Monday 26 October 2020

Wasimamizi Wa Vituo Vya Kupigia Kura, Makarani Waongozaji Wapewa Mafunzo

...


 Msimamizi wa Uchaguzi Mkuu Jimbo la Busega Anderson Njiginya Kabuko, amewataka wasimamizi, wasimamizi wasaidizi na makarani waongozaji wa vituo vya kupigia kura katika uchaguzi mkuu kuzingatia maelekezo na mafunzo yote wanayopewa ili kufanikisha zoezi la Uchaguzi mkuu wa tarehe 28/10/2020. Kabuko ameyasema hayo wakati akifungua semina ya mafunzo tarehe 24/10/2020 katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Bulima.  

Aidha amewataka wasimamizi na wasimamizi wasaidizi wa vituo kuwa makini na kutojihusisha na vitendo vitakavyowatia hatiana ikiwemo vitendo vya rushwa. “Katika kipindi hiki mnaweza kupata ushawishi mkubwa kutoka kwa makundi mbalimbali, ushawishi utakaoashiria vitendo vya rushwa, hivyo kufanya hivyo ni kinyume na taratibu za usimamizi wa Uchaguzi”, aliongeza Kabuko.

Wasimamizi, wasimamizi wasaidizi na makarani waongozaji wa vituo vya kupigia kura wamekula viapo mbele ya Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Busega huku sehemu yao wakikiri kwamba mafunzo hayo yamewafanya kufahamu mambo mengi hivyo wanatarajia kufanya kazi kwa uadilifu mkubwa.

Semina ya mafunzo kwa wasimamizi wakuu wa vituo na wasimamizi wasaidizi yanafanyika kwa siku mbili kuanzia tarehe 25 hadi 26 Oktoba 2020 katika ukumbi wa Shule ya Msingi Bulima na Silsos, lakini awali pia yalifanyika mafunzo ya Makarani waongozaji wa vituo vya kupigia kura ambapo mafunzo yalifanyika tarehe 24/10/2020 katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Bulima.

Jumla ya wasimamizi wakuu, wasimamizi wasaidizi na makarani waongozaji wapatao 1,300 watashiriki katika Uchaguzi wa mkuu katika jumla ya vituo 325 jimbo la Busega.


Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger