Tuesday, 28 April 2026
Monday, 27 April 2026
MARIDHIANO YATALIPONYA TAIFA NA KUDUMISHA AMANI NA MSHIKAMANO- SHEIKH JALALA
Sheikh Mkuu wa Jumuiya ya Shia Ithnaasharia Tanzania (TIC), Maulana Sheikh Hemedi Jalala ameipongeza Tume huru ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani wakati na baada ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, akisema baada ya kuisikiliza ripoti ya Tume hiyo anaamini kuwa mapendekezo yake yanaenda kuondoa tofauti na changamoto za sasa na kurejesha umoja wa Kitaifa.
Sheikh Jalala ameyasema hayo leo Jumatatu Aprili 27, 2026 wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar Es Salaam, akimpongeza pia Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutangaza mchakato wa maridhiano Nchini, akisema kuwa maridhiano ndiyo yatakayotibu tofauti zote na majeraha mbalimbali kwa makundi tofauti ya kijamii na kisiasa.
"Kwakweli tayari tumepita kwenye matatizo, kwenye changamoto, sasa hivi muhimu ni kuangalia namna gani tunalirudisha taifa kwenye hali yake ya kawaida, namna gani watanzania wanarudi kwenye mshikamano, kwenye umoja wao wa Kitaifa na kwenye nchi yao ambayo ni kisiwa cha amani." Amesema Sheikh Jalala.
Kiongozi huyo wa dini amekumbusha pia umuhimu wa Viongozi wa dini nchini kuwa mstari wa mbele katika kuhubiri amani na maridhiano kwa waumini wao, akisema kuwa ikiwa yatatekelezwa yote yaliyosemwa katika ripoti ya Tume ya Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Othman Chande pamoja na kila mmoja kushiriki kwenye mchakato wa maridhiano, Taifa litabakia kuwa salama, lenye amani na mshikamano kwa kila mmoja.
WENZA WA MAJAJI WAWAFARIJI WAGONJWA WA SARATANI DAR
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM
Kikundi cha We Are Family kinachowahusisha wenza wa majaji nchini, kimetembelea wagonjwa wa saratani katika Ocean Road Cancer Institute jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira yao ya kufanya matendo ya huruma kwa jamii.
Kikundi hicho chenye wanachama 59 waliosajiliwa, kimeeleza kuwa pamoja na shughuli nyingine, pia kinalenga kuwafikia wenza wa majaji wastaafu na waliopo kazini kwa lengo la kuimarisha mshikamano na kusaidiana katika masuala ya kijamii.
Akizungumza Aprili 26, 2026, Makamu Mwenyekiti wa kikundi hicho, Edivije Nangela, amesema uamuzi wa kutembelea wagonjwa wa saratani ulifikiwa baada ya kufanya tathmini na kufuata taratibu zote muhimu zilizowezesha kuwafikia wahitaji hao.
Amebainisha kuwa, licha ya kulenga kuwafikia wagonjwa 100, wamefanikiwa kuwafikia wagonjwa 39 pekee, hali inayodhihirisha ukubwa wa uhitaji uliopo pamoja na changamoto ya gharama kubwa za matibabu.
“Uhitaji ni mkubwa sana na gharama za matibabu ni kubwa, hivyo kuna umuhimu wa kuendelea kuweka mikakati ya kuwafikia watu wengi zaidi,” amesema Nangela.
Ameongeza kuwa kikundi hicho kinatarajia kufanya kikao maalum kitakacholenga kuweka mikakati endelevu ya kusaidia makundi mbalimbali yenye uhitaji katika jamii.
Kwa upande wake, Mratibu wa Matukio wa kikundi hicho, Beatrice Mdemu, amesema zoezi hilo litakuwa endelevu na kuwahimiza wenza wengine wa majaji kujiunga na kikundi hicho ili kuongeza nguvu katika kufanikisha malengo yao ya kijamii.
Naye Afisa wa Ocean Road Cancer Institute, Karafuu Ally, kwa niaba ya uongozi wa taasisi hiyo, amekishukuru kikundi hicho kwa kutembelea wagonjwa na kutoa faraja, akisisitiza umuhimu wa kuendeleza moyo wa kujitolea kwa jamii.
Magazeti














