Monday, 31 December 2018

ZITTO KABWE AANIKA ORODHA YA VITABU 49 ALIVYOSOMA MWAKA 2018

Tangu Mwaka 2012 nimekuwa naorodhesha vitabu nilivyosoma katika mwaka. Si vitabu vyote huviweka hapa kwani vingine huwa nasoma na kuviacha njiani ama kutopendezwa navyo au kwa kusahau tu. 

Vitabu vingine huwa vitabu rejea na huvirudia kwa ajili ya mafunzo ili kufanya maamuzi Fulani Fulani au kwa ajili ya ibada (kwa mfano Quran) au kwa sababu nyenginezo. Nafurahi kuwa hivi sasa kwenye mitandao duniani kote watu wamekuwa wakiorodhesha vitabu ili kujengana katika utamaduni wa kusoma. Barack Obama yeye alianza kuweka orodha yake mwaka 2015 na tayari ameshaweka orodha ya mwaka huu. Obama pia huweka orodha ya muziki aliyopenda mwaka huo. Inavutia.

Mwaka huu nimesoma vitabu 49 (kutoka vitabu 36 + 3 vya mwaka 2017). Wakati natoa orodha yangu 23/12/2017 nilikuwa bado nasoma riwaya za Jumba Maro ya Ally Saleh na The Feast of the Goat cha Mario Vargos Llosa ambazo nilizimaliza nikiwa Maputo, Msumbiji. 

Pia niliweza kuongeza Simulizi iitwayo Zeitoun ya Dave Eggers kuhusu kimbunga cha Katrina huko New Orleans, Marekani. Hii ni simulizi ya wahamiaji kutoka Syria walivyoshiriki kuokoa makumi ya watu kutoka kwenye maafa ya Hurricane Katrina.

Mwaka 2018 nimesoma mchanyato kidogo kuliko mwaka 2017 ambapo dhima (themes) kadhaa ziliniongoza. Hata hivyo bado njaa yangu ya kuwasoma madikteta duniani iliendelea kuniongoza kwa lengo la kupata ufahamu na maarifa ya namna ya kuchangia katika kuzuia nchi yetu kuangukia kwenye utawala wa Imla. Pia nilijaribu kutafuta majawabu ya changamoto hizo. Kwenye dhima hiyo nilisoma:


- The Death of Democracy: Hitler’s Rise to Power
Benjamin C Hett


- The Plots Against Hitler
Danny Orbach


- Franco: Anatomy of a Dictator
Enrique Moradiellos


1 The New Sultan: Erdogan and the Crisis of Modern Turkey
Oner Cagaptey


- How Democracies Die
D Ziblatt and S Levitsky


Kama nilivyopata kusema, ninapenda na kujivunia sana historia ya ukombozi dhidi ya ukoloni barani Afrika na haswa Ukombozi wa Kusini mwa Afrika. 

Mwaka huu niliongeza maarifa katika eneo hilo kwa kusoma sio tu habari nzuri za vyama vya ukombozi bali pia baadhi ya makosa waliyofanya viongozi wetu. SWAPO Captive kilichoandikwa na Bwana Angula ni simulizi muhimu sana kusoma ili kuona namna baadhi ya watu walivyoonewa kwenye harakati za ukombozi. Kwa jina la ukombozi watu huonewa, huteswa na hata huuwawa. Pia nilisoma kuhusu mashujaa wa ukombozi na athari kwa familia zao. Katika dhima hii ya Ukombozi nilisoma:


- Cuito Cuanavale: 12 Months of War That Transformed a Continent
Fred Bridgland


- Africa Tomorrow
Edem Kadjo


- Umkontho we Sizwe: The ANC Armed Struggle
Thula Simpson


- Mozambique: Sowing the Seeds of Revolution
Samora Machel


- 491 Days
Winnie Mandela


- Thabo Mbeki
Adekeye Adebajo


- Umkontho we Sizwe
Janet Cherry


- Chris Hani
Hugh Macmillan


- Being Chris Hani’s Daughter
Lindiwe Hani and Melinda Ferguson


- SWAPO Captive: A Comrade’s Experience of Betrayal and Torture
Oiva Angula


Pia nilisoma vitabu vya hali ya sasa ya Afrika Kusini baada ya ukombozi:


- No Longer Whispering to Power: The Story of Thuli Madonsela
Thandine Gqubule


- How to Steal A City: The Battle for Nelson Mandela Bay, An Inside Account
Crispian Olver


- How to Steal A Country? State Capture and Hope for the Future in South Africa
Robin Renwick


- Coalition Country: South Africa After the ANC
Leon Schreiber


Kama Mtanzania ninayejiandaa kwa majukumu muhimu ya kitaifa nimekuwa nikipenda kupata maarifa Zaidi kuhusu Historia ya Zanzibar. Mwaka 2018 niliongeza maarifa kwa kusoma vitabu kadhaa ikiwemo:


- The Threat of Liberation: Imperialism and Revolution in Zanzibar
Amrit Wilson


- Social Memory, Silenced Voices and Political Struggle: Remembering the Revolution in Zanzibar.
(Ed) W. Cunningham and M. Fouere


Vitabu vinavyofuata ni mchanyato wa riwaya, historia za watu na mataifa mengine, mafunzo ya uchumi na kadhalika. Vitabu vinavyohusu Marekani na utawala wao mpya chini ya Trump ni kwa lengo la kujifunza nini kinaendelea huko. Kitabu cha Deng Xiaoping nilipewa na ndugu yangu Harith Ghassany katika mjadala wa kisomi wa kutafuta modeli sahihi ya kimaendeleo kwa nchi zetu za Afrika.


- Pakistan: Personal Story
Imran Khan


- Making Africa Work: A Handbook for Economic Success
Gregg Mills, O Obasanjo, et al


- Sidetracked
Henning Mankell


- In Praise of Blood: The Crimes of Rwandan Patriotic Front
Judi Rever


- Thomas Sankara Speaks
Thomas Sankara


- A Higher Loyalty
James Comey


- State Secrets: Deathly High Stakes in the Corridors of Power
Quintin Jardine


- Deng Xiaoping and The Transformation of China
Ezra F Vogel


- Gorbachev: His Life and Times
William Taubman


- Tell Tale
Jeffrey Archer


- The Growth Delusion
David Pilling


- CTRL ALT DELETE: How Politics and The Media Crashed Our Democracy
Tom Baldwin


- Unhinged: An Insider’s Account of The Trump White House
Omarosa Manigault


- Fire and Fury: Inside The Trump White House
Michael Wolf


- Why The Dutch are Different
Ben Coates


- The French Revolution: What Went Wrong
Stephen Clarke


- An Extra Ordinary Life: A Passion for Service
V J Mwanga


- Uwajibikaji Ndani ya Kalamu Isiyokuwa na Wino
Ludovich Utouh


- Betting the House: Inside Story of the 2017 Elections
Tim Ross and Tom McTaguwe


- In Defence of Bolsheviks
Max Shachtman


- The Future That Works: Selected Writings of A M Babu
(Ed) Salma Babu and Amrit Wilson


- Our Commonwealth: The Return of Public Ownership in USA
Thomas Hanna


- Democracy, Direct Action and Socialism: A Debate of Fundamentals
Michael Foot and Sean M


Mwaka huu ukiwa unaelekea ukingoni, Wachapishaji wa Vitabu Mkuki na Nyota Publishers walichapisha upya vitabu vya harakati za Willy Gamba, mpelelezi maarufu barani Afrika. Rafiki yangu katika kusoma vitabu Fadhy Mtanga (ambaye pia ni adui yangu kwenye soka – maana yeye ni shabiki mandazi wa Manchester United FC na mimi shabiki wa mabingwa watarajiwa Liverpool FC) alininunulia vitabu vyote 4 vya Mzee Elvis Musiba. Nilikuwa na muda wa kutosha na kuvisoma vyote bila kuweka chini. Namshukuru sana Fadhy kwa zawadi yake murua kabisa. Vitabu hivi ni:


- Kikosi Cha Kisasi
A E Musiba


- Njama
A E Musiba


- Kufa na Kupona
A E Musiba


- Hofu
A E Musiba


Kitabu changu cha mwisho mwaka 2018 ni :


- Dear Ijeawele OR A Feminist Manifesto in 15 Suggestions
Chimamanda Adichie


Vitabu 3 vilivyonigusa sana
The Death of Democracy: Hitler’s rise to power cha Benjamin Hett kilinigusa sana kutokana na namna wanasiasa wanavyoweza kufanya makosa yenye kudidimiza nchi kwa sababu tu ya kulinda madaraka. Katika kitabu hiki somo kubwa ni namna Wabunge wa vyama vyote vya Siasa walivyomruhusu Adolf Hitler kutunga sheria inayompa mamlaka makubwa wakiamini kuwa Hitler ana nia njema na atawalinda. 

Wabunge wa Chama cha SDP ndio pekee walikataa, walizomewa, kuzodolewa na hata kuuwawa. Wengine walikimbilia uhamishoni. Ndani ya miezi michache, hata wale waliomwunga mkono Hitler walishughulikiwa na Taifa la Ujerumani likaingia kwenye taharuki kubwa na hatimaye vita vya pili vya dunia. 

Waliompa madaraka Hitler waliamini kuwa watamdhibiti. Hawakuweza. Historia kama hii ipo lakini wanaadam hatujifunzi tunarudia makossa hayo kila wakati katika nchi mbalimbali duniani.


How Democracies Die cha Ziblatt na Levitsky kilinigusa sana kwa kuwa kinatoa majawabu ya changamoto za demokrasia kuanguka. Licha ya kwamba ni kitabu maalumu kwa muktadha wa nchi ya Marekani, kitabu hiki nilicholetewa na rafiki yangu Rakesh Rajani, kinatazama mifano ya nchi mbalimbali duniani kama Colombia na njia walizotumia kuhami demokrasia (walitumia sana Bunge na Mahakama), Venezuela (jinsi mgomo wa vyama vya upinzani kutoshiriki chaguzi ulivyotoa nafasi ubwete kwa chama tawala) na hata Ujerumani ambayo hali yake nimeeleza hapo awali. 

Somo kubwa kabisa kutoka kitabu hiki ni kwamba ni lazima wadau wote wa demokrasia kushirikiana pamoja kupambana na udikteta bila kujali tofauti ndogo ndogo au kubwa kubwa miongoni mwao. Bila ushirikiano dikteta husaga saga kila mmoja. Ni Kitabu nashauri kila mwana demokrasia akisome.


Dear Ijeawele Or A Feminist Manifesto in 15 Suggestions cha Chimamanda Adichie ni kitabu kidogo sana kwa idadi ya kurasa. Kwa hakika ni barua ambayo Chimamanda kamwandikia rafikiye ambaye amepata mtoto wa kike na anamshauri amkuze vipi mtoto huyu. Kijitabu hiki kimenigusa kwa sababu kinatoa changamoto kadhaa kwa sisi wanaume katika malezi. 

Kuna mambo ambayo tunafanya tunaona kama ni msaada kumbe inapaswa kuwa wajibu kwa familia. Kwa mfano, mara nyingi husikia wanaume tukisema ‘leo nafanya kazi ya kulea mke wangu kasafiri’ ama kwa kimombo ‘baby-sitting’. Chimamanda anatuambia hapa, Baba mtoto hafanyi ‘baby-sitting’ bali anatimiza wajibu wake kama baba. Pia kinachoitwa ‘gender roles’ kwenye nyumba zetu kiasi kwamba tunazuia watoto wa kike kukua na kukuza vipawa vyao vyote. 

Nashauri wenye watoto wa kike wasome kijitabu hiki, wababa na wamama kwani kinaweza kuchangia kubadili mtazamo wako wa namna tunalea watoto wetu wa kike. Mapendekezo 15 ya Chimamanda unaweza usiyakubali yote lakini yana mafunzo mengi ambayo yanaweza kukufaa kwenye malezi ya mabinti zetu.


Heri ya Mwaka mpya 2019


Zitto Kabwe
Dar es Salaam
30/12/2018
Share:

WENYE MIZANI FEKI WAENDELEA KUBANWA

Katika kuhakikisha kwamba mnunuzi wa bidhaa hapunjwi, Wakala wa Vipimo Nchini (WMA), wameendelea kufanya ukaguzi wa mizani zinazotumika sehemu tofauti hasa kwa wauzaji wa zao la korosho.

Lengo la kufanya hivyo ni kutaka kubaini mizani zisizo na viwango ambazo hazitoi kipimo kinachostahili.

WMA ilitembelea baadhi ya vyama vya msingi vya ushirika ili kushuhudia hali halisi ya upimaji korosho za wakulima.

Meneja wa WMA, mkoa wa Pwani, Evarist Masengo, alisema katika kuhakikisha wakulima wanauza mazao yao kwa kutumia mizani sahihi iliyohakikiwa na wakala huo, mizani 109 zimehakikiwa na kupigwa chapa ya Serikali.

Alisema mkoa wa Pwani una jumla ya vyama vya msingi (AMCOS) 95, ambavyo vinapatikana katika wilaya saba.

Wilaya na idadi ya vyama kwenye mabano ni Mkuranga (39), Kibaha (8), Bagamoyo (3), Chalinze (3), Kisarawe (2), Mafia (1), Rufi ji (13) na Kibiti (26).

Masengo alisema kutokana na elimu ambayo hutolewa na WMA kwa wakulima wa korosho na viongozi wa vyama vya msingi (AMCOS) kabla ya msimu, imesaidia kujua matumizi sahihi ya mizani.

Hatua hiyo imesaidia kupungua kwa tofauti ya uzito wa korosho unaotoka katika chama cha msingi na uzito unaopimwa kwenye ghala.

Pia, Masengo aliongeza kuwa hivi sasa wakala wa vipimo katika mkoa wa Pwani, unafanya ukaguzi wa kushtukiza kwenye mizani inayopatikana kwenye vyama vya msingi na ile ya maghala makuu ili kujiridhisha kama walivyohakiki na kuziruhusu, zinapima kwa usahihi.

“Nawapongeza vyama vya msingi, wamejitahidi mizani nyingi tunakopita tunakuta ni sahihi na pale tunapogundua dosari ndogo ndogo zinafanyiwa marekebisho mara moja ili mkulima aendelee kupata faida ya jasho lake la kulima korosho,”alisema Masengo.

Kwa Mujibu wa Sheria ya Vipimo Sura 340, Wakala wa Vipimo ndiyo yenye jukumu la kusimamia usahihi wa vipimo vinavyotumika au vinavyotarajiwa kutumika kufanyia biashara kwa lengo la kumlinda muuzaji na mnunuzi.

Naye Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi, Stella Kahwa kutoka WMA Makao Makuu, alipongeza juhudi zinazofanywa na ofi si ya wakala wa vipimo mkoa wa Pwani.
Share:

RC MWANRI AIAGIZA BODI YA PAMBA KUNUNUA PAMBA YA WAKULIMA

Na Tiganya Vincet
SERIKALI ya Mkoa wa Tabora imeagiza Bodi ya Pamba Tanzania (TCB) kuhakikisha inanunua pamba iliyobaki Daraja B (fifi) ya wakulima wa Urambo ili kutowakatisha tamaa ya kuendelea na kilimo hicho.

Kauli hiyo imetolewa jana na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri kufuatia malalamiko kutoka kwa wakulima wa zao hilo katika Kijiji cha Itengamatwi wilayani Urambo juu ya uwepo wa pamba ambao hadi hivi sasa iko katika maghala na wakulima hawajalipwa fedha.


Aliwataka wakulima kutokuwa na wasiwasi kwa kuwa jitihada zinaendelea ili kuhakikisha pamba yao fifi(daraja B) ambayo hadi hivi sasa bado iko katika maghali ya kuhifadhi mazao inanunuliwa na Bodi ya Pamba Tanzana baada ya wanunuzi wa awali kusimamisha ununuzi na kuzima mashine.


Aidha Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka wakulima kuzingatia kanuni 10 za kilimo cha zao hilo ili kuepuka kuzalisha pamba Daraja B ambalo ndio wakati mwingine linakuwa kigezo cha wanunuzi kuwapa bei mbaya na wakati mwingine kukataa kununua pamba yao.


Alisema azimo la Mkoa wa Tabora katika msimu wa kilimo cha zao ujao ni kila mkulima ni lazima azingatite kanuni kumi za zao hilo ikiwemo kuvuna kwa wakati na kuhifadhi katika hali ya usafi.


Mwanri alisema hatua hiyo itasaidia kulinda ubora wa zao hilo na kumsaidia mkulima kupata Daraja A na kulipwa bei ya juu itakayompa fedha nyingi ambazo zitasaidia kuboresha maisha yake.


Kwa upande wa Afisa Kilimo kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora Modest Kaijage aliwahakikishia wakulima wa pamba wilayani Urambo ambao wana pamba fifi(Daraja B) kuwa Bodi imeamua kuinunua na itawalipa malipo yao.


Alisema Mkurugenzi Mkuu wa TCB amesema kuwa wanafanya utaratibu ili waweze kununua pamba iliyobaki ambapo wao ndio wataifanyia uchambuzi kwa ajili ya msimu ujao.


Awali baadhi ya wakulima walisema kuwa walipokuwa wakihamasishwa kulima pamba na wakati wa ununuzi waliambiwa kuwa pamba ina madaraja mawili lakini wakati wa mauzo pamba yao daraja B haikununuliwa na bado ipo katika maghali jambo linalowakatisha tamaa kuendelea na kilimo hicho.
Share:

TETESI ZA SOKA ULAYA JUMATATU DEC, 31 2018

Kiungo wa kati wa Real Madrid Isco, 26, amepuuzilia uwezekano wake wa kuhamia klabu ya Chelsea ya England. Amesema hataondoka Bernabeu wakati wa kipindi cha kuhama wachezaji Januari. (Deportes Cuatro, kupitia Metro)

Manchester City wanamfuatilia kwa karibu beki wa kushoto wa Real Betis Junior Firpo lakini wanakabiliwa na ushindani mkali kutoka kwa Real Madrid ambao pia wanataka saini ya mchezaji huyo mwenye miaka 22. (Mirror)

Mshambuliaji wa Liverpool Dominic Solanke, 21, amefanyiwa vipimo vya matibabu katika klabu ya Crystal Palace huku akikaribia kuhamia Selhurst Park kwa mkopo. (Mail)

Winga wa klabu ya Lille ya Ufraansa Nicolas Pepe mwenye miaka 23 ambaye amehusishwa na Arsenal, Barcelona na Manchester City, anaonekana kuwa tayari kuhama mwisho wa msimu. (Le Voix du Nord, kupitia Star)Dominic Solanke alichezea timu ya taifa ya England mara ya kwanza Novemba 2017 mechi ya kirafiki dhidi ya Brazil.

Kiungo wa kati wa Chelsea Tiemoue Bakayoko, 24, amesema yuko radhi kusalia AC Milan hata baada ya kipindi chake cha kuwa na klabu hiyo ya Italia kwa mkopo wa msimu mmoja kukamilima mwisho wa msimu. (MilanNews, kupitia Mail)Bakayoko alichezea Chelsea mechi 43 msimu uliopita

West Brom wanakaribia kutia saini mkataba na beki wa Everton Mason Holgate, 22, kwa mkopo Januari. (Express na Star)

Klabu ya RB Leipzig ya Ujerumani imejitosa kwenye mbio za kutaka kumnunua winga wa Chelsea mwenye miaka 18 Callum Hudson-Odoi. (Kicker - German)Callum Hudson-Odoi alijiunga na Chelsea mwaka 2007

Mchezaji anayenyatiwa sana na Liverpool ambaye kwa sasa Borussia Dortmund Christian Pulisic, 20, anaonekana kukaribia kujiunga na Chelsea kwa mujibu wa tangazo lililotolewa na msambuliaji wa zamani wa Marekani Eddie Johnson kwenye mitandao ya kijamii. (Calciomercato)

Middlesbrough wanatumai wataweza kumsaini kiungo wa kati wa Huddersfield Rajiv van La Parra, 27, kwa mkopo kukiwa na uwezekano wa kumchukua kwa mkataba wa kudumu baadaye mwisho wa msimu. (Yorkshire Post)Christian Pulisic

Meneja Brendan Rodgers amesema Celtic wana kazi kubwa ya kufanya sokoni Januari kuwanunua wachezaji wapya. (Irish Times kupitia Celtic TV)

Meneja msaidizi wa timu ya taifa ya England Steve Holland amesema timu hiyo haikujiandaa na kucheza nusufainali yao ya Kombe la Dunia Urusi ilivyofaa. (Telegraph)
Share:

BWANA HARUSI AFARIKI GHAFLA KANISANI AKISUBIRI KUFUNGA NDOA

Sherehe ya harusi iliyokuwa ifanyike juzi jioni katika Kanisa la Nabii wa Utukufu wa Bwana lilipo Olmatejoo, Kata ya Sakina jijini Arusha na kwenye ukumbi wa Sariko Olasiti Garden, iligeuka msiba baada ya bwana harusi kufariki dunia ghafla akiwa kanisani.

Tukio hilo lilitokea majira ya saa 11 jioni katika kanisa hilo ambapo bwana harusi huyo, Heaven Makupa (47) alikuwa kanisani tangu saa saba mchana akisubiri kufunga ndoa na Jane Kimaro.

Hata hivyo, wakati sherehe, nderemo na vifijo vikiendelea vikiongozwa na kikundi cha matarumbeta nje ya kanisa huku bibi harusi akiingia kanisani, Heaven alianza kujisikia vibaya na kupoteza fahamu.

Kutokana na hali hiyo alikimbizwa Hospitali ya St Elizabeth, lakini alifikishwa akiwa tayari amefariki na mwili wake kupelekwa chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru.

Ndoa hiyo ilikuwa ifungwe na kiongozi wa kanisa hilo, Nabii Peter Alayce na tayari taratibu zote zilikuwa zimekamilika tangu mchana alipofika bwana harusi na ujumbe wake.

Wakati kifo hicho kinatokea mamia ya watu walikuwa tayari wamefika katika ukumbi wa Sariko Olasiti Garden kuwasubiri maharusi hao ili kuendelea na sherehe.

Mmoja wa wageni waalikwa, Juliana Mosha alisema kabla ya kifo hicho hakukuwa na taarifa yoyote ya kuugua kwa bwana harusi na walishikiri naye vikao vya harusi hadi dakika ya mwisho. “Hili ni jambo la miujiza, hatujui kilichotokea nadhani hii ni kazi ya Mungu,” alisema Juliana.

Alisema baada ya taarifa kufikishwa ukumbini juu ya msiba huo, watu walianza kutawanyika na kurejea majumbani.






Na Mussa Juma,Mwananchi
Share:

RADI YAUA,KUJERUHI TUNDURU


Mkazi wa Kijiji cha Nambalapi mashambani, Kata ya Masonya, wilayani Tunduru, Awetu Adam (33), amefariki dunia baada ya kupigwa na radi iliyoambatana na upepo mkali akiwa shambani.

Mvua hiyo iliyonyesha Desemba 29, mwaka huu kwa saa nne kuanzia saa 9 hadi 12 jioni imeripotiwa pia kuezua na kubomoa zaidi ya nyumba 250 za wananchi wa tarafa hiyo.

Pia imeharibu na kuvunja miundombinu ya Shirika la Ugavi Umeme Tanzania (Tanesco) kwa kung`oa baadhi ya nguzo na kusababisha ukosefu wa nishati hiyo katika baadhi ya maeneo ya mji huo.

Mbali na tukio la kifo, mtoto wa miaka miwili Bakari Said, alijeruhiwa kwa kupigwa na radi wakati akiwa amebebwa mgongoni na mama yake ambaye alikufa kwa kupigwa na radi.

Diwani wa Kata ya Mchangani, Haillu Hemed Mussa, alisema jumla ya nyumba 141, madarasa matano na ofisi za walimu katika Shule ya Msingi Mchangani, zimezuliwa.

Alifafanua kuwa pamoja na uharibifu huo pia kata yake iliripoti kujeruhiwa wananchi watatu waliotambuliwa kama, Kawale Bakari, Alli Ambe na Shekhe Mohamed Salum, ambao walikimbizwa Hospitali ya Serikali ya Wilaya kwa ajili ya matibabu.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Majengo, Abdalah Rajabu, alisema kuwa tukio la mvua hiyo limesababisha kuezuliwa kwa mapaa ya maghala mawili ya kuhifadhia korosho mali ya Chama Kikuu cha Wakulima (TAMCU) na kulowesha tani 536 za korosho, mali ya serikali.

Alisema pamoja na madhara hayo pia upepo na mvua hizo ziliezua nyumba 13 mali ya wakazi wa eneo la kata yake.

Diwani Rashid Mkwawa kutoka Kata ya Nanjoka, alisema kuwa jumla ya wakazi 11 walikosa makazi kutokana na nyumba zao kuezuliwa na mvua hizo.

Taarifa zilizotolewa na maofisa tabibu katika Hospitali ya Wilaya ya Tunduru, zinaeleza kuwa majeruhi wote wanaendelea vizuri baada ya kuanza kupatiwa matibabu.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maafa, Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Juma Homera, alithibitisha kuwapo kwa tukio hilo na tayari amewaagiza viongozi wa serikali za vijiji kuzunguka katika maeneo yao na kufanya tathmini ili kubaini hali halisi ya uharibifu huo.
Share:

WAHAMIAJI HARAMU 13 WAFARIKI BAADA YA KUTUPWA MOROGORO

Wahamiaji 13 kati ya 26 raia wa Ethiopia wamefariki dunia baada ya kutupwa eneo la Sangasanga mkoani Morogoro Barabara Kuu ya Iringa- Morogoro na gari aina ya lori ambalo halijajulikana.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Jumapili Desemba 30, 2018, Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro, Wilbroad Mutafungwa alisema tukio hilo liliripotiwa saa 9 alasiri jana na Vyombo vya usalama kwenda eneo la tukio na kukuta raia 26 kati yao 13 wakiwa wamepoteza maisha.


Mutafungwa amesema watumiaji wa barabara hiyo waliiona miili ya raia hao pembeni mwa barabara na kutoa taarifa kwa askari wa kikosi cha usalama barabarani eneo la Sangasanga.


Kamanda huyo amesema kati ya raia hao yumo mtoto wa miaka minane na polisi wanaendelea na uchunguzi ili kulibaini lori na wahusika wa tukio hilo.
Share:

MAMA MJAMZITO NA MWANAE WAFARIKI KWA UZEMBE WA WAUGUZI

Mkuu wa Wilaya ya Igunga, John Mwaipopo
** 
Mkuu wa Wilaya ya Igunga, John Mwaipopo, ametoa saa 72 sawa na siku tatu kwa uongozi wa hospitali ya wilaya, kuwachukulia hatua kali watumishi wanaodaiwa kusababisha
kifo cha mjamzito.


Milo Peter (29), mkazi wa mtaa wa Masanga, Igunga, alifariki Desemba 29, mwaka huu na kuzikwa katika makaburi ya Masanga.

Baadhi ya wajawazito waliolazwa katika hospitali hiyo, waliwalalamikia watumishi wawili kufanya kazi kizembe, hali inayodaiwa kusababisha kifo cha Milo na mtoto.

Mbele ya diwani wa kata ya Igunga Charles Bomani, wajawazito hao, walidai mwenzao hakupata matibabu yanayostahili mapema, licha ya kuomba msaada kwa wauguzi waliokuwa zamu.

Kwa nyakati tofauti Blandina Enock, Rahel John, Rusia Ramadhani na Sikudhani Mrisho, walidai mwenzao alifikishwa hospitalini hapo Desemba 27, mwaka huu saa mbili usiku kwa ajili ya kujifungua.

Walisema kuwa, Milo alipofika alipewa kitanda huku ndugu zake waliomfikisha hospitalini, wakipewa ruhusa kuondoka.

"Jamani mnajua ufike wakati tuseme ukweli kwani kifo cha mama mwenzetu, kinaonekana kabisa uzembe umechangia.

"Sisi wenyewe tumeshuhudia kabisa namna ambavyo alikuwa akiomba msaada kwa wauguzi," alidai Rahel kwa niaba ya wenzake.

Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Igunga, Amada Kasigwa, alikiri kutokea kwa kifo hicho cha mjamzito na mtoto mchanga mwenye uzito wa kilogramu 3.8.

Alisema kuwa vifo hivyo vilitokea Desemba 28, mwaka huu na kudai hali hiyo imetokana na uzembe wa muuguzi wa zamu, Matinde Muhonye. 

Kwa mujibu wa Amada, mtumishi huyo alionywa kuhusu madai hayo ya ufanyaji kazi kizembe.
Share:

TATIZO LA AJIRA KWA VIJANA NI KUBWA KULIKO TATIZO LA KIKOKOTEO CHA MAFAO YA KUSTAAFU


Ameandika Dotto Bulendu kwenye ukurasa wake wa Facebook
Tatizo la ajira kwa vijana nchini Tanzania ni kubwa kuliko tatizo la kikokoteo cha mafao ya kustaafu.

Kama tulivyopiga kelele kuitaka Serikali itazame upya uamuzi wake wa kuwalipa wastaafu asilimia 25 ya mafao yao ya kustaafu na kilichobaki walipwe kidogo kidogo,kelele hizo hizo zinatakiwa kupigwa ili tupate ufumbuzi wa tatizo la ajira nchini maana tunajitengeneza bomu wenyewe.

Ikiwa kati ya Mwaka 2015 mpaka Disemba 18.2018 Jumla ya vijana Laki tano ,tisini na nne elfu na mia tatu(594,300)waliomba kazi serikalini na waliopata kazi walikuwa ni elfu sita na mia tano hamsini na nne(6,554) ukiwa ni wastani wa watu mia moja(100) wanaoomba kazi serikalini ni mmoja tu ndiye mwenye uhakika wa kupata kazi,tunahitaji kupiga kelele,kushauri,kuonya juu ya athari za kuwa na kundi kubwa la vijana wanaosaka kazi.

Rafiki yangu mmoja aliandika mtandaoni kuwa vijana wengi ni "Book Smart" huku wakikosa ujuzi wa namna ya kukabili changamoto za mtaani (Street smart)ndiyo maana tuna kundi kubwa la vijana waliokata tamaa na maisha huku wakiwa na shahada zao mkononi.

Kama ni hivyo lazima tuje na mpango wa haraka utakaobadili elimu yetu ili vijana hao wenye shahada zinazovutia ila wanahangaika mtaani wanapokuwa vyuoni mpaka vyuo vikuu wapate vyote, yaani wawe "Book smart" na "street smart",wazijue fursa zilizopo mtaani na namna ya kuzitumia ili tujinasue na hatari ya kuwa na kundi kubwa la vijana wasio na kazi.

Kama ndani ya miaka mitatu vijana zaidi ya laki tano na nusu walipambana kusaka kazi serikali na wakapata watu elfu sita na mia tano, hii maana yake nini?kufikia mwaka 2020 tunaweza kubwa na kundi kubwa linalopindukia vijana milioni moja wenye sifa za kitaaluma na wapo nyumbani hawana cha kufanya,maana vyeti vyao vyenye GPA haviwapi kazi wala hawawezi vitukia kupata mkopo benki wala serikalini.

Hivi karibuni,shirika la afya duniani lilipata kusema vijana milioni 3.7 wanaugua ugonjwa wa Sonona(Depression),kutokana na changamoto za maisha wanazokutana nazo ikiwemo ukosefu wa ajira na ugumu wa maisha,achilia mbali sababu za kimahusiano na usaliti kwenye ndoa zao.

Vijana nchini Tanzania sasa wanakutana na fursa chache za ajira huku wale waliomo makazini wakikumbana na changamoto za kulipwa kidogo,kukopwa mishahara yao huku wakifanyishwa kazi kwa muda mrefu na katika mazingira magumu.

Vijana wengi walio makazini wanakilio cha kukaa kazini muda mrefu bila kupandishiwa malipo yao huku ukali wa maisha ukipanda kila kukicha,lakini hili ni kundi dogo,kundi kubwa lipo mtaani.

Nilipokuwa namsikiliza Rais John Magufuli wakati akizungumzia sakata la kikokoteo ,alisema mpaka mwaka 2023 kutakuwa na wastaafu takribani elfu 58 watakaotakiwa lipwa mafao,hawa kilio chao kimesikika.

Tujiulize kwa pamoja,kama kati ya mwaka 2015 mpaka Disemba 2018 vijana zaidi ya laki tano waliomba kazi serikalini na laki tano na zaidi wakakosa,je mpaka kufikia mwaka 2023 tutakuwa na kundi la vijana wangapi wanaopambania kazi serikalini?

Sasa hivi sekta binafsi imepunguza kasi ya kuajiri ,inachokifanya sasa ni kupunguza wafanyakazi wake na kimbilio lake ni serikali ambayo watu ambao imewaajiri hawafiki hata milioni moja!

Tunawasaidiaje vijana wetu wenye changamoto ya kuwa "Book smart"?je tuwalaumu tu kuwa wamesoma na hawajui maisha ya mtaani?na je ni kweli shuleni,vyuoni mpaka vyuo vikuu vijana wetu hawafundishwi namna ya kuyaishi maisha ya mtaani na changamoto zao?kama ndiyo nani alaumiwe?je ni wao ndiyo waliotengeneza mtaala ambao mwisho wa siku unawaacha wakiwa "Book smart" wasiojua maisha ya mtaani?

Tunawasaidiaje vijana wetu?

Juzi nilikuwa nasafiri kati ya Mwanza na Shinyanga nikapita eneo linaitwa Mabuki nikaambiwa wakati wa Nyerere kulikuwa na mashamba makubwa ya mazao na mifugo leo pamebaki hamna kitu,tukifufua hapo tutaajiri vijana wangapi?

Nilipofika Shinyanga nikaona kiwanda cha Nyama kimefungwa,nikauliza mbona wasukuma wanafuga na watu wanakula nyama kwa nini hakifanyi kazi?sikupata majibu na ninaambiwa kiwanda hiki kilijengwa mwaka 1974 na Mwalimu Nyerete,tukifufua hiki tutaajiri vijana wangapi?
Hapa Mwanza kila nikienda Airport napita kiwanda cha Ngozi Ilemela,huwa nakumbuka siku moja kabla ya uchaguzi mkuu wa 2015,Rais Magufuli akiwa mgombea alisema akishinda atahakikisha kiwanda hicho kinafufuka na akatoa siku saba kianze kazi.

Kiwanda hicho kilijengwa na Serikali ya Nyerere,lakini jana nimepita hapo sioni kinachoendelea,najiuliza kwani wasukuma hawafugi tena?kwani watanzania hawavai viatu vya ngozi?tukifufua hiki kiwanda tutaajiri vijana wangapi?
Kila napoenda Nyakato hupita kiwanda cha nguo ya Mwatex,nchi kilijengwa na Serikali ya Nyerere lakini sasa sioni kinachoendelea,najiuliza dada na mama zetu hawavai tena kanga?wasukuma hawalimi tena pamba?tukifufua hiki kiwanda tutatengeneza ajira ngapi?

Ni kama nilipokwenda Tabora wiki mbili zimepita nikaambiwa kile kiwanda cha nyuzi kilichokuwa kinaajiri kundi kubwa la vijana pale Tabora nacho ni kama kishaenda halijojo kitambo,nikajiuliza hivi watanzania hawashoni? siku hizi?nguo zao hazichaniki?nikaambiwa nyuzi siku hizi zinatoka China,nikajiuliza hivi tukifufua hiki tutaajiri vijana wangapi?

Bahati mbaya sana,fikra za viongozi wetu ni kuwa wanadhani serikali itajenga viwanja,itarejesha,italima na kuendesha mashamba makubwa ,Itafuga mifugo,itavua yenyewe.
Tusipoamua kuotekeleza Sera ya ubia kati ya serikali na sekta binafsi,sera ya wazawa ili kuhakikisha tunatengeneza matajiri wakubwa wazawa wakashikilia njia kuu za uchumi kwa ubia na serikali huku tukiwa wakali kwenye Rushwa hatutatoka abadani.

Tunawalaumu vijana na kuwataka wajiajiri,je tumewapa mitaji?maana siku hizi utawasikia watu wanasema wewe ukiwa na wazo tu unatoka,unabaki na maswali hivi hawa vijana laki tano wote hawana mawazo ya kujiajiri kweli?
Ukimsikiliza anayesema hivyo yeye alianza na mtaji wa zaidi ya milioni kumi,tena yupo kazini,kachukua mkopo kwa dhamana ya kazi yake,hawa vijana masikini hawa tunawasaidiaje na vyeti vyao vya chuo kikuu?

Hebu serikali ijaribu kuwaambia hawa vijana kuwa Cheti chako cha stashahada,shahada,shahada ya uzamili ama uzamivu kinaweza kuwa dhamana ya kuchukuliwa mkopo kwa Riba ndogo na tuwe na mpango kabambe wa kuwafanya vijana wetu wazijue fursa zilizopo ndani na nje ya nchi kutoka sekta ya kilimo,uvuvina ufugaji tuone kama utawaona wa akimbizana Wizara ya Utumishi kuomba kazi.

Vijana wetu wanahitaji zaidi ya hiki wanachopata vyuoni,wanahitaji "Skills" zaidi na binafsi wengi naowafahamu mimi wana "Skills" za kutosha katila maeneo waliyoyasomea lakini wanakosa mtaji ili wajiajiri wenyewe.
Tunaweza jidai hatuoni,hatusikii sauti zao,lakini ukweli ni kwamba tatizo la ajira kwa vijana tukilibeza na kubaki kupigana vijembe,tunatengeneza bomu kubwa na kuongeza idadi ya vijana wanaougua Sonona.

Wasalaaam
Muwe na maandalizi mema ya mwaka mpya wa 2019.
soma maoni hapa
Share:

Sunday, 30 December 2018

MWANAUME AFARIKI KWA KUBANWA KATIKATI YA MAPAJA YA MWANAMKE


Mwanaume mmoja katika kijiji cha Gionsaria,kaunti ya Kisii Nchini Kenya amefariki dunia baada ya mwanamke mmoja kumbana /kufungia kichwa cha mwanaume huyo katikati ya mapaja. 




Mkasa huo wa aina yake umetokea siku ya Ijumaa Disemba 28,2018. 


Chifu wa eneo hilo Bwana Oganda Matego amesema mwanaume huyo anayejulikana sana kwa jina ‘Doctor’,ambaye pia ni taniboi wa magari ya kusafirisha majani chaieneo hilo, alishikiliwa kichwa katikati ya mapaja/miguu na mwanamke mmoja huku rafiki wa mwanamke huyo ambaye pia ni mwanamke akiwa ameshikilia miguu ya ‘Doctor’na kumuinua hewani.


Bwana Oganda amesema inashukiwa kuwa wawili hao walikuwa wapenzi na kifo cha ‘Doctor’ kilitokea wakicheza ambapo Baada ya dakika moja mwanaume akaachilia kichwa na kugonga kichwa barabarani



Inaelezwa kuwa wanawake hao walimpeleka ‘Doctor’ katika hospitali ya wilaya ya Nyamache na madaktari walipompima wakabaini kuwa tayari alikuwa amefariki dunia.



Tayari wanawake hao wanashikiliwa na polisi kwenye kituo cha polisi cha Nyangusu huku wakisubiri kufunguliwa mashtaka.



Aidha baada ya habari ya kifo cha ‘Doctor’ kuwafikia majirani wa wanawake hao,waliamua kuchoma nyumba nne zinazomilikiwa na hao wanawake. 


Hali ya utulivu imeshuhudiwa kwa sasa na Chifu wa eneo hilo Bwana Oganda Matego amewasihi wakazi wa eneo hilo kutochukua sheria mikononi mwao kiholela.




Share:

WAZIRI AWAPIGA MARUFUKU TRA KUFUNGIA BIASHARA ZA WADAIWA KODI

Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango amepiga marufuku Mamlaka ya Mapato nchini TRA kuwafungia wafanyabiashara, biashara zao kwasababu ya madeni ya kodi wanayodaiwa.

Ametoa kauli hiyo jijini Dodoma  Desemba 30, 2018 wakati akitoa taarifa ya hali ya uchumi wa taifa na utekelezaji wa bajeti ya serikali kwa kipindi cha miezi sita katika mwaka wa fedha 2018/19.

"Ninaukumbusha uongozi wa Mamlaka ya Mapato utekeleze maagizo ya Mhe Rais aliyoyatoa wakati wa ufunguzi wa kikao cha utendaji kazi wa mamlaka kilichofanyika ukumbi wa Mwl Nyerere tarehe 10 Desemba 2018," amesema.

"Utaratibu wa kumfungia mfanyabiashara biashara yake ili kushinikiza alipe kodi anayodaiwa, usitishwe isipokuwa kwa mkwepaji sugu na kwa kibali cha Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania," ameongeza.

Pamoja na mambo mengine, Waziri Mpango amesema makusanyo ya ndani yameongezeka na kufikia shilingi trilioni 7.37 sawa na asilimia 88.9 huku mapato yatokanayo na kodi yakiwa ni trilioni 6.23 sawa na asilimia 88 ya lengo lililowekwa kwa kipindi hicho.

Waziri Dk Mpango pia amesema mapato yasiyo ya kodi yamevuka zaidi ya lengo na kufikia asilimia 121 kwa kukusanya bilioni 936.03 ambayo ni zaidi ya lengo la shilingi bilioni 775.36 huku mapato ya halmashauri yakifikia bilioni 203.8 ikitokana na kuimarishwa kwa mfumo wa ukusanyaji mapato wa serikali hasa kwa njia za kielektroniki.

Aidha Wziri Mpango ameitaka mamlaka ya mapato nchini TRA kuhakikisha inatoza kodi kwa mujibu wa sheria na kanuni zake na kuondoa manyanyaso kwa wafanyabiashara ili wahamasike kuchangia kodi
Chanzo:Eatv

Share:

KATIKA KUFUNGA MWAKA UWT PWANI YAFUNGA 2018 NA HILI

Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) mkoa wa Pwani,Bibi Farida Mgomi, ametoa shukrani nzito kwa viongozi wote wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na Serikali kwa kuonesha ushirikiano mkubwa kipindi ambacho walikuwa ziarani katika wilaya zote za mkoa huo. UWT Mkoa wa Pwani walianza ziara yao mwanzoni mwa mwezi wa saba (7)na kumaliza mwanzoni mwa mwezi wa Kumi na mbili (12) Wakiwa katika Ziara zao huko wilayani walipokelewa vizuri na Viongozi mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Chama wa Wilaya, Mkuu wa Wilaya,Mwenyekiti wa Halmashauri, Mbunge wa Jimbo husika, Viongozi wa Jumuiya…

Source

Share:

MBUNGE NJOMBE ASIMAMA JUU YA KITANDA KUTAFUTA MTANDAO WA SIMU

Na.Amiri kilagalila Changamoto ya mawasiliano kwa Njia ya simu ni moja ya shida ambayo imekuwa ikiyakumba baadhi ya maeneo hapa nchini hususani katika maeneo ambayo ni mapya kiutawala kama ilivyo katika maeneo machache ya wilaya ya Ludewa na jimbo la Lupembe mkoani Njombe. Kutokana na changamoto hiyo,Mbunge wa jimbo la Lupembe lililopo halmashauri ya wilaya ya Njombe kaskazini mwa mkoa huo mh.Joram hongoli,amemuomba Naibu waziri wa ujenzi Elias kwandikwa wakati akizungumza na wananchi wa kijiji cha Lupembe kuwasaidia kutatua changamoto hiyo kwa kuwa yeye ni miongoni mwa waathirika wakubwa wanaokosa…

Source

Share:

SERIKALI YATOA UFAFANUZI KUHUSU SAKATA LA MWANANCHI KUKAMATWA AKISAFIRISHA VITANDA VIWILI

Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umepokea taarifa kupitia mitandao ya kijamii na wadau mbalimbali zinazohusisha namna Afisa Misitu wa Wilaya ya Korogwe alivyokuwa akitekeleza majukumu ya kusimamia Sheria ya Misitu Na. 14 ya Mwaka 2002 pamoja na Kanuni zake za Mwaka 2004.

 Afisa huyo alikuwa akitekeleza majukumu hayo kwa mujibu wa kifungu cha 93 (Powers of officers with respect to offences) inayompa mamlaka Afisa Misitu au Afisa wa Jeshi la Polisi kukagua, kukamata na kuzuia mazao yanayodhaniwa kupatikana kinyume na sheria.

Kufuatia taarifa hizo, uongozi wa TFS umefanya uchunguzi wa haraka na kubaini kuwa abiria mmoja alikuwa akisafirisha vitanda viwili (2) vipya kwa basi. Vitanda hivyo vililipiwa ushuru wa Serikali kupitia mfumo wa Kielektroniki wa Malipo Serikalini (GePG) na kupewa stakabadhi halali ya tarehe 26 Disemba, 2018 katika kituo cha Mkata, Handeni Mkoani Tanga.

Katika kutekeleza majukumu yake, Afisa wetu alimtaka abiria huyo kuonesha Hati ya Kusafirishia (Transit Pass) bidhaa hizo kwa mujibu wa Kanuni ya 13(4) ambayo inakataza mwenye chombo chochote cha usafiri kusafirisha mazao ya misitu ambayo hayana hati ya usafirishaji ambapo abiria huyo hakuwa nayo. 

Hata hivyo, Afisa wetu alishindwa kutafsiri masharti ya kifungu hiki na mahitaji ya utoaji wa Hati ya Usafirishaji kwani kama msafirishaji binafsi kwa matumizi ya nyumbani asingeweza kukidhi vigezo vya kuwa na hati hiyo. 

Hati ya Usafirishaji huhitaji msafirishaji kuonesha usajili, leseni ya biashara, utambulisho wa mlipa kodi na namba ya usajili wa chombo kinachotumika kusafirisha mazao hayo pamoja na kuonesha vituo atakavyopaswa kukaguliwa.

Kufutia tukio hilo, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania unamwomba radhi abiria huyo na umma wa watanzania kwa tukio hilo na usumbufu uliojitokeza. Wakala unaendelea kufuatilia suala hili, na utahakikisha kuwa tukio kama hili halijirudii tena.

 Aidha, hatua za kinidhamu zitachukuliwa kwa mujibu wa Kanuni za utumishi wa umma dhidi ya mtumishi aliyehusika na utoaji wa lugha isiyo na staha wakati akitekeleza sheria ya misitu ambapo alitegemewa kutoa elimu stahiki kwa umma. Hivyo, TFS inapenda kufafanua mambo yafuatayo:- 2

1. Kwamba ikiwa mwananchi yeyote amenunua samani mpya kutoka kwa watengenezaji au wauzaji mahali popote kuhakikisha anapatiwa risiti halali kwa malipo aliyofanya. Hivyo, mmiliki wa samani mpya kwa matumizi binafsi halazimiki kuwa na Hati ya Usafirishaji anaposafirisha toka eneo moja kwenda jingine isipokuwa awe tayari kuonesha uthibitisho wa nyaraka za malipo halali ya samani hizo kwa ukaguzi pale itakapohitajika.

2. Mwananchi yeyote anayesafirisha samani zilizotumika kutoka eneo moja hadi jingine halazimiki kuwa hati za malipo wala kuwa na hati ya kusafirishia samani hizo.

3. Serikali itaendelea kufanya mapitio ya Sheria ya Misitu na Kanuni zake ili kuepuka mkanganyiko wowote wa tafsiri ya sheria unaoweza kujitokeza na kuondoa usumbufu kwa wananchi.

Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania unapenda kutoa rai kwa wananchi wote kuendelea kuzingatia Sheria za uhifadhi wa misitu. Aidha, Wakala hauna nia ya kuzuia utengenezaji, usafirishaji na matumizi ya samani za mbao mahali popote nchini ilimradi tu upatikanaji wa malighafi zake uwe umefuata utaratibu. Lengo ni kuhakikisha kuwa rasilimali za misitu zinatunzwa na kutumika kwa njia endelevu kwa maendeleo ya Taifa. Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania utaendelea kutoa elimu kwa umma pamoja na watumishi wake kuhusu taratibu za uvunaji, usafirishaji na biashara ya mazao ya misitu nchini kupitia njia mbalimbali na kuhakikisha huduma bora kwa wananchi.

IMETOLEWA NA
KITENGO CHA HABARI NA MAWASILIANO KWA UMMA
WAKALA WA HUDUMA ZA MISITU TANZANIA (TFS)
Share:

TETESI ZA SOKA JUMAPILI DEC, 30 2018

Christian Pulisic
Chelsea wametoa ofa ya hadi pauni milioni 45 kumsaini mshambuliaji wa Borussia Dortmund Christian Pulisic msimu ujao lakini klabu hiyo ya Ujerumani itacheleweza uamuzi wake inaposubiri ofa kutoka kwa vilabu vingine kwa mchezaji huyo raia wa Marekani mwenye miaka 20. (ESPN)

Meneja wa Newcastle Rafael Benitez anataka kumwendea straika wa Leeds Kemar Roofe, 25, ikiwa atapewa pesa mwezi Januari. (Sunday Mirror)

Meneja wa muda wa Manchester United Ole Gunnar Solskjaer amewashauri kipa wa Uhispania David de Gea, 28, na mshabuliaji Mfaransa Anthony Martial, 23, kusaini mikataba mipya na klabu hiyo. (Mail on Sunday)David de Gea
Chelsea wameambiwa kuwa ni lazma walipe pauni milioni 30 ikiwa wanataka beki mjerumani Mats Hummels, 30, mwezi Januari. (Sun on Sunday)

Meneja wa Juventus Massimiliano Allegri amekana madai kuwa anataka kuwa meneja mpya wa msimu ujao. (Mail on Sunday)

Meneja wa Watford Javi Gracia anasema sio jambo la kushangaza kuwa Abdoulaye Doucoure, 25 anahusishwa na kuhama licha ya yeye kutarajia raia huyo wa Ufransa kuendelea kubaki kwa muda zaidi. (Independent)Nathaniel Clyne
Cardiff wanaongoza mbio za kumwinda beki wa Liverpool Nathaniel Clyne, licha ya Fulham na Leicester nao kuwa na nia ya kumsaini kiungo huyo wa miaka 27 raia wa England. (Sunday Mirror)

Mlinzi wa Manchester United raia wa Italia Matteo Darmian, 29, analengwa na Inter Milan na Lazio. (Calciomercato)

Lazio watajia kuwasaini mlinzi wa Chelsea raia wa Italia Davide Zappacosta, 26 ikiwa Manchester United watakataa kumuuza Darmian. (Sunday Mirror)

Arsenal wamejiunga na mahasimu wao Tottenham kutaka kumsiani beki wa Norwich City mwennye miaka 18 Max Aarons. (Sunday Mirror)Davide Zappacosta

Liverpool wanammezea mate kiungo wa kati wa Trabzonspor Abdulkadir Omur, 19, lakini wanakabaliwa na ushindani kutoka Manchester City and Roma. (Fotomac, via Star on Sunday)

Meneja wa Southampton Ralph Hasenhuttl anataka kumiania beki wa Olympiakos na Norway Omar Elabdellaoui, 27, mwezi Januari. (Mail on Sunday)

Beki wa Leicester City raia wa Australia Callum Elder, 23, anajifunza na Ipswich Town na anatarajiwa kujiunga kwa mkopo mwezi Januari. (East Anglian Daily Times)
Share:

CCM WAANIKA SIFA ZA WAGOMBEA UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA 2019

Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally amesema atakayejihusisha na vitendo vya rushwa katika mchakato wa chama hicho tawala kusaka wagombea wake katika uchaguzi wa Serikali za mitaa, atapoteza sifa za kugombea.

Ametoa kauli hiyo leo Jumapili Desemba 30, 2018 alipokutana na wajumbe wa kamati ya siasa ya wilaya za Muleba na Biharamulo mkoani Kagera.

Amesema kila kiongozi wa CCM atakayejitokeza kugombea uenyekiti wa kijiji au mtaa, lazima awe mwadilifu na mwaminifu.

Amebainisha kuwa baadhi ya wagombea wanatumia majukwaa kupinga rushwa licha ya kuwa wanajihusisha nayo, ikiwa ni pamoja na kukiuka maadili ndani ya chama.


"Makatibu wa CCM kila ngazi hata nyie msiwe wa kupokea rushwa kupitisha majina ya wagombea wasiokuwa na sifa lazima kiongozi afuate miiko na ahadi za mwanachama,” amesema Bashiru.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger