama hiyo inamwachia kwa dhamana mshtakiwa huyo.

“Mahakama haichukulii maneno maneno ndio yaongoze kumpa dhamana mshtakiwa bali ushahidi wa maelezo ndio unaweza kumsababishia mshtakiwa kupewa dhamana au la hivyo nakupa dhamana uwe na madhamini wawili ambao wataweza kusaini bondi ya Sh milioni tano kila mmoja pamoja na kuonesha mahakamani hapa vitambulisho vinavyokubalika kisheria,” alisema hakimu huyo.

Baada ya uamuzi huo, Wakili wa mshtakiwa Mosses Mahuna alidai mahakamani hapo kuwa wapo tayari kwa uamuzi wa dhamana ya mshtakiwa huyo na baadaye wadhamini wa mshtakiwa huyo walitimiza masharti ya dhamana yake. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Mei 17, mwaka huu.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger