Wednesday 26 June 2019

Dirisha la Maombi ya mikopo elimu ya juu kufunguliwa Julai Mosi

...
Tunapenda kuwafahamisha waombaji mikopo ya elimu ya juu kwa mwaka wa masomo 2019/2020 kuwa dirisha la kuomba mkopo kwa njia ya mtandao litafunguliwa rasmi Jumatatu, Julai 1, 2019 na kufungwa Alhamisi, Agosti 15, 2019. Maombi yote yatafanywa kupitia mtandao utakaopatikana kupitia www.heslb.go.tz.
 
Kati ya leo (Jumanne, Juni 25) na Julai 1, 2019 wakati dirisha litakapofunguliwa, wanafunzi wanashauriwa kuhakikisha wanakamilisha nyaraka muhimu zinazotajwa katika ‘Mwongozo wa Utoaji Mikopo na Ruzuku kwa 2019/2020’ unaopatikana katika tovuti ya HESLB (www.heslb.go.tz).
 
Nyaraka hizo na maelezo mengine ya ufafanuzi pia yanapatikana katika kitabu kidogo cha ‘Maswali na Majibu 26’ kuhusu uombaji mkopo kinachopatikana katika tovuti hiyohiyo.
 
Kwa ajili ya kumbukumbu, nyaraka muhimu ni pamoja na:
  1. Nakala ya cheti cha kuzaliwa cha mwombaji wa mkopo iliyothibitishwa na Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) au Wakala wa Usajili wa Matukio ya Kijamii Zanzibar (ZCSRA);
  2. Nakala ya cheti cha kifo cha mzazi wa mwombaji mkopo iliyothibitishwa na Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) au Wakala wa Usajili wa Matukio ya Kijamii Zanzibar (ZCSRA);
  3. Barua ya Mganga Mkuu wa Mkoa (RMO), Mganga Mkuu wa Wilaya (DMO) au Mganga wa Hospitali ya Halmashauri ya Mji, Wilaya, Manispaa au Jiji inayothibitisha ulemavu wa mwombaji mkopo au mzazi wake; na
  4. Barua kutoka kwa taasisi iliyofadhili masomo ya sekondari au stashahada ya mwombaji mkopo.
Ufafanuzi kwa wanafunzi waliomaliza kidato cha sita na stashahada mwaka huu
Baada ya wanafunzi waliomaliza kidato cha sita au stashahada (diploma) wamekuwa wakiuliza maswali kadhaa kuhusu utaratibu wa ujazaji wa fomu za uombaji mkopo wakiwa katika kambi za Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na iwapo wanaweza kujaza fomu kabla matokeo ya mitihani hayajatoka.
 
Ufafanuzi ni kuwa HESLB inawasiliana na Makao Makuu ya JKT ili kuweka utaratibu bora kuwawezesha wanafunzi wahitaji waliopo katika kambi za JKT kuwasilisha maombi kwa njia ya mtandao.
 
Aidha, mfumo wa uombaji mikopo kwa njia ya mtandao utakaofunguliwa Julai 1 mwaka huu haumlazimishi mwombaji kuwa na matokeo ya kidato cha sita. Mwombaji atapaswa kuwa na namba ya mtihani wake wa kidato cha nne tu.
 
Wito
Waombaji wa mikopo watarajiwa wanashauriwa kusoma mwongozo uliotolewa na kuandaa nyaraka zote muhimu zinazohitajika kuthibitisha uhitaji wao kabla ya kuingia katika mfumo wa uombaji. Uzoefu unaonesha kuwa mwombaji mkopo anaweza kutumia dakika 30 kukamilisha maombi yake katika mfumo ikiwa ana nyaraka zote muhimu.
 
Imetolewa na:
Mkurugenzi Mtendaji,
Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu,
Dar es salaam
Jumanne, Juni 25, 2019


Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger