Saturday 29 March 2014

Kura mchanganyiko Bunge la Katiba

...

Kura mchanganyiko Bunge la Katiba

Mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, Profesa Abdul Shariff (kulia) akipiga kura ya siri wakati Bunge hilo jana lilipokuwa likipitisha utaratibu wa kupiga kura za aina mbili (siri na wazi). . 
Kwa ufupi
Mjumbe Vuai Ali Vuai alisema, wamefikia maridhiano hayo, ili kuwezesha kuendelea na mchakato wa katiba mpya kwani kila upande uliendelea kutetea msimamo wake hata katika kikao cha maridhiano.


Dodoma.Wajumbe wa Kamati ya Maridhiano jana walinusuru Bunge Maalumu la Katiba kuvunjika, baada ya kukubaliana kutumika kwa utaratibu wa upigaji kura wa wazi na siri kama ilivyopendekezwa na Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge.
Wajumbe hao walitangaza uamuzi huo bungeni kutokana na makubaliano yaliyofikiwa katika kamati ndogo ya maridhiano iliyofanyika jana asubuhi baada ya kushindwa kuafikiana katika kikao cha awali kilichofanyika juzi kuanzia saa 3:00 usiku hadi usiku wa manane ili kunusuru kukwama kwa Bunge hilo.
Kabla ya uamuzi huo, Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta alisema juzi usiku walikutana hadi usiku wa manane baada ya hapo, walikabidhi kamati ndogo yenye mchanganyiko wa wajumbe kutoka Kamati ya Kanuni na Kamati ya Maridhiano.
“Baada ya kukamilisha kazi, wajumbe wa kamati ndogo watatoa taarifa hapa ambao ni John Mnyika, Profesa Ibrahimu Lipumba, Vual Ali Vual na Askofu Donald Mtetemela,”alisema Sitta.
Akitoa taarifa ya maridhiano hayo, kwa niaba Freeman Mbowe, Mjumbe John Mnyika alisema, alianza kwa kunukuu kitabu kilichoandikwa na Mwalimu Nyerere, mwaka 1962 chenye ujumbe mahususi kwa Chama cha TANU akisema ujumbe huo kwa sasa ni sahihi kwa watu wengi na taasisi ikiwamo CCM.
Mnyika pia alisema Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) hawana nia yoyote ya kuvuruga mchakato wa katiba kama ambavyo imeelezwa katika siku za karibuni na viongozi, kwani wazo la kutaka Katiba Mpya imekuwa ni kilio chao cha muda mrefu.
Naye Profesa Lipumba alisema suala ambalo tumekuwa tukisimamia kwa muda mrefu suala ambalo lina utata, kati ambao wanapenda kura za uwazi na wale wa siri.
Alisema: “Tuliletewa mchanganyiko wa uwazi na siri, lakini maana yake ni kura ya uwazi, wenzetu wamekuwa na msimamo mkali hata hili la kufanya uamuzi ilikuwa tufanye kwa siri, lakini hata hivyo hawakukubali.”
“Tulifanya uamuzi ili tusonge mbele, basi tulipendekeza upigaji kura wa kuamua tupige kura kwa mfumo wa siri, lakini pia wenzetu walikataa,”alisema Profesa Lipumba.
Alisema kwa kuzingatia kutokwama kwa zoezi la kuanza kujadili rasimu, wameamua kukubali kutokubaliana.
“Ili kusonga mbele tunahitaji kusonga mbele tuanze kujadili Katiba, natoa wito kwa wenzangu wa chama tawala kwa kuwa mpo wengi mnadhamana kubwa, ni vyema mkawa na utaratibu wa kuwasikiliza wachache,” alisema.
Mjumbe Vuai Ali Vuai alisema, wamefikia maridhiano hayo, ili kuwezesha kuendelea na mchakato wa katiba mpya kwani kila upande uliendelea kutetea msimamo wake hata katika kikao cha maridhiano.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger