Saturday 21 May 2022

TAKUKURU KUINGIA KAZINI UNUNUZI WA PAMBA

...
Mrajis msaidizi wa ushirika mkoa wa Geita, Doreen Mwanri, akizungumza na wajumbe wa chama kikuu cha ushirika wa mazao Chato.
Baadhi ya wajumbe wa Chama Kikuu cha Ushirika wa mazao Chato (CCU)wakiendelea kupokea maelekezo ya viongozi wa ushirika
Na Daniel Limbe, Chato

MSIMU wa ununuzi wa zao la pamba ukiwa umefunguliwa rasmi nchini, Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (Takukuru)wilayani Chato mkoani Geita imesema imejiandaa vyema kufuatilia vitendo vyote vya rushwa kwa viongozi wa vyama vya msingi (Amcos).

Aidha imewaonya viongozi wa Amcos 53 zinazounda ushirika wa mazao wa "Chato Co-Operative Union (CCU) kutojihusisha na wizi wa pembejeo za wakulima pamoja na fedha za ushirika huo.

Kaimu kamanda wa Takukuru wilaya ya Chato, Felix Vedastus, ameyasema hayo leo,mbele ya wajumbe zaidi ya 100 ambao wameshiriki mkutano mkuu wa uchaguzi wa viongozi wa Ushirika wa CCU.

Hatua hiyo ni baada ya Mrajisi msadizi wa Ushirika mkoa wa Geita, Doreen Mwanri, kuzilalamikia baadhi ya amcos ambazo zinadaiwa kupata hasara kila msimu, huku baadhi ya wajumbe wakidaiwa kuiba pembejeo za wakulima.

Mbali na hilo, Mwanri, amedai serikali haitawaonea huruma baadhi ya makatibu wa amcos ambao watabainika kujihusisha na wizi wa fedha za ununuzi wa zao la pamba, kwa kuwa hali hiyo isipodhibitiwa inaweza kufifisha jitihada za serikali kuinua ushirika nchini.

"Lazima mtambue kuwa fedha zinazoletwa kwenu kununua pamba ni mkopo...na mnapaswa kuzilejesha kwa mujibu wa sheria...haiwezekani makatibu wachache watuharibie ushirika wetu kwa tamaa zao binafsi hatutakubali"amesema.

Kadhalika amesisitiza umoja miongoni mwa wajumbe na viongozi na kujiepusha na vitendo vya kuhujumu ushirika huo kwa kuwauzia pamba safi makampuni ya watu binafsi badala ya CCU, ambacho ndiyo chama kikuu cha ushirika huo.

Mkutano huo maalumu umeandaliwa na Mrajis wa ushirika mkoa wa Geita ili kutekeleza takwa la kisheria la kuwachagua viongozi wa Chama hicho ambapo wajumbe hupaswa kuchaguliwa kila baada ya miaka mitatu.
Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger