Friday, 5 July 2019

Jengo jipya la tatu JNIA kuanza kutumika mwezi ujao

Christopher Philemon - Uchukuzi
NAIBU Waziri  wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano(Sekta Uchukuzi na Mawasiliano),  Mhandisi Atashasta Nditiye, amesema ujenzi wa jengo la  tatu la abiria wa kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA),  kinatarajia  kukamilika mwanzoni mwa Agosti  mwaka huu kwa kuanza kuhudumia abiria
 
 Amesema amefurahishwa  kwa  kukamilika  kwa ujenzi wa kiwanja hicho  ambapo kwa  vimefungwa vifaa vya kisasa. 
 
 Akizungumza mara  baada ya ziara ya kukagua kiwanja hilo, amesema  kuwa katika idadi ya miruko ya ndege Barani Afrika  inachukua nafasi ya tano  na nafasi ya sita kwa abiria.

‘’ Nimefurahishwa kwa kukamilika kwa ujenzi wa jengo la tatu la abiria wa  kiwanja cha Ndege ambapo utakapoanza kuhudumia abiria natarajia tutachukua nafasi mzuri zaidi Barani Afrika kwani ni kiwanja cha kisasa nahuduma zetu ni mzuri,’’ alisema.
 
Nae Mkurugenzi  wa Kiwanja cha Ndege cha Mwalimu Julius Nyerere( JNIA),  Paul  Rwegasha, amesema  kukamilika kwa jengo hilo litaweza  kuhudumia  jumla abiria milioni nane kwa mwaka.
 
Rwegesha alisema  ujenzi wa jengo la kwanza lina uwezo wa kuhudumia abiria 500,000 kwa mwaka na ujenzi wa pili abiria  milioni 1.5
 
Alisema kukamilika kwa Jengo la tatu la abiria  litaongeza idadi ya ndege, abiria pamoja na watalii baada ya kuwa na miundombinu  bora na yakisasa.
 
Vile vile alisema ujenzi wa kiwanja cha tatu ni kwa ajili ya abiria wa safari za Kimataifa ambapo kwa sasa yako mashirika na Kampuni 20 na kiwanja cha  pili kwa ajili ya abiria wa safari za   ndani ya nchi na Kimataifa  ambapo yana Kampuni sita  huku kiwanja cha kwanza  safari za  ujumla za ndani ya nchi Kampuni ni  12.
 
Alisema ujenzi wa jengo la tatu la abiria  litakuwa na uwezo wa kuhudumia abiria 2,800, kwa saa na maegesho ya magari mchanganyiko yasiopungua 2,075 kwa wakati mmoja.
 
Mkurugenzi Mkuu wa  Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini(TAA), Mhandisi Julius Ndyamukama, alisema wako katika maandalizi ya wakuu wanchi na Serikali watakaohudhuria mkutano wa 39 wa SADAC  ambapo maadalizi yameambatana na ukarabati wa maboresho ya miundombinu  na samani katiaka jengo  la pili la Abiria.


Share:

MKUTANO MKUU WA 26 WA SHIRIKISHO LA TASISI ZA TEHAMA AFRIKA MASHARIKI(EACO) WAFUNGULIWA JIJINI MWANZA

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Mhandisi Isack Kamwelwe (MB) (aliyesimama  akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 26 wa Shirikisho la Tasisi za TEHAMA Afrika Mashariki(EACO) Jijini Mwanza, Julai 5, 2019. Wengine pichani katikati ni  Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Mawasliano Tanzania (TCRA), Dkt. Jones Killimbe  Mkurugenzi Mkuu, TCRA Mhandisi James M. Kilaba. Mkutano huo unahudhuriwa na wajumbe kutoka nchi wanachama za Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na Sudani Kusini.
 Washiriki wakisikiliza hotuba ya Mhe. Waziri.
 Washiriki wakisikiliza hotuba ya Mhe. Waziri.
 Washiriki wakisikiliza hotuba ya Mhe. Waziri.
 Wadau wa sekta ya mawasiliano nchini.
 Waziri  wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isaack Kamwelwe (Mb), (wapili kulia), akiwa na Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Mhandisi James M. Kilaba (kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya TCRA, Dkt. Jones Killimbe (watatu kulia) na Mtendaji Mkuu wa EACO, Dkt. Ally Simba.
 Meza kuu wakiwa wamesimama kwa heshima wakati wa kupigwa wimbo wa Taifa na ule wa Afrika Mashariki.
 Picha ya pamoja.
  Picha ya pamoja.
 Kikundi cha Wachezaji Ngoma cha  BUJORA Kikibudisha Vongozi na Washiriki kwenye Mkutano Mkuu wa EACO, Mwanza
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Mhandisi Isack Kamwelwe (MB) (wapili kulia)  akitoka baada ya kufungua Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Tasisi za TEHAMA Afrika Mashariki(EACO) Jijini Mwanza, Julai 5, 2019. Wengine pichani kutoka kulia, mwakilishi wa Katibu Mkuu (Mawasiliano) Bw.Mulembwa Manuku, Mkurugenzi Mkuu, TCRA Mhandisi James M. Kilaba na Mtendaji Mkuu wa EACO Dr. Ally Simba. 
Share:

NEC yatangaza uchaguzi Jimbo la Tundu Lissu

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imetangaza uchaguzi mdogo katika Jimbo la Singida Mashariki, mkoani Singida utakaofanyika Julai 31, mwaka huu.

Akitangaza hatua hiyo, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi,  Jaji Semistocles Kaijage amesema ratiba inatokana na barua ya Spika inayoeleza kuwa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo, Tundu Lissu amepoteza sifa ya kuwa Mbunge kutokana na kushindwa kuwasilisha kwa Spika tamko la mali na madeni na kushindwa kuhudhuria mikutano saba mfululizo bila ruhusa ya Spika.

“Tumezingatia  matakwa ya kifungu cha 37 (1) (b) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi sura ya 343, kutoa taarifa kwa umma kuhusu uwepo wa uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Singida Mashariki,” amesema.

Jaji Kaijage amesema, fomu za uteuzi wa wagombea zitatolewa kati ya Julai 13 hadi 18 mwaka huu, uteuzi wa wagombea utafanyika Julai  18, na kampeni za uchaguzi zitafanyika kuanzia Julai 19 hadi 30 na siku ya uchaguzi itakuwa ni Julai 31, mwaka huu.


Share:

WAREMBO 13 KESHO KUCHUANA FAINALI SHINDANO LA MISS SHINYANGA 2019


Jumla ya warembo/walimbwende 13 kutoka halmashauri sita za mkoa wa Shinyanga ambazo ni Kishapu,Kahama Mji, Ushetu,Shinyanga na Manispaa ya Shinyanga kesho watachuana kuwania taji la Miss Shinyanga 2019.

Fainali ya Mashindano ya kutafuta Mrembo wa Mkoa wa Shinyanga(Miss Shinyanga 2019) yatafanyika kesho Jumamosi kuanzia saa moja kamili katika ukumbi wa CCM Mkoa (NSSF ya Zamani Mjini Shinyanga).

Meneja Mkuu wa Kampuni ya Burudani ya Makumbusho Entertainment ambao waandaaji wa Shindano la Miss Shinyanga 2019, George Foda amesema maandalizi yamekamilika hivyo kuwaomba wakazi wa Shinyanga na maeneo ya jirani kufika kujionea jinsi wanavyoonesha vipaji vyao katika tasnia ya urembo ya ubunifu.

Amesema zawadi ya pesa taslimu na ufadhili wa masomo ya vyuo mbalimbali kwa washiriki wa mashindano hayo zitatolewa.

Miongoni mwa wasanii watakaotumbuiza katika mashindano hayo ni Linah Sanga,Daz Baba na Five Star Modern Taarabu.
 
Na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Washiriki wa Shindano la Miss Shinyanga 2019.
Washiriki wa Shindano la Miss Shinyanga 2019.
Washiriki wa Shindano la Miss Shinyanga 2019.
Washiriki wa Shindano la Miss Shinyanga 2019.
Share:

Mwalimu ataka kujiua kwa kujikata na chupa kisa ugumu wa maisha

Mwalimu wa Shule ya Msingi Rung’abure iliyopo Serengeti Mkoani Mara, Godfrey Tarimo amejikata na chupa eneo lake la shingo katika jaribio la kutaka kujiua kwa kile alichosema ni kuzidiwa na ugumu wa maisha na mahusiano mabaya na jirani zake.

Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Nyerere, Wilaya ya Serengeti, Dkt Tanu Warioba amethibitisha kumpokea mwalimu usiku wa Julai 3, 2019 akiwa ameletwa kwa msaada wa walimu wenzake.

Mkuu wa Wilaya ya Serengeti, Nurdin Babu amesema hatua kali za kinidhamu na sheria zitachukuliwa kwa mwalimu huyo ikiwezakana hata kufukuzwa kazi.


Share:

JESHI NA UPINZANI WAKUBALIANA KUUNDA SERIKALI YA MPITO SUDANI

Viongozi wa jeshi nchini Sudani wameafikiana na muungano wa upinzani nchini humo juu ya kuundwa kwa serikali ya mpito ambayo itaandaa njia kwa kurejeshwa kwa utawala wa kiraia.

Kwa mujibu wa wasuluhishi, jeshi na upinzani wamekubali kushirikiana katika kuongoza serikali hiyo itakayodumu kwa miaka mitatu na kisha kusimamia uchaguzi huru na wa haki.

Pande hizo mbili zilishindwa kufikia muafaka hapo kabla kutokana na mvutano wa kila upande ukitaka uwe na uwakilishi mkubwa zaidi kwenye baraza litakalounda serikali hiyo.

Lakini sasa wameahidi kuunda serikali huru itakayoongozwa kitaalamu pamoja na kuchunguza ghasia za hvi karibuni zilizosababisha mamia kufariki, Umoja wa Afrika (AU) umesema.

Taarifa za makubaliano hayo zilipokelewa kwa shangwe mitaani.

Sudani imejikuta ikitumbukia katika lindi la ghasia na suitafahamu toka alipong'olewa madarakani rais Omar al-Bashir kwa mapinduzi ya kijeshi mwezi Aprili.

Mapinduzi hayo yalizaliwa baada ya maandamano makubwa ya raia dhidi ya Bashir, ambaye aliingia madarakani kwa mtutu wa bunduki mwaka 1989.

Siku tatu kabla ya makubaliano hayo ya mpito, makundi makubwa ya waandamanaji wakitaka baraza la kiongozi la kijeshi kuachia ngazi na kupisha utawala wa kiraia.

Watu saba waliuawa na wengine 181 walijeruhiwa katika vurumai hizo, vyombo vya serikali viliripoti.

Mazungumzo ya safari hii yalifanyika jijini Khartoum kupitia usuluhishi ulioongozwa na Waziri Mkuu wa Ethiopia na wanachama wa AU.

Wamekubaliana nini hasa?

"Pande mbili zimekubaliana kuunda baraza huru litakalokuwa na rais wa kupokezana baina ya jeshi na raia kwa kipindi cha miaka mitatu au zaidi," msuluhishi wa AU Mohamed Hassan Lebatt amewaambia wanahabari Ijumaa asubuhi.

Uchaguzi utafanyika pale kipindi cha mpito kitakapofikia tamati.

"Pia wamekubaliana kuwa na uchunguzi wa wazi, huru na kina juu ya matukio yote ya ghasia yaliyoikumba nchi hiyo katika wiki za hii karibuni," ameongeza.

Pia wamekubaliana kuahirisha kuanzishwa kwa baraza la wawakilishi.

"Tunaamini kuwa huu ni mwanzo wa zama mpya," amesema Omar al-Degair, kiongozi wa muungano wa wapinzani nchini humo FFC.

Naibu kiongozi wa baraza la mpito la jeshi TMC, Jenerali Mohamed Hamdan Dagalo, amesema: "Makubaliano haya yatakuwa ni makubwa na hayatamuacha mtu yeyote.

"Tunaushukuru Umoja wa Afrika na Ethiopia kwa kutuma wasuluhishi na kuwa wavumilivu."
Matukio kabla ya makubaliano

Mwezi uliopita, wawakilishi wa waandamanaji walikuwa katika meza ya mazungumzo juu ya nani anatakiwa kuongoza Sudani.

Lakini majadiliano yakavunjika baada ya jeshi kushambulia waandamanaji Juni 3 na kuua makumi ya waandamanaji.

Jeshi likatangaza kuwa limevunja makubaliano yote na wapinzani baada ya tukio hilo, na uchaguzi ungefanyika ndani ya miezi tisa.

Lakini wanaharakati wakasisitiza kuwa serikali ya mpito ya miaka mitatu inahitajika ili kuhakikisha uchaguzi huru na wa haki unafanyika.

Baada ya mazungumzo kuvunjika, Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed alipaa mpaka Sudani ili kupatanisho pande hizo mbili.

Baada ya siku kadhaa za mazungumzo, mwakilishi wa Abiy bwana Mahmoud Dirir, akatangaza kuwa viongozi wa maandamano wamekubali kurudi kwenye meza ya mazungumzo na wanajeshi.
Chanzo - BBC
Share:

JOGOO AFIKISHWA MAHAKAMANI KWA KUSUMBUA MAJIRANI ...'ANAWIKA SANA'

Jogoo huyu ambaye mmiliki wake amempatia jina la Maurice, amekuwa kero kwa majirani kwa kuwika kila alfajiri na malambuno kumhusu sasa yanajadiliwa katika mahakama moja nchini Ufaransa.

Analaumiwa kwa kusababisha kalele na familia moja katika kisiwa cha Oléron huko Ufaransa.

Mmiliki wake, Corinne Fesseau, anasema jogoo Maurice anafanya kile majogoo wote wanafanya 'kuwikaa'.

Waliomshtaki Maurice na Maurice mwenyewe hawakufika mbele ya mahakama ya mji wa magharibi wa Rochefort siku ya Alhamisi kesi ilipoanza kusikilizwa.

Lakini jogoo huyo ambaye amekuwa maarufu kutokana na kesi inayomkabili, amepata uungwaji mkono kutoka kwa wafugaji kuku wengine ambao walikusanyika nje ya mahakama.Corinne Fesseau akiwa na jogoo wake

Walalamishi, Jean-Louis Biron na Joëlle Andrieux, walijenga nyumba yao mapumziko katika kijiji cha Saint-Pierre-d'Oléron karibu miaka 15 iliyopita, lakini baadae wakaigeuza kuwa nyumba ya kuishi walipostaafu.

Sababu moja iliyowafanya kuchagua sehemu hiyo ni utulivu wake lakini tatizo ni kuwa jogoo Maurice, amekuwa kero kwao kwani amekuwa akiwapigia kelele kila aalfajiri anapowika.

Wanasema tatizo hilo lilianza tangu mwaka 2017 jirani yao alipomnunua.

Walipowasilisha lalama zao kwa Bi Fesseau, ambaye ameishi Oléron kwa miaka 35, mabishano makali yalizuka mpaka mzozo kati yao ukagonga vichwa vya habari ulipofikishwa mahakamani.

Bi Fesseau, na majirani zake wengine, walisema hakuna mjadala kuhusu swala hilo - kwa sababu ufugaji wa kuku ni sehemu ya maisha ya vijijini na kwamba hawaelewi kwa nini walalamishi wanaomba jogoo huyo azuiliwe kuwika.

Utatuzi wa mzozo huo unasalia na mahakama ambayo inasubiriwa kutoa uamuzi wa kesi mwezi Septemba mwaka huu.
Chanzo - BBC
Share:

Mali za Freeman Mbowe Kupigwa Mnada Kesho

Mali za Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema),  zinatarajiwa kupigwa mnada Julai 6, mwaka huu.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kampuni ya udalali ya Fosters Auctioneers & General Traders ya jijini Dar es Salaam, mali zitakazopigwa mnada ni kila kitu kilichokuwamo ndani ya Ukumbi wa Bilicanas uliopo Mtaa wa Mkwepu, jijini Dar es Salaam.

“Mnada huo utafanyika kuanzia saa nne asubuhi kwenye ghala la Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) karibu na geti namba 3, bandarini,” imesema taarifa hiyo.



Share:

Shirika La Posta Kuanza Kupokea Maombi Ya Fomu Za Mikopo Ya Wanafunzi Julai 8 Mwaka Huu

Na Mwandishi Wetu,MAELEZO
SHIRIKA la Posta Nchini (TPC) kupitia Ofisi zake 170 zilizopo nchini kuanzia Julai 8 mwaka huu litaanza kupokea na kusafirisha vifurushi vyenye fomu za maombi ya mikopo ya wanafunzi wa Juu nchini na kuziwasilisha katika Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB).

Akizungumza  Alhamisi (Julai 4, 2019) katika Maonesho ya 43 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, Meneja wa Usimamizi wa Fedha za Kigeni wa TPC, John Tinga alisema fomu zitasafirishwa zikiwa na bahasha maalum yenye nembo za HESLB na TPC.

Tinga alisema ili kurahisha zoezi hilo, TPC imeweka mawakala wake maalum watakaotumika kwa ajili ya kusaidia huduma za usafirishaji wa maombi hayo ikiwemo kutumia pikipiki katika maeneo yaliyopo sehemu za vijijini ili kuwezesha fomuhizo  kufika kwa urahisi katika ofisi za TPC zilizopo katika Ofisi zake za mikoa na Wilaya zote nchini.

Kwa mujibu wa Tinga alizitaja gharama za usafirishaji wa vifurushi hivyo ni Tsh 16,000 kwa fomu za maombi yatakayotumwa  kutoka mikoani ambayo yatawasilisha katika mfumo wa EMS wakati kwa upande wa DSM gharama za kutuma zitakuwa ni Tsh 8000 na hakutokuwa na gharama nyingine zozote zitakazotozwa kwa wateja hao.

Aliongeza kuwa TPC kwa kushirikiana na HESLB zimejipanga katika kuhakikisha kuwa zoezi hilo linaendeshwa kwa ufanisi mkubwa ili kuwawezesha wanafunzi wote nchini kuwasilisha maombi yao kwa wakati na kuepukana na usumbufu wa kutuma maombi hayo katika tarehe za mwisho.

“TPC imejipanga vizuri kwa ajili ya kufanikisha zoezi hili na hakuna fomu yoyote ya maombi itakayopotea tunachokihitaji ni kwa waombaji kukamilisha taratibu zote za msingi ikiwemo kuweka jina lake nyuma ya bahasha zetu” alisema Tinga.

Akifafanua zaidi Tinga alisema malengo ya Shirika hilo ni kutoa huduma bora kwa wananchi na wateja wote nchini ili kuhakikisha malengo ya Shirika hilo yanaweza kufikiwa ikiwemo kutoa huduma bora zinazozingatia viwango vya kimataifa.

Katika hatua nyingine, Tinga alisema Shirika hilo pia limeanzisha huduma ya mfumo mpya wa mawasiliano wa ‘Net Smart’ inayowezesha kutuma na kupokea vifurushi vyote kwa njia ya haraka zaidi.


Share:

Tume Ya Madini Yatoa Mafunzo Kwa Wachimbaji Wadogo 350

Na Mwandishi Wetu,MAELEZO
SERIKALI kupitia Tume ya Madini imetoa mafunzo kwa wachimbaji wadogo wa madini 350 katika mikoa ya Arusha na Katavi yaliyolenga kuwajengea uwezo wa kutumia njia bora na za kisasa ili kuwawezesha kuachana na matumizi ya matumizi ya Zebaki yanayoathiri mazingira.

Akizungumza  Alhamisi (Julai 4, 2019) katika Maonesho ya 43 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF) yanayoendelea katika Viwanja vya Julius Nyerere , Mkaguzi wa Madini na Mazingira wa Tume hiyo, John  Mataro alisema Tume hiyo imekusudia kuhakikisha kuwa suala la uhifadhi na utunzaji wa mazingira linapewa na kila mchimbaji wa madini nchini.

Mataro alisema Ofisi hiyo imekuwa ikiotoa miongozo mbalimbali kupitia sheria zilizopo kwa ajili ya kuwaelimisha wachimbaji wadogo, na kampeni hiyo itakuwa endelevu ili kuhakikisha kuwa maeneo yote yanayotumiwa na wachimbaji madini hususani wachimbaji wadogo yanazingatia maelezo hayo ili kuweza kuwa na uchimbaji endelevu na salama.

“Malengo ya Serikali ni kuhakikisha kuwa wachimbaji wetu wanaweza kupata kipato cha kutosha ili kuweza kujikwamua kiuchumi, na hili litafanyika kwa kuhakikisha kuwa tunajenga mazingira yenye usalama wa hali ya juu katkika maeneo yote ya uchimbaji yaliyopo nchini” alisema Mataro.

Aidha Mataro aliongeza kuwa Tume hiyo kwa kutambua mchango wa wachimbaji wadogo nchini imekuwa ikiwajengea uwezo wachimbaji hao kwa kujenga mazingira wezeshi ikiwemo kupata mikopo nafuu kupitia taasisi za kifedha ikiwemo Benki, hatua inayolenga kuwapa morali na uwezo wa kumiliki vifaa bora na vya kisasa kwa ajili ya uchimbaji wa madini.

Akifafanua zaidi Mataro alisema mara kwa mara Tume hiyo imekuwa ikifanya ziara katika migodi mbalimbali iliyopo nchini yenye lengo la kuwakumbusha wachimbaji wote hususani wachimbaji wadogo kuzingatia miongozo mbalimbali ikiwemo kuwepo matangazo mbalimbali ya tahadhari katika maeneo ya uchimbaji ili kuweza kutoa taarifa kwa wahusika wanaofika katika maeneo hayo kwa mara ya kwanza.


Share:

Serikali Yasema ni Marufuku mbolea kuchelewa kufika kwa wakulima

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Dar es salaam
Serikali imetangaza kiama kwa wanaochelewesha mbolea kuwafikia wakulima kwa wakati kwani kuchelewa kwa mbolea ni miongoni mwa sababu zinazopunguza uzalishaji wa mazao mbalimbali ya wakulima nchini.

Mbolea kutofika kwa wakulima kwa wakati ni wazi kuwa Taasisi iliyopewa jukumu la kusimamia na kudhibiti mbolea ya TFRA imeshindwa kufanya kazi yake kwa ufasaha hivyo ikibainika kuchelewa kwa mbolea pasina sababu za msingi watendaji hao watachukuliwa hatua za kisheria.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) ametoa kauli hiyo ya onyo leo tarehe 4 Julai 2019 Jijini Dar es salaam wakati akizungumza kwenye kikao kazi na wafanyakazi wa Taasisi ya udhibiti wa mbolea Tanzania (TFRA).

Alisema kuwa mbolea inayohitajika kwa wakulima ni Lazima ipatikane kwa wakati katika maeneo ya kilimo. “Kupatikana kwa wakati maana yake ni kwamba kila mtu anapoishi anapaswa kuipata kirahisi kupitia maduka au masoko” Alisema

Aliongeza kuwa kazi ya Taasisi ya udhibiti wa mbolea Tanzania ni kuhakikisha mbolea inawafikia wakulima sio kusalia Jijini Dar es salaam ilihali wakulima wapo mikoa yote Tanzania na endapo mbolea ikikosekana kwa wakulima watendaji wa TFRA watachukuliwa hatua za kinidhamu.

Kadhalika alisema kuwa kupatikana pekee kwa mbolea kwa wakulima ni jambo moja lakini muhimu ni kuwa na bei nafuu ambazo wakulima wataweza kuzimudu.

“Sasa hivi kuna malalamiko mengi kwa wakulima kuwa mbolea zinauzwa bei ya juu hivyo wameshindwa kuzimudu, haiwezekani mbolea itoke Ulaya ikiwa na bei nafuu lakini kumfikia mkulima inakuwa na bei ghali, hapo ni wazi kuwa TFRA hamjafanya kazi yenu sawasawa” Alikaririwa Mhe Hasunga

Alisema kuwa endapo TFRA itatekeleza majukumu yake ipasavyo mbolea itapungua bei na wakulima watanufaika na serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe Dkt John Pombe Magufuli, Rais wa Tanzania.

“Na kama tatizo la gharama linaongezeka kutokana na usafirishaji kuna sababu gani za kutumia magari kusafirisha wakati kuna usafiri muhimu wa reli (TRC) ambapo mawakala wangepakua na kusambaza mizigo hiyo baada ya kufika katika maeneo mbalimbali inapoishia reli” Alisema

Hata hivyo amesisitiza kuwa serikali imeanzisha mchakato wa kupitia mbolea kote nchini ili uagizaji wa mbolea iweze kuagizwa itakayoendana na uwezo wa udongo.


Share:

Kamati Ya Ulinzi Na Usalama Mkoa Simiyu Yaridhishwa Na Kasi Ya Tba Ujenzi Wa Ofisi Ya DC Busega

Na Stella Kalinga, Simiyu
Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Simiyu ikiongozwa na Mkuu wa Mkoa, Mhe. Anthony Mtaka imeridhishwa na kasi ya Ujenzi  wa  jengo la ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Busega na majengo ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu, chini ya Mkandarasi Wakala wa Majengo nchini  (TBA ).

Hayo yamebainishwa na kamati hiyo ,mara baada ya kukagua ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Busega ambapo ujenzi umeanza mwezi Aprili mwaka huu na  unatarajia kukamilika ifikapo mwezi Oktoba mwaka huu.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amesema miradi yote inayotekelezwa na TBA Simiyu imekuwa ikitekelezwa kwa wakati na wakati mwingine imekuwa ikitekelezwa na kukamilika kabla ya muda uliopangwa katika mkataba, huku akiishukuru serikali kwa kutenga fedha za  ujenzi wa ofisi ya mkuu wa wilaya ya Busega  ambayo itatua changamoto za  wananchi za upatikanaji wa huduma kwa karibu .

“Tumepata Meneja mzuri wa TBA ambaye anatekeleza miradi yake kwa wakati, miradi yote tuliyompa imetekelezwa mbele ya muda uliowekwa kwenye mkataba; kwa mradi huu umeenda kwa kasi ambayo inaendana na uhitaji wa wananchi wa Busega waliokuwa wanahitaji mahali pa kupata huduma” alisema Mtaka.

Mkuu wa wilaya ya Busega Mhe.Tano Mwera amesema utendaji wa kazi kwa sasa ni mgumu kutokana na ufinyu wa jengo wanalolitumia kama ofisi, hivyo kukamilika kwa jengo hilo kutawasaidia kufanya kazi kwa ufanisi.

“Tunamshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kutupa fedha za ujenzi wa jengo hili, litakapo kamilika litatuwezesha kufanya kazi kwa ufanisi kwa sababu ofisi tunayoitumia sasa hivi ni finyu sana na watendaji wametawanyika sana hivyo inatuwia vigumu kiutendaji”alisema Mwera.

Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini amesema kazi zote  zinazofanywa na Wakala wa majengo nchini TBA Mkoa wa Simiyu zimekuwa zikifanywa kwa viwango na zinakamilika kwa wakati, huku akiahidi kulipa fedha zilizobakia kwa wakati.

Kwa upande wake Meneja wa Wakala wa Majengo nchini TBA Mhandisi Likimaitare Naunga amesema mkataba wa ujenzi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Busega ni miezi mitano na wanatarajia kukamilisha ujenzi kabla ya mwezi Oktoba mwaka huu.

Kukamilika kwa ujenzi awamu ya kwanza ya jengo hilo  utagharimu kiasi cha shilingi milioni mia saba  nukta saba.


Share:

Iran yamuita balozi wa Uingereza kuhusiana na kuakamatwa meli yake

Iran imemuita balozi wa Uingereza mjini Tehran kuhusiana na kile ilichosema ni kukamatwa leo kinyume cha sheria meli ya mafuta ya Iran katika kisiwa cha Gibraltar. 

Televisheni ya serikali ya Iran imemnukuu msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nchi za Kigeni Abbas Mousavi akithibitisha habari hizo. 

Jeshi la wanamaji wa Uingereza lilikamata meli hiyo ya mafuta ikituhumiwa kwa kupeleka mafuta nchini Syria ikiwa ni hatua ya kukiuka vikwazo vya Umoja wa Ulaya. 

Kitendo hicho kinazusha hofu ya kuongeza mgogoro kati ya nchi za Magharibi na Iran. 

Waziri Kiongozi wa Gibraltar Fabian Picardo alisema katika taarifa kuwa wanaizuilia meli hiyo na shehena yake. 

Meli hiyo inasafiri kwa bendera ya Panama na inaaminika kuwa imebeba mafuta ya Iran.


Share:

Kijana Atiwa Mbaroni Kwa Kumlawiti Mama Yake Mzazi

Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma.
Jeshi la polisi Mkoani Dodoma linamshikilia  Kijana mmoja Donald Justine(25] baada ya kumvizia na kumbaka bibi kizee mwenye umri wa miaka 95 huku yakitajwa Matukio ya ukatili kuongezeka kutoka 174 mwaka 2018 hadi matukio 517 mwaka 2019 mkoani humo.

Akizungumza na  waandishi wa Habari Julai 4,2019,Kamanda wa polisi mkoa wa Dodoma, Kamishna msaidizi wa polisi, Gilles Muroto amesema Katika eneo la Nane nane kata ya Nzuguni, Dodoma Mjini,  kikongwe wa miaka 95, mkazi wa eneo hilo  alibakwa na kijana mmoja Donald Justine(25) aliyemvizia akiwa amelala na kumkaba shingoni kisha kumtendea unyama huo. 

Kamanda Muroto ameyataja matukio mengine ,Katika kijiji cha Mlazo, tarafa ya Mpyayungu, Wilaya ya Chamwino, Makame Wambura, (28) na mtoto wake Fidelika Walioba miezi mitatu(3) baada ya kumwagiwa mafuta ya petrol na mume wake aitwae Elias Warioba (30) na wote wawili kujeruhiwa vibaya na wamelazwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Dodoma, na hapa kamanda anaelezea tukio lilivyotokea.

Tukio la tatu  katika kijiji cha Manchali, tarafa ya Chilonwa, Wilayani  Chamwino, walimkamata Mazengo Chilatu(28) kwa kosa la kumlawiti mama yake mzazi ambaye  hakujulikana jina wala umri wake kwa kumvizia akiwa amelala.

Lingine katika eneo la Maili mbili jijini humo ,ni tukio la Mwanaume mmoja anayekadiliwa kuwa na umri wa miaka 25- 30 ambaye hakufahamika jina lake alifanya matukio matatu ya ubakaji kabla ya kukamatwa na wananchi na kupigwa na wananchi kabla ya kuokolewa na polisi na baadaye kufariki. 

Ambapo alifanya matukio hayo kwa watu watatu tofauti kabla ya Julai 4  kukamatwa na  wananchi wenye hasira kali na kuupigwa vibaya na kuokolewa na jeshi la polisi hata hivyo alifariki baadaye. 

Hata hivyo, amepongeza kazi nzuri inayofanyawa na wanahabari katika kuripoti habari za ukatili huo, ambapo amesema kwa sasa kumekuwa na mwamko mkubwa wa wananchi kuripoti matukio hayo kwa  jeshi la polisi. 

Hata hivyo Kamanda Muroto        amesema matukio  ya ukatili mkoani Dodoma yameongezeka kutoka matukio 174 kwa mwaka 2018 na kufikia matukio 517 huku vyanzo vikitajwa kuwa ni ulevi,mmomonyoko wa maadili,uvivu,imani za kishirikina ,tamaa na ukatili.


Share:

Rais Magufuli kuzindua rasmi hifadhi mpya ya Taifa ya Burigi iliyoko Chato

Rais John  Magufuli anatarajiwa kuzindua rasmi Hifadhi ya Taifa ya Burigi huko Chato siku ya Jumanne Julai 9,  mwaka huu, ambayo imepandishwa hadhi hivi karibuni kutoka lililokuwa pori la akiba la Burigi, ambapo pamoja na mambo mengine, atakabidhi vibali na hati kwa wawekezaji mbalimbali ili kuwekeza katika eneo hilo.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamis Kigwangalla amesema hayo jijini Mwanza jana, katika mkutano wa mwaka wa Wahariri na Waandishi waandamizi ulioandaliwa na Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (Tanapa).

Alisema ili sekta ya hifadhi iweze kuleta mabadiliko ni lazima jamii wakiwamo wanahabari washiriki katika kutangaza vivutio vya utalii kama njia ya kuongeza idadi ya wageni wa ndani na nje.

“Bila wanahabari sekta ya utalii haiwezi kujulikana hivyo tushirikiane pamoja katika hili.

“Na pia kama mnakumbuka hivi karibuni tumetangaza hifadhi mpya za taifa na Jumanne Rais Magufuli, atazindua hifadhi ya Burigi Chato, lengo ni kuhakikisha wageni waweze kuona maliasili zetu popote pale Tanzania,” alisema Dk. Kigwangalla.


Share:

Profesa Anna Tibaijuka Atangaza Kung'atuka Ubunge

Mbunge wa Muleba Kusini, Profesa Anna Tibaijuka (CCM), amesema hatagombea tena nafasi ya ubunge Uchaguzi Mkuu ujao. Tibaijuka  alitoa kauli hiyo wakati akihojiwa na  Ayo Tv

Pamoja na mambo mengine, alisema anastaafu kwa sababu yeye ni kizazi cha Mwalimu Julius Nyerere ambaye aliwafundisha kung’atuka.

“Mimi 2020 ninastaafu, ninang’atuka kwa sababu sisi ni kizazi cha Mwalimu Nyerere na katika vitu alivyotufundisha ni kung’atuka.

“Katika uchaguzi wa 2015, Muleba Kusini pamoja na kampeni ya Escrow bado nilipita kidedea, kwa kweli nawashukuru wananchi wa Muleba, ni watu wanaotafuta maendeleo, wana kiu ya maendeleo.

“Na ninaposema nastaafu ubunge, haimaanishi kwamba nastaafu Muleba, hivi ni vitu viwili tofauti, mimi ninastaafu uwakilishi, Bunge letu hili lingekuwa Seneti ningesema nitaendelea.

“Lakini sasa ni Bunge la Uwakilishi, hatuna Bunge la Seneti, yaani Bunge ambalo sasa hoja zinalinda masilahi mapana ya umma, hapa tunawakilisha wananchi na mimi naamini tunaweza kupata mwakilishi mzuri wa Muleba,” alisema.

Alisema anaamua kung’atuka si kwa sababu ya kuhofia kushindwa, kwani ingekuwa hivyo angeshindwa katika uchaguzi uliopita kutokana na kampeni chafu juu yake.

“Mimi kama kupigwa chini, ningepigwa chini mwaka 2015 au sio. Asiyekubali kushindwa si mshindani, kwa hiyo mimi sistaafu kwa ajili ya hofu, kwanza Muleba anayenishinda ni nani? Ni Mwenyezi Mungu peke yake.

“Kwa kipindi cha miaka 10 nimejifunza, nimeelewa matatizo ya wananchi na wakati ule nilipotoka Umoja wa Mataifa, nilikuja na nia moja ya kujifunza kwamba taifa letu lina tatizo gani.

“Tufanye nini ili tuweze kusogea mbele, kwa hiyo hata bungeni ninaposimama, nikiona kitu hakijakaa sawa huwa sisimami kiitikadi, pia sitaki ushabiki ambao hauna mantiki,” alisema. 



Share:

TTCL Yavuna Wateja Wapya 215,000 Na Kuitikia Wito Wa Rais Magufuli

Na Mwandishi Wetu, MAELEZO
SHIRIKA la Mawasiliano Nchini (TTCL) katika kipindi cha siku 30 limeweza kusajili wateja wapya 215,000, ikiwa ni Mpango Mkakati wa Shirika hilo katika kujiinua kibiashara na kuongeza wigo huduma ya Mawasiliano kwa Watanzania ikiwa ni utekezaji wa agizo la Rais Dkt. John Magufuli.

Akizungumza Alhamisi (Julai 4, 2019) katika Maonesho ya 43 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam yanayoendelea katika Viwanja vya Julius Nyerere, Meneja Mawasiliano wa TTCL Nicodemus Mushi alisema Shirika hilo limetekeleza kwa vitendo agizo la Rais Dkt. John Magufuli alilolitoa kwa Shirika hilo tarehe 21 Mei, mwaka huu.

Mushi alisema hadi sasa huduma za Mawasiliano za Kampuni hiyo katika Mfumo wa 4G zinapatikana katika Mikoa 16 nchini na mpango uliopo ni kuhakikisha kuwa maeneo yaliyobaki yanapata huduma za Shirika kupitia  Mpango Mkakati wa Shirika hilo uliojiwekea na hivyo kuweza kuleta ushindani wa huduma ya mawasiliano na makampuni mengine nchini.

“Mwaka uliopita tulijiwekea Mpango Mkakati wetu ambao utahakikisha kuwa tunaweza kuleta ushindani na makampuni mengine na hivi sasa kama unavyoona tumeweza kupata wateja wapya 215,000 na kupitia maonesho hayo tutaweza kuongeza wateja wengi zaidi ” alisema Mushi.

Aliongeza kuwa kwa sasa Shirika hilo limeweza kupata wateja wengi zaidi wakiwemo watumishi wa serikali, ambapo kwa kutambua umuhimu huo, TTCL imeanzisha kifurushi maalum cha ‘watumishi pack’ ambacho kinaweza kutumiwa na wafanyakazi wote wa serikali kwa kuweza kukamilisha taratibu mbalimbali ikiwemo vitambulisho vya kazi.

Akifafanua zaidi Mushi, alisema kauli zinatolewa na watu mbalimbali kuhusu kauli ya Rais Dkt. John Magufuli kuwataka wafanyakazi wa serikali kutumia huduma za mawasiliano za shirika hilo, ni kuwa zitawahusu watumishi wa umma ambao wanalipiwa huduma za mawasiliano ya simu na serikali na si kinyume na maelekezo hayo.

Aliongeza kuwa malengo ya Taasisi hiyo ni kuweza kujipanga ili kuendelea kutoa huduma bora na zenye viwango ili kuweza kuongoza na kuwa kampuni bora ya mawasiliano inayotoa huduma bora kwa wateja wake nchini.

“Sisi kwa upande wetu tumeendelea kuwalipa vizuri mawakala wetu ikiwemo kutoa kamisheni nzuri kwao ili kuhakikisha kuwa huduma zetu zinazotolewa zinakuwa zinakidhi matakwa ya wateja na soko la mawasiliano kwa ujumla” alisema Mushi.


Share:
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger