Sunday 1 August 2021

Picha : BITEKO AFUNGA MAONESHO YA BIASHARA NA TEKNOLOJIA YA MADINI SHINYANGA....ATANGAZA KUZINGUA WALIOSHIKILIA LESENI ZA UCHIMBAJI


Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko akizungumza wakati akifunga Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko leo Jumapili Agosti 1,2021 amefunga Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga yaliyoanza Julai 23,2021 katika uwanja wa Zainab Telack kijiji cha Butulwa kata ya Old Shinyanga Manispaa ya Shinyanga yakiongozwa na kauli mbiu “Uwekezaji wa Madini na Viwanda Shinyanga kwa Uchumi Endelevu”.

Akizungumza wakati wa kufunga Maonesho hayo, Biteko amewataka Wawekezaji walioshikilia leseni za uchimbaji madini kuendeleza na kuwazuia wananchi wenye uwezo wa kuchimba kuendeleza maeneo hayo na kwamba Serikali imewapa siku 60 baada ya hapo itafuta leseni hizo.

Amesema kumekuwapo na tatizo kwa baadhi ya wawekezaji wa madini kuhodhi lesseni kwa muda mrefu na kutozitumia na pale yanapovumbuliwa madini na wachimbaji wadogo ndipo hujitokeza na kudai eneo hilo ni lao.

Kufuatia hali hiyo, Biteko amesema wametoa siku 60 za kutaifisha leseni za uchimbaji wa madini zilizohodhiwa na wawekezaji kwa muda mrefu bila kuzitumia akibainisha kuwa Serikali imedhamiria kuinua Sekta ya Madini, pamoja na kumaliza migogoro yote ambayo hujitokeza baina ya wachimbaji wadogo na wakubwa.

"Naomba mfikishe salamu kwa wawekezaji wa madini ambao wana leseni za uchimbaji na hawazitumii, tumetoa siku 60 tu zianze kutumika, zaidi ya hapo tunazitaifisha na kutoza gharama ambazo Serikali imeingia kutokana kutolipiwa kodi kwa muda mrefu na kusababisha Serikali kukosa mapato  na fedha hizi lazima zilipwe hatutakuwa na msalia mtume, hatutaki migogoro ya uchimbaji madini," amesema Biteko.

Biteko pia amewataka wachimbaji wenye Leseni walipe kodi na waepuke vitendo vya utoroshaji madini akibainisha kuwa atakayetorosha madini atakuwa anachoma madini kwa tochi hivyo akikamatwa hatabaki salama.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Madini mkoa wa Shinyanga 'Shinyanga Region Miners Association – SHIREMA', Hamza Tandiko amezishukuru Taasisi za Kifedha kwa kuanza kuwapatia mikopo Wachimbaji wa Madini huku akiomba serikali kupeleka Umeme wenye nguvu ya kuendesha mitambo kwenye maeneo ya machimbo kwani umeme uliopo sasa ni kwa ajili ya mwanga tu.

Kwa upande wake, Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Said Pamui ambao ni miongoni mwa Wadhamini wakuu wa Maonesho hayo, amesema taasisi za kifedha ikiwemo Benki ya CRDB zimeanza kuwezesha mikopo vikundi vya Wachimbaji wa Madini na Wajasirimali hivyo kuwakaribisha kupata huduma katika Benki yao ambayo pia inatoa Bima za aina mbalimbali.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Philemon Sengati amesema maonesho hayo yamesaidia kuutangaza Mkoa huo na kuonyesha fursa za biashara hasa katika sekta ya madini. 

Amesema wataendelea kuboresha maonesho na kuwaunganisha wafanyabiashara na wajasirimali akiongeza kuwa Maonesho hayo ni muhimu kwa sababu mkoa wa Shinyanga una madini mengi na una madini ya pekee ya Almasi ambayo yanaendelea kuchochea ukuaji wa uchumi taifa.

"Kupitia maonesho haya washiriki wamepata fursa ya kutambulisha biashara zao, kuuza bidhaa na kujifunza teknolojia ya kisasa na kujua wapi wapate mitaji",amesema.

Hata hivyo amesema atakuwa mkali kwa watu wanaotorosha madini na atakayekamatwa atafirisika hivyo kuwataka wachimbaji madini kuzingatia sheria, kanuni na taratibu.

Tazama picha hapa chini
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko akizungumza wakati akifunga Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga yaliyoanza Julai 23,2021 katika uwanja wa Zainab Telack kijiji cha Butulwa kata ya Old Shinyanga Manispaa ya Shinyanga leo Jumapili Agosti 1,2021. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko akizungumza wakati akifunga Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga yaliyoanza Julai 23,2021 katika uwanja wa Zainab Telack kijiji cha Butulwa kata ya Old Shinyanga Manispaa ya Shinyanga leo Jumapili Agosti 1,2021.
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Prof. Idris Kikula akizungumza wakati wa ufungaji Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Philemon Sengati akizungumza wakati wa ufungaji Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko akiwapongeza Wanakwaya wa AICT Shinyanga wakitoa burudani kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, Bi. Zuwena Omary na Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga , Jasinta Mboneko wakicheza na Wanakwaya wa AICT Shinyanga kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga yaliyoanza Julai 23,2021
Mwenyekiti wa TCCIA Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Meshack Kulwa akizungumza wakati akifunga Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga yaliyoanza Julai 23,2021.
Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Madini mkoa wa Shinyanga ‘Shinyanga Region Miners Association – SHIREMA', Hamza Tandiko akizungumza wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi Kusini Mashariki ya Ziwa Victoria Dk. Emmanuel Joseph Makala akizungumza wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Said Pamui akizungumza wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, Zuwena Omary akizungumza wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Mkuu wa Mkoa wa Geita, Rosemary Senyamule akizungumza wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Katibu wa CCM mkoa wa Shinyanga, Donald Magesa akizungumza wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Mwakilishi wa Mkoa wa Mwanza akizungumza wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Said Pamui ambao ni miongoni mwa Wadhamini wakuu wa Maonesho hayo akionesha zawadi aliyopewa na Kamati ya Maonesho wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Mwakilishi wa Kampuni ya Barrick ambao ni miongoni mwa Wadhamini wakuu wa Maonesho hayo akionesha zawadi aliyopewa na Kamati ya Maonesho wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Wanafunzi wa shule za Little Treasures wakitoa burudani wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Kikundi cha Ngoma cha Mabulo ya Jeshi kikitoa burudani wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Wadau wakifuatilia matukio wakati wa kufunga Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Wanafunzi wa Shule za Hope wakitoa burudani wakati wa ufungaji wa Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (katikati) akiwa katika Banda la Tume ya Madini Mkoa wa Shinyanga kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga yaliyoanza Julai 23,2021 katika uwanja wa Zainab Telack kijiji cha Butulwa kata ya Old Shinyanga
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (katikati) akiangalia madini ya Almasi katika Banda la Tume ya Madini Mkoa wa Shinyanga kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (katikati) akiwa katika Banda la Wachimbaji Wadogo wa Madini Mgodi wa Mwakitolyo kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (kulia) akiwa katika Banda la Waundaji wa Miundo Michundo ' Shinyanga Best Iron kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga. Kushoto ni Mwenyekiti wa Shinyanga Best Iron, Kashi Salula akimuomba Waziri Biteko serikali ipeleke umeme wenye nguvu ya kuwasha mitambo kwenye maeneo ya machimbo.
Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Madini mkoa wa Shinyanga ‘Shinyanga Region Miners Association – SHIREMA', Hamza Tandiko akizungumza wakati Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (katikati) akiwa katika banda la SHIREMA kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Madini mkoa wa Shinyanga ‘Shinyanga Region Miners Association – SHIREMA', Hamza Tandiko akizungumza wakati Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko akiwa katika banda la SHIREMA kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (kulia) akiwa katika Banda la Mgodi wa Williamson 'Mgodi wa Mwadui' kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (wa tatu kulia) akiwa katika Banda la Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Barrick kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (kulia) akiwa katika Banda la Kampuni ya Barrick kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (kulia) akiwa katika Banda la Mgodi wa ZEMD kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (kulia) akiwa katika Banda la Stamigold kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko na msafara wake wakielekea katika mabanda mbalimbali kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (kushoto) akiwa katika Banda la SIDO kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (kulia) akiwa katika Banda la Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA) kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga. Kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa SHUWASA, Mhandisi Yusuph Katopola akielezea huduma zinazotolewa na SHUWASA.
Kushoto ni Meneja Biashara wa Benki ya CRDB tawi la Shinyanga, Mwanahamisi Iddi akimwelezea Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko huduma zinazotolewa na Benki ya CRDB ambayo sasa ina Akaunti ya HODARI isiyo na makato kwa ajili ya Wajasiriamali kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Kulia ni Meneja wa Benki ya NMB tawi la Manonga, Sebastian Kayaga akimwelezea Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko huduma zinazotolewa na Benki ya NMB alipotembelea banda la NMB kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Kulia ni Meneja wa Benki ya NBC tawi la Shinyanga, Joyce Chagonja akimwelezea Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko huduma zinazotolewa na Benki ya NBC alipotembelea banda la NBC kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (kulia) akiwa katika Banda la shule za Hope kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (kushoto) akiwa katika Banda la TANESCO kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga.
Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko (kulia) akiwa katika Banda la Kampuni ya Uzalishaji na Uuzaji wa dawa za asili maarufu Faraja Natural Herb Kigoma kwenye Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga. Kushoto ni Dkt. Faraja Peter akionesha dawa inayotibu matatizo ya upumuaji.

Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Share:

Vyombo Vya Ulinzi Na Usalama Na Mapambano Dhidi Ya Corona

 Na Abubakari Akida, MOHA
Vyombo vya Ulinzi na Usalama nchini vimetakiwa kutokujiweka kando na mapambano dhidi ya ugonjwa wa Virusi vya Korona katika kipindi hiki ambacho nchi inapitia katika vita ya wimbi la tatu la ugonjwa huo.

Rai hiyo imetolewa leo mkoani Tabora na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Khamis Hamza Chilo wakati akizungumza na Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama mkoani hapo ambapo ameeleza mapambano ya ugonjwa huo ni suala linalotakiwa kushirikisha wizara zote zikiongozwa na wizara husika ya afya.

“Vyombo vya Ulinzi na Usalama mnayo nafasi kubwa katika mapambano dhidi ya maradhi ya Virusi vya Korona,mna mahabusu wako vituo vya polisi sehemu mbalimbali nchini,mna mahabusu wako katika magereza,tuna askari wetu wa usalama barabarani basi ili mradi kila sehemu mnahusiana na jamii moja kwa moja hivyo natoa wito kwa vyombo vyetu vyote vya ulinzi na usalama nchi nzima mhakikishe katika kazi zenu za kila siku mtoe elimu ya kujikinga na maradhi hayo” alisema Naibu Waziri Chilo

“lakini pia tahadhari hiyo ya kujikinga na maradhi hayo pia iende kugusa shughuli zenu za kila siku ikiwemo na  nyie wenyewe kujikinga ili tusipoteze nguvu kazi ya taifa,Rais Samia Suluhu Hassani anawategemeeni sana katika kulinda amani na utulivu wan chi hii” aliongeza  Naibu Waziri Chilo

BONYEZA HAPA KUJUA VITUO VITAKAVYOTOA CHANJO YA CORONA TANZANIA


Awali akisoma taarifa ya hali ya ulinzi na usalama ya mkoa huo,Kamanda wa Polisi mkoa wa Tabora,Kamishna Msaidizi wa Polisi Sophia Jongo amesema kumekuwepo na kupungua kwa matukio ya uhalifu katika mkoa huo huku jeshi la polisi likiendelea na operesheni mbalimbali katika kuhakikisha matendo ya uhalifu yanapungua.

“Mheshimiwa Naibu Waziri katika mkoa wetu kulikuwepo na matukio ya kihalifu ikiwemo mauaji,Watoto watukutu kujikusanya makundi na kufanya uhalifu katika sehemu mbalimbali ikiwemo uporaji lakini sasa hivi tumedhibiti hiyo hali na sasa mkoa uko salama ama kwa upande wa mauaji tulikua tunashuhudia mauaji ya watu watatu mpaka watano kwa wiki lakini sasa hivi matukio hayo yameisha kabisa huku jeshi likiendelea kuimarisha ulinzi kupitia doria tulizonazo” alisema ACP Sophia Jongo

Naibu Waziri yuko mkoani Tabora kwa ziara ya kikazi ambapo anatumia ziara hiyo pia kutembelea makazi ya wakimbizi ya Ulyankulu yaliyopo wilayani Kaliua ambayo yanatumiwa na wakimbizi waliokimbia machafuko ya kikabila nchini Burundi.


Share:

Wachimbaji Wadogo Kupokea Kifuta Jasho Cha Milioni 90 -Singida


Na. Steven Nyamiti – Mkalama Singida
Jumla ya Wachimbaji Wadogo wa Dhahabu 90 katika eneo la kijiji cha Tumuli wataanza kupokea kifuta jasho kuanzia  tarehe 2 Agosti, 2021 baada ya utaratibu wa kupewa kifuta jasho kukamilika.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Madini Doto Biteko tarehe 31 Julai, 2021 katika kijiji cha Tumuli wilaya ya Mkalama Mkoani Singida wakati wa ziara ya kukagua na kutembelea shughuli za wachimbaji wadogo.

Ameeleza kuwa, wachimbaji watakaopokea kifuta jasho hicho ni wale walioandikishwa na ambao taarifa zao zipo kwenye Kanzidata kufuatia kuondolewa kuchimba kwenye eneo lenye leseni.

“Mgogoro huu una historia ndefu sana zaidi ya miaka 9, mwanzo walikua wachimbaji 26 wanaopaswa kupewa  lakini sasa wameongezeka zaidi ya 100, lazima tutende haki kwa watu wote kuanzia mchimbaji  hadi mwekezaji ili pande zote ziridhike,” amesema Biteko.

Aidha, Waziri Biteko ameagiza mgodi wa Chama cha Ushirika cha Uchimbaji Madini (Sekenke One Mining Cooperative Society) uliosimamishwa mwezi Disemba 2019, kutokana na zuio la kiusalama katika mgodi huo ufunguliwe mara moja  ili shughuli za uchimbaji ziendelee.

Biteko amemuagiza Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Singida, Chone Lugangizya kuzungumza na kampuni ya Sekenke One ili wakubaliane  waendelee kuchimba dhahabu kwa kuzingatia Sheria na Taratibu.

“Mimi ninachotaka kuona shughuli zinaendelea, utaratibu wa kufunga funga migodi huu huwa hautusaidii sana, tunaopoteza ni sisi, tunachotaka kuona wachimbaji wanarudi kwenye uchimbaji ili masoko haya yaweze kupanuka Zaidi,” amesisitiza Biteko.

Kuhusu utatuzi wa mgogoro baina ya Nabii Elia Makuli na kikundi cha Bathlomew Waziri Biteko amerejesha suala hilo kwenye ngazi ya Mkoa na Wilaya kwa ajili ya kulitatua ambapo Mkuu wa Wilaya ya Iramba Suleiman Mwenda amehaidi kufanyia kazi mgogoro huo kuanzia siku ya Jumatatu tarehe 2 Agosti.

Naye, Mkuu wa wilaya ya Mkalama Sophia Kizigo amethibitisha kuwa wilaya yake imepokea fedha hizo kutoka kampuni ya uchimbaji madini ya PuBo (PuBo Mining Limited) kiasi cha Shilingi Milioni 90 ambazo zimekabidhiwa kwenye ofisi ya TAKUKURU ili kifuta jambo hicho wapatiwe wananchi 90 waliopo kwenye kanzidata ambao watapokea kiasi cha Shilingi Milioni moja kila mmoja.

Kizigo ametoa onyo kwa wachimbaji wanaotaka kufanya udanganyifu ili kuongezea majina zaidi ya yale yanayotambulika.

“Wapo wananchi wananipigia simu wakitaja kuwa wao ni sehemu ya kupata kifuta jasho hicho, majina yao hayapo kati ya majina 90 ambayo tumeyapokea kutoka ofisi ya madini, nasisitiza tutafuata kanzidata ya Wizara ya Madini kama Waziri alivyoelekeza,” amesema Kizigo.

Waziri Biteko amehitimisha ziara ya siku mbili Mkoani ambapo ametembelea wachimbaji wadogo na kukagua Mgodi wa Kati wa Shanta, kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wachimbaji wadogo pamoja na kutoa elimu ya Sheria ya madini kwa wadau waliojitokeza. Katika ziara hiyo pia aliambatana na Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahembe na Viongozi mbalimbali wa Serikali ya Vijiji na Halmashauri


Share:

Waziri Mkuu Mgeni Rasmi Uzinduzi Mafunzo Ya Uanagenzi Mbeya


Na. MWANDISHI WETU
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika Uzinduzi wa Programu ya Mafunzo ya Uanagenzi kwa Awamu ya Tatu tarehe 2 Agosti, 2021 katika Chuo kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST).

Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama alipokutana na Waandishi wa Habari kwenye Ukumbi wa Chuo cha MUST kwa lengo la kutoa taarifa kwa umma kuhusu tukio la uzinduzi huo na shughuli zitakazoambatana na uzinduzi.

Kaulimbiu katika uzinduzi huu ni “NGUVUKAZI YENYE UJUZI STAHIKI, MSINGI IMARA KATIKA MAENDELEO YA TAIFA”. Kaulimbiu hii inatokana na dhana nzima ya masuala ya ajira, inatoa fursa kwa kila mmoja kuweza kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, ambapo anahitaji kuwa na ujuzi stahiki unaohitajika kufanya shughuli husika.

Akifafanua kuhusu programu hiyo, alieleza kuwa Ofisi yake imeendelea kuimarisha utekelezaji wa Programu ya Kukuza Ujuzi nchini kwa kuhakikisha inawafikia vijana wengi zaidi katika Mikoa yote nchini ambapo  Programu hii ina vipengele vikuu vinne (4) ambavyo ni mafunzo uzoefu wa kazi kwa wahitimu (internship), urasimishaji wa ujuzi uliopatikana nje ya mfumo rasmi wa mafunzo (RPL), mafunzo ya uanagenzi (apprenticeship) na mafunzo ya kuhuisha ujuzi kwa wafanyakazi (skills upgrading).

Mafunzo ya Uanagenzi yanahusisha mhusika kutumia asilimia 40 ya muda wake kwa masomo ya nadharia darasani na asilimia 60 ya muda wake kwa masomo ya vitendo sehemu ya kazi. Mafunzo haya ni ya muda wa miezi sita na yalianza kutolewa Mwezi Juni, 2021 na yanatarajiwa kukamilika Mwezi Disemba, 2021 ambapo Serikali inayafadhili  kwa asilimia 100 kulingana na kibali kilichotolewa na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

“Tangu kuanzishwa kwa Programu ya kukuza ujuzi nchini, mafunzo ya uanagenzi yamefanyika awamu mbili ambazo jumla ya vijana 28,941 wamenufaika. Awamu hii ya tatu yanatolewa kwa vijana 14,440 na yanafanyika kupitia vyuo 72 katika Mikoa 26 ya Tanzania Bara”,alisisitiza Waziri Mhagama

Aliongezea kuwa mafunzo haya yanatolewa katika fani mbalimbali kama vile ufundi umeme wa majumbani na viwandani, umeme wa jua, useremala, ufundi magari, umeme wa magari, uchomeleaji na uungaji vyuma, utengenezaji wa vifaa vya aluminiam, upishi, uhudumu wa hoteli na vinywaji, ushonaji, uchenjuaji wa madini, ufundi bomba, ufundi uashi, uwekaji wa terazo na marumaru, ufundi viyoyozi na majokofu.

Aidha hadi Disemba, 2021 kutatarajia kuwa na jumla ya wanufaika wa kupitia programu zote nne kufikia 80,320. Kati ya hawa, vijana 43,381 ni kupitia mafunzo ya uanagenzi, vijana 20,334 kupitia mafunzo ya urasimishaji ujuzi, vijana 5,975 kupitia mafunzo ya uzoefu wa kazi (internship), vijana 9,080 (100 nchini Israel) kupitia mafunzo ya kilimo cha kisasa kwa kutumia kitalu nyumba (green house), na vijana 1,550 kupitia mafunzo ya kukuza ujuzi wa waajiriwa (skills upgrading).

Sambamba na uzinduzi huo Mhe.Waziri Mkuu anatarajiwa kuwa na shughuli mbalimbali zitakazofanyika Mkoani Mbeya.

“Mhe. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atatembelea vyuo vinavyotoa mafunzo ya Uanagenzi Jijini Mbeya, atatembelea Kyela Polytechnic College, VETA Busokelo, VETA Mbeya, Chuo cha Ufundi cha Magereza Ruanda na Chuo cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST) ili kuona na kukagua namna mafunzo yanavyotolewa, na kuweza kuzungumza na vijana wanaopata mafunzo husika”,alisema Waziri Mhagama.

Akihitimisha Waziri alitumia nafasi hiyo kuwaasa wananchi wote kuzingatia suala zima la afya hususan kipindi hiki ambapo tuna mlipuko wa COVID 19 nchini kwa kuchukua tahadhari zote huku wakizingatia maelekezo yanayotolewa na wataalamu wetu nchini.

“Ninapenda kutoa wito kwa wananchi watakaoshiriki kwenye tukio la uzinduzi huu kuchukua tahadhari zote ikiwemo kuvaa barakoa, kutumia vitakasa mikono na kunawa mikono kama inavyoelekezwa na wataalamu wa afya ili kujilinda na kulinda wengine”.


Share:

Rais Samia kufanya ziara ya kiserikali ya siku mbili nchini Rwanda

 Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan anatarajia kufanya ziara ya kiserikali ya siku mbili nchini Rwanda kuanzia Agosti 2, 2021 kwa mwaliko rasmi wa wa Rais wa nchi hiyo, Paul Kagame

Akiwa Rwanda, Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na mengine atafanya mazungumzo rasmi na mwenyeji wake, kisha atashuhudia utiaji saini hati za makubaliano na kuzungumza na vyombo vya habari

Taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu imeeleza kuwa ziara hiyo ya siku mbili inalenga kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano baina ya Rwanda na Tanzania.



Share:

BARRICK KUFANIKISHA KANUNI YA USHIRIKISHWAJI WATANZANIA KATIKA MNYORORO WA UCHUMI WA MADINI KWA VITENDO

Mwenyekiti wa Tume ya Madini,Profesa Idris Kikula (Kushoto) akibadilishana mawazo na Meneja wa Barrick nchini,Georgia Mutagahywa (Kulia) na Kamishna wa Madini kutoka Tume ya Madini,Janeth Lekashingo wakati wa warsha hiyo.
 ***
Kampuni ya madini ya Barrick, imeeleza dhamira yake ya kujipanga zaidi kuhakikisha inafanikisha kutekeleza kwa vitendo kanuni ya Serikali inayoyataka makampuni ya madini kushirikisha Watanzania katika mnyororo wa uchumi wa madini.

Haya yamebainishwa katika warsha ya siku mbili kuhusiana na utekelezaji wa kanuni hiyo, iliyoandaliwaTwiga Minerals Corporation na Barrick na kuhudhuriwa na Mameneja Waandamizi wa kampuni hizo, Mwenyekiti na watendaji waandamizi wa Tume ya Madini , wadau kutoka taasisi mbalimbali za Serikali iliyofanyika katika mgodi wa Barrick North Mara.

Akitoa mada kuhusu jitihada zinazofanywa na Barrick kutekeleza kanuni hiyo, Meneja wa barrick nchini, Georgia Mutagahywa, alisema kampuni imeanza kutekeleza kanuni kwa vitendo katika maeneo ya ajira, utoaji wa zabuni, sambamba na kuendesha miradi ya kusaidia jamii katika maeneo yanazozunguka migodi yake ya Buzwagi, Bulyanhulu na North Mara, kupitia sera ya kampuni ya kuhudumia jamii (CSR).

Miradi inayotekelezwa na Barrick imelenga kuboresha miundo mbinu mashuleni na vituo vya afya ,kuwapatia wananchi elimu ya ujasiriamali, maji safi na miundo mbinu ya barabara .

Hata hivyo alisema kampuni inahitaji ushirikiano zaidi katika kukabiliana na changamoto mbalimbali inazokumbana nazo katika utekelezaji wa Sheria ya Madini na kanuni hii.

Mutagahywa, alisema kampuni iko mbioni kuanzisha programu ya kuendeleza biashara za wananchi (Local Business Development Programme (LBD), ambayo itakuwa kitovu cha kusimamia kanuni hii na kuhakikisha watanzania wananufaika nayo kwa asilimia kubwa kwa kuboresha maisha yao kupitia uwekezaji katika sekta ya madini,

Katika hotuba yake ya ufunguzi wa warsha hii, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa.Idrisa Kikula, alisema kuwa tangia tume hiyo ianze kufanya kazi, imekuwa mstari wa mbele kuratibu ushirikishwaji wa watanzania katika sekta ya madini.”Tumekuwa tukifuatilia kuhakikisha watanzania na makampuni ya wazawa yanapewa kipaumbele katika zabuni za kuuza bidhaa na kutoa huduma kwenye migodi isipokuwa huduma ambazo hazipatikani na ufuatiliaji huu umeanza kuleta matokeo mazuri”alisema.

Profesa Kikula, aliendelea kueleza kuwa tume ya madini iko tayari kusaidia Twiga kuhakikisha inafanikiwa kutekeleza kanuni hii inayotoa fursa kwa watanzania kunufaika na ushirikishwaji katika mnyororo wa uchumi wa madini kwa kutoa ufafanuzi wa changamoto mbalimbali ambazo kampuni inapambana nazo katika utekelezaji wake.

Warsha hii iliendeshwa kwa njia ya majadiliano na mafunzo ambapo wataalamu wa uendeshaji shughuli za madini kutoka Tume ya Madini, Janeth Lekashingo, Terrence Ngole na Godfrey Nsemwa, walitoa mada mbalimbali zinazoelekeza na kufundisha ufanikishaji wa utekelezaji wa kanuni hii.

Kanuni ya ushirikishwaji wa watanzania katika mnyororo wa uchumi wa madini, inaelekeza wawekezaji katika sekta hii kuweka kipaumbele katika matumizi ya bidhaa na huduma zinazozallishwa nchini isipokuwa bidhaa zinazohitajika ambazo hazipatikani nchini ambapo wazabuni wanaotumika kuagiza bidhaa hizo wanapaswa kushirikiana na makampuni ya wazawa, hali ambayo itakuza sekta ya biashara nchini na hivyo kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla,Kanuni hii pia inaelekeza kutoa ajira kwa watanzania na kuondoa tofauti ya mishahara kwa wanaofanya kazi zinazofanana
Washiriki wa warsha hiyo wakifuatilia mada mbalimbali


Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAPILI AGOSTI 1,2021



Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger