Monday 19 August 2024

KAMATI YA BUNGE YA SHERIA NDOGO YAIPONGEZA OSHA KWA KUTEKELEZA MAAGIZO YAKE

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo, Mhe. Dkt. Jasson Rweikiza (Kushoto) akifuatilia wasilisho la Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Mhe. Patrobas Katambi, kuhusu utekelezaji wa maagizo ya Kamati hiyo yaliyotolewa Oktoba 2023.

**********************

Na Mwandishi Wetu

Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) umewasilisha maboresho ambayo yamefanyika katika kanuni mbili za usalama na afya mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo.

Maboresho hayo ambayo yamefanyika katika kanuni za Igonomia na Mazingira ya Kazi yalishauriwa kufanyika na Kamati hiyo katika kikao chake cha Oktoba 26, 2023 baada ya OSHA kuwasilisha kanuni hizo mpya mbele ya Kamati hiyo.

Wasilisho hilo limefanywa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Patrobas Katambi, ambaye alimwakilisha Waziri wake Mhe. Ridhiwani Kikwete. Katambi ameambatana na Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, Kamishna wa Kazi, Bi. Suzan Mkangwa na Watendaji wengine wa Wizara na Taasisi ya OSHA.

Mhe. Katambi ameiambia Kamati kuwa mapendekezo yote yaliyotolewa ikiwemo kujumuisha tafsiri ya neno Mamlaka pamoja kuondoa maudhui yanayojirudia katika kanuni hizo yameshughulikiwa ipasavyo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. Jasson Rweikiza, ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) pamoja na Taasisi ya OSHA kwa kupokea na kutekeleza maagizo ya Kamati yake.

Aidha, ameahidi Kamati yake kuendelea kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi chini yake katika kuwahudumia Watanzania kupitia ushauri na maelekezo mbalimbali yanayolenga kuboresha utendaji wa Serikali.

Wakati huo huo, OSHA imekutana na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti na kufanya wasilisho kuhusu utendaji wa Taasisi hiyo ambapo Mtendaji Mkuu, Bi. Khadija Mwenda, ameieleza Kamati hiyo umuhimu wa kulinda nguvukazi ya Taifa kupitia uimarishaji wa mifumo ya usalama na afya katika sehemu za kazi.

“Hadi inapofika hatua ya mtu kuajiriwa kama mfanyakazi serikali inakuwa imewekeza rasilimali nyingi sana kwake kuanzia anapozaliwa, kukua, kusoma hadi kuajiriwa hivyo inakuwa ni hasara kubwa kwa Taifa endapo mfanyakazi huyu atapata ulemavu au kupoteza maisha kabla ya kutoa mchango wake wa kutosha katika uzalishaji,” ameeleza Mtendaji Mkuu wa OSHA na kuongeza:
“Tunachokifanya OSHA ni kushauri na kusimamia maeneo ya kazi kuweka mifumo madhubuti ya kuwalinda wafanyakazi dhidi ya vihatarishi vya magonjwa pamoja na kulinda mitaji ya wawekezaji ili kuleta tija katika uzalishaji pamoja na kulinda ustawi wa wafanyakazi.”

Akihitimisha mjadala wa wajumbe wa Kamati hiyo ya Bajeti baada ya wasilisho la OSHA, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Oran Njeza, amesema Kamati yake itaendelea kutoa ushauri unaolenga kuboresha utendaji wa Serikali ikiwemo Taasisi ya OSHA.
Mjadala ukiendelea katika kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo ambapo OSHA iliwasilisha maboresho ya kanuni mbili za usalama na afya.
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Mhe. Patrobas Katambi, akifanya wasilisho mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu maboresho ya kanuni za Igonomia na Mazingira ya Kazi ambayo Kamati hiyo ilielekeza yafanyike.

Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda na Kamishna wa Kazi, Bi. Suzan Mkangwa wakifuatilia wasilisho la Naibu Waziri, Mhe. Katambi katika kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria NdogoWatendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) na Taasisi ya OSHA wakifuatilia wasilisho la Naibu Waziri, Mhe. Katambi katika kikao cha Kamati ya ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo.



Share:

WALIOTUMWA NA AFANDE KUMDHALILISHA BINTI WAFIKISHWA MAHAKAMANI.. KESI KUSIKILIZWA SIKU TANO MFULULIZO



Na, Mwandishi wetu - Dodoma

Watuhumiwa wanne wamefikishwa mahakamani kwa tuhuma za kutumwa na afande kumdhalilisha binti wa Yombo Dovya Jijini Dar es salaam Leo Agosti 19, 2024 na kusomewa mashtaka mawili ya kubaka kwa kikundi (gang rape) na kumwingilia kinyume na maumbile binti ambaye hakutajwa jina lake mahakamani.


Akizungumza na waandishi wa habari nje ya mahakama kuu ya Tanzania Mkoani Dodoma Mkurugenzi msaidizi kutoka Ofisi ya Mashtaka Makao Makuu, Renatus Mkude amesema vijana hao wamekana mashtaka hayo na kutokana na unyeti wa shauri hilo wataendelea kuwa mahabusu huku shauri lao likisikilizwa kwa siku tano mfululizo.

Watuhumiwa hao waliofikishwa mahakamani ni MT. 140105 Clinton Honest Damas maarufu Nyundo,Amin Lord Lema ,Nickson Idala Jackson na C.1693 Playgod Edwin Mushi huku jina la binti aliyefanyiwa ukatili huo kutotajwa mahakamani ili kulinda utu wake kwa mujibu wa sheria za nchi.
Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMAMOSI AGOSTI 17,2024













Share:

MANALA AANDIKA BARUA YA WAZI KWA RAIS SAMIA , UJENZI WA UWANJA WA NDEGE KAHAMA


Barua ya Wazi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan 
Kupitia Waziri wa Ujenzi na Wizara ya Uchukuzi

Mhe. Rais,

YAH: OMBI LA UJENZI WA UWANJA WA NDEGE KATIKA MANISPAA YA KAHAMA

Kwa heshima na taadhima, napenda kuchukua nafasi hii kukupongeza Mhe. Rais kwa kazi kubwa na nzuri inayoendelea kufanyika chini ya uongozi wako thabiti. Nikiwa mwananchi na mdau wa maendeleo katika Manispaa ya Kahama, napenda kuwasilisha ombi langu la kujenga uwanja wa ndege ndani ya manispaa hii muhimu, ili kuleta mapinduzi ya kiuchumi na kijamii katika eneo hili na nchi kwa ujumla.

Manispaa ya Kahama, kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, inakadiriwa kuwa na idadi ya watu takribani milioni 1. Hii inaashiria kwamba nusu ya wakazi wa Wilaya ya Kahama wanatoka ndani ya manispaa hii. Ukosefu wa uwanja wa ndege katika eneo hili umekuwa kikwazo kikubwa kwa maendeleo ya kiuchumi, kijamii, na usafirishaji wa haraka wa abiria na mizigo. Watu wengi wanakosa huduma hii muhimu, hali inayosababisha gharama kubwa za usafiri na muda mwingi kwa wakazi wa Kahama na maeneo jirani wanapotumia viwanja vya ndege vya Shinyanga au Mwanza.

Kahama ni miongoni mwa wilaya zinazochangia kwa kiasi kikubwa katika Pato la Taifa kupitia vitega uchumi mbalimbali kama vile madini, kilimo, na biashara. 

Uwepo wa uwanja wa ndege katika Manispaa ya Kahama utachochea zaidi ukuaji wa sekta hizi kwa kuvutia wawekezaji wa ndani na nje, kurahisisha usafirishaji wa bidhaa na huduma, na kuongeza mapato ya serikali. Takwimu zinaonyesha kuwa uwepo wa uwanja wa ndege unaweza kuongeza mapato ya serikali kwa kiasi kikubwa kupitia ada na kodi mbalimbali zinazohusiana na shughuli za usafiri wa anga.

Pamoja na faida hizo kwa serikali, wananchi, wafanyabiashara, na makundi mengine yatakayohusishwa moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja na huduma hii, watapata fursa za ajira, kuongezeka kwa usafirishaji wa bidhaa za kilimo, madini, na biashara, pamoja na kuboresha hali ya maisha kwa ujumla. Manispaa ya Kahama ikiwa na vitega uchumi vingi, mabadiliko haya yatakuwa na athari chanya kwa uchumi wa eneo hili na taifa kwa ujumla.

Iwapo utekelezaji wa mradi huu muhimu utachelewa kutokana na sababu mbalimbali, napendekeza hatua mbadala kama ifuatavyo:

1. Kutathmini na kupanua uwanja wa ndege wa Buzwagi: Uwanja huu ambao sasa ni mali ya serikali, unaweza kufanyiwa tathmini na kupanuliwa ili kukidhi mahitaji ya usafiri wa anga kwa Kahama na maeneo jirani.

2. Kupitia upya ratiba za ndege: Kupitia na kuongeza idadi ya siku za safari za ndege zinazotumia uwanja huo kwa wiki, ili kupunguza gharama kwa wakazi wa Kahama na maeneo jirani wanapolazimika kusafiri hadi Shinyanga au Mwanza kwa huduma hiyo.

Napenda kumalizia kwa kutoa pongezi kwa serikali inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake za kuendelea kutekeleza ahadi kwa Watanzania, wakiwemo wananchi wa Kahama.

 Naomba maombi yangu yaweze kupokelewa na kufanyiwa kazi kwa ajili ya maendeleo ya Manispaa ya Kahama na taifa kwa ujumla.

Nakutakia kazi njema na utekelezaji wa majukumu yenu kwa maslahi ya Watanzania wote.

Wako katika ujenzi wa taifa,
Mhandisi Dkt. Manala Tabu Mbumba  
Mdau wa Maendeleo Kahama


 

Share:

TANZANIA MWENYEJI MKUTANO WA MAFUTA NA GESI MACHI 2025



Na Mwandishi wetu.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko ameshiriki katika kikao cha maandalizi ya Mkutano na Maonesho ya 11 ya Petroli ya Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAPCE'25) unaotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 5 hadi 7 Machi, 2025 katika ukumbi wa JNICC jijini Dar es Salaam.
Mkutano huo wa siku tatu wa kimataifa utafanyika chini ya kauli mbiu “Unlocking Investment in Future Energy: The Role of Petroleum Resources in the Energy Mix for Sustainable Development in East Africa” ambapo utatanguliwa na kufuatiwa na safari za kutembelea maeneo ya kijiolojia na kujionea vivutio mbalimbali kitalii vilivyopo katika nchi wanachama wa jumuiya hiyo.

Aidha, watazungumzia masuala ya mabadiliko kuelekea katika matumizi ya nishati safi na kuwakutanisha wadau zaidi ya 1000 kutoka mataifa mbalimbali wanatarajiwa kushiriki katika mkutano huo.
Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Biteko alisema “Kama nchi tumepata fursa ya kuandaa mkutano huu wa kimataifa na Serikali imepanga kufanya hivyo kwa kushirikiana na sekta binafsi ili kuandaa mkutano wenye tija kwa nchi na kutoa nafasi kwa Watanzania kufaidika na uwepo wa mkutano huu”.

Dkt. Biteko alitoa rai kwa wahudhuriaji wa kikao hicho kutumia vema fursa ya uwepo wa mkutano wa EAPCE’25 kutangaza biashara, huduma na utaalamu wao pamoja na kujenga mitandao na washirika kutoka mataifa mbalimbali.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mha. Felchesmi Mramba alieleza kuwa mkutano wa EAPCE’25 pia utahusisha maonesho ya huduma na bidhaa mbalimbali na hivyo kutoa fursa kwa wadau kuchangamkia fursa hiyo.

“Sambamba na mkutano na maonesho eneo lingine ambalo wadau wanakaribishwa kuchangamkia ni udhamini wa mkutano ambao unatoa nafasi ya kujitangaza ndani na nje ya nchi kwa kuzingatia ukubwa wa mkutano wenyewe” alisema Mha. Mramba.

Kikao hicho ni cha awali cha maandalizi kuelekea mkutano wa EAPCE'25. Kwa taarifa zaidi tembelea tovuti (www.eapce25.eac.int)


Share:

HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO JUMATATU AGOSTI 19, 2024

Share:

Sunday 18 August 2024

WAKALA WA VIPIMO ZANZIBAR WAJIFUNZA KUTOKA WMA BARA

Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Zanzibar (ZAWEMA) Mohammed Simai (katikati), akisikiliza maelezo kutoka kwa Mussa Kongola, Msimamizi wa Mtambo wa kuchakata gesi asilia wa Kampuni ya Maurel & Prom, Madimba Mtwara (kushoto). Kulia ni Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Mtwara (WMA), Saad Haruna. Simai alitembelea Mtwara Agosti 16 na 17, 2024 kujifunza namna WMA mkoani humo inavyotekeleza majukumu yake.

********************

Veronica Simba – WMA

Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Zanzibar (ZAWEMA) Mohammed Simai amefanya ziara ya siku mbili mkoani Mtwara kwa lengo la kujifunza majukumu yanayotekelezwa na Wakala wa Vipimo Tanzania Bara (WMA) ambapo amekiri kunufaika zaidi ya alivyotarajia.

Akizungumza baada ya kuhitimisha ziara yake, Agosti 17, 2024 Simai amesema lengo hasa la ziara hiyo lilikuwa kutembelea eneo linalotumiwa na Wakala wa Vipimo Mtwara kwa ajili ya ukaguzi na uhakiki wa magari ya kusafirishia mafuta ili ZAWEMA ikatumie teknolojia hiyo na kuboresha zaidi huko Zanzibar.

“Hata hivyo, ziara hii imekuwa ya mafanikio makubwa kwetu kwa sababu tumepata zaidi ya kile tulichokusudia,” amesema.

Akifafanua, Simai ameeleza kwamba mbali na kujionea na kujifunza kuhusu uanzishaji wa mtambo wa ukaguzi na uhakiki wa magari ya kusafirishia mafuta, amepata fursa ya kutembelea maeneo mengine ambako WMA hutekeleza majukumu yake ikiwemo Bandari ya Mtwara na katika eneo ambalo gesi asilia huvunwa na kuchakatwa huko Madimba.

Amesema, matarajio yake ni kwenda kuibua miradi mbalimbali ukiwemo wa ujenzi wa eneo la ukaguzi wa magari ya mafuta ambao utaenda sanjari na ujenzi wa mtambo wa kisasa wa ukaguzi wa dira za maji kwa njia ya kielektroniki. “Hata hivyo kwa nilichokiona huku WMA Mtwara, iko haja kutumia mtambo wa kawaida pia pamoja na uwepo wa huo wa kielektroniki,” ameeleza.

Simai amemshukuru Mtendaji Mkuu wa WMA Tanzania Bara, Alban Kihulla kwa ushirikiano ambao amekuwa akiutoa kwa ZAWEMA katika kuhakikisha wanatimiza matarajio yao ya kutekeleza majukumu ya uhakiki vipimo kwa ufanisi na tija kwa manufaa ya wananchi wa Zanzibar.

Awali, akieleza kuhusu majukumu yanayotekelezwa na WMA mkoani Mtwara, Meneja wa Mkoa wa Wakala hiyo, Saad Haruna amesema ni pamoja na uhakiki wa vipimo ambavyo hutumika katika sekta za kilimo, biashara, mazingira pamoja na usalama.

Katika sekta ya kilimo, Haruna amesema WMA huhakiki mizani zinazotumika wakati wa kununua mazao pamoja na wakati wa kuyasafirisha.

Aidha, kwa upande wa biashara amesema WMA inawajibika kuhakiki vipimo vinavyohusiana na sekta hiyo ambapo ametoa mfano wa mafuta yanayosafirishwa kutoka nchi za nje kuletwa nchini kupitia Bandari ya Mtwara.

“WMA hufanya uhakiki kuanzia Bandarini mafuta yanaposhushwa na kupita kwenye kipimo maalum kijulikanacho kama ‘flow meter’ kwa lugha ya kigeni, zoezi ambalo huendelea kufanyika katika matenki ya kuhifadhi mafuta, vituo vya mafuta na katika pampu zinazotumika kujaza mafuta katika magari.”

Vilevile, Haruna amesema jukumu lingine ambalo hutekelezwa na WMA mkoani humo ni kuhakiki dira mpya za maji ambazo hutumika kuwafungia wateja maji pamoja na zile ambazo zilikwishaanza kutumika.

Pia, katika sekta ndogo ya gesi asilia, amesema WMA huwajibika kuhakiki vipimo vyote vinavyotumika kupima kiwango cha nishati hiyo kuanzia inapovunwa hadi kiwango kinachopelekwa kwa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa ajili ya kuzalisha umeme, kiwango kinachopelekwa kwa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na hata kile kinachopelekwa kwa Kampuni kubwa ya kuzalisha saruji ya Dangote.

Akizungumzia malengo ya kuhakiki vipimo, Haruna amesema ni jukumu la Serikali kupitia Wakala wa Vipimo, kuhakikisha pande zote zinalindwa yaani mlaji apate bidhaa kadri alivyolipia bila kupunjwa ilhali muuzaji apate malipo stahiki kulingana na kiwango alichouza.

Kwa upande wake, mmoja wa Wasimamizi wa Mtambo wa kuchakata gesi asilia katika Kiwanda kilichoko Madimba, Mussa Kongola ameipongeza Serikali kwa kuanzisha Wakala wa Vipimo akisema inatekeleza majukumu muhimu sana yanayozinufaisha pande zote.

“Uwepo wa jicho la tatu ni muhimu sana ili kuhakikisha pande zote zinanufaika kwa kupata kilicho stahiki na kwakweli nimewafahamu WMA kwa muda mrefu, kazi yao ni njema sana,” amesisitiza.

Ikumbukwe kwamba, kwa mujibu wa takwimu kutoka TPDC, asilimia 60 ya umeme unaozalishwa nchini kupitia TANESCO hutokana na gesi asilia. Aidha, korosho ambazo huzalishwa kwa wingi mkoani Mtwara ni moja ya mazao ya kimkakati yanayolimwa nchini. Vilevile, uwepo wa Bandari ya Mtwara pamoja na maeneo mengine mbalimbali ambayo yanatumia vipimo, vyote vinadhihirisha umuhimu wa uwepo wa Wakala wa Vipimo kwa manufaa ya uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Utendaji mzuri wa wataalamu wa Wakala wa Vipimo Tanzania Bara umekuwa ukivutia nchi mbalimbali kuja kujifunza namna bora ya kuendesha sekta hiyo.

Ziara ya mafunzo ya Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Zanzibar imefanyika mkoani Mtwara badala ya Dar es Salaam au Mkoa mwingine kulingana na ukubwa wa kazi zinazotekelezwa na ZAWEMA ambao unaelezwa kuwiana na majukumu yanayotekelezwa na WMA Mtwara.

Mojawapo ya Mita zinazopima kiwango cha gesi asilia inayovunwa na kuchakatwa katika kiwanda kilichoko Madimba, Mtwara, ikiwa na nembo/alama ya Wakala wa Vipimo (WMA) kuthibitisha kwamba Mita hiyo imehakikiwa na Wakala hiyo. Taswira hii ilichukuliwa Agosti 17, 2024 wakati wa ziara ya Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Zanzibar (ZAWEMA) Mohammed Simai, ilyolenga kujifunza namna WMA Mtwara inavyotekeleza majukumu yake katika sekta mbalimbali.
Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Zanzibar (ZAWEMA) Mohammed Simai (mwenye fulana nyeusi-kushoto), akiwa katika ziara ya mafunzo Bandari ya Mtwara. Agosti 17, 2024 kujionea na kujifunza namna majukumu yanayotekelezwa na Wakala wa Vipimo Tanzania Bara (WMA) katika sekta mbalimbali.

Mojawapo ya Mita zinazopima uzito wa magari yenye makaa yam awe kutoka katika Bandari ya Mtwara, ikiwa na nembo/alama ya Wakala wa Vipimo (WMA) kuthibitisha kwamba Mita hiyo imehakikiwa na Wakala hiyo. Taswira hii ilichukuliwa Agosti 17, 2024 wakati wa ziara ya Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Zanzibar (ZAWEMA) Mohammed Simai, ilyolenga kujifunza namna WMA Mtwara inavyotekeleza majukumu yake katika sekta mbalimbali.

Gari lililobeba makaa ya mawe likipimwa uzito katika Bandari ya Mtwara kwa kutumia Mizani iliyohakikiwa na Wakala wa Vipimo (WMA). Taswira hii ilichukuliwa Agosti 17, 2024 wakati wa ziara ya Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Zanzibar (ZAWEMA) Mohammed Simai, ilyolenga kujifunza namna WMA Mtwara inavyotekeleza majukumu yake katika sekta mbalimbali.

Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Zanzibar (ZAWEMA) Mohammed Simai (katikati), akisisitiza jambo kwa Mussa Kongola, Msimamizi wa Mtambo wa kuchakata gesi asilia wa Kampuni ya Maurel & Prom, Madimba Mtwara (kushoto) na Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Mtwara (WMA), Saad Haruna. Simai alitembelea kiwanda hicho cha kuchakata gesi asilia Agosti 17, 2024 kujifunza namna WMA mkoani humo inavyotekeleza majukumu yake katika sekta mbalimbali.

Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Zanzibar (ZAWEMA) Mohammed Simai (kushoto), akiwa katika ziara ya mafunzo katika kiwanda cha kuchakata gesi asilia kilichoko Madimba, Mtwara, Agosti 17, 2024 kujionea na kujifunza majukumu yanayotekelezwa na Wakala wa Vipimo Tanzania Bara (WMA) katika sekta mbalimbali.
Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger