Monday, 31 March 2025
SERIKALI YAANZA UTEKELEZAJI WA MRADI WA BILIONI 4 KUBORESHA HUDUMA YA MAJI MBINGA
Katibu Tawala wa Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma Pendo Damas,akizungumza kwenye hafla ya utiaji saini mkataba wa ujenzi wa mradi wa kuboresha huduma ya maji katika kata nane za Wilaya hiyo,katikati Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Mji wa Mbinga(Mbiuwasa)Mhandisi Yonas Ndomba na Mkuu wa Wilaya hiyo Kisare Makori.
Baadhi ya Wenyeviti wa mitaa Halamshauri ya Mji Mbinga Mkoani Ruvuma,wakifuatilia zoezi la utiliaji saini mkataba ya ujenzi wa mradi wa uboreshaji wa huduma ya maji katika kata nane za Wilaya ya Mbinga.
Na Regina Ndumbaro-Mbinga.
Halmashauri ya Mji Mbinga mkoani Ruvuma imeingia mkataba na kampuni ya Ngongo Engineering Ltd kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa uboreshaji wa huduma ya maji katika kata nane za Wilaya ya Mbinga.
Hafla ya utiaji saini mkataba huo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali, akiwemo Katibu Tawala wa Wilaya ya Mbinga, Pendo Damas, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mbinga (Mbiuwasa), Mhandisi Yonas Ndomba, na Mkuu wa Wilaya hiyo, Kisare Makori.
Mradi huo unatarajiwa kutekelezwa kwa kipindi cha miezi 12 kwa gharama ya shilingi bilioni 4, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita kuboresha huduma za maji safi na salama kwa wananchi.
Baadhi ya wakazi wa kata ya Masumuni wameishukuru Serikali kwa kuleta mradi huo mkubwa wa maji, wakisema utamaliza changamoto ya upatikanaji wa maji katika eneo hilo.
Mkazi wa Masumuni, Moses Mdaka Mapunda, amesema tangu Mji wa Mbinga ulipoanzishwa, haujawahi kupata fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maji kama ilivyo sasa.
Amesisitiza kuwa mradi huo utasaidia kupunguza adha ya upatikanaji wa maji kwa wananchi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakipata maji kwa mgao na mara nyingine kulazimika kutembea umbali mrefu kutafuta maji kwa matumizi ya familia zao.
Kwa upande wake, mkazi mwingine wa kata hiyo, John Yapesa, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) tawi la Masumuni, ametoa wito kwa mkandarasi wa mradi huo kuhakikisha kazi inafanyika kwa haraka na kwa ubora wa hali ya juu.
Ameeleza kuwa upatikanaji wa maji ni tatizo kubwa katika kata hiyo, na wanawake pamoja na watoto hutumia muda mwingi kutafuta maji, jambo ambalo linaathiri maendeleo yao.
Yapesa amependekeza mkandarasi kufanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kuanza kunufaisha wananchi haraka iwezekanavyo.
Mkazi wa mtaa wa Lusaka, Fides Ngonyani, naye amepongeza juhudi za Serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha wananchi wa Mbinga wanapata huduma bora za maji.
Ameomba kuhakikisha mtandao wa mabomba unapanuliwa ili wananchi wengi zaidi wafikiwe na huduma hiyo moja kwa moja kwenye makazi yao badala ya kuendelea kutegemea maji ya mgao.
Pia amewataka wananchi kushirikiana na Serikali kwa kulinda miundombinu ya maji na kutunza vyanzo vya maji ili kuhakikisha mradi huo unadumu kwa muda mrefu.
Katibu wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Mbinga, Ali Simba, amesema utekelezaji wa mradi huu ni sehemu ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM na unadhihirisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuboresha maisha ya wananchi.
Ameeleza kuwa mradi huu ni moja ya mikakati ya kumtua mama ndoo kichwani, huku akiwataka wananchi kushirikiana na Serikali katika miradi mingine ya maendeleo ili kuimarisha ustawi wa jamii na kukuza uchumi wa taifa.
Sunday, 30 March 2025
MBUNGE DKT. JOSEPH KIZITO MHAGAMA AELEZA UTEKELEZAJI WA MIRADI MADABA

Mbunge wa Jimbo la Madaba Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama akiwapungia mkono wananchi wa kijiji cha Lituta Halmashauri ya Madaba Mkoani Ruvuma

Mbunge wa Jimbo la Madaba Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama akicheza ngoma wakati wa mapokezi yake kijiji cha Lituta Halmashauri ya Madaba Mkoani Ruvuma
Wananchi wa kijiji cha Lituta Halmashauri ya Madaba Mkoani Ruvuma wakimshangilia Mbunge wa Jimbo hilo Dkt Joseph Kizito Mhagama
Na Regina Ndumbaro-Madaba.
Katika mkutano wa wananchi na wanachama wa Kijiji cha Lituta, Halmashauri ya Madaba, Mbunge wa Jimbo hilo, Dkt. Joseph Kizito Mhagama, ameishukuru jamii kwa mapokezi mazuri na uungwaji mkono wanaompa katika safari yake ya uongozi.
Wananchi wa Lituta walichanga fedha kwa ajili ya kumuwezesha kuchukua tena fomu ya ubunge kwa uchaguzi wa mwaka huu, jambo ambalo Mhagama amelipokea kwa furaha na shukrani.
Amewaahidi wananchi hao kuwa ataendelea kuwatumikia kwa bidii na kuhakikisha maendeleo yanaimarika katika maeneo yote ya jimbo hilo.
Katika hotuba yake, Mhagama ameeleza kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali yenye thamani ya shilingi bilioni 7.69 katika sekta tofauti kijiji cha Lituta.
Katika sekta ya afya, amesema kuwa hospitali ya wilaya imekamilika, ikiwa na vifaa vyote muhimu kwa utoaji wa huduma bora kwa wananchi.
Aidha, ameeleza kuwa maendeleo katika sekta za barabara, elimu, umeme na maji yamefanyika kwa kiwango kikubwa, na kuwa serikali inaendelea kuwekeza katika miradi hiyo ili kuimarisha maisha ya wakazi wa Madaba.
Pamoja na mafanikio hayo, Mhagama ameonesha masikitiko yake kuhusu vitendo vya wizi vilivyofanywa na baadhi ya watu walioiba vifaa vya Hospitali ya Halmashauri ya Madaba.
Amesema kuwa wahusika wamebainika, majina yao yamehifadhiwa, na hatua za kisheria zimechukuliwa dhidi yao.
Amehakikisha kuwa hospitali hiyo inaendelea kutoa huduma bila shida, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kushirikiana katika kulinda miundombinu ya umma ili kuendeleza maendeleo yaliyopatikana.
Katika sekta ya miundombinu, Mhagama ameeleza kuwa ujenzi wa barabara na madaraja unaendelea, huku zaidi ya shilingi bilioni 1.5 zikiwa zimetumika katika mradi huo.
Amesisitiza dhamira yake ya kuhakikisha barabara zote za lami zinajengwa ndani ya Halmashauri ya Madaba, ikiwa ni pamoja na barabara ya Kifaguro.
Vilevile, amesema mradi wa maji utaimarishwa zaidi ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za maji safi na salama.
Mhagama amewataka wananchi wa Lituta na Madaba kwa ujumla kuwa na mshikamano na kutoacha mtu yeyote kuvuruga maendeleo yao kwa maslahi binafsi.
Amesema kuwa maendeleo yaliyopatikana ni matokeo ya juhudi za pamoja, na akawataka wananchi kutokubali maneno ya upotoshaji dhidi ya viongozi wanaowahudumia.
Amewasihi kushiriki kikamilifu katika uchaguzi ujao kwa kuchagua viongozi wanaoleta maendeleo kwa Madaba.















































