Monday 26 October 2020

Kwa Jeshi Letu la JWTZ Najivunia Kutunza Amani, Kukuza Uchumi na Kuimarisha Huduma kwa Jamii

...


Na. Paschal Dotto-MAELEZO.
Jeshi la wananchi wa Tanzania (JWTZ), limeendelea kufanya mabadiliko makubwa ambayo matokeo yake  ni Amani, uzalishaji na ukuaji wa viwanda ambavyo vinaleta tija na kuifanya nchi kuingia kwenye uchumi wa kati kutokana na jeshi hilo kuwa sehemu ya uzalishaji na mmiliki wa njia kuu za uchumi.

JWTZ inaeleza kuhusu makampuni yake ambayo yanafanya kazi kubwa katika kutekeleza wajibu wake na kulifanya jeshi hilo kujivunia katika kutunza Amani, kukuza uchumi hususani katika sekta ya viwanda pamoja na huduma za afya.

Katika kutekeleza azma ya ukuaji wa uchumi JWTZ imewekeza kwenye makampuni ya Nyumbu,  Mzinga na Suma JKT makampuni ambayo yanafanya vizuri katika kuiwezesha JWTZ kuwa mzalishaji mzuri.

JWTZ kupitia shirika lake la Nyumbu pamoja na Mzinga yameendelea kufanya tafiti ambazo ni muhimu kwa ulinzi  na usalama wa nchi, tafiti ambazo zinalenga katika kukuza teknolojia ya ulinzi, kuinua maendeleo ya jamii na nchi kwa ujumla.

Shirika la Nyumbu limetekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ya utengenezaji wa gari la zima moto, gari la nyumbu, kutengeneza na kuzalisha nyuzi za mkonge, kuzalisha gesi na mradi wa kuzalisha trekta dogo ( power tiller), huku Mzinga ikiendelea na uzalishaji wa mazao ya chakula kwa ajili ya Majeshi ya Ulinzi na Usalama.

JWTZ, imejikita pia kutoa huduma za afya kwa wananchi kwani inamiliki hospitali ambazo zinatoa huduma ya moja kwa moja kwenda kwa wananchi zikiwemo za Lugalo Jijini Dar es Salaam, hospitali ya Kanda Jijini Mbeya, hospitali ya jeshi Jijini  Mwanza na Zanzibar.

Kwa Mujibu wa Ripoti ya jeshi hilo, hospitali hizo zimefungwa vifaa vya kisasa na  kutoa  huduma bora kwa wananchi kuashiria ushirikiano mkubwa kati ya JWTZ na raia wa kawaida kwani wanaotibiwa katika hospital hizo kwa asilimia 70, ni wananchi wa Tanzania.

Kutokana na ripoti hiyo vifaa vilivyonunuliwa ni pamoja na Dialysis Machine, CT-Scan na Ultra sound ambazo zimefungwa katika hospital hizo zinatoa huduma kwa wananchi katika maeneo husika.

Kwa upande mwingine ripoti hiyo inaeleza jinsi Shirika la Jeshi la Kujenga Taifa (Suma JKT), linavyokuja kwa kasi katika kujenga uimara kwenye  maeneo tofauti ya kiuchumi, shirika limamiliki kampuni inayotoa huduma ya chakula kwenye kumbi mbalimbali (Suma JKT Catering Services), Suma JKT Cleaning and Fumigation, Suma JKT Clearing and Forwading na nyinginezo ambazo zinatoa huduma na kuimarisha upatikanaji wa ajira kana vile Shiriki lina kampuni tanzu ya Suma JKT Guard.CO.LTD ambayo imeajiri vijana 10,000.

JWTZ, imeweza kuanzisha programu maalum ambayo inahususisha mafunzo ya kijeshi na inatoa shahada ya kwanza ya sayansi ya kijeshi (Bachelor of Military Science), amabayo inatolewa katika Chuo cha Maafisa Wanafunzi kilichopo  Monduli Mkoa wa  Arusha.

Pia, Ripoti inaeleza jinsi jeshi lilivyoimarisha kutoa mafunzo kwa vijana wa kujitolea kwa hiari na wale wa mujibu wa sheria, ambapo kuanzia 2007 hadi 2012 zimeanzishwa kambi za Kanembwa (Kigoma), Mtabila (Kigoma) na Mbweni (Dar es Salaam). Mwaka 2018 hadi 2020 kambi za Mpwapwa, Kibiti, Makuyuni, Itaka (Songea), Luwa (Rukwa) na Milundikwa (Katavi).

Pia, JWTZ inashiriki kwa ukaribu katika kukabili majanga kwani, mwaka 2016 iliweza kukarabati shule ya wavulana na Ihungo Mkoani Kagera baada ya kuharibiwa na tetemeko la ardhi.


Share:

0 comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

Popular Posts

Unordered List

Pages

Blog Archive


Copyright © MASWAYETU BLOG | Powered by Blogger