Friday 5 April 2024

WANAFUNZI WANAOTARAJIA KUHITIMU KIDATO CHA SITA WAHIMIZWA KUTUMIA VYEMA ELIMU WALIYOIPATA

...


Wanafunzi wanaotarajia kuhitimu   masomo ya kidato cha Sita katika Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera wamehimizwa kutumia elimu waliyoipata shuleni kuleta mabadiliko katika jamii inayowazunguka na kujiepusha na makundi yasiyofaa hasa wakati watakaokuwa wakisubiri matokeo ya mitihani yao.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Bukoba Mjini James Nyamanza wakati alipokuwa mgeni Rasmi katika Mahafari ya Kidato cha Sita ya  Umoja wa Wanafunzi Wasabato  Kanda ya Bukoba Mjini(ASSA) yaliyofanyika shule ya Sekondari Nyakato.

Nyamanza amewahimiza wanafunzi hao wanaotarajia kufanya mitihani yao ya kuhitimu kidato cha sita kuhakikisha elimu waliyoipata inakuwa chachu ya maendeleo katika jamii zao na sio kwenda kuwa kikwazo kwa kujiingiza katika makundi yasiyofaaa wakati watakaokuwa wakisubiri matokeo ya mitihani yao.

Amesema kuwa walimu wao wametumia muda mwingi kuhakikisha wanapata elimu hiyo lakini pia wazazi wametumia gharama kubwa ya kuwasomesha hivyo wanatakiwa kuwa mfano mzuri kwenye jamii na kuwa mfano bora wa kuigwa na wanafunzi wengine wanaoendelea na masomo.

Katika mahafali hayo mgeni Rasmi  aliendesha Harambee kwa kushirikiana na Wazazi,Viongozi wa dini, Walimu na Wageni waalikwa  ambapo katika harambee  hiyo kiasi kilichopatikana kilielekezwa   kukarabati  Kanisa lililopo jirani na shule ya Sekondari Nyakato.

Mahafali hayo yameshirikisha shule zote za Sekondari zenye wanafunzi Wasabato ambao wameshiriki kwa pamoja kuwaaga wanafunzi wenzao wanaotarajia kuhitimu kidato cha Sita  ikiwemo shule ya Sekondari Nyakato, Ihungo, Kahororo,Rugambwa, Kagemu,Bukoba Sekondari, Mugeza, Buhembe, Maruku na Bakoba.



Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger