Wednesday, 15 April 2026

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATANO APRILI 15 2026

Magazeti

 


Share:

CRDB YAWAPA DILI NONO WATEJA: WASHINDI KUSAFIRI MAREKANI KUSHUHUDIA KOMBE LA DUNIA 2026


Benki ya CRDB imeendelea kuwazawadia wateja wake kwa zawadi nono kupitia promosheni maalum ya matumizi ya kadi ya TemboCard Visa, huku zawadi kubwa ikiwa ni safari ya kwenda Marekani kushuhudia fainali za Kombe la Dunia 2026.

Zawadi hizo zimekabidhiwa Aprili 14, 2026 katika hafla iliyofanyika makao makuu ya benki hiyo yaliyopo Upanga, jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kuhamasisha matumizi ya mifumo ya malipo ya kidijitali nchini.

Kupitia kampeni hiyo, wateja wanahimizwa kutumia TemboCard Visa katika malipo yao ya kila siku kupitia mashine za POS au mtandaoni, ambapo kila muamala unaongeza nafasi ya kushiriki katika droo mbalimbali za ushindi.
Akizungumza na waandishi wa habari, Meneja Mwandamizi wa Kitengo cha Kadi (Card), Karington Chahe, amesema lengo la kampeni hiyo ni kuwapa wateja fursa ya kipekee ya kushinda zawadi kubwa huku wakinufaika na huduma salama, rahisi na za kisasa.

Ameeleza kuwa droo ya kwanza tayari imefanyika na kutoa washindi kadhaa waliopata zawadi mbalimbali ikiwemo runinga janja (Smart TV) za inchi 80 pamoja na vifurushi vya DSTV kwa washindi watatu.

Chahe amebainisha kuwa zawadi ya kilele katika kampeni hiyo ni tiketi nne kwa Watanzania kusafiri kwenda Marekani kushuhudia mashindano ya Kombe la Dunia 2026, yatakayowakutanisha mastaa wakubwa wa soka duniani kama Lionel Messi na Cristiano Ronaldo.

“Tunawahimiza wateja wetu kuendelea kutumia kadi zao katika malipo ya kila siku ili kuongeza nafasi ya kushinda zawadi hizi adhimu, ikiwemo safari ya kwenda kushuhudia Kombe la Dunia,” amesema Chahe.

Kampeni hiyo ilizinduliwa rasmi Machi 12, 2026, ikiwa na lengo la kuhamasisha matumizi ya teknolojia ya malipo ya kidijitali pamoja na kuwazawadia wateja kwa uaminifu wao kwa benki hiyo.

Kwa mujibu wa Benki ya CRDB, hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wake wa kuendeleza ubunifu katika huduma za kifedha, huku ikiwahamasisha Watanzania kupunguza matumizi ya fedha taslimu na kuhamia katika mifumo ya kisasa iliyo salama na yenye ufanisi.
Share:

Tuesday, 14 April 2026

SANGU APIGILIA MSUMARI TUNU ZA TAIFA: ASEMA AMANI NA MARIDHIANO NDIO MUHIMILI

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu akikabidhi risiti ya benki ya Tsh. Milioni 20,000,000 kwa Padri Didas Nandi, kwa ajili ya ujenzi wa Kanisa la Parokia ya Mt. Fransisco wa Asiz iliyopo Msandamungano, mkoani Rukwa, leo Aprili 12, 2026. Pesa hiyo imetolewa na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba,


Katika mkakati kabambe wa kuimarisha mshikamano wa kitaifa, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Mhe. Deus Sangu, ametoa wito mzito kwa Taasisi na Viongozi wa Dini nchini kutosimama kando, bali kuwa mstari wa mbele kushirikiana na Serikali kulinda na kudumisha Tunu za Taifa.

Akizungumza  mkoani Rukwa, Waziri Sangu amesisitiza kuwa Amani, Upendo, Mshikamano, na Umoja wa Kitaifa ndivyo vishikizo vikuu vinavyolishikilia Taifa la Tanzania, na bila misingi hiyo, ustawi na maendeleo ya kweli hayawezi kupatikana.

Mabilioni ya Harambee na Ishara ya Umoja

Mhe. Sangu aliyasema hayo alipomwakilisha Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, katika harambee ya ujenzi wa Kanisa la Parokia ya Mt. Fransisco wa Asizi, Msandamungano iliyofanyika kanisani hapo leo Aprili 12, 2026. 

Katika tukio hilo la kihistoria lililojaa hekaheka za kizalendo, zaidi ya Tsh. Milioni 53 zilichangwa, huku Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba akionyesha mfano kwa kuchangia Tsh. Milioni 20 taslimu—ishara tosha ya namna Serikali inavyothamini mchango wa taasisi za dini katika ujenzi wa nchi.

Dhamana ya Mahusiano na Dira ya 2050

Waziri Sangu ameweka wazi kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu imepewa dhamana nzito ya kuratibu mahusiano kati ya Serikali na makundi ya kijamii ili kuhakikisha maridhiano yanatawala. 

Alibainisha kuwa ushirikiano huo umedhihirishwa kwa vitendo kupitia ushirikishwaji wa viongozi wa dini katika kuandaa Dira ya Maendeleo 2050.

"Dhamira yetu ni kuijenga Tanzania tuitakayo kupitia maono ya pamoja. Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inatambua kuwa viongozi wa dini ni nguzo muhimu katika kulea vijana kiroho ili wawe wazalendo, wenye maadili mema na tabia njema zinazochochea jamii tulivu yenye amani," alisema Waziri Sangu.

Rai kwa Waumini na Viongozi
Waziri huyo hakusita kuwasihi waumini kumuunga mkono Rais Samia kwa vitendo, akisisitiza kuwa ujenzi wa taasisi za dini ni sehemu ya maendeleo ya kijamii ambayo Serikali itaendelea kuyaunga mkono.

 Alimshukuru Paroko wa Parokia hiyo, Padri Didas Nandi, kwa kuratibu vyema harambee hiyo inayolenga kukusanya jumla ya Tsh. Milioni 900 kwa ajili ya kukamilisha nyumba hiyo ya ibada.

Padri Nandi: Sisi ni Kiungo cha Amani
Kwa upande wake, Padri Didas Aisakus Nandi ameahidi kuwa Kanisa litaendelea kuwa kiungo muhimu kati ya waumini na Serikali. Alisisitiza kuwa juhudi zao za kiroho hazitaishia madhabahuni, bali zitakwenda mitaani kuhamasisha amani, ushirikiano na maendeleo endelevu ili kuhakikisha Tunu za Taifa hazitikisiki.







Share:

Monday, 13 April 2026

LALJI FOUNADATION YAENDESHA KAMBI YA MATIBABU YA MACHO BURE KIGOMA


Taasisi ya LALJI FOUNDATION kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Kigoma Hilltop Hotel, Ahlulybayt Academic Center, Vision 4 All Eye Centre pamoja na Supa Foam imeendesha kambi maalumu ya siku nne ya matibabu ya macho bure kwa wakazi wa mkoa wa Kigoma.

Kambi hiyo ilifanyika kuanzia tarehe 03 hadi 06 Aprili 2026 katika viwanja vya shule za Ahlulbayt Islamic Center Manispaa ya Kigoma Ujiji, ilitoa huduma mbalimbali muhimu ikiwemo uchunguzi wa macho, ushauri wa kitaalamu, utolewaji wa miwani, huduma za dawa pamoja na upasuaji wa mtoto wa jicho bila malipo.

Akizumza baada ya kukamilika kwa kambi hiyo mlezi wa Taasisi ya LALJI FOUNDATION Mohsen Lalji amesema Zaidi ya wananchi 6000 walijiotokeza kupata huduma ambapo watu 5079 walifanyiwa uchunguzi wa macho, 2218 walipatiwa miwani ya macho, 518 walifanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho na watu 3215 walipatiwa dawa za macho huku huduma zote zikitolewa bure bila malipo.

Amesema lengo la kambi hiyo ni kuunga mkono juhudi za serikali na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na endelevu kwa wakati na ukaribu zaidi.

Akizindua rasmi kambi hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Mh Balozi Simon Sirro aliipongeza LALJI FOUNDATION na washirika wake kwa jitihada hizo za kuwafikia wananchi na kuwapatia huduma muhimu za matibabu ya macho, hususan kwa wale wasio na uwezo wa kumudu gharama za matibabu.

Aidha, aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi ili kunufaika na huduma hizo, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali na taasisi zisizo za kiserikali katika kuboresha huduma za kijamii na kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

Wakizungumza baada ya kupatiwa huduma, wananchi wengi walieleza kuwa walikuwa hawana uwezo wa kumudu gharama za matibabu ya macho, ikiwemo upasuaji na ununuzi wa miwani, hali iliyowafanya kuendelea kuishi na matatizo ya macho kwa muda mrefu.

Wananchi hao pia waliomba juhudi kama hizi ziendelee kudumishwa ili kuwasaidia watu wengi zaidi, hasa wale wa kipato cha chini ambao bado wanakabiliwa na changamoto ya kumudu gharama za huduma za afya.

Kambi hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi za wadau wa maendeleo katika kuhakikisha jamii inapata huduma bora za matibabu ya macho hususan katika maeneo yenye uhitaji mkubwa kama Kigoma.
Share:

AMANI NA MARIDHIANO: NGUZO KUU INAYOIFUNGULIA SIDO MILANGO YA KUWAKOMBOA VIJANA KIUCHUMI


 NA MWANDISHI WETU

KATIKA kipindi hiki ambacho Tanzania inaweka msisitizo wa kipekee kwenye Amani, Upendo, na Maridhiano ya Kitaifa, imebainika kuwa utulivu huo ndio rasilimali namba moja inayoiwezesha Serikali kupitia taasisi zake kama Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO) kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. Bila mshikamano wa kitaifa, juhudi za kutengeneza mazingira rafiki ya ajira na ujasiriamali kwa vijana haziwezi kuzaa matunda ya kudumu.

Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi mahiri wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeweka kipaumbele cha dhati katika kulinda tunu hizi za Taifa ili kutoa nafasi kwa mashirika kama SIDO kuwafikia vijana na "nyenzo" za kisasa za uzalishaji mali. Hii ni dhihirisho kuwa amani si hali tu ya kutokuwepo kwa fujo, bali ni mazingira wezesha yanayomfanya kijana awe na utulivu wa kubuni, kuzalisha, na kujiajiri.

SIDO na Silaha ya Ubunifu: Kijana Jitambue!

Katika kukabiliana na changamoto ya ajira, SIDO imejipambanua kama kimbilio la vijana wanaotaka kuandika historia mpya ya kiuchumi. Shirika hilo limebeba jukumu la kukuza ubunifu, likiwapatia vijana mbinu za kisasa za utengenezaji bidhaa zinazoweza kushindana ndani na nje ya mipaka ya Tanzania.

Mhadhiri na wataalamu wa maendeleo wanasisitiza kuwa kijana mwenye shughuli ya kufanya na kipato cha uhakika ndiye mlinzi mkuu wa amani ya nchi. Kupitia programu za SIDO, vijana wanahamasishwa kuacha utamaduni wa kusubiri ajira za "kuchongwa" na badala yake waingie mitaani kwa hekaheka za uzalishaji zinazochochea utulivu wa kijamii.

Maridhiano ya Kitaifa: Msingi wa Masoko na Uzalishaji

Ushirikiano uliopo sasa kati ya Serikali na wadau mbalimbali umefungua milango ya masoko kwa bidhaa za vijana. SIDO haishii tu kumpa kijana mashine au utaalamu, bali inamsaidia kupata soko—jambo linalowezekana tu ikiwa kuna mshikamano na umoja wa kitaifa. Taasisi mbalimbali zimeunganishwa ili kuhakikisha elimu ya ujasiriamali inawafikia vijana wengi zaidi, ikijenga jamii yenye watu wanaojitegemea na wanaoheshimu tunu za amani na upendo.

Wito wa Uzalendo: Thamani ya Bidhaa na Taifa

Vijana nchini waaswa kuwa mzalendo si tu kulinda mipaka, bali ni pamoja na kuongeza thamani ya bidhaa za kitanzania. Kupitia elimu ya SIDO, vijana wanapata uwezo wa kuboresha ubora wa kazi zao, jambo ambalo ni chachu ya kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Tunapozungumzia maridhiano na umoja wa kitaifa, tunazungumzia pia haki ya kijana kupata fursa. SIDO imetoa rungu hilo kwa vijana; ni wakati wao sasa kulitumia kwa bidii, ubunifu, na uzalendo ili kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa kisiwa cha amani chenye neema ya kiuchumi kwa kila mwananchi.

Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger