Thursday 16 February 2017

NECTA yasitisha mtihani wa udahili kwa kidato cha kwanza Jambo Blog 10

...


BARAZA la Mitihani la Tanzania (NECTA) limesitisha mpango wa kuwafanyia mtihani wa udahili wanafunzi wote waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka huu katika shule za sekondari za serikali uliokuwa ufanyike Februari 28, mwaka huu.

Naibu Katibu Mtendaji wa Necta, Athumani Salumu alisema hayo juzi kwenye kikao cha wadau wa sekta ya elimu Mkoa wa Morogoro alipokuwa akihitimisha mada yake kwa wajumbe wa kikao hicho kilichoongozwa na mkuu wa mkoa huo, Dk Stephen Kebwe.

Salumu alisema mpango wa kuwafanyia mtihani wa udahili wanafunzi hao ulitokana na matakwa yaliyowasilishwa Necta na baadhi ya wakuu wa shule za serikali wakipendekeza kupitia maofisa elimu wa mikoa na wilaya kuwa wanafunzi wa kidato cha kwanza waliochaguliwa na kupangiwa shule zao wengi hawana sifa na uwezo wa kumudu masomo.

Naibu Katibu Mtendaji wa Necta alisema wakuu wa shule walikuwa wakiomba kupata idhini ya kuwafanyia mtihani wanafunzi ili kubaini uwezo wao na kwamba baraza liliwasiliana na maofisa elimu mkoa na wilaya likiwataka kuwasilisha orodha ya idadi ya wanafunzi wa kidato cha kwanza waliopangiwa kwenye shule ya zao.

Alisema baada ya kufahamika idadi ya wanafunzi hao, baraza ndilo litatunga maswali ya mitihani yenye kuzingatia mfumo na vigezo maalumu na kutumiwa wakuu wa shule hizo ili kuusimamia kwa lengo la kuweka uzani sawa wa mtihani huo.

Alisema moja ya masharti ni kwamba mtihani huo ulitakiwa ufanyike kwa wanafunzi wa kidato hicho kwa shule zote za serikali siku moja na kwa muda uliopangwa.

Hata hivyo, alisema baada ya kuwatumia masharti hayo, wakuu wa shule hizo walishindwa kuwasilisha orodha ya wanafunzi kwa maofisa elimu wa mikoa na wilaya ili itumwe Necta na kutokana na mazingira hayo, baraza limeamua kusitisha kuwadahili wanafunzi wa kidato cha kwanza na kuitaka mamlaka inayosimamia elimu kuendelea na utaratibu wao wa kawaida.

“Necta imewasiliana na wahusika kwa barua rasmi ya kusitisha mtihani huo ambao ulipangwa ufanyike Februari 28, mwaka huu na wanafunzi wote waliopangiwa kidato cha kwanza shule mbalimbali za serikali zikiwemo za bweni, waendelee na masomo kama yalivyopangwa,” alieleza Naibu Katibu Mtendaji wa Necta.

Novemba mwaka jana, serikali ilitangaza kuwa wanafunzi 526,653 sawa na asilimia 94.8 ya waliofaulu mtihani wa darasa la saba mwaka jana, wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza katika shule za sekondari za serikali katika awamu ya kwanza huku 28,638 wakishindwa kupangiwa shule katika awamu ya kwanza.

Kati ya wanafunzi hao, wasichana ni 268,052 sawa na asilimia 94.5 ya wasichana waliofaulu na wavulana ni 258,601 sawa na asilimia 95.2 ya wavulana waliofaulu.

Chanzo: Habari Leo
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger