Saturday, 21 September 2024

TANZANIA, SAUDIA ZAINGIA MAKUBALIANO KUDHIBITI UHALIFU


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Mhandisi Hamad Masauni akipeana mkono na Waziri wa Mambo ya Ndani wa Saudi Arabia, Mwanamfalme Abdul Aziz Bin Saudi Al- Saudi(kulia) baada ya kusaini hati ya makubaliano kati ya nchi hizo katika kushirikiana na udhibiti wa matukio ya uhalifu kupitia Jeshi la Polisi na majanga mbalimbali kupitia Jeshi la Zimamoto.Makubaliano hayo yamesainiwa nchini Saudi Arabia.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi,Ally Senga Gugu akisalimiana na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi wa Serikali ya Saudi Arabia, Mwanamfalme Abdul Aziz Bin Saudi Al- Saudi(kushoto) wakati wa kusaini hati ya makubaliano kati ya nchi hizo katika kushirikiana na udhibiti wa matukio ya uhalifu kupitia Jeshi la Polisi na majanga mbalimbali kupitia Jeshi la Zimamoto.Makubaliano hayo yamesainiwa nchini Saudi Arabia.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Mhandisi Hamad Masauni akisaini hati ya makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Saudi Arabia katika kushirikiana na udhibiti wa matukio ya uhalifu kupitia Jeshi la Polisi na majanga mbalimbali kupitia Jeshi la Zimamoto.Makubaliano hayo yamesainiwa nchini Saudi Arabia.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Mhandisi Hamad Masauni akizungumza na Waziri wa Mambo ya Ndani wa Saudi Arabia, Mwanamfalme Abdul Aziz Bin Saudi Al- Saudi(kulia) alisema wakati wa kusaini hati ya makubaliano kati ya nchi hizo katika kushirikiana na udhibiti wa matukio ya uhalifu kupitia Jeshi la Polisi na majanga mbalimbali kupitia Jeshi la Zimamoto.Makubaliano hayo yamesainiwa nchini Saudi Arabia.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Na Mwandishi Wetu,Riyadh

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imesaini hati ya makubaliano na Serikali ya Saudi Arabia makubaliano ambayo yanaenda kugusa sekta mbili muhimu za usalama ikiwemo udhibiti wa makosa mbalimbali ya uhalifu kwa kutumia utaalamu na teknolojia ya hali ya juu kwa Jeshi la Polisi sambamba na udhibiti wa majanga mbalimbali ikiwemo moto,ajali za bararani,maporomoko kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.

Hati hiyo ya makubaliano kwa upande wa Tanzania imesainiwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Mhandisi Hamad Masauni na upande wa Serikali ya Saudi Arabia imesainiwa na Mwanamfalme Abdul Aziz Bin Saudi Al- Saudi huku pande zote mbili zikionyesha nia ya kubadilishana uzoefu na vifaa mbalimbali ikiwemo vifaa vinavyotumia teknolojia katika udhibiti wa matukio ya uhalifu.

‘Nachukua fursa hii kumshukuru Waziri wa Mambo ya Ndani wa Saudi Arabia, Mwanamfalme Abdul Aziz Bin Saudi Al -Saudi kwa kunipa ushirikiano mkubwa katika ziara hii ambayo leo hii imepelekea kukamilisha uwekaji wa saini kwenye hati za makubaliano mbili, moja ikihusisha upande wa Jeshi la Polisi ambapo serikali mbili hizo zinaenda kushirikiana katika kupambana na uhalifu lakini hati ya pili inahusu mashirikiano kwenye Jeshi letu la Zimamoto na Uokoaji na tumezisaini leo hapa na zinakwenda kufungua milango ya kuweza kushirikiana kwa mapana zaidi katika maeneo hayo mawili,hati hii ambayo tumesaini leo itakwenda kufanya sasa nchi yetu kupitia Jeshi la Polisi kuweza kufaidika na fursa mbalimbali za mashirikiano ikiwemo katika kujenga uwezo wa askari wetu katika maeneo mbalimbali na kubadilishana uzoefu na teknolojia na nimefarijika kuona serikali ya Saudi Arabia imeweka msisitizo katika maeneo ambayo hata sisi tumeweka nguvu kuimarisha matumizi ya teknolojia ya Habari na Mawasiliano katika kutoa huduma bora kwa wananchi..’ alisema Waziri Masauni

Waziri Masauni pia aligusia usalama wa kimtandao ambapo alisisitiza uwepo wa kipengele hicho katika hati ya makubaliano ili kuweza kudhibiti uhalifu wa mitandaoni ambao hivi sasa umeanza kushika kasi nchini.

‘Tumeona wenzetu wameweza kuimarika sana katika matumizi ya teknolojia kudhibiti uhalifu wa kimtandao hivyo ni Imani yangu kwamba kupitia mashirikiano ambayo tumesaini kwenye hati ya makubaliano tunakwenda kufanikisha dhamira njema ya Mheshimiwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kuimarisha jeshi letu la polisi katika eneo hilo nak ama mnakumbuka serikali ya awamu ya sita imewekeza fedha nyingi sana kiasi cha dola za kimarekani milioni mia moja kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kisasa mbali ya vifaa vingine ambavyo tayari vishaingia mwaka huu ambavyo vinahitaji askari wetu wawe na uwezo na uweledi wa kuvitumia sambamba na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ambao tayari walishaanza kupokea magari.’ Aliongeza Masauni

Akizungumza kwa upande wa Serikali ya Saudi Arabia,Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwanamfalme Abdul Aziz Bin Saudi Al- Saudi alisema wapo tayari kushirikiana na serikali ya Tanzania katika kudhibiti matukio ya uhalifu huku akigusia uhalifu mbalimbali ulivyodhibitiwa nchini Saudi Arabia ambapo kila mwaka maelfu ya waumini wa dini ya kiislam na wageni kutoka mataifa mbalimbali hufika nchini humo.














Share:

AKIBA BENKI YAZINDUA KAMPENI "TUPO MTAANI KWAKO"



Na Mwandishi wetu- Dar es salaam

Taasisi za kifedha hazina budi kurahisisha upatikanaji wa huduma za kifedha kwa Wananchi kwa kuwasogezea karibu ili kusaidia kupunguza adha ya kutumia muda mwingi kufuata huduma umbali mrefu na kuchelewa kufanya shughuli zao za kiuchumi.

Wito huo ameutoa Septemba 21, 2024 Dar es salaam Kaimu Afisa Mkuu wa Kitengo Biashara Benki ya Akiba, Danford Muyango wakati akizindua rasmi kampeni ya “Tupo Mtaani Kwako” katika tawi la Kijitonyama la benki hiyo , Letsya Tower ambapo amesema wapo mtaani kila mahali wakitoa huduma ikiwemo elimu ya mikopo, jinsi ya kutumia huduma za kidigital VISA card,ACB Mobile, Akiba Wakala na Internet Banking.
"Tumezindua rasmi program yetu ya TUPO MTAANI KWAKO kupitia timu yetu bobezi ya mauzo sasa tunakufika popote ulipo nchi nzima kupitia timu yetu ya mauzo kupata huduma zetu za kufungua akaunti , elimu ya mikopo pamoja na jinsi ya kutumia huduma zetu za kidijitali za VISA card, ACB Mobile, Akiba Wakala na Internet Banking", amesema Afisa biashara

Muyango amesema Program hiyo inaenda sambamba na kampeni ya Road show ya kutoa utambulisho kwa timu ya “Tupo Mtaani kwako” katika vitongoji na mitaa mbali mbali ya jiji la Dar es salaam.
Share:

Friday, 20 September 2024

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAMOSI SEPTEMBA 21,2024

 

Magazeti ya leo
 
     
Share:

CCM YASISITIZA UHUSIANO WA KIMATAIFA KUIMARISHA UCHUMI NA MAENDELEO YA WATU


Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi amesema kuwa Serikali na Nchi ya Tanzania, chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan itaendelea kuweka msisitizo katika kuimarisha uhusiano wa kimataifa wenye manufaa ya kiuchumi na maendeleo ya watu.

Balozi Nchimbi amesema kuwa urafiki na uhusiano wa kidiplomasia unapaswa kuendelea kuwa mojawapo ya njia sahihi katika kuboresha ushirikiano wa pande mbili kimataifa, kati ya nchi na nchi, au nchi na majukwaa mbalimbali ya kimataifa.

Katibu Mkuu huyo wa CCM amesema hayo alipokutana na mabalozi wanaowakilishi nchi zao hapa nchini, kutoka nchi za Brazil na India, pamoja na Mkuu wa Idara ya Mambo ya Nje ya Chama Tawala cha Msumbiji (FRELIMO) na Mkurugenzi Mkaazi wa Shirika la Friedrich Ebert Stiftung (FES), nchini Tanzania.

Katika mazungumzo na viongozi hao, yaliyofanyika kwa nyakati tofauti tofauti, leo 19 Septemba 2024, Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba, jijini Dar Es Salaam, Balozi Nchimbi amesema mojawapo ya utekelezaji wa Ilani ya CCM unaofanywa na Serikali ya CCM, inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan ni pamoja na kuendelea kuboresha uhusiano wa kimataifa, hasa kupitia diplomasia ya uchumi, kwa ajili ya kuimarisha uchumi, maendeleo ya watu na kubadilishana uzoefu kwenye uongozi na demokrasia.

Wakati wa mazungumzo na Balozi wa Brazil nchini Tanzania, Mhe. Gustavo Martins Nogueira na Balozi Nchimbi, viongozi wote wawili walionesha msisitizo na utayari wa kuendelea kuboresha uhusiano kati ya Tanzania na Brazil kwa ajili ya manufaa ya pande zote mbili, hasa katika nyanja za afya, kilimo na michezo.

Kwenye mazungumzo ya Balozi Nchimbi na Balozi wa India nchini Tanzania, Mhe. Bishwadip Dey, viongozi hao wamezungumzia umuhimu wa kuendelea kuenzi ushirikiano wa kimkakati kati ya nchi hizo mbili katika nyanja mbalimbali, zikiwemo teknolojia, biashara na elimu, ikizingatiwa India ni mojawapo ya nchi zilizopiga hatua kubwa za kimaendeleo katika maeneo hayo.

Katika mazungumzo ya Balozi Nchimbi na Mkuu wa Idara ya Uhusiano wa Kimataifa wa FRELIMO, Komredi Alcinda Antonio de Abreu, pande zote mbili zimesema urafiki na udugu wa damu uliopo kati ya Tanzania na Msumbiji utaendelea kuenziwa kwa kushirikiana kadri inavyohitajika, kama ilivyo ada tangu wakati wa kupigania ukombozi wa kisiasa wa Nchi za Kusini mwa Afrika, na sasa mkazo umeelekezwa kwenye ukombozi wa kiuchumi na kuendelea kuboresha hali za maisha ya watu.

Aidha, katika mkutano wa Balozi Nchimbi na Mkurugenzi Mkaazi wa FES nchini Tanzania, Bwana Christian Denzin, ambaye alimtembelea Katibu Mkuu wa CCM kwa ajili ya kujitambulisha, pande zote mbili zimekubaliana kuendeleza ushirikiano wa muda mrefu kati ya CCM na shirika hilo la nchini Ujerumani, hasa katika kuimarisha uwezo na uzoefu katika nyanja za uongozi na demokrasi, kupitia miradi mbalimbali ya mafunzo ya viongozi.
Share:

AFISA MTENDAJI MKUU WAZOHURU ATOA RAI KWA WATANZANIA KUACHA KUMKEJELI RAIS SAMIA



Na Dotto Kwilasa, Singida

Afisa Mtendaji Mkuu wa WazoHuru Media Group Ltd Ndg Mathias Canal,ametoa rai kwa watanzania kumtia moyo na kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa maendeleo makubwa anayoyafanya kwa ajili ya watanzania na kuacha kumbeza au kumkejeli.

Afisa Mtendaji huyo ameeleza hayo 19 Septemba 2024 kwenye mahafali ya 61 ya Shule ya Msingi Kiomboi-Bomani iliyopo Wilayani Iramba Mkoani Singida ambapo amesema maendeleo huja kwa kupeana moyo na kushirikiana.

Amesema kuwa Rais Samia ni mwanasiasa mstahimilivu na mwenye utulivu wa hali ya juu katika uongozi wake jambo linalozidi kuchochea na kusukuma maendeleo kila sehemu.
Akitolea mfano Kwenye Wilaya ya Iramba, Canal amesema kulikuwa na shule 4 za msingi na sasa zipo za msingi 111 ambapo za serikali ni 108 na shule binafsi ni tatu.

Kwa upande wa shule ya sekondari Wilaya ya Iramba kulikuwa na shule 1 na sasa zipo 29 ambapo za serikali ni 26 na za binafsi zipo 3.

"Wakati Tanzania inapata uhuru mwaka 1961 kulikuwa na Chuo Kikuu kimoja pekee ambapo kwa sasa mambo yamebadilika kwani Serikali sasa imeimarisha sekta ya elimu na kuwa na vyuo vikuu 30 na vyuo vishiriki 12 mpaka sasa, " Ameeleza.

Canal ameeleza kuwa mwaka 2022 serikali ilifanya mapitio na Mabadiliko ya mitaala na Sera ya elimu ya mwaka 2014 hatimaye kuwa na toleo jipya la sera ya elimu ya mwaka 2023.
"Kwa ujumla katika sera hiyo ya elimu kutakuwa na mambo muhimu ikiwemo Kutoa elimu ujuzi badala ya taaluma pekee, na Elimu ya lazima itakuwa miaka 10 badala ya 7," Anasisitiza mkurugenzi huyo na mdau wa maendeleo hapa nchini.

Sambamba na hayo amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe Prof Adolf Mkenda kwa kuja na wazo la ujenzi wa vyuo vya Ufundi Stadi (VETA) ambapo Wilaya ya Iramba imepokea Bilioni 1.4 na ujenzi wa VETA unaendelea katika Kijiji cha Salala kata ya Old Kiomboi.

Hali kadhalika amempongeza Mbunge wa Jimbo la Iramba ambaye ni Waziri wa Fedha Mhe Dkt Mwigulu Mchemba kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa miradi mbalimbali nchini ikiwemo katika jimbo lake ambapo katika kipindi cha miaka minne 2020-2024 Wilaya ya Iramba imepokea Bilioni 6.682 kwa ajili ya sekta ya elimu.

Katika mahafali hayo Ndg Mathias Canal amechangia kiasi cha Shilingi 400,000 kwa ajili ya motisha kwa walimu, Mipira 6 na jezi jozi mbili. Mipira mitatu na jezi jozi moja kwa ajili ya mchezo wa mpira wa miguu (Football) na mipira mitatu na jezi jozi moja kwa ajili ya mchezo wa mpira wa pete (Netball).










Share:

Thursday, 19 September 2024

JAMBO FOOD PRODUCTS YAJA NA MUONEKANO MPYA WA BIDHAA ZAKE

Kampuni ya Jambo Group imezindua muonekano mpya wa bidhaa zake za Jambo Food Products ‘Jamukaya’ zenye muonekano mzuri na wa kuvutia wenye radha ile ie.

Hafla ya uzinduzi huo umefanyika Septemba 17, 2024 kwenye kiwanda hicho ukiongozwa na Mkurugenzi Nassoro Salum Hamis pamoja na Meneja Mkuu wa Jambo Fm ambaye pia ni msimamizi wa Chapa group Nickson George, huku ukihudhuriwa na wananchi pamoja na wafanyakazi wa jambo.

Akizungmza wakati wa uzinduzi huo George amesema mbali na uzalishaji wa bidhaa bora pia imejidhatiti kutoa ajira za kudumu 400,000 ukijumlisha na wale wa ajira ya muda mfupi wanakuwa 600,000 hivyo kila siku watu hao wako kazini na serikali inapata mapato yake.

“Tumeamua kubadilisha muonekana wa sura ya mpya ya bidhaa baada ya kampuni kufikisha miaka 20 ya uzalishaji wa bidhaa zake hivyo tumeheshimu wateja wetu na hatua hiyi llni kuunga mkono juhudi za serikali kupunguza wimbi la vijana wasio na ajira,” amesema George.

Ameongeza kuwa mteja akiona muonekano mpya asiwe na mashaka kwani kuna usemi unaoeleza ‘Hawa ndio sisi’ ikimaanisha muonekano huo usiwape wasiwasi bali ni kampuni hiyo hiyo ikiendelea kuwapa furaha wateja wake.

Nao baadhi ya wananchi waliohudhuria hafla hiyo, wamepongeza muonekano mpya wa bidhaa za jambo, huku wakitoa wito kwa watanzania kwamba wawaunge wawekezaji wazawa kwa kununua bidhaa zao.

Kauli mbiu ya uzinduzi wa sura mpya bidhaa za jambo inasema “Jambo hawa ni sisi,dukani mpaka nyumbani,sisi ndio sura mpya ya furaha na maisha mazuri”.

Meneja Mkuu wa Jambo Fm ambaye pia ni msimamizi wa chapa group Nickson George akizungumza wakati wa uzinduzi huo.



Meneja Mkuu wa Jambo Fm ambaye pia ni msimamizi wa chapa group Nickson George akizungumza wakati wa uzinduzi huo.

Baadhi ya watu waliojitokeza kwenye uzinduzi huo.




Share:

TANZANIA KUWA MWENYEJI WA MKUTANO WA 11 WA TAASISI YA MERCK FOUNDATION AFRIKA ASIA LUMINARY


Dar es Salaam, 18 Septemba 2024

TANZANIA inatarajiwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa 11 wa Taasisi ya Merck Foundation utakaofanyika Oktoba 29 na 30, 2024 Jijini Dar es Salaam ambapo mkutano huo utafunguliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salam Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum amesema Mkutano huo utahudhuriwa na wenza wa Marais kutoka nchi 15 za Botswana; Burundi; Cape Verde; Jamhuri ya Afrika ya Kati; Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC); Gambia; Ghana, Liberia; Malawi; São Tomé; Zambia, Zimbabwe

Amesema kwa mwenyeji Tanzania itawakilishwa pia na mwenza wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Mama Mariam Mwinyi.

Aidha amesema nchi nyingine ambazo zitashiriki mkutano huo ni Angola; Kenya; Mauritania. Nyingine ni Msumbiji; Nigeria; Rwanda; Afrika Kusini; Comoros; Eswatini; na Sierra Leone.

Amesema washiriki wengine ni Mawaziri wa Afya, Jinsia, Mawasiliano, Elimu, Ustawi wa Jamii kutoka nchihizo, Wajumbe 45 wataalam watakaoambatana na wenza wa Marais kutoka nchi hizo, Wataalamu wa huduma za afya 500, wasomi, watunga sera na waandishi wa habari, Mabalozi wanaowakilisha nchi ambazo wenza wa Marais wamealikwa, Mabalozi wa Tanzania kutoka nchi hizo; na Wajumbe wengine wapatao 500 kutoka sehemu mbalimbali duniani watashiriki kwenye Mkutano huo kwa njia ya mtandao.

Pamoja na hayo amesema washiriki wa mikutano hiyo hunufaika na mijadala kutoka kwa Wataalam wa Kimataifa katika masuala ya maendeleo ya jamii, huduma za afya na udhibiti wa magonjwa mbalimbali yakiwemo Kisukari, Uzazi, Embriolojia, Afya ya Uzazi, Dharura za Watoto, Saratani, Afya ya Wanawake, Huduma za kuzuia Magonjwa ya Moyo, Endokrinolojia, Huduma za wagonjwa mahututi na wenye changamoto za Upumuaji, Afya ya Akili na Tiba ya Ndani. Mijadala hii inalenga kuchangia jitihada za bara la Afrika kwenye kuboresha usimamizi, uzuiaji na ugunduzi wa mapema wa magonjwa sugu, kujenga uwezo na upatikanaji wa huduma bora za afya za usawa.
Share:

Wednesday, 18 September 2024

MASHIRIKA YAOMBWA KUENDELEA KUTOA ELIMU YA KUPINGA UKATILI TARIME DHIDI YA MAMA NA MTOTO



Na  Frankius Cleophace -Tarime Mara

Jamii wilayani Tarime Mkoani Mara imeomba Mashirika mbalimbali likiwemo shirika la Jukwaa la Utu wa Mtoto CDF Kuendelea kutoa elimu juu ya madhara ya ukatili wa kijinsia ili kupunguza vitendo hivyo ambavyo vimekuwa vikitokea hapa nchini.

Hayo yanabainishwa na baadhi ya wananchi katika kijiji cha Surubu kata ya Komaswa wilayani Tarime mkoani Mara wakati wa mjadala wa pamoja uliohusisha kundi la wananaume na wavulana baada ya kuandaliwa na shirika la Jukwaa la Utu wa mtoto CDF.

Agrey Solonyo ni mkazi wa Surubu kata ya Komaswa Wilayani Tarime mkoani Mara akichangia mada zilizoandaliwa alisema kuwa elimu indelee kutolewa kwa lengo la kubadili mitazamo hasi iliyojengwa kwenye jamii ili kuondokana na vitendo vya Ukatili hususani kwa watoto wadogo.

Ukiangalia matukio mengi yamekuwa yakitoke hapa Nchini yakiwemo ya Ubakaji, Ulawiti Vipigo na mara nyingi yanawakabili watoto wadogo ambao hawana uwezo wa kupaza sauti hivyo sasa ni jukumu la serikali pamoja na mashiriki kuendelea kupaza suti.

 “Ukatili bado upo kwa mfano vipigo kwa watoto wadogo ili kumaliza hivi vitendo elimu iendelee kutolewa kwa makundi yote kuanzia shule za msingi hadi sekondari pia elimu iwe endelevu”alisemo Solonyo.

Kwa upande wake Hassan Bijampole aliongeza kuwa kuna haja kubwa ya kuendelea kujengea uwezo mkubwa viongozi wa dini ili nao sasa waeneza elimu hiyo kwenye jamii kwa lengo la kupunguza vitendo vya Ukatili wa kijinsia.

“Viongozi wa dini wanahaminika kwenye jamii sasa serikali pamoja na mashirika waweke nguvu kubwa kwa viongozi hao wa dini ili elimu iendelee kutolewa kwa lenmgo la kulinda kizazi chetu misingi bora ya utu inapaswa kulindwa alisema Bijampola”.

 Hassan aliongeza kuwa jamii imeona ni kawaida kutendeka kwa ukatili huo sasa nguvu ya pamoja iunganishwe kwa lengo la kuhakikisha wanaotenda ukatili kwa watoto waweze kufikishwa sehemu huska nakupatiwa adhabu kali na kwa wakati kwani wengi wamekuwa wakiachiwa nakurudi kutisha wale waliotoa taarifa za ukatili huo.

Naye Raphael Wambura aliongeza kuwa kuna haja kubwa ya kutungwa kwa sheria ndogondogo kuanzia ngazi ya familia vijiji, kata wilaya hadi hadi taifa ili kuwatia nguvuni wale wote wanaendeleza ukatili wa kijinsia.

Alice Mtuga ni mratibu wa mtandao wa Ushiriki wa wanaume na wavulana Tanzania kutoka Shirika la Jukwaa la utu wa Mtoto CDF anasema kuwa wameamua kuusisha kundi la wanaume kwa sababu limesaulika pia lina sauti kwenye familia hivyo elimu watakayopatiwa itaaidia kuelimisha jamii ili kupunguza vitendo vya Ukatili wa kijinsia ikiwa ni pamoja na kulinda kundi la watoto.

“Watoto n Tunu ya Taifa motto anapaswa kulindwa akiwa tumboni na wakati wa kuzaliwa sasa kundi la wanaume limesaulika hivyo kupitia elimu hii tunayoitoa nadhani watoto watakuwa salama zaidi”, alisema Alice.

Aidha Lucy John ambaye ni mkurugenzi wa shirika la  Wadada Solutions on Gender  Based Violence anasema kuwa serikali kwa kushirikiana na mashiriki ione sasa njia bora ya kuweza mazingira rafiki kwa wale wote wanaotoa taarifa za ukatili ili wasiweze kuzuliwa kwenye jamii zinazowazunguka.

“Tumeona hoja imeibuka kwenye huu mjadala kuwa wale wanaotoa taarifa za ukatili wanatishiwa maisha yao sasa ni jukumu le serikali  kwa kushirikiana na Mashiriki kuhakikisha wanalinda watu hao ili taarifa za ukatili ziendelee kutolewa kwenye jamii kwa lengo kufanyia kazi ukatili huo” alisema Lucy.

Uandaaji wa Programu Jumuishi ya Taifa ya MMMAM umezingatia ushirikishwaji wa wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na serikali, wadau wa maendeleo, na mashirika yasiyo ya kiserikali hivyo sasa wakiendeleza umoja wao watoto kuanzia miaka 0-8 wakilindwa na kujengewa misingi bora tutakuwa na Taifa lenye watoto salama ambao hawajakumbwa na Ukatili wa aina yeyote
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger